Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Uganda
    2010 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
    • MAPAINIA WENYE KUSTAHIMILI

      Ijapokuwa hali hazikuwa shwari, sikuzote ndugu na dada kadhaa walishiriki katika utumishi wa painia. Painia mmoja mwenye bidii wa enzi hizo ni James Luwerekera, soroveya wa serikali aliyebatizwa mwaka wa 1974. Punde baada ya kubatizwa alianza kufanya ukulima ili awahubirie habari njema jirani zake kijijini kwao. Mke wake pia alijifunza kwa muda, lakini kadiri wakati ulivyopita, alizidi kuwa mpinzani.

      Kwa mfano, asubuhi moja, kukiwa na giza bado, James na ndugu kadhaa walifunga safari kuelekea Nairobi ili kuhudhuria kusanyiko la wilaya. Baadaye, waliposimamishwa na polisi katika kituo cha ukaguzi, ndugu hao walishangaa kuona mavazi ya James—nguo zake hazikuwa na mpangilio wowote wala hazikumtoshea. Mwanzoni aliwatania kwa kuwaambia alivaa mbiombio gizani. Lakini waliposisitiza kujua ni kwa nini, alikiri kwamba mke wake alificha nguo zake za mikutano ili asihudhurie kusanyiko na kwa hiyo alilazimika kuvalia nguo alizopata. Ndugu hao walimpa baadhi ya nguo zao, naye akawasili kusanyikoni akiwa amevalia ifaavyo.

      Nyakati fulani upinzani nyumbani kwa James na katika ujirani ulikuwa usumbufu tu, lakini nyakati nyingine ulikuwa mkali zaidi. Hali iliendelea hivyo kwa miaka kadhaa. Wakati wote huo, James alivumilia kwa upole na kuwa mwaminifu hadi alipokufa mwaka wa 2005. Imani yake ingali yawachochea ndugu zake, na bila shaka, inakumbukwa na Mungu wake, Yehova.

  • Uganda
    2010 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
    • SAMUEL MUKWAYA

      ALIZALIWA 1932

      ALIBATIZWA 1974

      MAELEZO MAFUPI KUMHUSU Kwa miaka mingi Samuel aliwakilisha tengenezo katika mambo ya kisheria, na pia alitumikia akiwa mzee na painia.

      ◼ SITASAHAU kamwe siku tuliyotembelea ofisi ya tawi ya Kenya huko Nairobi.

      “Pini hizi zenye rangi tofauti-tofauti ni za nini?” nikauliza nilipokuwa nikitazama ramani ya Uganda.

      “Haya ni maeneo yaliyo na watu wengi wenye kupendezwa,” akajibu Robert Hart, ndugu wa Halmashauri ya Tawi ya Kenya.

      “Na hapa je, mtatuma mapainia lini?” nikauliza nikimwonyesha pini ya Iganga, nyumbani kwetu.

      “Hatutumi mtu yeyote huko,” akasema. Kisha akanitazama kwa tabasamu na kusema, “Wewe ndiwe utakayekwenda huko.”

      Nilishangazwa na jibu la Ndugu Hart kwa kuwa sikuwa painia, wala sikuwa nikiishi nyumbani. Hata hivyo, jambo hilo lilibaki akilini mwangu, na baada ya kustaafu, niliamua kurudi nyumbani na kuwa painia wa kawaida. Tulifurahi kuona kikundi kidogo cha wahubiri kikiongezeka na kuwa kutaniko kubwa lenye Jumba la Ufalme!

      Patrick Baligeya alipotumwa Iganga akiwa painia wa pekee, tuliishi pamoja na kufanya upainia pamoja. Pia tulipanda mahindi ili kujitegemeza. Kila siku tulianza kwa kuchunguza andiko la siku, kisha kufanya kazi katika shamba la mahindi kwa saa kadhaa. Halafu mwendo wa saa nne hivi tukaanza utumishi hadi jioni.

      Mahindi yetu yalipoanza kukua, baadhi ya majirani walidai kwamba tunapuuza shamba letu kwa sababu ya kazi ya kuhubiri. Tulijua kwamba mahindi yanahitaji kulindwa kwa sababu ya tumbili. Hata hivyo, hatukutaka kukatiza uvunaji wetu wa kiroho ili kufukuza tumbili.

      Muda si muda tukaona mbwa koko wawili wakubwa karibu na shamba letu. Hatukujua wametoka wapi wala ni wa nani, lakini badala ya kuwafukuza, tukawa tukiwawekea chakula na maji kila siku. Hakuna tumbili waliokanyaga shamba letu maadamu mbwa hao walikuwapo. Kisha, baada ya majuma manne, mbwa hao wakatoweka ghafula, vile tu walivyokuja—nao ulikuwa wakati barabara kwa kuwa mahindi yetu hayakuwa hatarini! Tulimshukuru Yehova kwa mavuno tele tuliyopata. Zaidi ya yote, tulithamini sana kwamba Mungu alibariki mavuno yetu ya kiroho pia!

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki