-
Uganda2010 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
-
-
WAMISHONARI WAFANYA KAZI MUHIMU
Mwaka wa 1962, nchi ya Uganda ilipata uhuru kutoka kwa serikali ya Uingereza. Mwaka uliofuata Ndugu Henschel alizuru Nairobi, Kenya, na kuzungumzia uwezekano wa kutuma wamishonari nchini Uganda. Ni nani wangepata mgawo huo?
Tom na Bethel McLain, wa darasa la 37 la Gileadi, walikuwa wamewasili kutumikia Nairobi. Walishangaa kupata mgawo wa kwenda Kampala! Hata hivyo, waliukubali mgawo huo nao wakawa wamishonari wa kwanza kutoka Gileadi kutumikia nchini Uganda. Tom anasema: “Mwanzoni tulitamani kurudi Kenya, lakini baada ya muda tuliipenda Uganda sana. Kulikuwa na watu wenye urafiki na waliokuwa tayari kusikiliza ujumbe wetu.”
Tom na Bethel walikuwa wameanza kujifunza Kiswahili nchini Kenya, lakini sasa walihitaji kujifunza lugha mpya—Kiganda. Hawakuwa na mwalimu. Walichokuwa nacho ni azimio lao, tegemeo lao kwa Yehova, na kitabu cha kujifunza wenyewe. Katika miezi ya kwanza nchini Uganda, mbali na saa 100 walizotumia katika huduma ya shambani, walitumia saa 250 kujifunza lugha hiyo mpya mwezi wa kwanza, na saa 150 mwezi wa pili. Hatua kwa hatua wakaijua lugha hiyo na kufurahia matokeo mazuri katika utumishi wa shambani.
Januari 1964, Gilbert na Joan Walters wa darasa la 38 la Gileadi walijiunga na Tom na Bethel. Wanafunzi wengine wa darasa hilohilo, Stephen na Barbara Hardy na Ron na Jenny Bicknell, walikuwa wametumwa Burundi, lakini kwa sababu hawakupata vibali vya kuingia nchini humo, wao pia wakatumwa Uganda. Makao mapya ya wamishonari mjini Kampala yalihitajiwa haraka!
Kutaniko la awali la Kampala haliwezi kamwe kusahaulika. Lilikuwa na Ndugu Kadu na familia yake; John na Eunice Bwali, mapainia wa pekee kutoka Rhodesia ya Kaskazini, na watoto wao; na Margaret Nyende na watoto wake. Hawakuwa na mahali pazuri pa kukutania. “Wapita-njia wangeweza kutuona na kutusikia, ingawa tulikuwa wachache,” akumbuka Gilbert Walters. “Familia ya Bwali iliimba kwa sauti nyimbo za Ufalme bila kinanda chochote, bila kuwaogopa wapita-njia. Hilo lilitupa ujasiri kuendelea.”
Baadaye, Gilbert na Joan Walters walipewa mgawo wa kuhamia Jinja, ambako kazi ya kuhubiri haikuwa imefanywa vizuri. Wamishonari wengine walitumwa Mbale, karibu na mpaka wa Kenya, na wengine wakatumwa Mbarara. Wamishonari wote hao walifanya kazi bega kwa bega na mapainia wa pekee waliokuwa wamekuja kutoka nchi nyingine. Ni wazi kwamba mashamba yalikuwa “meupe kwa ajili ya kuvunwa.” (Yoh. 4:35) Hivyo basi, ni nini kingeweza kufanywa ili kuharakisha kazi ya kuvuna?
MAMBO YAFANYWA KWA UTARATIBU
Watumishi wa wakati wote nchini Uganda walijitahidi kuhubiri eneo lao kubwa kwa mpangilio mzuri. Katikati ya juma, walikuwa wakihubiri mitaa yenye nyumba zenye mpangilio mzuri. Hata hivyo, vipi maeneo ambayo hayakuwa na mitaa yenye majina wala nyumba zenye nambari?
“Tuligawa maeneo hayo kulingana na vilima,” aeleza Tom McLain. “Wawili walihubiri upande mmoja wa kilima, huku wengine wawili wakihubiri upande wa pili. Tulifuata vijia, tukihubiri mpaka sote wanne tulipokutana.”
Baada ya muda, ndugu wa kigeni walianza kufaidika kutokana na ongezeko miongoni mwa wenyeji ambao walilifahamu vizuri eneo na utamaduni. Nao wenyeji walipata uzoefu. Kwa mfano, huko Jinja, tayari ndugu wenyeji walikuwa wakihubiri pamoja na wamishonari. Jumapili walikuwa wakihubiri nyumba kwa nyumba kuanzia saa mbili asubuhi hadi saa nne. Kisha, ziara za kurudia kwa saa moja na kuongoza funzo la Biblia mpaka saa sita. Kwa kufanya hivyo, wote kutanikoni walifaidika kutokana na uzoefu wa kila mmoja na kutiana moyo.
Kwa kuwa Jinja, mji wa pili kwa ukubwa nchini, una kituo cha kuzalishia umeme, ni eneo lenye viwanda vingi. Wamishonari walipata matokeo mazuri kwa kuhubiri katika vituo vya magari ya umma. Wasafiri kutoka mbali walikubali magazeti na vitabu vya Biblia ambavyo walivisoma wakiwa safarini. Hivyo, mbegu ya Ufalme ilienezwa hadi vijijini.
Pia, ndugu walitumia redio kutangaza habari njema kwa watu wengi iwezekanavyo. Walipewa nafasi ya kila juma katika idhaa ya taifa ya kipindi kinachoitwa “Mambo Ambayo Watu Wanafikiria.” Akina ndugu walizungumzia habari zenye kusisimua kama vile “Kukabili Matatizo ya Familia” na “Jinsi ya Kujilinda Kutokana na Uhalifu na Jeuri,” kwa njia ya mjadala kati ya “Bwana Robbins” na “Bwana Lee.” Ndugu mmoja akumbuka: “Ilikuwa ajabu kusikiliza kipindi cha mazungumzo kati ya Mmarekani na Mskoti katika redio barani Afrika. Bila shaka, kipindi hicho kilitimiza mengi kwa sababu mara nyingi tulipokuwa katika huduma ya shambani watu walituambia jinsi wanavyokifurahia.”
KUWASAIDIA WAHUBIRI WAPYA
Wakati huo kikundi cha Jinja kilikuwa kikifanyia mikutano yao katika jumba la umma katika mtaa wa Walukuba. “Ndugu wengi walikuwa wapya,” akumbuka Tom Cooke, “nao walikuwa na vichapo vichache ambavyo wangeweza kutumia kutayarishia migawo yao.” Msaada ungetoka wapi?
“Wamishonari waliweka maktaba katika nyumba ya ndugu mmoja aliyekuwa akiishi katikati ya mtaa huo,” asema Tom. “Kila Jumatatu (Siku ya 1) usiku, waliokuwa na migawo walienda kwa ndugu huyo kutumia maktaba ili kutayarisha hotuba zao.” Leo, kuna makutaniko mengi Jinja yanayoendelea na kazi ya uvuvi wa kiroho katika eneo hilo ambalo ni chanzo cha Mto Nile.
-
-
Uganda2010 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
-
-
[Picha katika ukurasa wa 80]
Tom na Bethel McLain, wamishonari wa kwanza kutoka Gileadi kutumwa nchini Uganda
[Picha katika ukurasa wa 81]
Makao ya kwanza ya wamishonari mjini Jinja
[Picha katika ukurasa wa 83]
Barbara na Stephen Hardy, wamishonari kutoka Gileadi
-