Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Kumwiga Mungu wa Ukweli
    Mnara wa Mlinzi—2003 | Agosti 1
    • Watumishi wa Yehova Wanajua Ukweli

      5. Kulingana na nabii Danieli, ni nini kingetukia “wakati wa mwisho,” na unabii huo umetimizwaje?

      5 Katika ufafanuzi wake kuhusu “wakati wa mwisho,” nabii Danieli alitabiri jambo tofauti kabisa ambalo lingetukia miongoni mwa watu wa Mungu—kurudishwa kwa ukweli wa kidini. Aliandika hivi: “Wengi wataenda mbio huko na huko, na maarifa yataongezeka.” (Danieli 12:4) Watu wa Yehova hawatatanishwi au kupofushwa na yule Mdanganyifu mkuu. Wamepata ujuzi sahihi kwa kuenda huko na huko katika Biblia. Katika karne ya kwanza, Yesu aliwaelimisha wanafunzi wake. ‘Alifungua kabisa akili zao ili wafahamu maana ya Maandiko.’ (Luka 24:45) Yehova ametuelimisha pia katika siku zetu. Kupitia Neno lake, roho yake, na tengenezo lake, amewezesha mamilioni ya watu ulimwenguni pote kuelewa kile ambacho yeye tayari anakijua, yaani, ukweli.

      6. Watu wa Mungu leo wanaelewa kweli gani za Biblia?

      6 Tukiwa watu wa Mungu, tunaelewa mambo mengi ambayo hatungeweza kuelewa. Tunajua majibu ya maswali ambayo yamewasumbua watu wenye hekima ya kilimwengu kwa maelfu ya miaka. Kwa mfano, tunajua kwa nini watu wanateseka, wanakufa, na kwa nini wanadamu hawawezi kuleta amani na umoja ulimwenguni. Pia tuna pendeleo la kujua yale yatakayotukia wakati ujao—Ufalme wa Mungu, dunia paradiso, na uzima mkamilifu usio na mwisho. Tumemjua Yehova, Aliye Mkuu Zaidi. Tumejifunza kuhusu utu wake wenye kuvutia, na pia mambo tunayopaswa kufanya ili kupata baraka zake. Kujua ukweli hutuwezesha kutambua mambo yasiyo ya kweli. Kuishi kupatana na ukweli hutusaidia tuepuke kufuatia mambo yasiyo na faida, hutuwezesha kuishi maisha bora zaidi, na hutupa tumaini zuri la wakati ujao.

      7. Ni nani ambao wanaruhusiwa kuelewa kweli za Biblia, na ni nani wasioruhusiwa?

      7 Je, unaelewa ukweli wa Biblia? Ikiwa ndivyo, wewe umebarikiwa kwelikweli. Mtungaji anapoandika kitabu, kwa kawaida yeye hukiandika kwa njia itakayowavutia watu wa kikundi fulani hususa. Vitabu fulani huandikwa kwa ajili ya wale wenye elimu ya juu, vingine kwa ajili ya watoto, na vingine kwa ajili ya wataalamu katika nyanja mbalimbali. Ingawa Biblia hupatikana kwa urahisi kwa watu wote, ni watu wa kikundi fulani hususa ambao wamekusudiwa kuielewa na kuifurahia. Yehova aliitunga kwa ajili ya wanyenyekevu na wapole wa dunia. Watu hao wanaweza kuielewa Biblia bila kujali elimu, utamaduni, hadhi, au kabila lao. (1 Timotheo 2:3, 4) Kwa upande mwingine, wale wasio na mwelekeo unaofaa, hata wawe ni werevu au wawe na elimu ya juu kadiri gani, hawaruhusiwi kuelewa ukweli wa Biblia. Watu wenye majivuno na wenye kiburi hawawezi kuzielewa kweli zenye thamani za Neno la Mungu. (Mathayo 13:11-15; Luka 10:21; Matendo 13:48) Ni Mungu tu ambaye angeweza kutunga kitabu kama hicho.

  • Kumwiga Mungu wa Ukweli
    Mnara wa Mlinzi—2003 | Agosti 1
    • Watumishi wa Yehova Hufunua Ukweli

      14. Kwa nini watumishi wa Mungu hasa ndio wenye daraka kubwa la kutetea ukweli?

      14 Ni kweli kwamba huenda watu wengine wasio Mashahidi wa Yehova wakasema ukweli na kujaribu kuwa wanyofu. Lakini tukiwa Mashahidi wa Yehova, tuna jukumu kubwa la kutetea ukweli. Tumekabidhiwa kweli za Biblia—kweli ambazo zinaweza kumwongoza mtu kwenye uhai wa milele. Hivyo, tuna daraka la kuwaambia wengine ukweli huo. Yesu alisema kwamba “kila mtu ambaye alipewa mengi, mengi yatadaiwa kutoka kwake.” (Luka 12:48) Bila shaka, ‘mengi yanadaiwa’ kutoka kwa wale ambao wamebarikiwa kuwa na ujuzi wenye thamani wa Mungu.

      15. Unapata furaha gani unapowaeleza wengine ukweli wa Biblia?

      15 Tunapata furaha tunapowaeleza wengine ukweli wa Biblia. Kama vile wanafunzi wa Yesu wa karne ya kwanza, tunatangaza habari njema—ujumbe wa tumaini unaochangamsha moyo—kwa wale ‘waliochunwa ngozi na kutupwa huku na huku kama kondoo wasio na mchungaji’ na kwa wale waliopofushwa na kutatanishwa na “mafundisho ya roho waovu.” (Mathayo 9:36; 1 Timotheo 4:1) Mtume Yohana aliandika hivi: “Sina kisababishi cha shukrani kilicho kikubwa zaidi kuliko mambo haya, kwamba niwe nikisikia kwamba watoto wangu waendelea kutembea katika kweli.” (3 Yohana 4) Yohana alifurahi sana kwa sababu ya uaminifu wa “watoto” wake ambao labda ni watu aliowahubiria ukweli. Tunafurahi kuona watu wakikubali na kulithamini Neno la Mungu.

      16, 17. (a) Kwa nini si wote wanaokubali ukweli? (b) Unaweza kupata furaha gani unapotangaza ukweli wa Biblia?

      16 Ni kweli kwamba si wote watakaokubali ukweli. Yesu alisema ukweli kumhusu Mungu hata kama watu wengi hawakuupenda. Aliwaambia wapinzani wake Wayahudi hivi: “Kwa nini hamniamini? Yeye atokaye kwa Mungu husikiliza semi za Mungu. Hii ndiyo sababu hamsikilizi, kwa sababu nyinyi hamtoki kwa Mungu.”—Yohana 8:46, 47.

      17 Sisi, kama vile Yesu, hatusiti kuwaeleza wengine kweli zenye thamani kumhusu Yehova. Hatutazamii kila mtu akubali yale tunayomwambia, kwa kuwa si wote waliokubali yale ambayo Yesu alisema. Hata hivyo, tunafurahi kujua kwamba tunafanya lililo jema. Kwa sababu ya fadhili zake zenye upendo, Yehova anataka wanadamu wafunuliwe ukweli. Kwa kuwa Wakristo wana ukweli, wao ni wachukuaji-nuru katika ulimwengu wenye giza. Kwa kuacha nuru ya ukweli iangaze kupitia maneno na matendo yetu, tunaweza kuwasaidia wengine wampe utukufu Baba yetu wa mbinguni. (Mathayo 5:14, 16) Tunajulisha hadharani kwamba tunakataa kweli bandia ya Shetani na kulitetea Neno la Mungu lililo safi na lisiloghushiwa. Kweli tunayojua na kuwaeleza wengine inaweza kuwapa uhuru wale wanaoikubali.—Yohana 8:32.

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki