-
Kuzimu na JehanamuKutoa Sababu kwa Kutumia Maandiko
-
-
‘Kuteswa milele’ kunakotajwa katika Ufunuo kunamaanisha nini?
Ufu. 14:9-11; 20:10, UV: “Mtu awaye yote akimsujudu huyo mnyama na sanamu yake, na kuipokea chapa katika kipaji cha uso wake, au katika mkono wake, yeye naye atakunywa katika mvinyo ya ghadhabu ya Mungu iliyotengenezwa, pasipo kuchanganywa na maji, katika kikombe cha hasira yake; naye atateswa kwa moto na kiberiti mbele ya malaika watakatifu, na mbele za Mwana-Kondoo. Na moshi wa maumivu [Kigiriki, basa·ni·smouʹ] yao hupanda juu hata milele, wala hawana raha mchana wala usiku, hao wamsujuduo huyo mnyama na sanamu yake, na kila aipokeaye chapa ya jina lake.” “Na yule Ibilisi, mwenye kuwadanganya, akatupwa katika ziwa la moto na kiberiti, alimo yule mnyama na yule nabii wa uwongo. Nao watateswa mchana na usiku hata milele na milele.”
Maandiko hayo yanazungumzia ‘kuteswa’ gani? Inafaa kutambua kwamba andiko la Ufunuo 11:10 (UV) linataja ‘manabii wanaotesa wao wakaao juu ya nchi.’ Mateso hayo yanatokana na ujumbe ambao manabii hao wanatangaza, unaofichua mambo kwa njia yenye kuaibisha. Andiko la Ufunuo 14:9-11 (UV) linasema kwamba wamsujudiao ‘mnyama huyo wa mfano na sanamu yake, wanateswa kwa moto na kiberiti.’ Hilo haliwezi kurejelea kuteswa kwa watu wenye fahamu baada ya kifo kwa sababu “wafu hawajui neno lo lote.” (Mhu. 9:5, UV) Basi, ni nini kinachowatesa wakiwa wangali hai? Ni lile tangazo linalotolewa na watumishi wa Mungu la kwamba wamsujudiao “mnyama na sanamu yake” watapatwa na kifo cha pili, kinachofananishwa na “ziwa la moto na kiberiti.” Moshi, unaohusianishwa na uharibifu wao unaofananishwa na moto, unaendelea kupanda milele kwa sababu uharibifu huo utakuwa wa milele na hautasahauliwa kamwe. Andiko la Ufunuo 20:10 humaanisha nini linaposema kwamba Ibilisi ‘atateswa milele na milele’ katika “ziwa la moto na kiberiti”? Andiko la Ufunuo 21:8 (UV) husema waziwazi kwamba “lile ziwa la moto na kiberiti” humaanisha “kifo cha pili.” Kwa hiyo, ‘kuteswa’ kwa Ibilisi humo milele na milele kunamaanisha kwamba hatapata kitulizo kamwe; atazuiwa milele, katika kifo cha milele. Matumizi ya neno hilo ‘kuteswa’ (kutokana na neno la Kigiriki baʹsa·nos) humkumbusha mtu matumizi yake katika Mathayo 18:34, ambamo neno hilohilo la msingi la Kigiriki linatafsiriwa “watesaji” (UV, ZSB, VB), “walinzi wa jela” (NW), na “askari wa gereza” (NAJ).
-
-
Kuzimu na JehanamuKutoa Sababu kwa Kutumia Maandiko
-
-
Yesu aliposimulia kuhusu tajiri na Lazaro, je, alikuwa akifundisha juu ya kuteswa kwa waovu baada ya kifo?
Je, masimulizi ya Luka 16:19-31, ni matukio halisi au ni mfano tu wa jambo jingine? Katika kichwa kidogo, Verbum Bible inayaita masimulizi hayo “mfano wa mtu tajiri na Lazaro maskini.” Ikiwa hayo ni masimulizi kuhusu tukio halisi, ingemaanisha kwamba watu wote wenye kibali cha Mungu wangeweza kutoshea katika kifua cha mtu mmoja, Abrahamu; kwamba maji kwenye ncha ya kidole kimoja cha mtu hayangeweza kukaushwa na moto wa Hadesi; kwamba tone moja tu la maji lingeweza kumtuliza mtu anayeteswa. Je, unafikiri kwamba jambo hilo linapatana na akili? Ikiwa ni tukio halisi, lingepingana na sehemu nyingine za Biblia. Ikiwa Biblia ingekuwa yenye kujipinga hivyo, je, mtu anayependa ukweli angeitumia kuwa msingi wa imani yake? Lakini Biblia haijipingi yenyewe.
Mfano huo unamaanisha nini? “Tajiri” aliwakilisha Mafarisayo. (Ona mstari 14.) Yule mwombaji Lazaro aliwakilisha Wayahudi wa kawaida waliodharauliwa na Mafarisayo lakini ambao walitubu na kuwa wafuasi wa Yesu. (Ona Luka 18:11; Yohana 7:49; Mathayo 21:31, 32.) Vifo vyao pia vilikuwa vya mfano, vikiwakilisha badiliko la hali. Kwa hiyo, wale ambao zamani walikuwa wakidharauliwa walikuja kupata kibali cha Mungu, nao wale ambao zamani walikuwa wakionekana kuwa wana kibali cha Mungu, walikataliwa, huku wakiteswa na ujumbe wa hukumu uliotolewa na wale ambao walikuwa wamewadharau.—Mdo. 5:33; 7:54.
-