-
Tahiti2005 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
-
-
Kati ya wahubiri wa kwanza wa Ufalme kutoa ushahidi kikamili huko Polinesia ya Ufaransa ni Jean-Marie na Jeanne Félix, mume na mke waliojifunza kweli huko Algeria, ambayo wakati huo ilikuwa koloni la Ufaransa. Walibatizwa mwaka wa 1953. Mwaka wa 1955, wahubiri wa Ufalme walitiwa moyo wahamie maeneo yaliyokuwa na uhitaji mkubwa wa wahubiri. Polinesia ya Ufaransa ilikuwa mojawapo ya maeneo hayo. Ndugu na Dada Félix na mwana wao mchanga, Jean-Marc, waliitikia mwito huo, nao wakahamia Tahiti mwaka wa 1956. Lakini, Jean-Marie, aliyekuwa injinia, hakuweza kupata kazi kisiwani Tahiti. Hivyo, wakahamia Makatéa, kimojawapo cha Visiwa vya Tuamotu vilivyo umbali wa kilometa 230 upande wa kaskazini-mashariki wa Tahiti, ambako Jean-Marie alipata kazi katika kampuni ya fosfati.
Mara moja, Ndugu na Dada Félix walianza kuwahubiria majirani na watu waliofanya kazi pamoja na Jean-Marie. Jeanne anaandika hivi: “Wenyeji wa kisiwa hicho waliiheshimu sana Biblia, wakasikiliza ujumbe wa Ufalme kwa makini, na kujifunza Biblia kwa bidii. Jambo hilo lilitutia moyo. Hata hivyo, makasisi wa eneo hilo walitupinga sana. Hata waliwaonya wafuasi wao wajihadhari na ‘manabii wa uwongo’ walio katikati yao, na wasiongee nasi au hata kupita karibu na nyumba yetu!”
Lakini baada ya muda, watu walio wengi walibadili maoni yao kuwahusu Wakristo hao. Wakaaji wengi wa visiwa hivyo hata walipata kuwaheshimu sana Jean-Marie na Jeanne kwa sababu hawakuwadharau Wapolinesia, kama Wazungu wengine kwenye kisiwa cha Makatéa.
Hata hivyo, walihitaji ujasiri ili waendelee na kazi ya kuhubiri, kwa sababu mkurugenzi wa ile kampuni ya fosfati alikuwa na uwezo wa kumfuta kazi mfanyakazi yeyote wakati wowote. Isitoshe, nyakati nyingine wale polisi wawili wa kisiwa hicho waliwatembelea Jean-Marie na Jeanne, na kuwahoji kuhusu kazi yao ya kuhubiri. Pole kwa pole, polisi hao Wafaransa walitambua kwamba Jean-Marie na Jeanne hawakuwa watu hatari. Hata wakawa wenye urafiki.
Mpolinesia Maui Piirai, aliyefanya kazi na Jean-Marie, ndiye mwanafunzi wa kwanza wa Biblia kufanya maendeleo ya kiroho. Kweli ilipoingia moyoni mwake, Maui alifanya mabadiliko makubwa maishani mwake. Kwa mfano, aliacha ulevi na kuvuta sigara, naye akamwoa mwanamke aliyekuwa ameishi naye kwa miaka 15. Maui aliyebatizwa Oktoba 1958, ndiye Mpolinesia wa kwanza katika eneo hilo kujiweka wakfu kwa Yehova. Yeye pia alianza kuhubiri habari njema, jambo ambalo liliwakasirisha makasisi. Kasisi mmoja hata alipanga njama ili Maui afutwe kazi. Lakini njama hiyo ilishindwa kwa sababu Maui alikuwa mfanyakazi mwenye bidii na mwenye sifa nzuri.
Mwanamke aitwaye Germaine Amaru ndiye mtu wa pili kisiwani Makatéa kukubali Neno la Mungu. Germaine alikuwa mkuu wa shule na alihubiriwa kwa mara ya kwanza na mmoja wa wanafunzi wake, Jean-Marc, mwana wa Ndugu na Dada Félix. Ingawa Jean-Marc alikuwa na umri wa miaka saba tu, mwalimu wake alivutiwa sana na ujuzi wake wa Biblia hivi kwamba aliwapigia wazazi wake simu. Wazazi hao wakaanza kumfundisha mwalimu huyo Biblia. Lakini mambo hayakuishia hapo kwa kuwa Germaine naye alimsaidia mwalimu mwenzake anayeitwa Monique Sage, na mumewe Roger, kumjua Yehova.
Ndugu na Dada Félix na Maui Piirai walianza pia kujifunza na Manuari Tefaatau, aliyekuwa shemasi kijana katika kanisa la Kiprotestanti la Makatéa, na vilevile pamoja na rafiki yake, anayeitwa Arai Terii. Mwanzoni, watu hao wawili waliendelea kwenda katika kanisa lao na kuwahubiria waamini wenzao kweli za Maandiko kuhusu Utatu, moto wa mateso, kutoweza kufa kwa nafsi, na mafundisho mengineyo. Jambo hilo lilisababisha mgogoro miongoni mwa wafuasi wa kanisa la Kiprotestanti. Hata hivyo, kama watu wa mji wa Beroya wa kale, wengi wenye mioyo minyoofu walichunguza Biblia zao ili kuona kama mambo waliyokuwa wakiyasikia yalikuwa ya kweli.—Mdo. 17:10-12.
Bila shaka kasisi wa kanisa hilo alikasirika. Hata alitisha kumfukuza kanisani mtu yeyote aliyeendelea kuwasikiliza Mashahidi. Baadhi yao waliacha kusikiliza kwa sababu ya woga, lakini wengine wakafanya maendeleo ya kiroho na kuliacha kanisa. Miongoni mwa wale walioacha kanisa ni Manuari na Arai, Moea, mke wa Maui Piirai, na Taina Rataro, anayetajwa baadaye katika masimulizi haya.
Mwanzoni, wahubiri na wanafunzi wa Biblia, ambao waliendelea kuongezeka, walifanya mikutano nyumbani kwa Ndugu na Dada Félix, ambako Jean-Marie alitoa hotuba katika Kifaransa na Maui akafasiri katika Kitahiti. Familia ya Félix ilipohama Makatéa mwaka wa 1959, mikutano ilifanywa nyumbani kwa Maui, ambaye wakati huo alikuwa amebatizwa. Jean-Marie na Jeanne walionaje utumishi wao katika visiwa hivyo? Jeanne, ambaye sasa ni mjane anayeishi nchini Italia, anatoa maoni yake mwenyewe na ya mumewe aliyekufa anaposema: “Hatukujuta hata kidogo. Huduma yetu katika kisiwa cha Makatéa ndilo jambo bora zaidi katika maisha yetu.”
-
-
Tahiti2005 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
-
-
[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 77]
Alikuwa Shemasi wa Kanisa, Sasa Ni Mhubiri wa Ufalme
Manuari Tefaatau
Alizaliwa: 1913
Alibatizwa: 1959
Maisha yake: Manuari, aliyekuwa shemasi katika Kanisa la Kiprotestanti, alifundishwa kweli na baadhi ya wanafunzi wa kwanza wa Biblia kisiwani Makatéa.
Baada ya Mashahidi Jean-Marie na Jeanne Félix kufika kisiwani Makatéa mwaka wa 1956, wanafunzi wao wa kwanza wa Biblia, Maui Piirai na Germaine Amaru, walinihubiria. Muda si muda nikaanza kuwahubiria watu wa kanisa langu, jambo ambalo lilisababisha mgogoro kanisani. Hata, kasisi aliniamuru niache kuzungumza na Mashahidi wa Yehova.
Bila kusita niliacha kanisa na kuanza kuhudhuria mikutano iliyofanywa nyumbani kwa familia ya Félix. Wafuasi wengine wachache wa kanisa langu la zamani walianza pia kujifunza na kuhudhuria mikutano. Ninafurahia sana kuwa miongoni mwa wale wanafunzi wachache wa kwanza wa Biblia katika eneo la Polinesia ya Ufaransa.
-