-
“Nitamhofu Nani?”Mnara wa Mlinzi—2012 | Julai 15
-
-
TEGEMEA MSAADA WA MUNGU
9, 10. Uhakikisho unaotolewa katika Zaburi 27:10 unamaanisha nini?
9 Daudi anakazia jinsi alivyotegemea sana msaada wa Yehova kwa kusema hivi: “Hata ikiwa baba yangu na mama yangu wangeniacha, Yehova mwenyewe angenichukua.” (Zab. 27:10) Tunaweza kukata kauli kutokana na matukio yanayotajwa katika 1 Samweli sura ya 22 kwamba wazazi wa Daudi hawakumwacha. Hata hivyo, watu wengi leo wamelazimika kuvumilia kwa sababu ya kukataliwa kabisa na familia zao. Lakini, wengi ambao wameachwa na familia zao wamepata msaada na ulinzi katika kutaniko la Kikristo lenye upendo.
10 Kwa kuwa Yehova yuko tayari kuwategemeza watumishi wake wakati watu wengine wanapowaacha, je, hilo halionyeshi kwamba atawategemeza pia wanapokabili dhiki nyingine yoyote? Ikiwa, kwa mfano, tunahangaika kuhusu jinsi ya kuiandalia familia yetu mahitaji ya kimwili, je, hatupaswi kuwa na uhakika wa kwamba Yehova atatusaidia? (Ebr. 13:5, 6) Anaelewa hali na mahitaji ya watumishi wake wote washikamanifu.
11. Kumtegemea Yehova kunaweza kuwa na matokeo gani juu ya wengine? Toa mfano.
11 Fikiria kisa cha Victoria, ambaye ni mwanafunzi wa Biblia huko Liberia. Alipokuwa akifanya maendeleo ili abatizwe, mwanamume aliyekuwa akiishi naye alimwacha yeye na watoto wake watatu. Licha ya kwamba hakuwa na nyumba wala kazi, Victoria aliendelea kufanya maendeleo ya kiroho. Baada ya Victoria kubatizwa, binti yake mwenye umri wa miaka 13 aliokota kibeti kilichojaa pesa. Ili kuepuka kushawishiwa, waliamua kwamba hata hawangehesabu pesa hizo. Badala yake, walimtafuta haraka askari-jeshi mwenye kibeti hicho. Askari-jeshi huyo aliwaambia kwamba ikiwa watu wote wangekuwa wanyoofu kama Mashahidi wa Yehova, ulimwengu wote ungekuwa bora na wenye amani zaidi. Victoria alitumia Biblia kumwonyesha askari-jeshi huyo ahadi ya Yehova ya ulimwengu mpya. Alivutiwa sana na imani na unyoofu wa Victoria hivi kwamba akampa kiasi kikubwa cha pesa zilizookotwa. Kwa kweli, kuamini kabisa kwamba Yehova anaweza kuwaandalia mahitaji yao kumewafanya Mashahidi wa Yehova wajulikane waziwazi kuwa watu wanyoofu.
12. Tunaonyesha nini tunapoendelea kumtumikia Yehova licha ya kupoteza kazi au pesa? Toa mfano.
12 Au fikiria jinsi ambavyo Thomas, mhubiri ambaye hajabatizwa huko Sierra Leone, alihisi. Alianza kufanya kazi akiwa mwalimu wa shule ya sekondari, lakini hakulipwa mshahara wake kwa karibu mwaka mmoja hadi alipomaliza kazi yake. Thomas alihitaji kutimiza takwa gani la mwisho kabla ya kupokea mshahara wake? Alihitaji kuhojiwa na msimamizi wa shule hiyo ambaye ni kasisi. Kasisi huyo alimweleza Thomas kwamba mafundisho ya Mashahidi wa Yehova hayapatani na mafundisho ya shule hiyo. Kasisi huyo alisisitiza kwamba Thomas achague ama kazi au mafundisho yake yanayotegemea Biblia. Baada ya kuacha kazi hiyo na kupoteza mshahara wa karibu mwaka mmoja, Thomas alipata kazi nyingine ya kurekebisha redio na simu za mkononi. Mfano huo na mifano mingine kama hiyo inaonyesha kwamba tukimtegemea Yehova, hatutaogopa kamwe kwamba tutakosa mahitaji yetu kama watu wengine wanavyoogopa. Lakini kwa kuwa Yehova ndiye Muumba wa kila kitu na Mlinzi wa watu wake, tuna hakika kwamba atatuandalia mahitaji yetu.
13. Kazi ya kuhubiri kuhusu Ufalme inaendeleaje katika nchi ambako wahubiri hawana vitu vingi vya kimwili?
13 Katika nchi nyingi ambazo zina hali ngumu ya maisha, kwa kawaida wahubiri wa Ufalme wanahubiri kwa bidii sana. Kwa nini? Ofisi moja ya tawi inaandika hivi: “Wenye nyumba wengi wanaokubali kujifunza Biblia hawana kazi na hivyo wana wakati zaidi wa kujifunza wakati wa mchana. Ndugu pia wana wakati zaidi wa kuhubiri. Watu, hasa katika maeneo yenye hali ngumu zaidi za maisha, hawahitaji kuambiwa kwamba tunaishi katika siku za mwisho; wanaona hali mbaya kila mahali.” Mmishonari mmoja ambaye ametumika kwa miaka zaidi ya 12 katika nchi moja ambako kila mhubiri anaongoza, kwa wastani, zaidi ya mafunzo matatu ya Biblia, anaandika hivi: “Kwa kuwa wahubiri wengi wanaishi maisha rahisi na hawana mambo mengi yanayowakengeusha fikira, kwa ujumla wana wakati mwingi wa kuhubiri na kuongoza mafunzo ya Biblia.”
14. Umati mkubwa unaweza kufurahia ulinzi wa Mungu katika njia zipi?
14 Yehova ameahidi kuwasaidia, kuwalinda, na kuwakomboa watu wake kimwili na kiroho wakiwa kikundi, na tunaamini kwamba atatimiza ahadi yake. (Zab. 37:28; 91:1-3) Bila shaka, kutakuwa na umati mkubwa utakaookoka ile “dhiki kuu.” (Ufu. 7:9, 14) Kwa hiyo, umati huo mkubwa, ukiwa kama kikundi, utalindwa ili usiangamizwe katika kipindi chote kinachobaki cha siku za mwisho. Wataandaliwa kila kitu watakachohitaji ili kuvumilia majaribu na kulinda uhusiano wao pamoja na Yehova. Na katika kipindi chote cha mwisho cha ile dhiki kuu, Yehova atawalinda watu wake.
-
-
“Nitamhofu Nani?”Mnara wa Mlinzi—2012 | Julai 15
-
-
16 Tukimruhusu Yehova atufundishe na kutuongoza katika njia ya uadilifu, hatutakuwa na sababu yoyote ya kuhofu. Painia mmoja wa kawaida huko Marekani alipoomba kazi ambayo ingemsaidia yeye na familia yake yote kuendelea katika utumishi wa wakati wote, msimamizi wake alimwambia kwamba hangeweza kamwe kupata kazi hiyo bila kuwa na digrii ya chuo kikuu. Ikiwa ungeambiwa hivyo, je, ungejuta kwa sababu ulifuatia utumishi wa wakati wote badala ya elimu ya juu zaidi? Majuma mawili baadaye, msimamizi huyo alifutwa kazi, na msimamizi mwingine akamuuliza ndugu huyo kuhusu miradi au malengo yake. Ndugu huyo alimweleza kwamba yeye na mke wake walikuwa wahudumu wa wakati wote wa Mashahidi wa Yehova na walitaka kuendelea na utumishi wao. Kabla ndugu huyo hajasema neno lingine lolote, msimamizi huyo alisema hivi: “Nilijua kulikuwa na jambo fulani linalokufanya uwe tofauti! Baba yangu alipokuwa karibu kufa, waamini wenzenu wawili walikuja na kumsomea Biblia kila siku. Niliahidi kwamba ikiwa ningepata nafasi ya kumsaidia Shahidi wa Yehova, ningefanya hivyo.” Asubuhi iliyofuata, ndugu huyo alipewa kazi ileile ambayo msimamizi aliyetangulia alikataa kumpa. Kwa kweli, tukitanguliza masilahi ya Ufalme maishani mwetu, Yehova atatimiza ahadi yake ya kwamba hatutakosa mahitaji yetu ya lazima.—Mt. 6:33.
-