Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Kupambana Sana kwa Ajili ya Habari Njema Huko Thesalonike
    Mnara wa Mlinzi—2012 | Juni 1
    • KARIBU mwaka wa 50 W.K., Paulo na mwandamani wake Sila walifika Thesalonike. Walikuwa katika safari ya pili ya Paulo ya umishonari. Hiyo iliwapa fursa ya kupeleka habari njema kumhusu Kristo katika eneo ambalo leo ni bara Ulaya.

      Bila shaka, walipofika Thesalonike, bado walikuwa wakikumbuka jinsi walivyopigwa na kufungwa huko Filipi, jiji kuu la Makedonia. Hata baadaye Paulo aliwaambia Wathesalonike kwamba alipowatembelea alikuwa akiwahubiria “habari njema ya Mungu kwa kupambana sana.” (1 Wathesalonike 2:1, 2) Je, hali katika jiji la Thesalonike ingekuwa nzuri kwao? Huduma yao ingekuwaje katika jiji hilo? Je, ingekuwa na matokeo mazuri?

  • Kupambana Sana kwa Ajili ya Habari Njema Huko Thesalonike
    Mnara wa Mlinzi—2012 | Juni 1
    • Paulo Awasili Thesalonike

      Kwa kawaida Paulo alipofika katika jiji, alikuwa akianza kuzungumza na Wayahudi kwa sababu walifahamu Maandiko na hivyo angeweza kuyatumia katika mazungumzo yake na kuwasaidia kuelewa habari njema. Msomi fulani anadokeza kwamba huenda Paulo alifanya hivyo kwa kuwa aliwajali sana watu wa nchi yake au alitaka kuwatumia Wayahudi na watu waliomwogopa Mungu ili kuanza kazi yake ya kuwafikia Watu wa Mataifa.​—Matendo 17:2-4.

      Hivyo alipofika Thesalonike, Paulo aliingia katika sinagogi, na “akajadiliana nao [Wayahudi] kwa kutumia Maandiko, akieleza na kuthibitisha kwa marejeo kwamba ilikuwa lazima Kristo ateseke na kufufuliwa kutoka kwa wafu, akisema: ‘Huyu ndiye Kristo, Yesu huyu ninayewatangazia ninyi.’”​—Matendo 17:2, 3, 10.

      Jambo ambalo Paulo alizungumzia, yaani, daraka la Masihi na utambulisho wake, lilikuwa jambo lililokuwa likibishaniwa. Wayahudi walitazamia Masihi ambaye angewakomboa kutoka kwa utawala wa Waroma, hivyo kuteseka kwa Masihi kulikuwa kinyume cha matarajio yao. Ili afaulu kuwashawishi Wayahudi, Paulo ‘alijadiliana,’ ‘akaeleza,’ na ‘kuthibitisha kwa kurejelea’ Maandiko—mbinu inayotumiwa na mwalimu mwenye ustadi.a Lakini wasikilizaji wa Paulo waliitikiaje alipokuwa akiwafundisha mambo hayo mazuri?

      Walipitia Hali Ngumu Lakini Wakapata Matokeo Mazuri

      Wayahudi fulani na wageuzwa-imani wengi Wagiriki na pia “si wachache kati ya wanawake wenye vyeo,” walikubali ujumbe wa Paulo. Usemi “wanawake wenye vyeo” ulifaa sana, kwa sababu wanawake huko Makedonia walikuwa na vyeo katika jamii. Walikuwa na vyeo katika ofisi za serikali, walimiliki mali, na kufurahia haki fulani za kijamii, na wakajihusisha na biashara. Hata walijengewa minara ya ukumbusho ili kuwaonyesha heshima. Kama vile tu mwanamke aliyeitwa Lidia, mfanyabiashara Mfilipi alivyokubali habari njema, pia kulikuwa na itikio zuri kutoka kwa wanawake Wathesalonike wenye vyeo vya juu, huenda walikuwa wanawake kutoka kwa familia za kitajiri au wake wa watu waliokuwa maarufu.​—Matendo 16:14, 15; 17:4.

      Hata hivyo, Wayahudi walijawa na wivu. Wakawakusanya “wanaume fulani waovu kati ya wazururaji wa sokoni na kufanyiza kikundi chenye ghasia ili kuzusha fujo jijini.” (Matendo 17:5) Hao walikuwa watu wa aina gani? Msomi mmoja wa Biblia anaeleza kwamba “walikuwa watu waovu na wasiofaa kitu.” Anaongeza hivi: “Inaonekana kwamba hawakupendezwa kwa njia yoyote ile na ujumbe wa Paulo; lakini kama vile tu kikundi chenye ghasia, watu hao walisisimuka haraka, na kuchochewa kujihusisha na matendo ya fujo.”

      Kikundi hicho chenye fujo ‘kikaishambulia nyumba ya Yasoni [aliyekuwa amemkaribisha Paulo] na kuanza kujaribu kuwaleta mbele ya watu wenye kufanya ghasia.’ Kwa sababu hawakumpata Paulo, walianza kutafuta usaidizi kutoka kwa watawala wa kuu zaidi wa jiji. Hivyo “wakamkokota Yasoni na akina ndugu fulani na kuwapeleka kwa watawala wa jiji, wakipaaza sauti hivi: ‘Watu hawa ambao wameipindua dunia inayokaliwa wapo hapa pia.’”​—Matendo 17:5, 6.

      Kwa sababu lilikuwa ndilo jiji kuu la Makedonia, jiji la Thesalonike lilikuwa likijitawala kwa kadiri fulani. Sehemu ya mamlaka yake ilikuwa ni baraza la watu au baraza la wananchi ambalo lilishughulikia matatizo ya watu. “Watawala wa jiji,” au mapolitaki,b walikuwa maofisa wakuu walio na jukumu la kudumisha utaratibu na kutatua hali ambazo zingefanya Waroma waingilie kati na hivyo kufanya jiji lipoteze mapendeleo yake. Hivyo basi, watawala hao wa jiji wangekuwa na wasiwasi kusikia kwamba amani ya watu imeharibiwa na “watu hao waliosababisha fujo.”

      Kisha wakatoa shtaka zito sana wakisema: ‘Watu hawa wanapingana na maagizo ya Kaisari, wakisema kuna mfalme mwingine, Yesu.’ (Matendo 17:7) Mchambuzi mmoja anasema kwamba shtaka hilo lilikuwa “uchochezi na uasi” dhidi ya wakuu ambao “hawangeruhusu jina la mfalme [mwingine] litajwe katika mikoa waliyoteka isipokuwa wawe wamewaruhusu.” Vilevile, kwa kuwa Yesu, ambaye Paulo alikuwa akimtaja kuwa Mfalme, alikuwa ameuawa na mamlaka ya Waroma kwa shtaka hilohilo la uchochezi jambo hilo lingefanya watawala hao waamini kuwa ni kweli.​—Luka 23:2.

      Watawala hao wa jiji walichukizwa na jambo hilo. Lakini kwa sababu hakukuwa na ushahidi wa kutosha na washtakiwa hawakupatikana, basi “baada ya kuchukua dhamana ya kutosha kutoka kwa Yasoni na wale wengine wakawaacha waende zao.” (Matendo 17:8, 9) Huenda utaratibu huo ulirejelea aina fulani ya malipo ambayo yalimaanisha kwamba Yasoni na Wakristo wengine walipaswa kuhakikisha kuwa Paulo angeondoka jijini na hangerudi na kusababisha fujo tena. Yaelekea Paulo alirejelea kisa hicho aliposema “Shetani aliizuia njia [yake]” na kumfanya asirudi katika jiji hilo.​—1 Wathesalonike 2:18.

      Kwa sababu ya hali hiyo, Paulo na Sila walisaidiwa kuondoka usiku-usiku kuelekea Beroya. Utumishi wa Paulo ulikuwa na matokeo mazuri huko pia, lakini matokeo hayo yaliwafanya wapinzani wake Wayahudi walio Thesalonike wakasirike na kufunga safari ya kilomita 80 hadi Beroya ili kuuchochea umati na kuufanya umpinge Paulo na Sila.

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki