-
Karne Moja na Nusu ya Reli za Chini ya ArdhiAmkeni!—1997 | Machi 22
-
-
WACHIMBA-HANDAKI walitazama kwa butaa kile walichogundua. Ulikuwa mwaka wa 1912. Chini kabisa ya barabara za New York City, walipokuwa wakichimba nyongeza ya reli ya chini ya ardhi, wao walitokea katika chumba kikubwa kilichokuwa kimejificha. Chumba hicho kilikuwa kimepambwa sana—kama jumba la mfalme! Kwenye kuta zayo palikuwa na vioo, vinara vya taa, na michoro. Mapambo ya mbao, yakiwa yanaporomoka kwa sababu ya umri, bado yalikuwa yangali yamepamba kuta. Katikati ya chumba kulikuwa na pambo la bomba la kurusha maji, likiwa liliacha zamani kurusha maji.
Chumba hicho kiliingia katika handaki. Kwa mshangao wa wafanyakazi hao, palikuwa na gari-moshi lililopambwa vizuri sana la kubeba watu 22 likiwa kwenye reli. Je, kulikuwa na reli nyingine chini ya New York kabla ya hii waliyokuwa wakichimba? Ni nani aliyejenga mahali hapa?
-
-
Karne Moja na Nusu ya Reli za Chini ya ArdhiAmkeni!—1997 | Machi 22
-
-
Reli ya Chini ya Ardhi ya Kwanza ya New York
Ng’ambo ya Atlantiki kutoka London, mvumbuzi mwingine mwenye kipawa, Alfred Ely Beach, alikuwa akifikiria juu ya hali mbaya sana ya msongamano katika New York. Akiwa mchapishaji wa jarida Scientific American, Beach alikuwa mteteaji wa masuluhisho ya kisasa kwa matatizo ya zamani, kama vile barabara za jiji zilizosongamana sana. Katika 1849 yeye alipendekeza mpango tofauti kabisa: “Handaki la Broadway,” mojawapo ya barabara zenye kusongamana zaidi, “lenye vijia na ngazi katika kila pembe. Njia hiyo ya chini ya ardhi inapaswa kuwekewa reli mbili, kukiwa na njia ya watembeaji kwa kila upande.”
Katika miongo miwili iliyofuata, wasitawishaji wengine wa usafiri pia walitoa mapendekezo ya kuharakisha usafiri katika New York. Hayo yote yalikataliwa hatimaye. Mwanasiasa mwenye uwezo aliye mfisadi, Boss Tweed, hakutaka kampuni za usafirishaji zipate upinzani wowote, hizo zilikuwa chanzo kikubwa cha mapato yake yasiyo halali. Lakini Bw. Beach aliye mwerevu, ambaye hakupata kuacha wazo lake, akamshinda Boss mwenye majivuno.
Beach alipata kibali cha kisheria cha kujenga mahandaki mawili yenye kukabiliana, madogo sana kuweza kusafirisha abiria, chini ya Broadway. Mahandaki hayo yalikuwa yatumike “kupeleka barua, vifurushi na bidhaa” kwa posta kuu. Kisha akaomba afanye rekebisho ambalo lingemruhusu kujenga handaki moja kubwa, eti kuokoa gharama. Kwa njia fulani ujanja wake haukutambuliwa, na rekebisho hilo likakubaliwa. Mara moja Beach akaanza kazi lakini kichini-chini. Alianza kuchimba kwenye chumba cha chini cha duka fulani la nguo, akiondoa udongo wakati wa usiku kwa mabogi yenye magurudumu yaliyofunikwa ili yasipige kelele. Kwa usiku 58 tu, handaki hilo la meta 95 lilimalizika.
“Kamba ya Hewa”
Beach alifahamu sana uchafuzi mkubwa ulio katika mahandaki ya London yaliyosababishwa na kutumia magari-moshi ya makaa-mawe. Yeye aliendesha gari lake kwa “kamba ya hewa”—msongo kutoka kwa kipepeo kikubwa kilichojengwa juu kwenye mwisho mmoja wa handaki. Hewa hiyo ilisukuma gari kwa upole kwa mwendo wa kilometa 10 kwa saa, ingawa gari hilo lingeenda mara kumi zaidi ya mwendo huo. Gari hilo lilipofika mwisho mwingine wa handaki, kipepeo hicho kilibadilishwa kivute gari nyuma! Ili kufanya watu wasisite-site kuingia chini ya ardhi, Beach alihakikisha kwamba chumba kikubwa cha kungojea kilikuwa kimetiwa nuru nyingi ya kutosha kwa taa za zircon, ambazo zilikuwa miongoni mwa taa zenye kuwaka zaidi zilizopatikana wakati huo. Naye alikipamba kwa umadaha kwa viti, sanamu, madirisha bandia yenye pazia, na hata piano kubwa pamoja na tangi la samaki aina ya dhahabumikia! Reli hiyo ndogo ilifunguliwa kwa umma usiokuwa na habari Februari 1870 na ikawa na mafanikio makubwa sana mara moja. Kwa mwaka mmoja, watu 400,000 walizuru reli hiyo ya chini ya ardhi.
Boss Tweed alighadhabika! Hila za kisiasa zikatokea, na Tweed akamshawishi gavana aidhinishe mpango wenye kupinga huo wa kuwa na gari-moshi la juu ya ardhi lenye kugharimu mara 16 kuliko lile la chini ya ardhi lililopendekezwa na Beach. Muda mfupi baadaye, Tweed alishtakiwa, akafungwa maisha. Lakini hofu ya ghafula iliyoshika soko la hisa katika 1873 iliondosha akili za waweka-rasilimali na maofisa kwenye reli ya chini ya ardhi, na hatimaye Beach akafunga hilo handaki. Kwa hiyo likasahaulika mpaka lilipogunduliwa bila matarajio katika 1912, zaidi ya miaka saba baada ya kufunguliwa kwa reli ya chini ya ardhi ya sasa ya New York katika 1904. Sehemu ya handaki la awali la Beach baadaye ikawa sehemu ya Stesheni ya City Hall ya sasa, jijini Manhattan.
-