-
Je, Unaitegemeza Enzi Kuu ya Yehova?Mnara wa Mlinzi—2007 | Desemba 1
-
-
Kielelezo cha Kufuata
12, 13. (a) Watu wanaitikia jinsi gani habari njema ya Ufalme leo? (b) Tunapaswa kufikiria nini ikiwa tunataka kufuata hatua za Kristo?
12 Leo, habari njema ya Ufalme inahubiriwa katika nchi nyingi, kama Yesu alivyotabiri. (Mathayo 24:14) Matokeo ni kwamba mamilioni ya watu wameweka maisha yao wakfu kwa Mungu. Wanasisimuka kwa sababu ya baraka ambazo Ufalme huo utaleta. Wanatazamia kuishi milele kwa amani na usalama katika paradiso duniani, na kwa shangwe wanawaambia wengine kuhusu tumaini lao. (Zaburi 37:11; 2 Petro 3:13) Je, wewe ni mmoja wa watangazaji hao wa Ufalme? Ikiwa ndivyo, unastahili pongezi. Hata hivyo, kuna jambo lingine ambalo kila mmoja wetu anapaswa kufikiria.
13 Mtume Petro aliandika hivi: “Kristo aliteseka kwa ajili yenu, akiwaachia ninyi kielelezo ili mfuate hatua zake kwa ukaribu.” (1 Petro 2:21) Ona kwamba katika andiko hilo, Petro hakutaja bidii ya Yesu ya kuhubiri au ustadi wake wa kufundisha, alitaja mateso yake. Petro alijionea hayo, kwa hivyo alijua vizuri jinsi Yesu alivyokuwa tayari kuteseka ili ajitiishe chini ya enzi kuu ya Yehova na kuthibitisha kwamba Shetani ni mwongo. Basi, tunaweza kufuata hatua za Yesu jinsi gani? Tunapaswa kujiuliza: ‘Niko tayari kuteseka kadiri gani ili niitegemeze na kuiletea heshima enzi kuu ya Yehova? Je, maisha na huduma yangu inaonyesha kwamba ninahangaikia hasa kuitegemeza enzi kuu ya Yehova?’—Wakolosai 3:17.
14, 15. (a) Yesu alifanya nini alipopewa mapendekezo yenye kupotosha, na kwa nini alifanya hivyo? (b) Tunapaswa sikuzote kukazia akilini suala gani? (Tia ndani maelezo kutoka katika sanduku lenye kichwa “Simama Upande wa Yehova.”)
14 Kila siku, tunakabili majaribu na maamuzi, makubwa na madogo. Tunapaswa kufikiria nini tunapoyashughulikia? Kwa mfano, tunaposhawishiwa moja kwa moja tufanye jambo fulani ambalo litahatarisha msimamo wetu wa Kikristo, tunatenda jinsi gani? Petro alipomwambia Yesu ajitendee kwa fadhili, Yesu alisema nini? Alisema hivi kwa uthabiti: ‘Nenda nyuma yangu, Shetani! Unafikiri, si fikira za Mungu, bali za wanadamu.’ (Mathayo 16:21-23) Au tunapopewa nafasi za kupata pesa zaidi au kupandishwa cheo na kuhatarisha hali yetu ya kiroho, je, tunafanya kama Yesu alivyofanya? Yesu alipotambua kwamba wale walioona miujiza yake “walikuwa karibu kuja kumkamata wamfanye kuwa mfalme,” aliondoka haraka na kwenda zake.—Yohana 6:15.
15 Kwa nini Yesu alichukua hatua imara katika pindi hizo na pindi nyingine? Kwa sababu aliona wazi kwamba mambo mengine yalihusika zaidi ya usalama wake au faida yake ya kibinafsi. Alitaka kufanya mapenzi ya Baba yake na kuitegemeza enzi kuu ya Yehova chini ya hali zozote. (Mathayo 26:50-54) Hivyo, ikiwa hatukazii akilini nyakati zote suala linalohusika la enzi kuu, kama Yesu alivyofanya, tutakabili daima hatari ya kulegeza msimamo wetu au tutashindwa kufanya yaliyo sawa. Kwa nini? Kwa sababu tunaweza kudanganywa kwa urahisi na mbinu zenye hila za Shetani, ambaye ni fundi katika kufanya mambo yasiyofaa yapendeze, kama alivyofanya alipokuwa akimshawishi Hawa.—2 Wakorintho 11:14; 1 Timotheo 2:14.
-
-
Je, Unaitegemeza Enzi Kuu ya Yehova?Mnara wa Mlinzi—2007 | Desemba 1
-
-
[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 29]
SIMAMA UPANDE WA YEHOVA
Kama ndugu wengi wa Korea na wa nchi nyinginezo wanavyojua, Wakristo wanapokabili majaribu makali, kuna faida ya kuelewa vizuri kabisa kwa nini wanapata majaribu hayo.
Shahidi mmoja wa Yehova aliyefungwa gerezani wakati wa utawala wa Sovieti alisema hivi: “Niliweza kuvumilia kwa sababu nilielewa vizuri kabisa suala lililotokezwa katika bustani ya Edeni, suala la haki ya Mungu ya kutawala. . . . Tulijua kwamba tulikuwa na nafasi ya kuutegemeza utawala wa Yehova. . . . Hilo lilitutia nguvu na kutuwezesha kushika utimilifu wetu.”
Shahidi mwingine alieleza kilichomsaidia na kuwasaidia Mashahidi wenzake katika kambi ya kazi ngumu. Alisema hivi: “Yehova alitutegemeza. Hata ingawa tulikuwa katika hali ngumu, tulikuwa macho kiroho. Sikuzote tulitiana moyo kwa kukumbushana kwamba tulikuwa tunasimama upande wa Yehova wa suala la enzi kuu ya ulimwengu wote.”
-