-
Wakristo Huabudu kwa Roho na KweliMnara wa Mlinzi—2002 | Julai 15
-
-
Wakristo Huabudu kwa Roho na Kweli
“Mungu ni Roho, na wale wanaomwabudu yeye lazima waabudu kwa roho na kweli.”—YOHANA 4:24.
1. Mungu hupendezwa na ibada ya aina gani?
YESU KRISTO, Mwana mzaliwa-pekee wa Yehova alionyesha waziwazi ibada ambayo inampendeza Baba yake wa mbinguni. Alipokuwa akimtolea ushahidi wenye kusisimua mwanamke mmoja Msamaria kwenye kisima kimoja karibu na jiji la Sikari, Yesu alisema: “Nyinyi mwaabudu kile msichojua; sisi twaabudu kile tujuacho, kwa sababu wokovu hutokana na Wayahudi. Hata hivyo, saa inakuja, nayo ipo sasa, wakati waabudu wa kweli watakapomwabudu Baba kwa roho na kweli, kwa maana, kwa kweli, Baba anawatafuta wa namna hiyo wamwabudu yeye. Mungu ni Roho, na wale wanaomwabudu yeye lazima waabudu kwa roho na kweli.” (Yohana 4:22-24) Maneno hayo yanamaanisha nini?
2. Ibada ya Wasamaria ilitegemea nini?
2 Wasamaria walikuwa na maoni ya kidini yasiyo ya kweli. Walikubali tu vitabu vitano vya kwanza vya Maandiko Matakatifu kuwa ndivyo vilivyoandikwa kwa mwongozo wa roho ya Mungu. Lakini walikubali tafsiri yao wenyewe ya vitabu hivyo, iliyoitwa Pentateuki ya Wasamaria. Ingawa Wasamaria hawakumjua Mungu, Wayahudi walikuwa wamefundishwa Maandiko. (Waroma 3:1, 2) Wayahudi waaminifu na watu wengineo wangeweza kupata kibali cha Yehova. Lakini walipaswa kufanya nini?
3. Ni nini kinachohitajiwa ili kumwabudu Mungu “kwa roho na kweli”?
3 Wayahudi, Wasamaria, na watu wengine walipaswa kufanya nini ili kumpendeza Yehova? Walipaswa kumwabudu “kwa roho na kweli.” Nasi tunapaswa kufanya hivyo. Ingawa tunapaswa kumtumikia Mungu kwa bidii na kuchochewa na moyo uliojaa upendo na imani, kumwabudu Mungu kwa roho hasa huhitaji tuwe na roho yake takatifu na kuiruhusu ituongoze. Kujifunza na kufuata Neno la Mungu kunapaswa kutusaidia kuwa na mtazamo kama wa Mungu. (1 Wakorintho 2:8-12) Ili Yehova akubali ibada yetu, ni lazima pia tumwabudu katika kweli. Lazima ibada hiyo ipatane na yale ambayo Neno la Mungu, Biblia, hufunua kumhusu na kuhusu makusudi yake.
Kweli Inaweza Kupatikana
4. Watu wengine huionaje kweli?
4 Watu fulani wanaojifunza falsafa wamekuwa na maoni kwamba wanadamu hawawezi kupata kweli kamili. Hata mwandishi Alf Ahlberg kutoka Sweden aliandika hivi: “Kuna maswali mengi ya kifalsafa ambayo hayawezi kujibiwa kikamili.” Ingawa wengine husema kwamba hakuna kweli inayoweza kutegemeka kabisa, je, ndivyo ilivyo? Yesu Kristo hakuwa na maoni hayo.
5. Kwa nini Yesu alikuja ulimwenguni?
5 Na tuwazie kwamba tunatazama tukio lifuatalo: Ni mapema mwaka wa 33 W.K., na Yesu amesimama mbele ya Gavana Mroma Pontio Pilato. Yesu anamwambia Pilato hivi: “Kwa ajili ya hili mimi nimezaliwa, na kwa ajili ya hili nimekuja kuingia ulimwenguni, ili nitoe ushahidi juu ya ile kweli.” Kisha Pilato anamwuliza hivi: “Kweli ni nini?” Lakini hangojei Yesu aeleze zaidi.—Yohana 18:36-38.
6. (a) “Kweli” imefafanuliwaje? (b) Yesu aliwapa wafuasi wake mgawo gani?
6 “Kweli” imefafanuliwa kuwa “kinyume cha uongo.” (Kamusi ya Kiswahili Sanifu) Hata hivyo, je, Yesu alitoa ushahidi juu ya kweli kwa ujumla? La. Yesu alikuwa anazungumzia kweli hususa. Aliwapa wafuasi wake mgawo wa kuitangaza kweli hiyo, kwa kuwa aliwaambia hivi: ‘Fanyeni wanafunzi kutoka kwa watu wa mataifa yote, kuwabatiza katika jina la Baba na la Mwana na la roho takatifu, kuwafundisha kushika mambo yote ambayo mimi nimewaamuru nyinyi.’ (Mathayo 28:19, 20) Kabla “ya umalizio wa mfumo wa mambo,” wafuasi wa kweli wa Yesu wangetangaza “kweli ya habari njema” duniani pote. (Mathayo 24:3; Wagalatia 2:14) Kwa kufanya hivyo wangetimiza maneno haya ya Yesu: “Habari njema hii ya ufalme itahubiriwa katika dunia yote inayokaliwa kwa ajili ya kuwa ushahidi kwa mataifa yote; na ndipo mwisho utakapokuja.” (Mathayo 24:14) Kwa hiyo, ni muhimu kuwatambua wale wanaofundisha mataifa ile kweli kwa kuhubiri habari njema ya Ufalme.
Jinsi Tunavyoweza Kujifunza Kweli
7. Unaweza kuthibitishaje kwamba Yehova ndiye Chanzo cha ile kweli?
7 Yehova ndiye Chanzo cha ile kweli ya kiroho. Hata mtunga-zaburi Daudi alimwita Yehova “Mungu wa kweli.” (Zaburi 31:5; 43:3) Yesu alikubali kwamba neno la Baba yake ni kweli, na pia akatangaza hivi: “Imeandikwa katika Manabii, ‘Na wote watafundishwa na Yehova.’ Kila mtu ambaye amesikia kutoka kwa Baba na ambaye amejifunza huja kwangu.” (Yohana 6:45; 17:17; Isaya 54:13) Hivyo basi, lazima wale wanaotafuta kweli wafundishwe na Yehova, yule Mfunzi Mtukufu. (Isaya 30:20, 21, NW) Wale wanaotafuta kweli wanahitaji “kumjua Mungu.” (Mithali 2:5) Na kwa upendo Yehova amefundisha au kutupatia kweli kwa njia mbalimbali.
8. Mungu amefundisha au kutupatia ile kweli kwa njia zipi?
8 Kwa mfano, Mungu aliwapa Waisraeli Sheria yake kupitia malaika. (Wagalatia 3:19) Kupitia ndoto, aliahidi kuwabariki wazee wa ukoo, Abrahamu na Yakobo. (Mwanzo 15:12-16; 28:10-19) Mungu hata alizungumza kutoka mbinguni, kama wakati wa ubatizo wa Yesu ambapo maneno haya yenye kusisimua yalisikiwa duniani: “Huyu ni Mwana wangu, mpendwa, ambaye nimemkubali.” (Mathayo 3:17) Tunaweza pia kushukuru kwamba Mungu ametupatia kweli yake kwa kutumia roho yake takatifu kuwaongoza waandikaji wa Biblia. (2 Timotheo 3:16, 17) Kwa kujifunza Neno la Mungu tunaweza kuwa na ‘imani katika kweli.’—2 Wathesalonike 2:13.
Kweli na Mwana wa Mungu
9. Mungu amemtumiaje Mwana wake ili kuifunua ile kweli?
9 Mungu ametumia hasa Mwana wake, Yesu Kristo kuwafunulia wanadamu ile kweli. (Waebrania 1:1-3) Kwa kweli, Yesu alifundisha kweli kwa njia isiyo na kifani. (Yohana 7:46) Hata baada ya kupaa mbinguni, alifunua kweli kutoka kwa Baba yake. Kwa mfano, mtume Yohana alipokea “ufunuo kupitia Yesu Kristo, ambao Mungu alimpa, kuonyesha watumwa wake mambo ambayo lazima yatukie upesi.”—Ufunuo 1:1-3.
10, 11. (a) Kweli ambayo Yesu alitoa ushahidi juu yake inahusiana na nini? (b) Yesu aliifanya kweli iwe halisi jinsi gani?
10 Yesu alimwambia Pontio Pilato kwamba Alikuja duniani kutoa ushahidi juu ya ile kweli. Wakati wa huduma yake, Yesu alifunua kwamba kweli hiyo ilihusiana na kutetewa kwa enzi kuu ya Yehova kupitia Ufalme wake chini ya Kristo akiwa Mfalme. Ili kutoa ushahidi juu ya ile kweli, Yesu alihitaji kufanya mengi zaidi ya kuhubiri na kufundisha. Yesu alifanya kweli hiyo iwe halisi kwa kuifuata katika maisha yake. Kwa hiyo, mtume Paulo aliandika: “Msiache mtu yeyote awahukumu nyinyi katika kula na kunywa au kwa habari ya msherehekeo au mwadhimisho wa mwezi mpya au wa sabato; kwa maana mambo haya ni kivuli cha mambo yajayo, bali uhalisi ni wa Kristo.”—Wakolosai 2:16, 17.
11 Kweli ilipata kuwa halisi Yesu alipozaliwa Bethlehemu kama ilivyokuwa imetabiriwa. (Mika 5:2; Luka 2:4-11) Kweli pia ilipata kuwa halisi wakati unabii wa Danieli kuhusu kutokea kwa Mesiya ulipotimizwa baada ya ‘majuma 69 ya miaka.’ Jambo hilo lilitukia Yesu alipojitoa kwa Mungu wakati wa ubatizo na kutiwa mafuta kwa roho takatifu mwaka wa 29 W.K., wakati barabara uliokuwa umetabiriwa. (Danieli 9:25; Luka 3:1, 21, 22) Kweli pia ilipata kuwa halisi kupitia huduma ya Yesu ya kuelimisha watu akiwa mtangazaji wa Ufalme. (Isaya 9:1, 2, 6, 7; 61:1, 2; Mathayo 4:13-17; Luka 4:18-21) Pia kweli ilipata kuwa halisi kupitia kifo na ufufuo wake.—Zaburi 16:8-11; Isaya 53:5, 8, 11, 12; Mathayo 20:28; Yohana 1:29; Matendo 2:25-31.
12. Kwa nini Yesu angeweza kusema, ‘Mimi ndiyo kweli’?
12 Kwa kuwa kweli ilikazia Yesu Kristo, yeye angeweza kusema hivi: “Mimi ndiyo njia na kweli na uhai. Hakuna ajaye kwa Baba ila kupitia mimi.” (Yohana 14:6) Watu huwekwa huru kiroho wanaposimama “upande wa ile kweli” kwa kukubali daraka la Yesu kuhusiana na kusudi la Mungu. (Yohana 8:32-36; 18:37) Watu wenye mfano wa kondoo watapata uhai udumuo milele kwa sababu wao huikubali kweli na humfuata Kristo kwa imani.—Yohana 10:24-28.
13. Tutachunguza kweli ya Kimaandiko katika maeneo gani matatu?
13 Kweli iliyofundishwa na Yesu na wanafunzi wake walioongozwa na roho ya Mungu, ndiyo hufanyiza mafundisho ya Wakristo wa kweli. Kwa hiyo, wale ‘walio watiifu kwa imani huendelea kutembea katika kweli.’ (Matendo 6:7; 3 Yohana 3, 4) Hivyo basi, ni nani wanaotembea katika kweli leo? Ni nani hasa wanaofundisha mataifa ile kweli? Ili kujibu maswali hayo, tutakazia fikira Wakristo wa mapema na kuchunguza kweli ya Kimaandiko kuhusiana na (1) imani, (2) njia ya kuabudu, na (3) mwenendo wa mtu binafsi.
Kweli na Imani
14, 15. Ungesema Wakristo wa mapema na Mashahidi wa Yehova wana maoni gani kuhusu Maandiko?
14 Wakristo wa mapema waliliheshimu sana Neno la Yehova lililoandikwa. (Yohana 17:17) Walilitumia kuamua ni imani na desturi gani zinazofaa na zisizofaa. Clement wa Alexandria aliyeishi katika karne ya pili na ya tatu alisema: “Wale wanaojitahidi kupata sifa bora hawataacha kuitafuta kweli hadi watakapothibitishiwa imani yao kupitia Maandiko.”
15 Kama Wakristo wa mapema, Mashahidi wa Yehova wanaiheshimu sana Biblia. Wanaamini kwamba “Andiko lote limepuliziwa na Mungu na ni lenye manufaa kwa kufundisha.” (2 Timotheo 3:16) Kwa hiyo, na tuchunguze mambo kadhaa ambayo Wakristo wa mapema waliamini na kuyalinganisha na yale ambayo watumishi wa Yehova wa siku hizi wamejifunza kwa sababu Biblia ndicho kitabu chao kikuu cha mafundisho.
Kweli Kuhusu Nafsi
16. Ukweli ni nini kuhusu nafsi?
16 Kwa kuwa waliyaamini Maandiko, Wakristo wa mapema walifundisha kweli kuhusu nafsi. Walijua kwamba ‘mtu alipata kuwa nafsi hai’ Mungu alipomwumba. (Mwanzo 2:7) Zaidi ya hayo, walijua kwamba nafsi ya mwanadamu hufa. (Ezekieli 18:4, ZSB; Yakobo 5:20) Pia walijua kwamba “wafu hawajui neno lo lote.”—Mhubiri 9:5, 10.
17. Unaweza kuelezaje tumaini la wafu?
17 Wanafunzi wa mapema wa Yesu walikuwa na tumaini hakika kwamba wafu walio katika kumbukumbu la Mungu watafufuliwa waishi tena. Imani yao ilidhihirishwa na Paulo aliyesema: “Nina tumaini kuelekea Mungu . . . kwamba kutakuwa na ufufuo wa waadilifu na wasio waadilifu pia.” (Matendo 24:15) Hata Minucius Felix, aliyedai kuwa Mkristo, aliandika hivi baadaye: ‘Ni nani ambaye ni mpumbavu au amekosa akili sana hivi kwamba angethubutu kudai kuwa Mungu ambaye alimwumba mwanadamu hawezi kumwumba tena upya?’ Kama Wakristo wa mapema, Mashahidi wa Yehova wanaamini kweli ya Maandiko kuhusu nafsi ya mwanadamu, kifo, na ufufuo. Hebu sasa tuchunguze Mungu ni nani na Kristo ni nani?
Kweli na Utatu
18, 19. Kwa nini tunaweza kusema kwamba Utatu si fundisho la Kimaandiko?
18 Wakristo wa mapema hawakuamini kwamba Mungu, Kristo, na roho takatifu ni Utatu. Kichapo The Encyclopædia Britannica kinasema: “Hakuna neno Utatu wala fundisho lililo wazi kuhusu Utatu katika Agano Jipya. Hata Yesu na wafuasi wake hawakutaka kupinga Shema [sala ya Waebrania] katika Agano la Kale inayosema: ‘Sikiliza, Ee Israeli; Bwana Mungu wetu ni Bwana mmoja’ (Kum. 6:4).” Wakristo hawakuabudu utatu wa Waroma au miungu mingine yoyote. Walikubali maneno ya Yesu kwamba Yehova peke yake ndiye anayepaswa kuabudiwa. (Mathayo 4:10) Zaidi ya hayo, waliamini maneno haya ya Kristo: “Baba ni mkubwa zaidi kuliko mimi.” (Yohana 14:28) Mashahidi wa Yehova wanaamini vivyo hivyo leo.
19 Wakristo wa mapema walijua vizuri tofauti kati ya Mungu, Kristo, na roho takatifu. Hata waliwabatiza wanafunzi (1) kwa jina la Baba, (2) kwa jina la Mwana, na (3) kwa jina la roho takatifu, bali si kwa jina la Utatu. Mashahidi wa Yehova pia hufundisha kweli hiyo ya Kimaandiko na hivyo wao huonyesha tofauti kati ya Mungu, Mwana wake, na roho takatifu.—Mathayo 28:19.
Kweli na Ubatizo
20. Wale wanaotaka kubatizwa wanahitaji kujua nini?
20 Yesu aliwapa wafuasi wake mgawo wa kuwafanya watu kuwa wanafunzi kwa kuwafundisha ile kweli. Ili wastahili kubatizwa, wanahitaji kuwa na ujuzi wa msingi wa Maandiko. Kwa mfano, ni lazima wajue cheo na mamlaka ya Baba na ya Mwana wake, Yesu Kristo. (Yohana 3:16) Wale wanaotaka kubatizwa wanahitaji kujua kwamba roho takatifu si mtu bali ni nguvu ya utendaji ya Mungu.—Matendo 2:1-4.
21, 22. Kwa nini unaweza kusema kwamba ubatizo ni wa wale wanaoamini?
21 Wakristo wa mapema walibatiza tu watu waliokuwa na ujuzi, waliotubu, na ambao walikuwa wamejiweka wakfu kwa Mungu bila masharti yoyote ili kufanya mapenzi yake. Wayahudi na wageuzwa imani ambao walikusanyika Yerusalemu kwenye Pentekoste 33 W.K., walijua Maandiko ya Kiebrania. Walipomsikia mtume Petro akizungumza kuhusu Mesiya, watu 3,000 hivi ‘walikubali neno lake kwa ukunjufu wa moyo’ na ‘kubatizwa.’—Matendo 2:41; 3:19–4:4; 10:34-38.
22 Ubatizo wa Kikristo ni wa wale wanaoamini. Watu wa Samaria walikubali kweli, na “walipomwamini Filipo, aliyekuwa akitangaza habari njema ya ufalme wa Mungu na juu ya jina la Yesu Kristo, waliendelea kubatizwa, wanaume na pia wanawake.” (Matendo 8:12) Akiwa mgeuzwa imani mwenye bidii na aliyemjua Yehova, towashi Mwethiopia kwanza alikubali maelezo ya Filipo kuhusu utimizo wa unabii wa Kimesiya, kisha akabatizwa. (Matendo 8:34-36) Baadaye, Petro alimwambia Kornelio na watu wengine wasio Wayahudi kwamba “mtu ambaye humhofu [Mungu] na kutenda uadilifu akubalika kwake” na kwamba kila mtu anayemwamini Yesu Kristo husamehewa dhambi. (Matendo 10:35, 43; 11:18) Mambo hayo yote yanapatana na amri ya Yesu ya ‘kufanya wanafunzi na kuwafundisha kushika mambo yote ambayo aliamuru.’ (Mathayo 28:19, 20; Matendo 1:8) Mashahidi wa Yehova hufanya vivyo hivyo, nao hukubali tu kubatiza watu ambao wana ujuzi wa msingi wa Maandiko na ambao wamejiweka wakfu kwa Mungu.
23, 24. Ubatizo wa Kikristo unaofaa ni gani?
23 Wanaoamini wanapaswa kubatizwa kwa kuzamishwa kabisa katika maji. Baada ya Yesu kubatizwa katika Mto Yordani, “alipanda kutoka majini.” (Marko 1:10) Yule towashi Mwethiopia alibatizwa katika “maji fulani.” Yeye na Filipo ‘waliteremka na kuingia katika maji’ kisha ‘wakapanda kutoka kwenye maji.’ (Matendo 8:36-40) Maandiko yanafananisha ubatizo na kuzikwa, jambo ambalo pia linaonyesha kuzamishwa kabisa katika maji.—Waroma 6:4-6; Wakolosai 2:12.
24 Kichapo The Oxford Companion to the Bible kinasema: ‘Maelezo katika Agano Jipya kuhusu ubatizo yanaonyesha kwamba mtu aliyebatizwa alichovywa ndani ya maji.’ Kitabu cha Kifaransa Larousse du XXe Siècle (Paris, 1928) kinasema kwamba, “Wakristo wa mapema walibatizwa kwa kuzamishwa mahali popote ambapo maji yalipatikana.” Nacho kitabu After Jesus—The Triumph of Christianity kinasema: ‘Kwa kawaida, yule anayetaka kubatizwa alipaswa kutangaza imani, kisha kuzamishwa kabisa katika maji katika jina la Yesu.’
25. Ni nini kitakachozungumziwa katika makala inayofuata?
25 Mambo yaliyotajwa kuhusu imani na desturi za Wakristo wa mapema ambazo zilitegemea Biblia ni mifano tu. Tunaweza kutaja mambo mengine ambayo Wakristo hao wa mapema waliamini ambayo Mashahidi wa Yehova wanaamini pia. Katika makala inayofuata, tutazungumzia njia nyingine za kuwatambua wale wanaofundisha watu ile kweli.
-
-
Wanaendelea Kutembea Katika KweliMnara wa Mlinzi—2002 | Julai 15
-
-
Wanaendelea Kutembea Katika Kweli
“Sina kisababishi cha shukrani kilicho kikubwa zaidi kuliko mambo haya, kwamba niwe nikisikia kwamba watoto wangu waendelea kutembea katika kweli.”—3 YOHANA 4.
1. “Kweli ya habari njema” hukazia nini?
YEHOVA huwakubali tu wale wanaomwabudu “kwa roho na kweli.” (Yohana 4:24) Wao hutii kweli na kukubali mafundisho yote ya Kikristo yanayotokana na Neno la Mungu. ‘Kweli hii ya habari njema’ hukazia Yesu Kristo na kutetewa kwa enzi kuu ya Yehova kupitia Ufalme. (Wagalatia 2:14) Mungu huruhusu “utendaji wa kosa” uwaendee wale wanaopendelea uwongo, lakini wokovu unategemea kuwa na imani katika habari njema na kutembea katika kweli.—2 Wathesalonike 2:9-12; Waefeso 1:13, 14.
2. Mtume Yohana alikuwa mwenye shukrani kwa mambo gani hasa, naye alikuwa na uhusiano gani pamoja na Gayo?
2 Watangazaji wa Ufalme ni “wafanyakazi wenzi katika kweli.” Kama mtume Yohana na rafikiye Gayo, wao hufuata kweli bila kuyumbayumba na hutembea katika kweli. Huku akimfikiria Gayo, Yohana aliandika: “Sina kisababishi cha shukrani kilicho kikubwa zaidi kuliko mambo haya, kwamba niwe nikisikia kwamba watoto wangu waendelea kutembea katika kweli.” (3 Yohana 3-8) Hata ingawa Yohana hakumfundisha Gayo kweli, mwanamume huyo, ambaye yaonekana alikuwa na umri mdogo, alifaa kuitwa mtoto wa kiroho wa Yohana. Hiyo ni kwa sababu mtume huyo alikuwa mzee kwa umri na alikuwa Mkristo mkomavu mwenye upendo kama wa baba.
Kweli na Ibada ya Kikristo
3. Mikutano iliyofanywa na Wakristo wa mapema ilikuwa na kusudi na manufaa gani?
3 Ili kujifunza kweli, Wakristo wa mapema walikutana pamoja wakiwa kutaniko. Mara nyingi walikutana katika nyumba za watu. (Waroma 16:3-5) Kwa hiyo, walitiana moyo na kuchocheana kwenye upendo na kazi zilizo bora. (Waebrania 10:24, 25) Kuhusu wale waliodai kuwa Wakristo nyakati za baadaye, Tertullian (wapata mwaka wa 155 W.K.–baada ya mwaka wa 220 W.K.) aliandika hivi: “Tunakutana ili kusoma vitabu vya Mungu . . . Kwa maneno hayo matakatifu tunajenga imani yetu, tunakuza tumaini letu, na kuimarisha uhakika wetu.”—Apology, sura ya 39.
4. Kuimba kumetimiza fungu gani katika mikutano ya Kikristo?
4 Yaelekea Wakristo wa mapema waliimba kwenye mikutano. (Waefeso 5:19; Wakolosai 3:16) Profesa Henry Chadwick aandika kwamba Celsus, mchambuzi mmoja wa karne ya pili, aligundua kwamba nyimbo tamu zilizoimbwa na wale waliodai kuwa Wakristo ‘zilikuwa nzuri sana hivi kwamba alichukizwa na jinsi zilivyovutia hisia za watu.’ Naye Chadwick anaongeza kusema: “Clement wa Alexandria, ndiye mwandikaji Mkristo wa mapema zaidi kuandika kuhusu aina ya muziki unaofaa kwa Wakristo. Anasema kwamba muziki huo haupaswi kuhusisha dansi yenye kuchochea hisia za kingono.” (The Early Church, ukurasa wa 274-275) Inaonekana wazi kwamba Wakristo wa mapema waliimba walipokutana pamoja. Vivyo hivyo Mashahidi wa Yehova huimba nyimbo zilizotungwa kutoka kwa Biblia, ambazo zina maneno yenye nguvu ya kumtukuza Mungu na Ufalme.
5. (a) Mwongozo wa kiroho ulitolewaje katika makutaniko ya Wakristo wa mapema? (b) Wakristo wa kweli wamefuataje maneno ya Yesu kwenye Mathayo 23:8, 9?
5 Katika makutaniko ya Wakristo wa mapema, wazee walifundisha kweli, nao watumishi wa huduma waliwasaidia waamini wenzao katika njia mbalimbali. (Wafilipi 1:1) Baraza linaloongoza ambalo lilitegemea Neno la Mungu na roho takatifu liliandaa mwongozo wa kiroho. (Matendo 15:6, 23-31) Hakukuwa na vyeo vya kidini kwa kuwa Yesu aliamuru wanafunzi wake hivi: “Msiitwe Rabi, kwa maana mmoja ni mwalimu wenu, lakini nyinyi nyote ni akina ndugu. Zaidi ya hayo, msiite yeyote baba yenu duniani, kwa maana mmoja ni Baba yenu, Aliye wa kimbingu.” (Mathayo 23:8, 9) Katika njia hiyo na njia nyingine mbalimbali, kuna ufanani kati ya Wakristo wa mapema na Mashahidi wa Yehova.
Wanyanyaswa kwa Kuhubiri Kweli
6, 7. Ingawa wanatangaza ujumbe wa amani, Wakristo wa kweli wametendewaje?
6 Ingawa walitangaza ujumbe wa amani wa Ufalme, Wakristo wa mapema walinyanyaswa kama Yesu alivyonyanyaswa. (Yohana 15:20; 17:14) Mwanahistoria John L. von Mosheim alisema kwamba Wakristo wa karne ya kwanza walikuwa ‘kikundi cha watu ambao hawakuwa hatari kwa watu wengine. Hawakuwa na uadui kuelekea serikali.’ Dakt. Mosheim alisema kwamba “Wakristo waliwakasirisha Waroma kwa sababu ya ibada yao sahili, ambayo haikufanana hata kidogo na sherehe takatifu za ibada za watu wengine.” Aliendelea kusema hivi: ‘Hawakutoa dhabihu wala hawakuwa na mahekalu, sanamu, watabiri, wala makasisi. Mambo hayo yalifanya watu wasiojua ukweli wa mambo wawashutumu kwa kuwa walifikiri kwamba hakuna dini isiyokuwa na sherehe takatifu za ibada. Hivyo Wakristo hao walionwa kuwa waatheisti, yaani, watu wasioamini kuna Mungu; na kulingana na sheria za Waroma, waatheisti walionwa kuwa watu waliosumbua jamii.’
7 Makasisi, wasanii, na watu wengineo ambao walipata riziki yao kutokana na ibada ya sanamu walichochea watu dhidi ya Wakristo ambao hawakuabudu sanamu. (Matendo 19:23-40; 1 Wakorintho 10:14) Tertullian aliandika hivi: “Wao huamini kwamba Wakristo ndio husababisha kila jambo baya linalowapata watu. Ikiwa maji ya Mto Tiber yanafurika na kufikia kuta za jiji lao, ikiwa maji ya Mto Nile si mengi kuweza kunyunyizia mashamba, ikiwa hakunyeshi, au ikiwa kuna tetemeko la ardhi, njaa, au msiba, mara moja watu hupaaza sauti: ‘Watupeni Wakristo kwa simba!’” Hata wapatwe na nini, Wakristo wa kweli ‘hujilinda wenyewe na sanamu.’—1 Yohana 5:21.
Kweli na Maadhimisho ya Kidini
8. Kwa nini wale wanaotembea katika kweli hawasherehekei Krismasi?
8 Wale wanaotembea katika kweli huepuka maadhimisho yasiyo ya Kimaandiko kwa sababu ‘nuru haina ushiriki na giza.’ (2 Wakorintho 6:14-18) Kwa mfano, hawasherehekei Krismasi, sherehe inayofanywa Desemba 25. “Hakuna mtu anayejua tarehe kamili ya kuzaliwa kwa Kristo,” kinasema kichapo The World Book Encyclopedia. Kichapo The Encyclopedia Americana (Chapa ya 1956) kinasema: ‘Desturi nyingi za kujifurahisha zinazofuatwa wakati wa Krismasi zinatokana na Saturnalia, sherehe ya Waroma iliyofanywa katikati ya mwezi wa Desemba.’ Ensaiklopedia ya M’Clintock na Strong inasema: ‘Mwadhimisho wa Krismasi haukuagizwa na Mungu, wala hautokani na Agano Jipya.’ Nacho kitabu Daily Life in the Time of Jesus kinasema: ‘Wakati wa baridi kali, makundi ya kondoo hayakutoka nje; na jambo hilo peke yake linatuonyesha kwamba haielekei kwamba tarehe iliyowekwa ya kusherehekea Krismasi wakati wa baridi kali, ni ya kweli, kwa kuwa kitabu cha Injili kinasema kwamba wachungaji walikuwa nje.’—Luka 2:8-11.
9. Kwa nini watumishi wa Yehova wa zamani na wa siku hizi hawasherehekei Ista?
9 Inasemekana kwamba Ista ni sikukuu ya kukumbuka kufufuka kwa Kristo, lakini vitabu vyenye kutegemeka vinaihusianisha na ibada isiyo ya kweli. Kamusi The Westminster Dictionary of the Bible inasema kwamba “mwanzoni Ista ilikuwa sherehe ya kumtukuza Teutonic, mungu wa kike wa Wajerumani aliyeaminika kuleta nuru na majira ya mvua nyingi. Wajerumani walioitawala Uingereza zamani walimwita Eastre,” au Eostre. Vyovyote vile, kichapo Encyclopædia Britannica (Chapa ya 11) kinasema: “Agano Jipya halitaji lolote kuhusu kuadhimishwa kwa sikukuu ya Ista.” Wakristo wa mapema hawakusherehekea Ista wala haisherehekewi na watu wa Yehova leo.
10. Ni mwadhimisho gani ambao Yesu alianzisha, na ni nani wanaouadhimisha ifaavyo?
10 Yesu hakuwaamuru wafuasi wake waadhimishe kuzaliwa kwake wala kufufuka kwake, lakini alianzisha Ukumbusho wa kifo chake cha kidhabihu. (Waroma 5:8) Kwa kweli, hili ndilo tukio pekee ambalo aliwaamuru wanafunzi wake waadhimishe. (Luka 22:19, 20) Mashahidi wa Yehova bado huadhimisha mwadhimisho huo wa kila mwaka, ambao pia unaitwa Mlo wa Jioni wa Bwana.—1 Wakorintho 11:20-26.
Kweli Yatangazwa Ulimwenguni Pote
11, 12. Wale wanaotembea katika kweli hutegemezaje kazi yao ya kuhubiri?
11 Wale wanaoijua kweli huona kuwa ni pendeleo kutumia wakati wao, nguvu, na rasilimali zao nyingine katika kazi ya kuhubiri habari njema. (Marko 13:10) Kazi ya kuhubiri ya Wakristo wa mapema ilitegemezwa kwa michango ya hiari. (2 Wakorintho 8:12; 9:7) Tertullian aliandika: “Hata ikiwa kuna kisanduku cha michango, michango hiyo haitokani na pesa ambazo zinalipwa mlangoni ili kuingia, kana kwamba dini ni biashara. Kila mtu huleta kiasi kidogo cha pesa mara moja kila mwezi—au wakati wowote anaotaka, na ikiwa tu anataka na anaweza; kwa kuwa hakuna anayelazimishwa; ni utoaji wa hiari.”—Apology, sura ya 39.
12 Kazi ya kuhubiri Ufalme ambayo Mashahidi wa Yehova hufanya ulimwenguni pote hutegemezwa pia kwa michango ya hiari. Mashahidi na pia watu wanaopendezwa na wenye shukrani huliona kuwa pendeleo kutegemeza kazi hii kwa michango yao. Katika jambo hilo pia, kuna ufanani kati ya Wakristo wa mapema na Mashahidi wa Yehova.
Kweli na Mwenendo Wako
13. Kuhusiana na mwenendo, Petro alitoa ushauri gani ambao Mashahidi wa Yehova hufuata?
13 Wakristo wa mapema walitembea katika kweli nao walifuata ushauri huu wa mtume Petro: “Dumisheni mwenendo wenu ukiwa bora miongoni mwa mataifa, ili, katika jambo ambalo katika hilo wao wanasema dhidi yenu kuwa watenda-maovu, likiwa tokeo la kazi zenu bora ambazo wamekuwa mashahidi wa kujionea wapate kumtukuza Mungu katika siku ya ukaguzi wake.” (1 Petro 2:12) Mashahidi wa Yehova huchukua kwa uzito maneno hayo.
14. Wakristo wana maoni gani kuhusu vitumbuizo visivyo vya adili?
14 Hata baada ya uasi-imani kuenea, watu waliokuwa Wakristo kwa jina tu waliepuka vitendo vya ukosefu wa maadili. W. D. Killen, profesa wa historia ya makanisa ya Kikristo, aliandika hivi: ‘Katika karne ya pili na ya tatu, watu walipenda sana kwenda katika majumba ya michezo ya kuigiza yaliyokuwa katika kila mji mkubwa; na ingawa kwa ujumla waigizaji walikuwa watu wenye maadili mabaya sana, maonyesho yao yenye kuchochea hisia yaliendelea kutimiza tamaa zilizopotoka za watu wa kizazi hicho. Wakristo wote wa kweli walichukia maonyesho hayo. . . . Walichukia sana mambo ya aibu yaliyofanywa huko; na waliona maombi yaliyofanywa daima kwa miungu ya kipagani, ya kiume na ya kike kuwa kinyume kabisa na imani yao.’ (The Ancient Church, ukurasa wa 318-319) Leo wafuasi wa kweli wa Yesu pia huepuka vitumbuizo vyenye aibu, vinavyoshusha maadili.—Waefeso 5:3-5.
Kweli na “Mamlaka Zilizo Kubwa”
15, 16. “Mamlaka zilizo kubwa” ni nani, nao wanaotembea katika kweli huwaonaje?
15 Ingawa Wakristo wa mapema walikuwa na mwenendo mzuri, wafalme fulani Waroma waliwaelewa vibaya. Mwanahistoria E. G. Hardy anasema kwamba wafalme hao waliwaona kuwa “watu wa kudharauliwa kwa sababu walishikilia sana dini.” Barua ambazo Gavana Pliny the Younger wa Bithinia na Mfalme Trajan waliandikiana, zinaonyesha kwamba, kwa ujumla watawala hawakuujua Ukristo vizuri. Wakristo wana maoni gani kuhusu Serikali?
16 Kama wafuasi wa mapema wa Yesu, Mashahidi wa Yehova hujitiisha kwa kadiri fulani kwa “mamlaka zilizo kubwa” za kiserikali. (Waroma 13:1-7) Ikiwa matakwa ya wanadamu yanapingana na ya Mungu, wao huchukua msimamo huu: “Lazima sisi tumtii Mungu kuwa mtawala kuliko wanadamu.” (Matendo 5:29) Kitabu After Jesus—The Triumph of Christianity kinasema: ‘Ingawa Wakristo hawakuabudu mfalme, wao hawakuchochea watu wafanye fujo, nayo dini yao haikuwa hatari kwa ufalme ingawa wapagani waliiona kuwa tofauti na nyakati nyingine yenye kuchukiza.’
17. (a) Wakristo wa mapema walitetea serikali gani? (b) Wafuasi wa kweli wa Kristo wamefuataje andiko la Isaya 2:4 katika maisha yao?
17 Wakristo wa mapema walitetea Ufalme wa Mungu, kama vile wazee wa ukoo Abrahamu, Isaka, na Yakobo walivyoonyesha imani katika ‘jiji lililoahidiwa ambalo limefanywa na Mungu.’ (Waebrania 11:8-10) Kama Bwana-Mkubwa wao, wanafunzi wa Yesu ‘hawakuwa sehemu ya ulimwengu.’ (Yohana 17:14-16) Na kuhusiana na vita na ugomvi, wao walifuatia amani kwa ‘kufua panga zao kuwa majembe.’ (Isaya 2:4) Geoffrey F. Nuttall, mwalimu wa historia ya kanisa, alisema hivi kuhusu ufanani huu wenye kutokeza: ‘Mtazamo wa Wakristo wa mapema kuelekea vita ulikuwa kama wa watu ambao hujiita Mashahidi wa Yehova, na ingawa jambo hilo ni kweli, sisi hulikubali shingo upande.’
18. Kwa nini hakuna haja kwa serikali yoyote kuwaogopa Mashahidi wa Yehova?
18 Kwa kuwa Wakristo wa mapema walichukua msimamo wa kutokuwamo na walijitiisha kwa “mamlaka zilizo kubwa,” wao hawakuwa tisho kwa serikali yoyote, na ndivyo ilivyo na Mashahidi wa Yehova. ‘Mtu aliye na ubaguzi na mwenye kutia shaka ndiye tu anayeweza kuamini kwamba Mashahidi wa Yehova ni tisho kwa serikali yoyote,’ akaandika mhariri mmoja kutoka Amerika ya Kaskazini. ‘Wao wanapenda amani kama vile kikundi cha kidini kinavyotazamiwa kuwa, na hawajaribu kupindua serikali.’ Serikali zinazowafahamu vizuri zinajua kwamba hakuna haja ya kuwaogopa Mashahidi wa Yehova.
19. Tunaweza kusema nini kuhusu Wakristo wa mapema na Mashahidi wa Yehova kuhusu kulipa kodi?
19 Njia moja ambayo Wakristo wa mapema waliheshimu “mamlaka zilizo kubwa” ni kwa kulipa kodi. Alipomwandikia Antoninus Pius, Mtawala Mroma (138-161 W.K.), Justin Martyr alisema kwamba Wakristo walilipa kodi zao ‘kwa utayari zaidi kuliko watu wengine wote.’ (First Apology, sura ya 17) Naye Tertullian aliwaambia watawala Waroma kwamba wakusanya-kodi wao ‘walistahili kuwashukuru Wakristo’ kwa kuwa walilipa kodi zao kwa kuongozwa na dhamiri. (Apology, sura ya 42) Wakristo walinufaika wakati wa Pax Romana, au Amani ya Roma, kwa kuwa kulikuwa na sheria na utengamano, barabara nzuri, na usafiri wa baharini ambao kwa kadiri fulani ulikuwa salama. Kwa kuwa walitambua kwamba walikuwa na deni kwa jamii, walitii maneno haya ya Yesu: “Mlipeni Kaisari vitu vya Kaisari, lakini mlipeni Mungu vitu vya Mungu.” (Marko 12:17) Watu wa Yehova leo hufuata ushauri huo, nao wamepongezwa kwa unyofu wao, kama katika kulipa kodi.—Waebrania 13:18.
Kweli Ni Kifungo cha Muungano
20, 21. Kuhusiana na udugu wenye amani, kuna ufanani gani kati ya Wakristo wa mapema na watumishi wa Yehova leo?
20 Kwa sababu walitembea katika kweli, Wakristo wa mapema waliunganishwa katika udugu wenye amani, kama vile Mashahidi wa Yehova leo. (Matendo 10:34, 35) Barua moja iliyochapwa katika gazeti The Moscow Times inasema: ‘Mashahidi wa Yehova wanajulikana sana kuwa watu wema, wenye fadhili, na wanyenyekevu. Ni rahisi sana kushughulika nao. Wao hawalazimishi wengine kufanya mambo, na siku zote hujaribu kudumisha uhusiano wenye amani pamoja na wengine. Hawachukui hongo, wala hawalewi wala kutumia dawa za kulevya na ni rahisi kuelewa ni kwa nini hawafanyi hivyo: Katika yote wafanyayo, wao hujaribu kufuata imani yao inayotegemea Biblia. Kama watu wote ulimwenguni wangejaribu kufuata Biblia maishani mwao kama vile Mashahidi wa Yehova, ulimwengu wetu mkatili ungekuwa tofauti kabisa.’
21 Kichapo Encyclopedia of Early Christianity kinasema: ‘Washiriki wa kanisa la mapema walijiona kuwa jamii yenye uelewevu mpya, na Wayahudi na watu wasio Wayahudi ambao hapo awali walikuwa maadui wangeweza kuishi katika jamii hii kwa amani.’ Mashahidi wa Yehova pia ni udugu wa ulimwenguni pote wenye kupenda amani—kwa kweli jamii ya ulimwengu mpya. (Waefeso 2:11-18; 1 Petro 5:9; 2 Petro 3:13) Wakati ofisa mkuu wa usalama kwenye uwanja wa maonyesho wa Pretoria, huko Afrika Kusini, alipoona jinsi Mashahidi wa jamii zote walivyofanya kusanyiko lao kwa amani, alisema hivi: ‘Katika siku hizi chache zilizopita, kila mtu alikuwa mwenye adabu, watu walisemezana vizuri, na walionyesha mtazamo mzuri. Mambo hayo yathibitisha kwamba watu wenu wana maadili bora, na kwamba wote wanaishi pamoja kama familia moja yenye furaha.’
Wabarikiwa kwa Kufundisha Kweli
22. Ni nini ambacho kimetukia kwa sababu Wakristo wamefanya kweli iwe dhahiri?
22 Paulo na Wakristo wengine ‘walifanya kweli iwe dhahiri’ kupitia mwenendo wao na kazi ya kuhubiri. (2 Wakorintho 4:2) Je, hukubali kwamba Mashahidi wa Yehova wanafanya vivyo hivyo na wanafundisha mataifa yote ile kweli? Watu kotekote duniani wanaikubali ibada ya kweli na wanaendelea kumiminika kwa wingi kwenye “mlima wa nyumba ya BWANA.” (Isaya 2:2, 3) Kila mwaka, maelfu hubatizwa ili kuonyesha wakfu wao kwa Mungu na hivyo makutaniko mengi huanzishwa.
23. Una maoni gani kuhusu wale wanaofundisha mataifa yote ile kweli?
23 Ingawa Mashahidi wa Yehova wana malezi mbalimbali, wao wana umoja katika ibada ya kweli. Upendo wanaoonyesha huwatambulisha kuwa wanafunzi wa Yesu. (Yohana 13:35) Je, unaweza kuona kwamba ‘Mungu kwa kweli yumo miongoni mwao’? (1 Wakorintho 14:25) Je, umejiunga na wale wanaofundisha mataifa yote ile kweli? Ikiwa ndivyo, na uwe mwenye shukrani daima kwa ajili ya kweli na upate pendeleo la kutembea katika kweli hiyo milele.
-