-
Uganda2010 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
-
-
KAZI YA KUTAFSIRI YAHARAKISHA UKUSANYAJI WA WATU
Kiingereza hutumiwa kote nchini. Hata hivyo, Kiganda ndiyo lugha inayozungumzwa na wenyeji walio wengi, ijapokuwa lugha nyingine zaidi ya 30 huzungumzwa. Hivyo, jambo kuu ambalo limechangia ongezeko kubwa katika miaka ya karibuni ni maendeleo katika kazi ya kutafsiri.
“Ijapokuwa mama yangu alikuwa shahidi mwaminifu,” asema Fred Nyende, “alifaidika zaidi mikutanoni nilipotafsiri makala za funzo katika Kiganda. Jambo ambalo sikujua wakati huo ni kwamba nilikuwa nikipata mazoezi kwa ajili ya kazi kubwa zaidi ya kutafsiri.” Fred alimaanisha nini?
Muda mfupi baada ya kuanza kufanya upainia mwaka wa 1984, Fred aliombwa awafundishe wamishonari Kiganda. Mwaka uliofuata aliombwa ajiunge na kikundi cha watafsiri wa Kiganda. Mwanzoni, yeye na watafsiri wengine walifanyia kazi yao nyumbani walipopata nafasi. Baadaye kikundi hicho kikaanza kufanya kazi yao kikiwa pamoja katika chumba kidogo kando ya makao ya wamishonari. Wakati wa marufuku ya miaka ya 1970, matoleo kadhaa ya gazeti la Mnara wa Mlinzi yalikuwa yametafsiriwa katika Kiganda na nakala kadhaa kufanyizwa. Hata hivyo, baada ya muda, mradi huo ulisimamishwa. Mwaka wa 1987 ndipo gazeti la Mnara wa Mlinzi lilipoanza kuchapishwa tena katika Kiganda. Tangu wakati huo, kikundi cha kutafsiri kimeongezeka, nao watafsiri wamejitahidi kutafsiri vitabu vingi zaidi kwa ajili ya idadi inayozidi kuongezeka ya makutaniko ya Kiganda. Leo, karibu nusu ya makutaniko nchini ni ya Kiganda.
Baadaye, vitabu vyetu vilianza kutafsiriwa katika lugha nyinginezo. Kwa sasa kuna vikundi vya kudumu vya watafsiri wa Kicholi, Kikonzo, na Kinyankore. Isitoshe, vitabu kadha wa kadha vimetafsiriwa katika Kiteso, Kigbara, Kimadi, na Kitoro.
Vikundi vya Kicholi na Kinyankore vinafanyia kazi yao katika ofisi za kutafsiri mjini Gulu na Mbarara, ambako lugha wanazotafsiri zinazungumzwa na wengi. Hilo limewasaidia watafsiri kwenda sambamba na lugha zao na kutafsiri kwa njia inayoeleweka kwa urahisi. Kwa kuongezea, makutaniko yaliyo katika miji hiyo yanafurahia utegemezo wa watafsiri hao.
Bila shaka kazi ya kutafsiri inahitaji jitihada nyingi na gharama kubwa. Watafsiri wenye bidii wa Uganda, pamoja na vikundi vingine vya kutafsiri ulimwenguni pote, wamefaidika kutokana na mazoezi ya kuboresha ufahamu wa lugha na stadi za kutafsiri. Jitihada na gharama hizo hazikuwa kazi bure—watu wengi zaidi nchini Uganda, kutoka katika ‘makabila na vikundi vya watu na lugha,’ wanafaidika kwa kusoma ujumbe wa Biblia katika lugha zao wenyewe kuliko ilivyokuwa awali. (Ufu. 7:9, 10) Ndiyo sababu, kufikia mwaka wa 2003, kulikuwa na wahubiri wa Ufalme zaidi ya 3,000 nchini Uganda, na miaka mitatu tu baadaye, mwaka wa 2006, idadi hiyo ilifikia 4,005.
-
-
Uganda2010 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
-
-
[Picha katika ukurasa wa 118]
Vikundi vya Watafsiri
Kiganda
Kicholi
Kikonzo
Kinyankore
-