Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Je, Tuitegemee au Tusiitegemee?
    Amkeni!—2007 | Novemba
    • Je, Tuitegemee au Tusiitegemee?

      “Usitumaini mbao zilizooza,” akaandika William Shakespeare, mwandishi wa tamthilia Mwingereza. Kwa kweli, kabla ya kukanyaga mbao za mashua, unapaswa kuhakikisha kwamba hazijaoza.

      MANENO ya Shakespeare yanapatana na maneno ya Mfalme Sulemani mwenye hekima wa Israeli la kale ambaye aliandika hivi miaka 3,000 hivi iliyopita: “Mujinga anaamini kila neno: lakini mwenye akili anaangalia sana namna anavyokwenda.” (Methali 14:15, Zaire Swahili Bible) Naam, ni mjinga tu ambaye atakubali kila kitu anachosikia, akifanya maamuzi na kutenda kupatana na mashauri au mafundisho yasiyo na msingi. Kutegemea vitu visivyofaa, kama tu kukanyaga mbao zilizooza, kunaweza kutuletea msiba. Huenda ukajiuliza, ‘Je, kuna mwongozo wowote ambao kwa kweli tunaweza kuutegemea?’

      Mamilioni ya watu ulimwenguni pote hutegemea kabisa kitabu kimoja cha kale. Kitabu hicho ni Biblia Takatifu. Wanategemea kitabu hicho kiongoze hatua zao. Maamuzi yao yanategemea mashauri ya kitabu hicho na matendo yao yanapatana na mafundisho yake. Je, watu hao wanakanyaga mbao zilizooza? Jibu la swali hilo linategemea sana jibu la swali lingine, Je, kuna sababu nzuri za kuitegemea Biblia? Toleo hili la pekee la Amkeni! linachunguza uthibitisho uliopo.

      Toleo hili la Amkeni! halijakusudiwa kukulazimisha uwe na imani au maoni fulani ya kidini. Badala yake, limekusudiwa kuonyesha uthibitisho wenye nguvu ambao umewasadikisha mamilioni ya watu kwamba wanaweza kuitegemea Biblia. Baada ya kusoma makala zinazofuata, unaweza kujiamulia ikiwa unaweza kuitegemea Biblia.

      Unapaswa kuchunguza habari hii kwa uzito. Kwa kweli, ikiwa Biblia ni chanzo chenye kutegemeka cha kupata mwongozo kutoka kwa Muumba wetu, basi utafaidika ikiwa wewe na wapendwa wako mtachunguza kile ambacho Biblia inasema.

      Hata hivyo, acheni kwanza tutaje mambo fulani ya hakika kuhusu Biblia. Kwanza kabisa, Biblia ni kitabu cha pekee.

  • Kitabu cha Pekee
    Amkeni!—2007 | Novemba
    • Kitabu cha Pekee

      “Biblia ndicho kitabu kilichogawanywa kwa wingi zaidi katika historia.”—The World Book Encyclopedia.

      ZAIDI ya miaka 550 iliyopita, mwandishi Mjerumani, Johannes Gutenberg alianza uchapishaji kwa kutumia mashini ya kuchapishia yenye herufi zinazopangwa. Kitabu cha kwanza muhimu alichochapisha kilikuwa Biblia.a Tangu wakati huo mabilioni ya vitabu kuhusu habari mbalimbali vimechapishwa. Hata hivyo, Biblia ndicho kitabu cha pekee zaidi kati ya hivyo vyote.

      ◼ Inakadiriwa kwamba zaidi ya Biblia bilioni 4.7 (ikiwa nzima au sehemu yake) zimechapishwa. Hiyo ni mara tano zaidi ya idadi ya nakala za kitabu Quotations From Chairman Mao, ambacho ndicho kitabu cha pili kugawanywa kwa wingi zaidi.

      ◼ Hivi karibuni, zaidi ya nakala milioni 50 za Biblia au sehemu zake ziligawanywa kwa mwaka mmoja tu. “Kila mwaka, Biblia ndicho kitabu ambacho huuzwa zaidi,” inasema ripoti moja katika gazeti The New Yorker.

      ◼ Biblia imetafsiriwa katika zaidi ya lugha 2,400 ikiwa nzima au kwa sehemu. Angalau sehemu fulani ya Biblia inapatikana katika lugha zinazozungumzwa na zaidi ya asilimia 90 ya wanadamu.

      ◼ Karibu nusu ya waandikaji wa Biblia walikamilisha kazi yao ya kuandika kabla ya kuzaliwa kwa Mchina mashuhuri na mwenye hekima, Confucius, na Siddhārtha Gautama, mwanzilishi wa Ubudha.

      ◼ Biblia imekuwa na uvutano mkubwa sana katika sanaa, kutia ndani baadhi ya michoro, muziki, na fasihi zinazojulikana sana ulimwenguni.

      ◼ Biblia imeokoka licha ya kupigwa marufuku na serikali mbalimbali, kuteketezwa na wapinzani wa kidini, na kushambuliwa na wachambuzi. Hakuna kitabu kingine ambacho kimepata upinzani mkubwa kadiri hiyo na kikaokoka.

      Mambo hayo ambayo yametajwa ni yenye kuvutia sana, sivyo? Hata hivyo, habari zenye kupendeza na takwimu pekee hazithibitishi kwamba Biblia ni yenye kutegemeka. Sasa, tutachunguza sababu tano zinazowasadikisha mamilioni ya watu kwamba Biblia ni kitabu kinachostahili kutegemewa.

      [Maelezo ya Chini]

      a Biblia ya Gutenberg ilikuwa tafsiri ya Kilatini nayo ilikamilika mwaka wa 1455 hivi.

      [Picha katika ukurasa wa 4]

      Mashini ya kuchapishia ya Gutenberg na ukurasa wa Biblia yake

      [Hisani]

      Press: Courtesy American Bible Society; page: © Image Asset Management/age fotostock

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki