-
Waangalizi Wasafirio—Zawadi Zikiwa WanadamuMnara wa Mlinzi—1996 | Novemba 15
-
-
Waangalizi Wasafirio—Zawadi Zikiwa Wanadamu
“Alipopaa juu alichukua mateka; alitoa zawadi [zikiwa] wanadamu.”—WAEFESO 4:8, NW.
1. Ni kazi gani mpya iliyotangazwa katika jarida hili mwaka wa 1894?
ZAIDI ya karne moja iliyopita, gazeti Watch Tower lilitangaza jambo jipya. Hilo lilifafanuliwa kuwa “Sehemu Nyingine ya Kazi ya Kuhubiri.” Utendaji huo mpya ulitia ndani nini? Huo ulikuwa mwanzo wa kisasa wa kazi ya waangalizi wasafirio. Toleo la Septemba 1, 1894, la jarida hili lilieleza kwamba kuanzia wakati huo na kuendelea ndugu wanaostahili wangekuwa wakizuru vikundi vya Wanafunzi wa Biblia ‘kwa kusudi la kuvijenga katika kweli.’
2. Waangalizi wa mzunguko na wa wilaya wana wajibu gani mbalimbali?
2 Katika karne ya kwanza W.K., makutaniko ya Kikristo yalitembelewa na waangalizi hao kama Paulo na Barnaba. Wanaume hao waaminifu walikuwa na lengo la ‘kuyajenga’ makutaniko. (2 Wakorintho 10:8) Leo, tumebarikiwa kuwa na maelfu ya wanaume wanaofanya hivyo kwa njia yenye utaratibu. Baraza Linaloongoza la Mashahidi wa Yehova limewaweka rasmi kuwa waangalizi wa mzunguko na wa wilaya. Mwangalizi wa mzunguko hutumikia makutaniko yapatayo 20, kila moja yayo kwa juma moja karibu mara mbili kwa mwaka, akichunguza rekodi za kutaniko, akitoa hotuba, na kushiriki katika huduma ya shambani pamoja na watangazaji wa Ufalme wa mahali hapo. Mwangalizi wa wilaya ni mwenyekiti wa kila moja ya makusanyiko ya mzunguko ya kila mwaka kwa mizunguko kadhaa, yeye hushiriki katika huduma ya shambani pamoja na makutaniko yaliyo wakaribishaji kwenye kusanyiko, na hutoa kitia-moyo katika hotuba zinazotegemea Biblia.
Roho Yao ya Kujidhabihu
3. Kwa nini waangalizi wasafirio huhitaji kuwa na roho ya kujidhabihu?
3 Waangalizi wasafirio husafiri sikuzote. Hilo lenyewe hutaka roho ya kujidhabihu. Mara nyingi kusafiri kutoka kutaniko moja hadi jingine kwaweza kuwa jambo gumu, lakini wanaume hao pamoja na wake zao hufanya hivyo wakiwa na mtazamo wenye shangwe. Mwangalizi wa mzunguko mmoja alisema hivi: “Mke wangu ni mwenye kuunga mkono kabisa na halalamiki . . . Anastahili kusifiwa sana kwa sababu ya roho yake ya kujidhabihu.” Waangalizi fulani wa mzunguko husafiri kilometa zaidi ya 1,000 kati ya makutaniko. Wengi huendesha magari, lakini wengine husafiri mahali-mahali kwa kutumia usafiri wa umma, baiskeli, farasi, au miguu. Mwangalizi wa mzunguko mmoja wa Afrika huhitaji hata kupitia mtoni akiwa amembeba mkewe mabegani pake ili kufikia kutaniko moja. Katika safari zake za umishonari, mtume Paulo alilazimika kukabiliana na joto na baridi, njaa na kiu, usiku kadhaa bila usingizi, hatari mbalimbali, na mnyanyaso wenye jeuri. Alikuwa pia na hali ya “kuhangaikia makutaniko yote”—jambo lililo la kawaida kwa waangalizi wasafirio leo.—2 Wakorintho 11:23-29.
4. Matatizo ya afya yaweza kuwa na matokeo gani katika maisha za waangalizi wasafirio na wake zao?
4 Sawa na Timotheo, mwandamani wa Paulo, nyakati nyingine waangalizi wasafirio na wake zao huwa na matatizo ya kiafya. (1 Timotheo 5:23) Hayo huwawekea mkazo wa ziada. Mke wa mwangalizi wa mzunguko mmoja aeleza hivi: “Kuwa pamoja na akina ndugu sikuzote ni mkazo ninapokuwa mgonjwa. Nikiwa nimefikia mwanzo wa komahedhi, nimeona hilo kuwa jambo gumu hasa. Kuhitaji kufunga tu vitu vyetu vyote kila juma na kuhamia kwingineko ni jambo gumu kwelikweli. Mara nyingi, inanibidi nitue na kusali kwa Yehova anipe nguvu za kuendelea.”
5. Yajapokuwa majaribu mbalimbali, ni roho gani ambayo imeonyeshwa na waangalizi wasafirio na wake zao?
5 Yajapokuwa matatizo ya afya na majaribu mengine, waangalizi wasafirio pamoja na wake zao hupata shangwe katika utumishi wao nao huonyesha upendo wenye kujidhabihu. Waangalizi fulani wamehatarisha uhai wao ili kutoa msaada wa kiroho katika nyakati za mnyanyaso au vita. Wazurupo makutaniko, wamedhihirisha roho inayofanana na ile ya Paulo, aliyewaambia Wakristo Wathesalonike hivi: “Tulikuwa wapole katikati yenu, kama vile mlezi awatunzavyo watoto wake mwenyewe. Vivyo hivyo nasi tukiwatumaini kwa upendo mwingi, tuliona furaha kuwapa, si Injili ya Mungu tu, bali na roho zetu pia, kwa sababu mmekuwa wapendwa wetu.”—1 Wathesalonike 2:7, 8.
6, 7. Waangalizi wasafirio wenye bidii waweza kuwa na uvutano gani mzuri?
6 Sawa na wazee wengine katika kutaniko la Kikristo, waangalizi wasafirio ‘hujitaabisha kwa kuhutubu na kufundisha.’ Wazee wote hao wapasa “wahesabiwe kustahili heshima maradufu.” (1 Timotheo 5:17) Kielelezo chao chaweza kuthibitika kuwa chenye kunufaisha ikiwa, baada ya ‘kuuchunguza sana mwisho wa mwenendo wao, twaiga imani yao.’—Waebrania 13:7.
7 Wazee fulani wasafirio wamekuwa na uvutano gani juu ya wengine? “Ndugu P—— alikuwa na uvutano wa ajabu kama nini maishani mwangu!” akaandika Shahidi mmoja wa Yehova. “Alikuwa mwangalizi asafiriye katika Mexico tangu mwaka wa 1960 na kuendelea. Nikiwa mtoto, nilingoja ziara zake nikiwa na hamu na shangwe. Nilipokuwa na umri wa miaka kumi, aliniambia, ‘Wewe pia utakuwa mwangalizi wa mzunguko.’ Katika ile miaka migumu ya utineja, mara nyingi nilimtafuta kwa sababu sikuzote alikuwa na maneno yenye hekima ya kutoa. Hangaiko lake kuu maishani lilikuwa kulichunga kundi! Sasa kwa sababu mimi ni mwangalizi wa mzunguko, sikuzote mimi hujaribu kutumia wakati pamoja na vijana na kuwatia moyo wafuatie miradi ya kitheokrasi sawa na vile alivyonifanyia. Hata katika miaka ya mwisho-mwisho ya maisha yake, ajapokuwa na matatizo ya moyo, sikuzote Ndugu P—— alijaribu kutoa kitia-moyo. Siku moja tu kabla ya kifo chake katika Februari 1995, aliandamana nami kwenye siku ya kusanyiko la pekee akamtia moyo ndugu fulani ambaye ni msanifuujenzi afuatie miradi ifaayo. Papo hapo ndugu huyo akatoa ombi la kutumikia Betheli.”
Wanathaminiwa
8. Ni nani walio “zawadi zikiwa wanadamu” wafafanuliwao katika Waefeso sura ya 4, nao hunufaishaje kutaniko?
8 Waangalizi wasafirio na wazee wengine ambao wamependelewa kwa kupewa migawo ya utumishi kwa fadhili isiyostahiliwa ya Mungu wanaitwa “zawadi zikiwa wanadamu.” Akiwa mwakilishi wa Yehova na Kichwa cha kutaniko, Yesu ameandaa wanaume hao wa kiroho ili kila mmoja wetu aweze kujengwa na kufikia ukomavu. (Waefeso 4:8-15) Zawadi yoyote ile hustahili kuonyeshwa uthamini. Ndivyo ilivyo hasa kwa habari ya zawadi inayotutia nguvu tuendelee kumtumikia Yehova. Kwa hiyo basi, twaweza kuonyeshaje kuthamini kwetu kazi ya waangalizi wasafirio? Twaweza kuonyesha katika njia zipi kwamba ‘twahesabu watu kama hao kuwa watu wa kuheshimiwa’?—Wafilipi 2:29.
9. Twaweza kuonyesha katika njia zipi kuthamini kwetu waangalizi wasafirio?
9 Ziara ya mwangalizi wa mzunguko inapotangazwa, twaweza kuanza kufanya mipango ya kushiriki kikamili katika utendaji wa kutaniko kwa juma hilo. Labda twaweza kuweka kando wakati wa ziada ili kuunga mkono mipango ya utumishi wa shambani wakati wa hiyo ziara. Huenda tukaweza kutumikia tukiwa mapainia-wasaidizi mwezi huo. Kwa hakika tutataka kutumia madokezo ya mwangalizi wa mzunguko ili kuboresha huduma yetu. Roho hiyo ya kuitikia upesi itatunufaisha na itamhakikishia kwamba ziara yake ni yenye mafaa. Ndiyo, waangalizi wasafirio huzuru kutaniko ili kutujenga, lakini wao pia huhitaji kujengwa kiroho. Kulikuwa na nyakati ambazo Paulo alihitaji kitia-moyo, na mara nyingi aliwaomba Wakristo wenzake wasali kwa ajili yake. (Matendo 28:15; Warumi 15:30-32; 2 Wakorintho 1:11; Wakolosai 4:2, 3; 1 Wathesalonike 5:25) Waangalizi wasafirio wa sasa vilevile huhitaji sala zetu na kitia-moyo chetu.
10. Twaweza kusaidiaje kufanya kazi ya mwangalizi asafiriye iwe yenye shangwe?
10 Je, tumepata kumwambia mwangalizi wa mzunguko na mkewe jinsi tuthaminivyo ziara zao? Je, sisi humshukuru kwa sababu ya shauri lenye msaada analotutolea? Je, sisi humjulisha wakati madokezo yake ya utumishi wa shambani yaongezapo shangwe yetu katika huduma? Ikiwa sisi hufanya hivyo, hilo litasaidia kufanya kazi yake iwe yenye shangwe. (Waebrania 13:17) Mwangalizi wa mzunguko mmoja katika Hispania alieleza hasa kadiri yeye na mkewe wathaminivyo barua za shukrani ambazo wamepokea baada ya kuyazuru makutaniko. “Sisi huweka kadi hizo na kuzisoma tuhisipo tumevunjika moyo,” yeye asema. “Hizo ni chanzo cha kitia-moyo halisi.”
11. Kwa nini tuwajulishe wake wa waangalizi wa mzunguko na wa wilaya kwamba wanapendwa na kuthaminiwa?
11 Mke wa mwangalizi asafiriye kwa hakika hunufaika kutokana na maneno ya pongezi. Yeye ametoa dhabihu kubwa ili kumsaidia mumewe katika sehemu hii ya utumishi. Dada hawa waaminifu hujinyima tamaa ya asili ya kuwa na nyumba yao wenyewe, na pia katika visa vingi, ya kuwa na watoto. Binti Yeftha alikuwa mmoja wa watumishi wa Yehova aliyeacha kwa utayari fursa yake ya kuwa na mume na familia kwa sababu ya nadhiri aliyoweka babaye. (Waamuzi 11:30-39) Dhabihu yake ilionwaje? Waamuzi 11:40 lataarifu hivi: ‘Binti za Israeli walienda mwaka baada ya mwaka ili kumkumbuka huyo mwana wa Yeftha, Mgileadi, siku nne katika mwaka.’ Ni jambo zuri kama nini tujitahidipo kuwaambia wake wa waangalizi wa mzunguko na wa wilaya kwamba wanapendwa na kuthaminiwa!
“Msisahau Ukaribishaji-Wageni”
12, 13. (a) Kuna msingi gani wa Kimaandiko wa kuwa wenye ukaribishaji-wageni kwa waangalizi wasafirio na wake zao? (b) Toa kielezi cha jinsi ukaribishaji-wageni huo uwezavyo kuwa wenye kunufaisha kwa wote.
12 Kuonyesha ukaribishaji-wageni ni njia nyingine ya kudhihirisha upendo na uthamini kwa wale walio katika kazi ya kusafiri ya Kikristo. (Waebrania 13:2) Mtume Yohana alimpongeza Gayo kwa sababu ya kuonyesha ukaribishaji-wageni kwa wale waliozuru kutaniko wakiwa wamishonari wasafirio. Yohana aliandika hivi: “Mpenzi, kazi ile ni ya uaminifu uwatendeayo hao ndugu na hao wageni nao, waliokushuhudia upendo wako mbele ya kanisa; utafanya vizuri ukiwasafirisha kama ipasavyo kwa Mungu. Kwa maana, kwa ajili ya Jina hilo, walitoka, wasipokee kitu kwa Mataifa. Basi imetupasa sisi kuwakaribisha watu kama hao [“kuwapokea watu wa namna hiyo kwa ukaribishaji-wageni,” NW], ili tuwe watenda kazi pamoja na kweli.” (3 Yohana 5-8) Leo, twaweza kuendeleza utendaji wa kuhubiri Ufalme kwa kuwaonyesha waangalizi wasafirio na wake zao ukaribishaji-wageni uo huo. Bila shaka, wazee wa mahali fulani wapaswa kuhakikisha kwamba makao ni yenye kufaa, lakini mwangalizi wa wilaya mmoja alisema hivi: “Kushirikiana kwetu na ndugu hakuwezi kutegemea ni nani awezaye kutufanyia jambo fulani. Hata tusingetaka kudokeza hivyo. Ni lazima tuwe tayari kukubali ukaribishaji-wageni wa yeyote kati ya ndugu zetu, awe ni tajiri au maskini.”
13 Ukaribishaji-wageni waweza kuwa wenye kunufaisha kwa wote. “Katika familia yetu, tulikuwa na desturi ya kualika waangalizi wasafirio kukaa nasi,” akumbuka Jorge, aliyekuwa mwangalizi wa mzunguko hapo awali anayetumikia Betheli sasa. “Nahisi kwamba ziara hizo zilinisaidia zaidi ya vile nilivyong’amua wakati huo. Wakati wa ubalehe wangu, nilikuwa na matatizo ya kiroho. Mamangu alihangaikia jambo hilo lakini hakujua njia barabara ya kusaidia na basi akamwomba mwangalizi wa mzunguko azungumze nami. Mwanzoni nilimwepa, kwa kuwa niliogopa kuchambuliwa. Lakini njia yake yenye urafiki ilinishawishi nimfunulie yote. Alinialika kula mlo pamoja naye Jumatatu moja, nami nikamwambia yote yaliyokuwa moyoni mwangu kwa sababu nilihisi uhakika kwamba alikuwa akinielewa. Yeye alisikiliza kwa uangalifu. Madokezo yake yenye kutumika yalifanya kazi kwelikweli, nami nikaanza kufanya maendeleo kiroho.”
14. Kwa nini tuwe wenye uthamini badala ya kuwachambua wazee wasafirio?
14 Mwangalizi asafiriye hujaribu kusaidia kiroho vijana na wazee vilevile. Basi, kwa hakika twapaswa kuonyesha uthamini wetu kwa jitihada zake. Hata hivyo, namna gani ikiwa tungemchambua kwa sababu ya udhaifu wake mbalimbali au kumlinganisha isivyofaa na wengine ambao wamelizuru kutaniko? Yamkini, hilo lingevunja moyo sana. Halikuwa jambo la kumtia moyo Paulo kusikia kazi yake ikichambuliwa. Yaonekana, baadhi ya Wakristo Wakorintho walikuwa wakichambua sura yake na uwezo wake wa kusema. Yeye mwenyewe aliwanukuu wachambuzi hao kuwa wakisema: “Nyaraka zake ni nzito, hodari; bali akiwapo mwenyewe mwilini ni dhaifu, na maneno yake si kitu.” (2 Wakorintho 10:10) Lakini kwa furaha, waangalizi wasafirio kwa kawaida husikia maneno ya uthamini wenye upendo.
15, 16. Waangalizi wasafirio na wake zao huathiriwaje na upendo na bidii zionyeshwazo na waamini wenzao?
15 Mwangalizi wa mzunguko mmoja katika Amerika ya Latini hutembea kwa taabu katika vijia vyenye matope ili kuzuru ndugu na dada zake wa kiroho wanaoishi katika kanda inayodhibitiwa na wapiganaji wa kuvizia. “Inagusa moyo kuona jinsi ambavyo akina ndugu huonyesha uthamini wao kwa ziara,” yeye aandika. “Hata ingawa ni lazima nijitahidi sana kufika huko, nikikabili hatari na magumu mengi, yote hayo yanathawabishwa kwa ule upendo na bidii ambayo hao ndugu huonyesha.”
16 Mwangalizi wa mzunguko katika Afrika aandika hivi: “Kwa sababu ya upendo tulioonyeshwa na akina ndugu, tulilipenda eneo la Tanzania sana! Akina ndugu walikuwa tayari kujifunza kutoka kwetu, nao walifurahi kuwa nasi nyumbani mwao.” Kulikuwa na uhusiano wenye upendo na furaha kati ya mtume Paulo na wale wenzi wa ndoa Akila na Priska Wakristo wa karne ya kwanza. Kwa kweli, Paulo alisema hivi juu yao: “Nisalimieni Priska na Akila, watenda kazi pamoja nami katika Kristo Yesu; waliokuwa tayari hata kukatwa kichwa kwa ajili ya maisha yangu; ambao ninawashukuru, wala si mimi tu, ila na makanisa ya Mataifa yote pia.” (Warumi 16:3, 4) Waangalizi wasafirio na wake zao ni wenye shukrani kuwa na marafiki walio kama Akila na Priska wa siku ya kisasa ambao hufanya jitihada ya pekee kuonyesha ukaribishaji-wageni na kutoa uandamani.
Kuyaimarisha Makutaniko
17. Kwa nini yaweza kusemwa kwamba kuna hekima katika mpango wa kuwa na waangalizi wasafirio, nao hupata wapi maagizo yao?
17 Yesu alisema hivi: “Hekima imejulikana kuwa ina haki kwa kazi zake.” (Mathayo 11:19) Ni wazi kwamba kuna hekima katika mpango wa kuwa na waangalizi wasafirio kwa sababu huo husaidia kuyaimarisha makutaniko ya watu wa Mungu. Wakati wa safari ya umishonari ya pili ya Paulo, yeye na Sila ‘walipitia Siria na Kilikia wakiyaimarisha makanisa,’ kwa mafanikio. Kitabu cha Matendo chatuambia hivi: “Walipokuwa wakipita kati ya miji ile, wakawapa zile amri zilizoamriwa na mitume na wazee walioko Yerusalemu, ili wazishike. Makanisa yakatiwa nguvu katika ile Imani, hesabu yao ikaongezeka kila siku.” (Matendo 15:40, 41; 16:4, 5, linganisha Habari Njema kwa Watu Wote.) Waangalizi wasafirio wa sasa hupokea maagizo kupitia Maandiko na vichapo vya “mtumwa mwaminifu mwenye akili,” sawa na Wakristo wengine wote.—Mathayo 24:45.
18. Waangalizi wasafirio huyaimarishaje makutaniko?
18 Ndiyo, lazima wazee wasafirio waendelee kujilisha kwenye meza ya kiroho ya Yehova. Lazima wafahamu vizuri njia na miongozo inayofuatwa na tengenezo la Mungu. Ndipo wanaume hao wawezapo kuwa baraka halisi kwa wengine. Kupitia kielelezo chao chema cha bidii katika utumishi wa shambani, wao waweza kusaidia waamini wenzao waboreke katika huduma ya Kikristo. Zile hotuba zinazotegemea Biblia ambazo hutolewa na wazee hao wanaozuru hujenga wasikilizaji kiroho. Kwa kusaidia wengine watumie shauri la Neno la Mungu, watumikie kwa upatano na watu wa Yehova duniani pote, na watumie maandalizi ya kiroho yatolewayo na Mungu kupitia ‘mtumwa mwaminifu,’ waangalizi wasafirio huyaimarisha makutaniko wanayopendelewa kuzuru.
19. Ni maswali gani yanayosalia kufikiriwa?
19 Tengenezo la Yehova lilipoanzisha kazi ya wazee wasafirio miongoni mwa Wanafunzi wa Biblia karibu miaka mia moja iliyopita, jarida hili lilitaarifu hivi: “Tutachunguza ili kuona matokeo na kuona mwongozo zaidi wa Bwana.” Mwongozo wa Yehova umeonekana wazi. Kwa sababu ya baraka yake na usimamizi wa Baraza Linaloongoza, kazi hii imepanuliwa na kuboreshwa katika ile miaka ambayo imepita. Likiwa tokeo, makutaniko ya Mashahidi wa Yehova kotekote duniani yanafanywa imara katika imani na yanaongezeka kila siku. Kwa wazi, Yehova anabariki roho ya kujidhabihu ya zawadi hizo zilizo wanadamu. Lakini waangalizi wasafirio waweza kutimizaje kazi yao kwa mafanikio? Malengo yao ni nini? Wao waweza kuyanufaishaje makutaniko kikamili zaidi?
-
-
Jinsi Ambavyo Waangalizi Wasafirio Hutumikia Wakiwa Wasimamizi-Nyumba WaaminifuMnara wa Mlinzi—1996 | Novemba 15
-
-
Jinsi Ambavyo Waangalizi Wasafirio Hutumikia Wakiwa Wasimamizi-Nyumba Waaminifu
“Kwa kadiri ambayo kila mmoja amepokea zawadi, itumieni katika kuhudumiana kama wasimamizi-nyumba walio wema wa fadhili isiyostahiliwa ya Mungu iliyoonyeshwa katika njia mbalimbali.”—1 PETRO 4:10, NW.
1, 2. (a) Ungefasilije neno “msimamizi-nyumba”? (b) Ni nani wanaotiwa ndani miongoni mwa wasimamizi-nyumba wanaotumiwa na Mungu?
YEHOVA hutumia Wakristo waaminifu wote kuwa wasimamizi-nyumba. Mara nyingi msimamizi-nyumba ni mtumishi anayesimamia mambo ya nyumbani. Huenda pia akasimamia mambo ya kibiashara ya bwana-mkubwa wake. (Luka 16:1-3; Wagalatia 4:1, 2) Yesu alikiita kikundi chake cha watiwa-mafuta waaminifu-washikamanifu duniani “msimamizi-nyumba mwaminifu.” Amemkabidhi msimamizi-nyumba huyo “vitu vyake vyote,” kutia ndani utendaji mbalimbali wa kuhubiri Ufalme.—Luka 12:42-44; Mathayo 24:14, 45, linganisha NW.
2 Mtume Petro alisema kwamba Wakristo wote ni wasimamizi-nyumba wa fadhili isiyostahiliwa ya Mungu iliyoonyeshwa katika njia mbalimbali. Kila Mkristo ana mahali ambapo kutoka hapo yeye aweza kutekeleza usimamizi-nyumba mwaminifu. (1 Petro 4:10) Wazee Wakristo waliowekwa rasmi ni wasimamizi-nyumba na miongoni mwao kuna waangalizi wasafirio. (Tito 1:7) Wazee hao wasafirio waonweje? Wawe na sifa zipi na malengo yapi? Nao waweza kunufaishaje kikamili?
Kuwa Wenye Shukrani kwa Sababu ya Utumishi Wao
3. Kwa nini waangalizi wasafirio waweza kuitwa “wasimamizi-nyumba walio wema”?
3 Wenzi wa ndoa fulani Wakristo wakiwaandikia mwangalizi asafiriye na mkewe, walisema hivi: “Tungependa kutoa shukrani zetu kwa ule wakati na upendo wote ambao mmetutolea. Tukiwa familia, tumenufaika sana kutokana na kitia-moyo na mashauri yenu yote. Twajua kwamba twahitaji kuendelea kukua kiroho, lakini kwa msaada wa Yehova na tukiwa na ndugu na dada kama nyinyi, maumivu ya kukua yanapunguzwa.” Maelezo kama haya ni ya kawaida kwa sababu waangalizi wasafirio huonyesha upendezi wa kibinafsi katika waamini wenzao, sawa na vile msimamizi-nyumba mwema atunzavyo vema mahitaji ya watu wa nyumbani. Waangalizi fulani ni wasemaji wenye kutokeza. Wengi ni wenye kutokeza katika kazi ya kuhubiri, hali wengine wanajulikana kwa sababu ya uchangamfu wao na huruma yao. Kwa kusitawisha na kutumia zawadi hizo katika kuwahudumia wengine, waangalizi wasafirio waweza kwa kufaa kuitwa “wasimamizi-nyumba walio wema.”
4. Ni swali gani litakalofikiriwa sasa?
4 “Inayohitajiwa katika mawakili [“wasimamizi-nyumba,” NW], ndiyo mtu aonekane kuwa mwaminifu,” akaandika mtume Paulo. (1 Wakorintho 4:2) Kuhudumia Wakristo wenzi katika kutaniko tofauti kila juma ni pendeleo la kipekee na lenye shangwe. Hata hivyo, hilo ni daraka zito pia. Basi, waangalizi wasafirio waweza kutekelezaje usimamizi-nyumba wao kwa uaminifu na kwa mafanikio?
Kutekeleza Usimamizi-Nyumba Wao kwa Mafanikio
5, 6. Kwa nini kumtegemea Yehova kwa sala ni jambo la maana sana maishani mwa mwangalizi asafiriye?
5 Kumtegemea Yehova kwa sala ni jambo la lazima ikiwa waangalizi wasafirio watakuwa wasimamizi-nyumba wenye mafanikio. Kwa sababu ya ratiba na madaraka yao mengi, nyakati nyingine wangeweza kuhisi kulemewa. (Linganisha 2 Wakorintho 5:4.) Kwa hiyo wanahitaji kutenda kwa upatano na wimbo huu wa mtunga-zaburi Daudi: “Umtwike BWANA mzigo wako naye atakutegemeza, hatamwacha mwenye haki aondoshwe milele.” (Zaburi 55:22) Yenye kufariji pia, ni maneno haya ya Daudi: “Na ahimidiwe Bwana, siku kwa siku hutuchukulia mzigo wetu.”—Zaburi 68:19.
6 Paulo alipata wapi nguvu za kushughulikia madaraka yake ya kiroho? “Nayaweza mambo yote katika yeye anitiaye nguvu,” yeye aliandika. (Wafilipi 4:13) Ndiyo, Yehova Mungu alikuwa ndiye Chanzo cha nguvu za Paulo. Vivyo hivyo, Petro alishauri hivi: “Mtu akihudumu, na ahudumu kwa nguvu anazojaliwa na Mungu; ili Mungu atukuzwe katika mambo yote kwa Yesu Kristo.” (1 Petro 4:11) Ndugu mmoja aliyekuwa mwangalizi asafiriye kwa miaka mingi alikazia uhitaji wa kumtegemea Mungu, akitaarifu hivi: “Mtegemee Yehova sikuzote katika kushughulikia matatizo, na kutafuta msaada wa tengenezo lake.”
7. Usawaziko una sehemu jinsi gani katika kazi ya mwangalizi asafiriye?
7 Usawaziko unahitajiwa na mwangalizi asafiriye mwenye mafanikio. Sawa na Wakristo wengine, yeye hujitahidi “kuhakikisha mambo yaliyo ya maana zaidi.” (Wafilipi 1:10, NW)a Wazee wa mahali fulani wanapokuwa na maswali juu ya jambo fulani, ni jambo la hekima kwao kushauriana na mwangalizi wa mzunguko anayezuru. (Mithali 11:14; 15:22) Yamkini, maoni yake yenye usawaziko na shauri lake la Kimaandiko litathibitika kuwa lenye msaada sana hao wazee waendeleapo kushughulikia jambo hilo baada ya yeye kuondoka hilo kutaniko. Kuhusu jambo linalolingana na hilo, Paulo alimwambia Timotheo hivi: “Mambo yale uliyoyasikia kwangu mbele ya mashahidi wengi, hayo uwakabidhi watu waaminifu watakaofaa kuwafundisha na wengine.”—2 Timotheo 2:2.
8. Kwa nini funzo la Biblia, utafiti, na kutafakari ni mambo ya maana?
8 Kujifunza, kufanya utafiti, na kutafakari juu ya Maandiko kunatakiwa ili kutoa shauri lililo timamu. (Mithali 15:28) Mwangalizi wa wilaya mmoja alisema hivi: “Tunapokutana na wazee, hatupaswi kuogopa kukiri kwamba hatujui jibu kwa swali fulani.” Kujitahidi kupata “akili ya Kristo” juu ya jambo hufanya iwezekane kutoa shauri linalotegemea Biblia litakalosaidia wengine watii mapenzi ya Mungu. (1 Wakorintho 2:16, HNWW) Nyakati nyingine mwangalizi asafiriye anahitaji kuandikia Watch Tower Society ili kupata mwelekezo. Kwa vyovyote vile, imani katika Yehova na kuipenda kweli ni mambo yaliyo ya maana zaidi kuliko ufasaha na jinsi watu watuonavyo. Badala ya kuja “kwa ufasaha wa maneno, wala kwa hekima,” Paulo alianza huduma yake Korintho “katika hali ya udhaifu na hofu na matetemeko mengi.” Je, hilo lilimzuia asiwe na matokeo? La hasha, liliwasaidia Wakorintho wawe na imani, si “katika hekima ya wanadamu, bali katika nguvu za Mungu.”—1 Wakorintho 2:1-5.
Sifa Nyingine za Maana
9. Kwa nini hisia-mwenzi inahitajiwa na wazee wasafirio?
9 Hisia-mwenzi huwasaidia waangalizi wasafirio wapate matokeo mazuri. Petro aliwasihi sana Wakristo wote ‘waonyeshe hisia-mwenzi,’ au wawe “wenye kusikitikia.” (1 Petro 3:8, kielezi-chini, NW) Mwangalizi wa mzunguko mmoja huhisi uhitaji wa ‘kupendezwa na kila mtu kutanikoni na kuwa msikivu kikweli.’ Akiwa na roho iyo hiyo, Paulo aliandika hivi: “Furahini pamoja nao wafurahio; lieni pamoja nao waliao.” (Warumi 12:15) Mtazamo huo huwasukuma waangalizi wasafirio wajitahidi sana kuelewa matatizo na hali za waamini wenzao. Ndipo wawezapo kutoa shauri la Kimaandiko lenye kujenga liwezalo kunufaisha kihalisi ikiwa linatumiwa. Mwangalizi wa mzunguko atokezaye katika kuonyesha hisia-mwenzi alipokea barua hii kutoka kwenye kutaniko karibu na Turin, Italia: “Ikiwa wataka kuwa mwenye upendezi, uwe mwenye kupendezwa; ikiwa wataka kupendeza, uwe mwenye kupendeza; ikiwa wataka kupendwa, uwe mwenye kupendeka; ikiwa wataka kusaidiwa, uwe tayari kusaidia. Hilo ndilo tulilojifunza kutoka kwako!”
10. Waangalizi wa mzunguko na wa wilaya wamesema nini kuhusu kuwa mnyenyekevu, na Yesu aliweka kielelezo kipi kwa habari hii?
10 Kuwa mnyenyekevu na mwenye kufikika huwasaidia waangalizi wasafirio wanufaishe sana. Mwangalizi wa mzunguko mmoja alionelea hivi: “Ni jambo la maana zaidi kudumisha mtazamo mnyenyekevu.” Angewaonya waangalizi wasafirio wapya: “Msijiruhusu kuvutiwa isivyofaa na ndugu walio matajiri zaidi kwa sababu ya yale ambayo huenda wakawafanyia nyinyi, wala msiwaonyeshe urafiki wenu kwa watu hao pekee, bali mjitahidi sikuzote kushughulika na wengine bila ubaguzi.” (2 Mambo ya Nyakati 19:6, 7) Na mwangalizi asafiriye aliye mnyenyekevu kikweli hatakuwa na maoni ya kupita kiasi juu ya umaana wake mwenyewe akiwa mwakilishi wa Sosaiti. Mwangalizi wa wilaya alieleza hivi kwa kufaa: “Uwe mnyenyekevu na tayari kuwasikiliza akina ndugu. Uwe mwenye kufikika sikuzote.” Akiwa mtu mkuu zaidi aliyepata kuishi, Yesu Kristo angaliweza kufanya watu wasihisi ustarehe, lakini alikuwa mnyenyekevu sana na mwenye kufikika hivi kwamba hata watoto walihisi ustarehe wakiwa pamoja naye. (Mathayo 18:5; Marko 10:13-16) Waangalizi wasafirio wanataka watoto, matineja, wazee-wazee—kwa kweli yeyote yule na kila mtu kutanikoni—wahisi uhuru wa kuwafikia.
11. Kunapohitajiwa, kuomba radhi huweza kuwa na tokeo gani?
11 Bila shaka, “twajikwaa sisi sote pia katika mambo mengi,” na hakuna mwangalizi asafiriye yeyote ambaye hawezi kufanya makosa. (Yakobo 3:2) Wafanyapo makosa, kuomba radhi kwa moyo mweupe huwatolea wale wazee wengine kielelezo cha unyenyekevu. Kulingana na Mithali 22:4, “thawabu ya unyenyekevu ambao ni kumcha BWANA [kwa staha] ni utajiri, na heshima, nayo ni uzima.” Na je, watumishi wa Mungu wote hawahitaji ‘kwenda kwa unyenyekevu na Mungu wao’? (Mika 6:8) Alipoulizwa ni shauri gani angempa mzee asafiriye mpya, mwangalizi wa mzunguko mmoja alieleza hivi: “Stahi na kuheshimu sana ndugu wote, na kuwaona kuwa bora zaidi ya wewe. Utajifunza mengi kutoka kwa akina ndugu. Endelea kuwa mnyenyekevu. Uwe jinsi ulivyo kihalisi. Usijifanye.”—Wafilipi 2:3.
12. Kwa nini bidii kwa ajili ya huduma ya Kikristo ni ya maana sana?
12 Bidii kwa ajili ya huduma ya Kikristo huongezea umaana wa maneno ya mwangalizi asafiriye. Kwa kweli, yeye na mkewe wawekapo vielelezo vyenye bidii katika kazi ya kueneza evanjeli, wazee, wake zao, na wengine kutanikoni wanatiwa moyo kuonyesha bidii katika huduma yao. “Uwe mwenye bidii kwa ajili ya utumishi,” akasihi sana mwangalizi wa mzunguko mmoja. Aliongeza hivi: “Nimeona kwamba, kwa ujumla, kadiri kutaniko linavyokuwa lenye bidii zaidi katika huduma, ndivyo linavyokuwa na matatizo machache zaidi.” Mwangalizi wa mzunguko mwingine alisema hivi: “Naamini kwamba wazee wakihubiri shambani pamoja na ndugu na dada na kuwasaidia waifurahie huduma, hilo litatokeza amani ya akili na uradhi mkubwa zaidi katika kumtumikia Yehova.” Mtume Paulo ‘alijipa ujasiri kusema na Wathesalonike habari njema ya Mungu kwa kushindana sana.’ Si ajabu kwamba walikuwa na makumbukumbu yenye kupendeza juu ya ziara yake na utendaji wake wa kuhubiri, hata wakawa na hamu ya kumwona tena!—1 Wathesalonike 2:1, 2; 3:6, NW.
13. Mwangalizi asafiriye hufikiria nini anapohubiri pamoja na Wakristo wenzake katika utumishi wa shambani?
13 Anapohubiri na Wakristo wenzake katika huduma ya shambani, mwangalizi asafiriye hufikiria hali zao na mipaka yao. Ingawa madokezo yake huenda yakawa yenye msaada, yeye ajua kwamba wengine waweza kuwa waoga wanapohubiri na mzee mwenye uzoefu. Kwa hiyo, katika hali fulani, kitia-moyo chaweza kufaa zaidi kuliko shauri. Aandamanapo na watangazaji au na mapainia kwenye funzo la Biblia, huenda wakapendelea kwamba yeye aliongoze. Yamkini hilo litawajulisha baadhi ya njia za kuboresha njia zao za kufundisha.
14. Kwa nini yaweza kusemwa kwamba waangalizi wasafirio wenye bidii huchochea bidii katika wengine?
14 Waangalizi wasafirio wenye bidii huchochea bidii katika wengine. Mwangalizi wa mzunguko mmoja katika Uganda alitembea kupitia msitu wenye miti mingi kwa muda wa saa moja ili kuandamana na ndugu kwenye funzo la Biblia ambalo halikuwa likifanya maendeleo mengi. Walipokuwa wakitembea mvua ilinyesha kwa nguvu sana hivi kwamba walifika wakiwa wamelowa maji kabisa. Hiyo familia ya watu sita ilipopata kujua kwamba mgeni wayo alikuwa mwangalizi asafiriye, ilivutiwa sana. Watu hao walijua kwamba wahudumu wa kanisa lao wasingelionyesha kundi upendezi huo kamwe. Jumapili iliyofuata, walihudhuria mkutano wao wa kwanza wakaeleza tamaa ya kuwa Mashahidi wa Yehova.
15. Ni jambo zuri gani lililoonwa na mwangalizi wa mzunguko mwenye bidii katika Mexico?
15 Katika jimbo la Mexico la Oaxaca, mwangalizi wa mzunguko mmoja kwa kweli alijitahidi kwa njia isiyotazamiwa kwake. Alipanga kukaa katika seli ya gereza kwa usiku nne ili kutembelea kikundi cha wafungwa saba waliopata kuwa watangazaji wa Ufalme. Kwa siku kadhaa aliandamana na wafungwa hao walipokuwa wakitoa ushahidi kutoka seli hadi seli na kuongoza mafunzo ya Biblia. Kwa sababu ya upendezi ulioonyeshwa, baadhi ya mafunzo hayo yaliendelea hadi usiku sana. “Mwishoni mwa ziara hiyo, hao wafungwa na mimi tulihisi tukiwa tumejaa shangwe kwa sababu ya kutiana moyo,” akaandika mwangalizi wa mzunguko huyo mwenye bidii.
16. Kwa nini inanufaisha sana waangalizi wa mzunguko na wake zao watoapo kitia-moyo?
16 Waangalizi wasafirio hujaribu kuwa wenye kutia moyo. Paulo alipoyazuru makutaniko katika Makedonia, ‘aliyatia moyo kwa maneno mengi.’ (Matendo 20:1, 2, HNWW) Maneno ya kitia-moyo yaweza kuwa yenye msaada sana katika kuwaelekeza vijana na pia wazee kwenye miradi ya kiroho. Kwenye ofisi kubwa moja ya Watch Tower Society, uchunguzi usio rasmi ulifunua kwamba waangalizi wa mzunguko walikuwa wametia moyo karibu asilimia 20 ya wajitoleaji kuanza utumishi wa wakati wote. Kwa kielelezo chake chema akiwa mpiga-mbiu wa Ufalme wa wakati wote, mke wa mwangalizi asafiriye huthibitika pia kuwa chanzo kikubwa cha kitia-moyo.
17. Mwangalizi wa mzunguko mzee-mzee mmoja huhisije juu ya pendeleo lake la kuwatolea wengine msaada?
17 Wazee-wazee na nafsi zilizoshuka moyo wana uhitaji hasa wa kitia-moyo. Mwangalizi wa mzunguko mzee-mzee mmoja aandika hivi: “Sehemu ya kazi yangu itokezayo shangwe ya kindani isiyoelezeka ni pendeleo la kutolea msaada wale wasiotenda na walio wanyonge miongoni mwa kundi la Mungu. Maneno ya Warumi 1:11, 12 (HNWW), yana maana ya pekee kwangu, kwa kuwa mimi hupata kitia-moyo na nguvu nyingi ‘niwagawiapo watu kama hao zawadi ya kiroho na kuwaimarisha.’”
Thawabu za Kazi Yao Yenye Shangwe
18. Waangalizi wasafirio wana malengo gani ya Kimaandiko?
18 Waangalizi wasafirio hupendezwa kwa moyo mweupe na waamini wenzao. Wanataka kuyaimarisha makutaniko na kuyajenga kiroho. (Matendo 15:41) Mwangalizi mmoja asafiriye hujitahidi “kutoa kitia-moyo, kuandaa kiburudisho, na kuchochea tamaa ya kutimiza huduma na kuendelea kuishi kulingana na kweli.” (3 Yohana 3) Mwingine hujaribu kuwafanya waamini wenzake wawe thabiti katika imani. (Wakolosai 2:6, 7) Kumbuka kwamba mwangalizi asafiriye ni “mwenzi wa nira halisi,” si bwana-mkubwa juu ya imani ya wengine. (Wafilipi 4:3; 2 Wakorintho 1:24, linganisha NW.) Ziara yake ni pindi ya kupata kitia-moyo na ya utendaji wa ziada, na pia ni fursa kwa baraza la wazee kupitia maendeleo yaliyofanywa na kufikiria miradi ya wakati ujao. Kwa maneno yake na kielelezo chake, watangazaji wa kutaniko, mapainia, watumishi wa huduma, na wazee waweza kutazamia kujengwa na kuchochewa ili kufanya kazi iliyo mbele. (Linganisha 1 Wathesalonike 5:11.) Kwa hiyo, basi, unga mkono kwa moyo wote ziara za mwangalizi wa mzunguko, na kutumia kikamili utumishi unaotolewa na mwangalizi wa wilaya.
19, 20. Waangalizi wasafirio na wake zao wamethawabishwaje kwa sababu ya utumishi wao mwaminifu?
19 Waangalizi wa mzunguko na wake zao huthawabishwa sana kwa ajili ya utumishi wao mwaminifu, nao waweza kuwa na uhakika kwamba Yehova atawabariki kwa sababu ya yale mema wafanyayo. (Mithali 19:17; Waefeso 6:8) Georg na Magdalena ni wenzi wa ndoa wazee-wazee waliotumikia kwa miaka mingi katika kazi ya kusafiri. Kwenye mkusanyiko katika Luxembourg, Magdalena alifikiwa na mtu ambaye alikuwa amemtolea ushahidi miaka zaidi ya 20 mapema. Upendezi katika kweli wa mwanamke huyo Myahudi uliamshwa na fasihi za Biblia ambazo Magdalena alimwachia, na hatimaye akabatizwa. Georg alifikiwa na dada wa kiroho, aliyekumbuka ziara ya Georg nyumbani kwake karibu miaka 40 iliyopita. Utoaji wake wenye idili wa habari njema uliwaongoza hatimaye yeye na mumewe waikubali kweli. Bila shaka, Georg na pia Magdalena walibubujika shangwe.
20 Huduma ya Paulo yenye matokeo katika Efeso ilimletea shangwe na huenda ikawa ndiyo iliyomsukuma anukuu maneno haya ya Yesu: “Ni heri kutoa kuliko kupokea.” (Matendo 20:35) Kwa kuwa kazi ya kusafiri huhusisha kutoa sikuzote, wale wanaoshiriki katika kazi hiyo hupata furaha, hasa wapatapo kuona matokeo mazuri ya kazi yao ya jasho. Mwangalizi wa mzunguko mmoja aliyemsaidia mzee aliyevunjika moyo aliambiwa hivi katika barua: “Umekuwa ‘msaada wenye kutia nguvu’ sana katika maisha yangu ya kiroho—zaidi ya vile ujuavyo. . . . Hutapata kamwe kujua kikamili kadiri ambavyo umemsaidia Asafu wa siku ya kisasa, ambaye ‘miguu yake ilikuwa karibu na kupotoka.’”—Wakolosai 4:11; Zaburi 73:2, linganisha NW.
21. Kwa nini ungesema kwamba 1 Wakorintho 15:58 lahusu utendaji mbalimbali wa waangalizi wasafirio?
21 Mkristo mzee-mzee aliyekuwa katika kazi ya mzunguko kwa miaka kadhaa hupenda kufikiria 1 Wakorintho 15:58, ambalo katika hilo Paulo alisihi sana hivi: “Iweni imara, wasioondoleka, sikuzote mkiwa na mengi ya kufanya katika kazi ya Bwana, mkijua kwamba kazi yenu ya jasho si bure kuhusiana na Bwana.” Kwa hakika waangalizi wasafirio wana mengi ya kufanya katika kazi ya Bwana. Nasi twashukuru kama nini kwamba wao hutumikia kwa shangwe sana wakiwa wasimamizi-nyumba waaminifu wa fadhili isiyostahiliwa ya Yehova!
-