-
“Nilitaka Tu Kuchukua Barua Zangu”Amkeni!—2011 | Juni
-
-
“Nilitaka Tu Kuchukua Barua Zangu”
“SITASAHAU asubuhi hiyo ya Jumatatu (Siku ya 1) kwenye posta,” anasema Andre, mwanamume mzungu aliyezaliwa nchini Afrika Kusini lakini anayeishi Namibia. “Ofisi za posta zilikuwa zimejaa watu. Niliona mfuko uliokuwa umeachwa sakafuni. Nilichukua barua zangu na kuondoka. Baada ya kuendesha gari kwa dakika tatu hivi nilisikia mlipuko mkubwa. Baadaye, niligundua kwamba bomu lilikuwa limelipuka karibu sana na mahali nilipokuwa nimetoka kusimama.”
“Nilitaka tu kuchukua barua zangu,” anaeleza Andre. “Lakini nilishtuka sana kujua kwamba watu wasio na hatia, ambao baadhi yao nilikuwa ninawafahamu walikuwa wamelipuliwa vipande-vipande. Bado mimi huingiwa na hofu ninapokumbuka tukio hilo, ingawa lilitukia zaidi ya miaka 25 iliyopita. Nyakati nyingine, mimi huwakumbuka watu niliowaona wakiwa wamekufa au kujeruhiwa na kujiambia kwamba niliponea chupuchupu.”
Tatizo la Ulimwenguni Pote
Ingawa huenda usipatwe moja kwa moja na shambulio kama hilo, huenda umesikia kwamba matukio kama hayo yanatendeka mara nyingi ulimwenguni pote. Watu wengi zaidi wanatumia jeuri, matendo ambayo mara nyingi yanaitwa ya kigaidi ili kutimiza malengo yao.—Ona sanduku “Magaidi Ni Nani?” kwenye ukurasa unaofuata.
Mwandishi fulani wa habari anayechunguza mambo aligundua kwamba mnamo 1997 kulikuwa na “nchi nne tu ambako magaidi wa kujitoa mhanga walikuwa wakitenda kwa kuendelea.” Lakini katika mwaka wa 2008 mchunguzi huyohuyo aliandika kwamba “zaidi ya nchi 30 katika kila bara isipokuwa Australia na Antaktika zilikumbwa na mashambulizi mabaya ya ugaidi wa kujitoa mhanga.” Alimalizia kwa kusema kwamba mashambulizi hayo “yanatekelezwa na makundi mengi zaidi, na yanawaua watu wengi zaidi kila mwaka.”—The Globalization of Martyrdom.
Fikiria shambulizi lililotajwa mwanzoni mwa habari hii. Kikundi cha watu waliodai kwamba walilipua bomu hilo walijiita wapiganiaji uhuru. Walikuwa wakijaribu kujipatia uhuru kutoka kwa serikali iliyotawala nchi yao. Lakini ni nini ambacho huwachochea watu wafanye mambo kama hayo ili kutimiza malengo yao? Fikiria kisa cha Hafeni.
Hafeni alizaliwa nchini Zambia na kulelewa katika kambi za wakimbizi katika nchi jirani. “Nilikuwa na hasira,” akasema, “kwa sababu ya ukatili na ukosefu wa haki ambao familia yetu na nyingine zilikuwa zimetendewa.” Kwa hiyo, akajiunga na kikundi cha wanamgambo ambacho wazazi wake walishirikiana nacho.
Akifikiria kuhusu nyakati hizo, Hafeni anaendelea kusema: “Jambo lenye kusikitisha zaidi ni madhara ya kihisia unayopata kwa kuishi kama mkimbizi. Watoto walitenganishwa na mama, baba, na ndugu na dada zao. Wale wenye umri mkubwa walienda kupigana. Wengi wao hawakurudi. Sikuwahi kumwona baba yangu, hata katika picha. Ninachojua tu ni kwamba alikufa vitani. Bado ninakumbwa na maumivu makali ya kihisia hadi leo.”
Kwa kweli, mambo yanayohusika ni magumu. Kuelewa mambo hayo vizuri kutakuwezesha kuona kinachopaswa kufanywa ili wanadamu waishi bila jeuri ya aina hiyo.
[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 4]
MAGAIDI NI NANI?
Mtafiti Mark Juergensmeyer anaeleza: “Iwe mtu atatumia neno ‘gaidi’ kufafanua matendo ya jeuri au la, kunategemea ikiwa anafikiri matendo hayo ni ya haki. Kwa kiasi kikubwa utumizi wa neno hilo unategemea maoni ya mtu kuhusu ulimwengu: iwapo anaona ulimwengu kuwa wenye amani, basi matendo ya jeuri yanaonekana kuwa ugaidi. Iwapo anaona kuna vita ulimwenguni, basi huenda matendo ya jeuri yakaonekana kuwa halali.”
Kwa hiyo, mara nyingi kuna sababu za kisiasa wakati neno “gaidi” linatumika. Vikundi vingi hujiona kuwa vya wapiganiaji uhuru, si magaidi. Kupatana na mwandikaji mmoja, ugaidi unahusisha (1) matendo yaliyokusudiwa kuwaathiri raia na (2) utumizi wa jeuri ili kupitisha ujumbe, yaani, kuwaogopesha watu. Kwa hiyo, wapiganaji—wawe ni wanamgambo au ni wa serikali—mara nyingi wanaweza kutumia mbinu za kigaidi.
-
-
Kwa Nini Watu Fulani Hutenda kwa Jeuri?Amkeni!—2011 | Juni
-
-
Kwa Nini Watu Fulani Hutenda kwa Jeuri?
JOSEBA, anayeishi nchini Hispania, aliulizwa kwa nini alijiunga na kikundi cha wanamgambo. “Ukandamizaji na ukosefu wa haki tuliopatwa nao ulikuwa mwingi,” akasema. “Katika jiji kubwa la Bilbao, ambako nilikuwa nikiishi, polisi walikuwa wakija, wanawapiga watu, na kuwakamata.”
Joseba anaendelea kusema: “Asubuhi moja nilikamatwa kwa kueleza waziwazi hisia zangu kuhusu mbinu hizo za polisi. Nilikasirika sana hivi kwamba nilitaka kufanya jambo fulani—ujeuri wa aina fulani—ili kutuliza hali hiyo.”
Ukandamizaji na Kulipiza Kisasi
Bila kutetea jeuri, Biblia inakubali kwamba “uonevu mtupu unaweza kumfanya mtu mwenye hekima atende kiwazimu,” yaani, kwa njia isiyopatana na akili. (Mhubiri 7:7) Watu wengi hukasirika sana wanapotendewa kwa ukosefu wa haki kwa sababu ya jamii, dini, au taifa lao.
Kwa mfano, Hafeni, aliyetajwa katika habari inayotangulia alisema hivi: “Tulinyang’anywa ardhi yetu isivyo haki. Wanyama hupigana ili kutetea maeneo yao, kwa hiyo lilionekana kuwa jambo linalopatana na akili kupigania ardhi na haki zetu.” Mwanamgambo mmoja wa kujitoa mhanga alisema maneno haya yaliyochapishwa baada ya kifo chake: “Msipoacha kuwalipua watu wangu kwa mabomu, kuwaua kwa gesi, kuwafunga, na kuwatesa hatutaacha kupigana.”
Uchochezi wa Kidini
Ingawa kwa kawaida wanamgambo wanachochewa na sababu za kibinafsi, mara nyingi wao hutenda kwa jeuri kwa sababu za kidini. Kiongozi mmoja wa ulimwengu alipokea ujumbe huu kwenye faksi kutoka kwa msemaji wa wanamgambo: “Hatujarukwa na akili wala hatutamani mamlaka. Tunamtumikia Mungu na hilo ndilo linalotufanya tushikilie msimamo wetu kwa bidii.”
Daniel Benjamin na Steven Simon, waliandika hivi katika kitabu chao The Age of Sacred Terror kuhusu uchochezi wa kidini: “Katika ulimwengu unaozidi kuwa wa kidini, waumini wengi wa zile dini kubwa na wa madhehebu mapya wanaamini kwamba jeuri inapaswa kuwa sehemu ya utumishi wao kwa Mungu.” Baada ya kutaja kuhusu “matukio [kadhaa] yenye kustaajabisha ya ugaidi ulimwenguni pote,” mchunguzi mwingine alisema kwamba wote waliotekeleza matendo hayo waliamini kwamba matendo yao yaliruhusiwa, au kuamriwa, na Mungu.”
Lakini wanamgambo wengi wa kidini wana maoni yanayopita kiasi ambayo hayapatani na mafundisho wala na viwango vya msingi vya dini wanazoshirikiana nazo.
Hisia za Jeuri Zimekolea Mioyoni Mwao
Joseba aliyetajwa mapema, alitendewa vibaya sana alipokamatwa. Anasema: “Ukatili huo ulinihakikishia kwamba nilikuwa na haki ya kutenda kwa chuki. Iwapo ningekufa ili kuleta mabadiliko, ingekuwa sawa.”
Mara nyingi mambo yanayofundishwa katika vikundi hivyo huwachochea watu katika vikundi hivyo kujihusisha katika jeuri. “Tulipokuwa kwenye kambi za wakimbizi,” Hafeni anasema, “kulikuwa na mikutano ya wanamgambo iliyotufundisha kwamba kila wakati wazungu walikuwa wakitafuta njia za kuwakandamiza watu weusi.” Kulikuwa na matokeo gani?
Aliendelea kusema hivi: “Chuki yangu kuelekea wazungu iliongezeka. Sikumwamini yeyote kati yao. Mwishowe, singeweza kuvumilia zaidi na nikajiambia kwamba lazima kizazi chetu kichukue hatua.”
Kwa kushangaza, ingawa Joseba na Hafeni walikuwa na msimamo mkali hivyo, wote wawili waliacha kuwa na chuki na wakaanza kuwaamini watu wengine. Ni nini kilichogusa akili na moyo wao? Habari inayofuata itaeleza jinsi hilo litakavyotukia.
[Blabu katika ukurasa wa 6]
“Ukatili huo ulinihakikishia kwamba nilikuwa na haki ya kutenda kwa chuki. Iwapo ningekufa ili kuleta mabadiliko, ingekuwa sawa.”—Joseba
-
-
Je, Inawezekana Kuwa na Ulimwengu Usio na Ugaidi?Amkeni!—2011 | Juni
-
-
Je, Inawezekana Kuwa na Ulimwengu Usio na Ugaidi?
“TUNAHITAJI kujitahidi sana . . . ili tuiguse mioyo na akili.” Huo ndio mkataa uliofikiwa baada ya miaka 20 ya kuchunguza nyutu za watu waliosemekana kuwa magaidi.
Lakini ni nini kinachoweza kubadili mioyo na akili za watu ambao wamehusika sana katika matendo ya jeuri na kulipiza kisasi?
Kitabu Kinachoweza Kubadili Moyo
Katika miaka ya 1990, Hafeni, alianza kuchunguza mafundisho yake ya kidini na akaamua kutafuta Biblia. Anasema hivi: “Nilianza kwa kuchunguza Injili [vitabu vya Biblia vya Mathayo, Marko, Luka, na Yohana], ambavyo vilikuwa na masimulizi ya maisha ya Yesu. Nilipokuwa nikisoma, nilipendezwa upesi na utu wa Yesu na njia yake ya kushughulika na watu kwa fadhili na bila ubaguzi. Hilo liligusa sana moyo wangu.”
Hafeni anasema kwamba alipoendelea kusoma, “andiko moja la Biblia lilinisaidia kabisa kuelewa jinsi Mungu anavyohisi—Matendo 10:34 na 35.” Linasema hivi: “Mungu hana ubaguzi, bali katika kila taifa mtu ambaye anamwogopa na kutenda uadilifu anakubalika kwake.”
Hafeni anasema hivi: “Nilifikia mkataa kwamba wanadamu ndio wanaosababisha ubaguzi wa kikabila, kitaifa, na kijamii. Nilikuja kutambua kwamba ujumbe wa Biblia unaweza kubadili jinsi watu wanavyofikiri na kwamba jambo muhimu zaidi maishani ni kuwa na msimamo mzuri mbele za Mungu. Hilo ni muhimu zaidi kuliko kupigana kwa niaba ya watu wa kabila, jamii, au rangi fulani.”
Joseba, aliyenukuliwa katika habari iliyotangulia, alikuwa anasimamia kikundi kidogo cha kikosi maalumu kilichopanga kulipua kituo kimoja cha polisi. “Lakini kabla ya kutekeleza shambulizi hilo,” anaeleza Joseba, “nilikamatwa na nikafungwa gerezani kwa miaka miwili.” Baadaye, mke wake, Luci, akaanza kujifunza Biblia na Mashahidi wa Yehova. Mwishowe, Joseba alianza kushiriki katika mazungumzo hayo.
Joseba anasema hivi: “Kadiri nilivyojifunza mengi zaidi kumhusu Yesu, ndivyo alivyokuja kuwa kielelezo changu. Nilipendezwa hasa na maneno haya yake: ‘Wale wote wanaouchukua upanga wataangamia kwa upanga.’ Nilijua kwamba maneno hayo yalikuwa ya kweli.” (Mathayo 26:52) Joseba alisema hivi: “Kumwua mtu kunawachochea watu wa familia yake wawe na chuki na tamaa ya kulipiza kisasi. Jeuri inasababisha maumivu tu, haitokezi ulimwengu bora.” Joseba alianza kufanya mabadiliko katika kufikiri kwake.
Hafeni na Joseba walijionea kwamba mafundisho ya Biblia yanaweza kubadili maisha ya mtu. Biblia inasema kwamba “neno la Mungu liko hai nalo lina nguvu” na kwamba linaweza kutambua “fikira na makusudio ya moyo.” (Waebrania 4:12) Nguvu za Neno la Mungu zimewasaidia watu wengi kubadili njia yao ya kufikiri na matendo yao. Lakini je, kuna uthibitisho kwamba kuna umoja ulimwenguni pote kati ya wale ambao kwa kweli wanafuata mafundisho ya Biblia?
Undugu Unaochochewa na Upendo
Hafeni alipoanza kuhudhuria mikutano ya Mashahidi wa Yehova, alichochewa sana kuona jinsi watu wa jamii tofauti-tofauti walivyoshirikiana kwa upatano. “Ilisisimua sana kuketi kando ya wazungu,” anasema. “Sikuwahi kufikiri kwamba katika maisha yangu ningewahi kumwita mzungu ndugu yangu. Hilo lilinisadikisha kabisa kwamba lazima Mashahidi wawe ndio wenye dini ya kweli, kwa kuwa walikuwa na umoja kati yao ambao nilitamani na walikuwa na upendo kati yao licha ya tofauti za kijamii.”
Yesu alisema kwamba wafuasi wake wa kweli wangetambuliwa kwa sababu wana ‘upendo kati yao wenyewe.’ (Yohana 13:34, 35) Pia alikataa kujihusisha katika mizozo ya kisiasa na akawaambia wanafunzi wake hivi: “Ninyi si sehemu ya ulimwengu.” (Yohana 6:15; 15:19; Mathayo 22:15-22) Wakati huo Wakristo wa kweli walitambuliwa kwa upendo na msimamo wao wa kutounga mkono upande wowote katika mambo ya kisiasa, kama tu ilivyo leo.
Kufuata Mafundisho ya Yesu
Lakini ni kwa njia gani upendo unaweza kuwavutia watu kukiwa na mambo mengi yanayochochea ugaidi ulimwenguni? Masuala ya kisiasa yanapotokeza chuki, mara nyingi uaminifu kwa jamii, taifa, au kabila hutokeza mzozo kati ya watu wawili au kati ya mataifa.
Kwa mfano, kule nyuma katika mwaka wa 1914, utukuzo wa kikabila ulimfanya Gavrilo Princip amwue Dyuki Mkuu Francis Ferdinand, aliyepaswa kurithi kiti cha ufalme cha Austria-Hungaria. Princip alikuwa mshiriki wa kikundi kilichojiita Mkono Mweusi, ambacho kulingana na katiba yake, kilipendelea kujihusisha katika “mapambano ya kuleta mapinduzi badala ya . . . utendaji wa kitamaduni” ili kufikia malengo yake. Mauaji hayo yalianzisha vita kati ya mataifa yanayodai kuwa ya Kikristo, na hilo likaanzisha Vita vya Kwanza vya Ulimwengu vilivyosababisha vifo vya mamilioni ya watu waliodai kuwa wafuasi wa Yesu, yule “Mkuu wa Amani.”—Isaya 9:6.
Baada ya vita hivyo kwisha, kasisi fulani mashuhuri, Harry Emerson Fosdick, aliwakashifu viongozi wanaodai kuwa wa Kikristo kwa kutowafundisha washiriki wa makanisa yao kuiga mfano wa Yesu. “Tumewazoeza watu kwa ajili ya vita,” akaandika. “Tumewafanya askari kuwa mashujaa wetu na hata ndani ya makanisa yetu tumeziweka bendera za vita.” Fosdick alimalizia kwa kusema: “Kwa pembe moja ya mdomo wetu tumemsifu Mkuu wa Amani na kwa pembe ile nyingine tukatukuza vita.”
Tofauti na hilo, uchunguzi mmoja kuhusu mambo ya kijamii uliochapishwa mnamo 1975 ulisema hivi: “Mashahidi wa Yehova wamedumisha daima msimamo wao usio na jeuri wa ‘kutokuwamo kwa Kikristo’ wakati wa vile vita viwili vikubwa vya ulimwengu na mizozo ya kijeshi iliyofuata wakati wa kile kipindi cha ‘Vita Baridi.’” Ingawa Mashahidi walitendewa vibaya na kufungwa, “hawakuwahi kulipiza kisasi.” Uchunguzi huo ulifikia mkataa huu: “Mafundisho ya Mashahidi wa Yehova yanatokana na usadikisho wao kwamba Biblia ni neno la Mungu lililoongozwa kwa roho.”
Faida za Kufuata Mafundisho ya Biblia
Aliyekuwa waziri mkuu wa Ubelgiji alipopewa na jirani yake kitabu chenye kichwa Yule Mtu Mkuu Zaidi Aliyepata Kuishi kinachozungumza kuhusu maisha ya Yesu, alipendezwa sana na mambo aliyosoma. Alimwandikia jirani huyo hivi, “Ni wazi kwamba ikiwa watu wangependezwa zaidi na ujumbe wa Injili na wafuate kanuni za Yesu Kristo, ulimwengu leo ungekuwa tofauti kabisa.”
Aliongezea hivi, “Hatungehitaji Baraza la Usalama, wala hakungekuwa na mashambulizi ya kigaidi, [na] jeuri ingepigwa marufuku.” Lakini alifikia mkataa huu: “Yote hayo ni ndoto tu.” Lakini, je, hilo ni kweli? Hata sasa, katika ulimwengu huu uliojaa jeuri, Biblia imewasaidia watu wengi kutoka katika tamaduni zote wakatae jeuri na washinde chuki kali inayotokea wakati watu wanapoishi kwa makumi ya miaka katika maeneo yaliyojaa umwagaji wa damu.
Kama ilivyotajwa katika habari ya kwanza, karibu Andre afe katika bomu lililowaua baadhi ya rafiki zake. Lilikuwa limetegwa hapo na kikundi fulani cha wanamgambo. Baada ya hapo alijifunza na kufuata mashauri ya Biblia kwamba mtu anapaswa ‘kusamehe kwa hiari.’ (Wakolosai 3:13) Baadaye, Hafeni, ambaye baada ya miaka mingi alikuja kuwa mshiriki wa kikundi hichohicho, alijifunza kufuata kanuni za Biblia na akaacha matendo ya jeuri. (Zaburi 11:5) Sasa, wote wawili ni Mashahidi wa Yehova na wanafanya kazi pamoja katika ofisi ya tafsiri ya Mashahidi katika nchi moja ya Afrika.
Kutakuwa na Wakati Ujao Wenye Usalama
Mamilioni ya watu ulimwenguni pote wanaona kwamba kujifunza Biblia kunawapa uhakika kwamba kutakuwa na wakati ujao wenye usalama. Kwa mfano, siku moja Andre alikuwa akimwonyesha jirani yake ahadi ya Biblia ya ulimwengu mpya wenye uadilifu utakaokuja. (Isaya 2:4; 11:6-9; 65:17, 21-25; 2 Petro 3:13) Ghafula, askari-jeshi walizingira nyumba hiyo wakiwa na bunduki na kumwamuru Andre atoke akahojiwe. Baada ya kugundua kwamba Andre alikuwa mwalimu wa Biblia ambaye jirani yake alimthamini sana, askari hao waliondoka.
Andre alikuwa tu ameeleza kwamba Mungu ataingilia mambo ya wanadamu, kama alivyokuwa amefanya katika siku za Noa wakati ambapo ‘dunia ilikuwa imejaa jeuri.’ (Mwanzo 6:11) Mungu aliharibu ulimwengu wa wakati huo kupitia gharika ya ulimwenguni pote na akawahifadhi hai Noa pamoja na familia yake kwa sababu walikuwa wapenda-amani. “Kama vile siku za Noa zilivyokuwa,” Yesu alisema, “ndivyo kuwapo kwa Mwana wa binadamu kutakavyokuwa.”—Mathayo 24:37-39.
Yesu, yule “Mwana wa binadamu,” ndiye Mtawala aliyechaguliwa na Mungu wa serikali ya kimbingu inayoitwa Ufalme wa Mungu, naye atayaongoza majeshi ya kimbingu ya Mungu hivi karibuni yaondoe jeuri kutoka duniani. (Luka 4:43) Akiwa Mfalme wa kimbingu, Yesu ‘atamtendea kila mtu kwa haki, na kutakuwa na amani.’ Atawalinda raia zake “kutokana na vifo vya ukatili na jeuri.”—Zaburi 72:7, 14, Contemporary English Version.
Baadaye, wale wote wanaopenda mema na wanaokuwa raia wa Mfalme huyo wa kimbingu wataona dunia ikigeuzwa kuwa paradiso yenye amani. (Luka 23:42, 43) Biblia inaahidi hivi: “Milima itawazalia watu amani, na vilima . . . haki.”—Zaburi 72:1-3, Union Version.
Je, hungependa kuishi katika ulimwengu unaotawaliwa na mfalme kama huyo? Bila shaka, ulimwengu huo hautakuwa na ugaidi.
[Blabu katika ukurasa wa 7]
Hafeni na Joseba walijionea kwamba mafundisho ya Biblia yanaweza kubadili maisha ya mtu
[Blabu katika ukurasa wa 9]
‘Ikiwa watu wangefuata kanuni za Yesu Kristo, ulimwengu leo ungekuwa tofauti kabisa. Hatungehitaji Baraza la Usalama, wala hakungekuwa na mashambulizi ya kigaidi, na jeuri ingepigwa marufuku.’—Aliyekuwa waziri mkuu wa Ubelgiji
[Picha katika ukurasa wa 8]
Kufuata kanuni za Biblia kuliwasaidia Hafeni na Andre kupendana kikweli
-