-
Uganda2010 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
-
-
Akiwa ametoka tu katika Shule ya Gileadi, Mats Holmkvist alikuwa na bidii sana, naye alikuwa na hamu ya kujifunza lugha ya wenyeji ili kuwasaidia watu wapendezwe na kweli. Wakati huo, Fred Nyende alikuwa painia wa pekee mjini Entebbe, naye aliutumia ujuzi wake wa kutafsiri na ukalimani kuwafundisha wamishonari kuzungumza kwa ufasaha Kiganda, lugha ambayo nyakati nyingine maneno yake huwa magumu kutamka. Mats alitoa jasho.
“Mtu husemaje, ‘Ufalme wa Mungu’ katika Kiganda?” akauliza Mats mwanzoni-mwanzoni mwa masomo yake.
“Obwakabaka bwa Katonda,” akamjibu Fred, kana kwamba yuaimba.
‘Jamani,’ akawaza Mats huku akighairi kwamba laiti hangeuliza. Hata hivyo, Mats alipiga hatua kubwa na hatimaye aliweza kukizungumza Kiganda vizuri.
-
-
Uganda2010 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
-
-
Dada fulani alimwomba ndugu mmishonari, Mats Holmkvist, amtembelee Mutesaasira Yafesi. Alikuwa kasisi Msabato. Hata hivyo, alikuwa akipendezwa na ujumbe wa Mashahidi wa Yehova, naye alikuwa ametayarisha orodha ya maswali 20. Alipokutana na Mats akamkabidhi orodha hiyo.
Baada ya kuwa na mazungumzo ya Biblia kwa saa mbili, Mutesaasira akasema: “Hatimaye nimeipata dini ya kweli! Tafadhali usikose kuja kunitembelea kijijini. Kuna wengine pia ambao wangependa kujifunza kuhusu Mashahidi wa Yehova.”
Siku tano baadaye, Mats na mmishonari mwingine wakasafiri kwa pikipiki umbali wa kilomita 110 kupitia njia zenye matope katikati ya mashamba ya majani chai kwenda kumtembelea Mutesaasira katika kijiji cha Kalangalo. Akina ndugu walishangaa Mutesaasira alipowapeleka katika kibanda kilichoezekwa kwa nyasi ambacho kilikuwa na ishara “Jumba la Ufalme.” Tayari alikuwa amejenga kibanda ambacho kingeweza kutumiwa kwa ajili ya funzo la Biblia na mikutano!
Kulikuwa na watu wengine kumi waliopendezwa na kweli ambazo Mutesaasira alikuwa amewahubiria. Walianza kujifunza Biblia, na bila kujali umbali, Mats alijifunza nao mara mbili kwa mwezi. Watu hao walifanya maendeleo. Mbali na kutaniko lililo katika mji wa Mityana, katika kijiji cha Kalangalo watu zaidi ya 20 wamekuwa wahubiri. Naye Mutesaasira alifanya maendeleo haraka na kubatizwa. Sasa akiwa na umri wa miaka 70 na kitu, anatumikia akiwa mzee wa kutaniko.
-