-
“Ukosefu Mkubwa wa Kuaminiana”Amkeni!—2010 | Oktoba
-
-
“Ukosefu Mkubwa wa Kuaminiana”
Huko Afrika Magharibi, mvulana mwenye umri wa miaka 12 amelazwa hospitalini kwa sababu ya kupewa dawa bandia ya kutibu malaria ambayo mama yake alinunua kwenye duka la dawa. Daktari mmoja anasema, “Kwa miaka 15 tumekuwa tukipata dawa bandia zikiuzwa.”a
Huko Asia, wazazi wa mvulana mchanga sana wanashtuka kujua kwamba maziwa yaliyoongezwa lishe ambayo walikuwa wakimpa yalikuwa na sumu. Kwa kusikitisha, mvulana huyo anakufa.
Mfanyabiashara mmoja huko Marekani aliyeaminiwa sana amewalaghai wateja wake mabilioni ya dola! Maelfu ya watu wanagundua kwamba malipo yao ya uzeeni yametoweka katika kile ambacho kimetajwa kuwa “upunjaji mbaya zaidi katika karne hii.”
ULIMWENGUNI pote, karibu kila mtu amewahi kusalitiwa na mtu aliyemwamini sana. Hata kuzorota kwa uchumi ulimwenguni kumesababishwa kwa kiasi kikubwa na kile ambacho gazeti la Kifaransa Le Monde lilitaja kuwa “ukosefu mkubwa wa kuaminiana.”
Ni nini kimesababisha ‘ukosefu huo mkubwa wa kuaminiana’? Je, kuna yeyote unayeweza kumwamini?
[Maelezo ya Chini]
a Ripoti hiyo ilichapishwa katika gazeti Le Figaro, linalochapishiwa Paris, Ufaransa.
-
-
Je, Kuna Yeyote Anayeweza Kuaminiwa?Amkeni!—2010 | Oktoba
-
-
Je, Kuna Yeyote Anayeweza Kuaminiwa?
Daktari mmoja alionwa kuwa mwanzilishi wa tiba ya kupunguza maumivu. Hata hivyo, kwa zaidi ya miaka kumi, kuanzia mwaka wa 1996, daktari huyo wa unusukaputi anayeheshimiwa sana alikuwa amejitungia matokeo ya utafiti uliochapishwa katika majarida ya kitiba yanayojulikana sana.
“SIELEWI ni kwa nini mtu anaweza kufanya jambo kama hilo,” anasema Dakt. Steven L. Shafer, katika jarida Anesthesiology News.
Ni nini kinachoweza kumfanya mtaalamu anayeheshimika kuwadanganya wanadamu wenzake? Huenda ikawa mojawapo ya sababu hizi nne.
● Pupa. Dakt. Jerome Kassirer, aliyekuwa mhariri wa jarida The New England Journal of Medicine, alieleza hivi katika ripoti iliyochapishwa katika gazeti New York Times: “Watafiti wanapotegemea sana kampuni [za madawa] ili kupata riziki, kuna mwelekeo wa kutoa matokeo yanayopendelea kampuni hizo.”
● Kutafuta mafanikio kwa njia yoyote ile. Nchini Ujerumani, inaaminiwa kwamba wanafunzi wa vyuo vikuu wanaojifunza sayansi wamewalipa walimu maelfu ya euro kama rushwa ili kupata cheti cha Doktor, cheo ambacho katika nchi hiyo kinaonyesha kuwa mtu amefanikiwa sana. Uchunguzi uliochapishwa katika gazeti The New York Times ulionyesha kwamba wanafunzi wengi waliochukua njia hiyo ya mkato walisema kwamba “wanakusudia kufuata sheria zilizowekwa” baada ya kupata mafanikio.
● Hakuna mifano bora ya kuigwa. Gazeti The New York Times lilimnukuu profesa mmoja aliyesema hivi kuhusu wanafunzi wa shule za sekondari: “Huenda tukasema kwamba hawana viwango vya maadili . . . Lakini huenda ikafaa kusema kwamba walimu na washauri wao na jamii kwa ujumla haijawafundisha kusitawisha viwango vya maadili ambavyo wanapaswa kufuata.”
● Matendo ambayo hayapatani na viwango. Katika uchunguzi uliofanyiwa wanafunzi 30,000 hivi wa sekondari, asilimia 98 walisema kwamba wanaamini ni muhimu kuwa wanyoofu katika mahusiano. Hata hivyo, wanafunzi 8 kati ya 10 walikiri kwamba waliwadanganya wazazi wao, na 64 walikiri kwamba waliiba mtihani mwaka uliopita.
Kanuni Bora za Maadili
Kama ilivyotajwa katika sanduku lililo kwenye ukurasa huu, inaonekana kwamba wanadamu waliumbwa wakiwa na uwezo wa kuaminiana. Hata hivyo, Biblia inasema waziwazi kwamba “mwelekeo wa moyo wa mwanadamu ni mbaya tangu ujana wake na kuendelea.” (Mwanzo 8:21) Unaweza kupinga namna gani mwelekeo huo na kukataa ukosefu wa unyoofu ambao umeenea sana leo? Kanuni za Biblia zinazofuata zitakusaidia:
● “Usimtungie mwenzako jambo lolote baya, wakati anapokaa nawe na kujiona salama.”—Methali 3:29.
Kumpenda jirani yetu kutatuchochea tutangulize masilahi yake, na tusimtendee kwa hila kwa kuwa anatuamini. Kanuni hiyo inaweza kukomesha matendo mengi yanayochochewa na pupa kama vile kuuza madawa bandia, kama ilivyotajwa mwanzoni mwa habari hizi.
● “Ukweli hudumu milele, lakini uongo ni wa kitambo tu.”—Methali 12:19, “Biblia Habari Njema.”
Wengi leo wanaamini kwamba watu wanyoofu hawawezi kufanikiwa. Lakini hebu jiulize, ‘Ni jambo gani lililo la thamani zaidi—kupata thawabu sasa au kupata faida za muda mrefu, kutia ndani kujiheshimu?’ Mwanafunzi anaweza kuwadanganya wengine kuhusu ujuzi au ustadi wake kwa kuiba mtihani, lakini hali itakuwa namna gani anapoanza kufanya kazi?
● “Mwadilifu anatembea kwa utimilifu wake. Wanawe watakuwa na furaha baada yake.”—Methali 20:7.
Ikiwa wewe ni mzazi, wawekee watoto wako mfano mzuri kwa ‘kutembea kwa utimilifu.’ Waeleze jinsi ambavyo umefaidika kwa kuwa mnyoofu. Watoto wanapomwona mzazi akitembea kwa utimilifu, inaelekea watajitahidi kuwa watu wanaoaminika.—Methali 22:6.
Je, kanuni za Biblia zilizotajwa hapo juu zinafanya kazi? Je, kweli leo kuna watu wanaoweza kuaminiwa?
[Blabu katika ukurasa wa 4]
Gazeti Le Figaro, lilisema kwamba Wafaransa wengi “wanaamini kwamba watu mashuhuri—katika siasa, biashara, jamii, na utamaduni—si wanyoofu, na hivyo hawaoni kwa nini wao wanapaswa kuwa wanyoofu.”
[Sanduku katika ukurasa wa 5]
JE, TULIUMBWA TUAMINIANE?
Majaribio yaliyofanywa na Michael Kosfeld, profesa wa mambo ya biashara katika Chuo Kikuu cha Frankfurt, Ujerumani, yalimfanya akate kauli kwamba kuaminiana ni “sehemu ya utu wa mwanadamu.” Kosfeld aligundua kwamba watu wawili wanapowasiliana, ubongo wa mwanadamu hutokeza homoni inayoitwa oxytocin, ambayo huwachochea waaminiane. “Kwa kweli, hilo ni mojawapo ya mambo ya pekee katika wanadamu,” anasema Kosfeld. “Tunapoacha kuaminiana, tunapoteza sehemu muhimu ya utu wa mwanadamu.”
-
-
Watu Ambao Unaweza KuwaaminiAmkeni!—2010 | Oktoba
-
-
Watu Ambao Unaweza Kuwaamini
Santiago, dereva wa teksi huko Argentina, alijua alichopaswa kufanya. Mfuko fulani ulipoachwa ndani ya teksi yake, alimrudishia mwenyewe. Huenda tendo hilo la Santiago likaonekana kuwa jambo la kawaida tu, lakini mfuko huo ulikuwa na zaidi ya dola 32,000 za Marekani!
HEBU wazia ulimwengu uliojaa watu wanaoweza kuaminiwa. Hali zingekuwa tofauti kama nini! Ungeweza kumwachia yaya mtoto wako na usiwe na woga. Hungehitaji kufunga milango ya nyumba yako. Je, mambo hayo ni ndoto tu?
Matokeo ya Kufuata Viwango vya Maadili
Mtume Mkristo Paulo alisema hivi kujihusu na kuhusu Wakristo wenzake: “Tunataka kujiendesha kwa unyoofu katika mambo yote.” (Waebrania 13:18) Mashahidi wa Yehova hujitahidi kufanya hivyo. Lengo lao ni kuishi kupatana na sifa zinazotajwa katika Biblia kwenye Isaya 33:15: “Kuna yule anayetembea katika uadilifu wenye kuendelea na kusema jambo la unyoofu, anayekataa pato lisilo la haki kutoka kwa wapunjaji, anayetikisa mikono yake kabisa kukataa rushwa.” Wengine wamefuata njia hiyo ya unyoofu jinsi gani?
● ‘Sema jambo la unyoofu.’ Domingo ambaye ni Shahidi wa Yehova, hufanya kazi katika shamba la minazi huko Filipino. Anasema, “Watu wengi si wanyoofu kwa waajiri wao. Kwa mfano, wakivuna nazi, hawamwambii mwajiri wao wamevuna magunia mangapi. Kwa hiyo, wanauza magunia mengine kisiri.”
Domingo na familia yake karibu wafukuzwe kutoka kwenye shamba la minazi kwa sababu walikataa kusema uwongo kwa niaba ya mwajiri wao. Hata hivyo, Domingo anasema hivi: “Tulimwambia mwajiri wetu kwamba hatutasema uwongo hata kama hilo litafanya tufukuzwe. Mwishowe, mwajiri wetu alisema kwamba Mashahidi wa Yehova ni watu wazuri ambao wanaweza kuaminiwa, na akatupa shamba la ziada la kulima.”
● ‘Kataa pato lisilo la haki.’ Pierre, ambaye ni ofisa mkuu wa ushuru katika eneo moja huko Kamerun, amepata nafasi nyingi za kupata pesa kwa njia rahisi. Alipopewa mgawo wa kuwalipa mshahara wafanyakazi wa muda, aliona kasoro fulani. Pierre anaeleza: “Mishahara ilikuwa ikilipwa kwa watu ambao kandarasi zao ziliisha au walikuwa wamekufa. Badala ya kuchukua pesa hizo, niliandika majina hayo na kuweka pesa hizo vizuri.”
Matokeo yalikuwa nini? Pierre anasema: “Baada ya miaka miwili, mkaguzi wa hesabu alikuja. Nilifurahi kumpa rekodi zote na pesa nilizoweka, ambazo kufikia wakati huo zilikuwa kiasi kikubwa. Wakaguzi wa hesabu walinipongeza sana kwa unyoofu wangu.”
● ‘Kataa rushwa.’ Watu wengi wamejaribu kumhonga Ricardo, ambaye ni mthibitishaji wa hati za kisheria huko Rio de Janeiro, Brazili. Anasema hivi: “Pindi fulani, wakili mmoja alijaribu kunihonga. Alinitumia redio ya kuchezea CD. Wakati huo, redio ya aina hiyo iliuzwa kwa bei ya juu sana.”
Ricardo alifanya nini? Anasema: “Mimi na mke wangu tuliamua kuwa hatutafungua kifurushi hicho. Nilienda kwenye ofisi ya wakili huyo bila yeye kutarajia, na kuweka redio hiyo mezani. Nilipata nafasi nzuri ya kumweleza kwa nini singekubali zawadi hiyo. Karani wake alivutiwa sana na jambo hilo.”
Ingawa si Mashahidi wa Yehova peke yao ambao hujaribu kuwa wanyoofu, wakiwa kikundi wanajulikana kuwa watu wanyoofu. Jambo hilo lilifanya maduka fulani ya kuuza nguo huko Poland kuwaajiri Mashahidi wa Yehova peke yao. Meneja wao wa mauzo alisema hivi: “Kuna watu wanyoofu kila mahali, lakini Mashahidi wa Yehova wanaongozwa na kanuni, nao hushikamana nazo.”
Wanyoofu Licha ya Umaskini
Watu wengi hufikiri kwamba maskini ana sababu ya kutokuwa mnyoofu. Kwa mfano, ripoti moja ya Shirika la Habari la CNN ilitaja kisa cha mvulana mmoja mwenye umri wa miaka 14 kutoka Nigeria ambaye huwalaghai watu kupitia Intaneti. Anasema hivi kwa kujitetea: “Mnataka nifanye nini? Mimi ndiye hulisha familia yetu—dada yangu, mama yangu, [na baba] yangu. Lazima mtu atafute njia ya kuishi.”
Bila shaka, Biblia haiahidi kwamba wanyoofu watapata utajiri, lakini inawahakikishia kwamba watapata mahitaji yao ya lazima maishani. Isaya 33:16 inasema: “Hakika atapewa mkate wake; chemchemi yake ya maji haitaisha.”
Hata hivyo, huenda watu fulani wakauliza: ‘Kuwa mnyoofu kunaweza kunisaidia namna gani ninapopatwa na hali ngumu? Vipi wale ambao wanajitahidi juu chini ili wapate chakula cha kila siku?’
Mfikirie Berthe, mjane anayeishi Kamerun ambaye ana kibanda kidogo cha kuuza vipande vya mihogo vilivyowekwa vikolezo. Anasema: “Kwa kawaida, kuna vipande 20 vya mihogo katika kila pakiti. Wauzaji wengi huweka vipande 17 au 18, lakini mimi sipendi kupata faida kwa kuwadanganya wengine.”
Je, biashara ya Berthe inamletea faida? Si nyakati zote. Anasema: “Mara nyingi mimi hukaa siku nzima bila kuuza chochote. Lakini ninapowaambia wauzaji chakula kuwa sikuuza chochote na hivyo naomba chakula, wao hunipa kwa kuwa wanajua kwamba nitawalipa mara tu nitakapopata pesa. Wao huniamini kwa sababu nimekuwa mnyoofu sikuzote.”
Mungu Tunayepaswa Kumwamini
Sisi humwamini zaidi mtu anapotenda kulingana na maneno yake. Yoshua, aliyeliongoza taifa la Israeli la kale, alisema hivi kumhusu Mungu: ‘Hakuna ahadi hata moja iliyokosa kutimia katika ahadi zote nzuri ambazo Yehova alikuwa amewapa; mambo yote yalitimia.’ (Yoshua 21:45) Je, sisi pia tuna sababu nzuri za kumwamini Mungu?
Ahadi za Mungu zinategemeka sana hivi kwamba analinganisha neno lake na mvua. (Isaya 55:10, 11) Kwa kweli, ni nini kinachoweza kuzuia mvua isinyeshe, kulowesha udongo, na kufanya mimea ikue? Hakuna! Vivyo hivyo, hakuna kitu chochote kinachoweza kuzuia kutimizwa kwa ahadi za Mungu.
Mojawapo ya ahadi hizo inatajwa kwenye 2 Petro 3:13, ambayo inasema: “Kulingana na ahadi yake tunangojea mbingu mpya na dunia mpya, na humo uadilifu utakaa.” Mungu anakusudia kuwaharibu watu wote wanaowatumia wengine vibaya. Je, ungependa kujifunza jinsi ambavyo Mungu atatimiza kusudi lake? Wasiliana na Mashahidi wa Yehova wa eneo lenu, au waandikie barua ukitumia anwani inayofaa kati ya zile zilizoorodheshwa kwenye ukurasa wa 5 wa gazeti hili.
[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 8]
UNYOOFU WAKE WATHAWABISHWA
Lucio, ni Shahidi wa Yehova anayeishi huko Filipino. Pindi moja alipata nafasi ya kuiba. Alipata dola 27,500 za Marekani kwenye kabati moja katika ofisi aliyokuwa ameagizwa asafishe. Ofisi na pesa hizo zilikuwa za mwajiri wake ambaye alikuwa ameenda safari ya kibiashara. “Ilikuwa mara yangu ya kwanza kuona dola ya Marekani!” anasema Lucio.
Mwajiri wake aliporudi, Lucio alimpa pesa hizo. Matokeo yakawa nini? Lucio anasema: “Nilipandishwa cheo. Hata mwajiri wangu alinipa chumba ambacho ningeishi pamoja na familia yangu yote. Hata ingawa maisha ni magumu nchini Filipino, ninahisi kwamba kwa kuwa tumefuata sheria za Yehova Mungu, yeye ametutunza.”
[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 9]
MIZANI YA UNYOOFU
Kibanda cha Moïse kinajulikana sana katika soko moja huko Douala, Kamerun ambapo yeye huuza samaki. Anasema: “Nilikiita kibanda changu Mizani kwa sababu mizani ninayotumia ni moja kati ya mizani chache sana sahihi katika soko hilo lote. Ninajua kwamba watu hunijaribu kila wakati. Wakiagiza kilo moja ya samaki, mimi huwapa. Kisha wao huipeleka ikapimwe tena mahali pengine. Inapopimwa, wao huona ni kana kwamba uzani wake unazidi kilo moja! Wanajua kwamba sikuwadanganya! Watu wengi huniambia, ‘Sisi huja kwako kwa sababu wewe ni mnyoofu.’”
[Picha katika ukurasa wa 7]
“Tulimwambia mwajiri wetu kwamba hatutasema uwongo hata kama hilo litafanya tufukuzwe.”—Domingo, Filipino.
[Picha katika ukurasa wa 7]
“Wakaguzi wa hesabu walinipongeza sana kwa unyoofu wangu.”—Pierre, Kamerun.
[Picha katika ukurasa wa 7]
“Wakili mmoja alijaribu kunihonga. . . . Mimi na mke wangu tuliamua kuwa hatutafungua kifurushi hicho.”—Ricardo, Brazili.
[Picha katika ukurasa wa 7]
Mara nyingi Berthe hukaa siku nzima bila kuuza chochote. Lakini wauzaji chakula humpa chakula kwa kuwa wanajua kwamba atawalipa mara tu anapopata pesa.
-