Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Kujenga Pamoja Duniani Pote
    Mashahidi wa Yehova—Wapiga-Mbiu wa Ufalme wa Mungu
    • Kusitawisha Mbinu za Ujenzi wa Haraka

      Mapema katika miaka ya 1970, katika Marekani, Mashahidi zaidi ya 50 kutoka makutaniko ya karibu walikuja pamoja ili kusaidia kujenga Jumba la Ufalme jipya katika Carterville, Missouri, kwa ajili ya kikundi kilichokuwa kikikutana katika Jiji la Webb. Katika mwisho-juma mmoja walijenga kiunzi kikuu na kufanya kazi kubwa kwenye paa. Kulikuwa kungali na mengi ya kufanywa, na ilichukua miezi kadhaa kumaliza kazi; lakini sehemu ya maana yalo ilikuwa imekamilishwa kwa kipindi kifupi.

      Wakati wa mwongo uliofuata, kadiri akina ndugu walivyofanya kazi pamoja kujenga majumba kama 60, vizuizi vilishindwa, na njia zenye matokeo zaidi zikasitawishwa. Baada ya wakati, walipata kuona kwamba baada ya kazi ya msingi kufanywa, wangeweza kukaribia kukamilisha Jumba la Ufalme lote kwa mwisho-juma mmoja.

      Waangalizi kadhaa wa makutaniko—wote kutoka magharibi-kati mwa Marekani—walianza kujitahidi kufikia mradi huo. Wakati makutaniko yalipoomba msaada wa kujenga Jumba la Ufalme lao, mmoja au zaidi wa akina ndugu hao angezungumzia mradi huo pamoja nao na kuandaa mambo mengi madogomadogo kuhusu matayarisho ambayo lazima yashughulikiwe na wenyeji kabla ya kazi kuanza kufanywa. Miongoni mwa mambo mengine, ilibidi ruhusa za ujenzi zipatikane, ilibidi msingi na bamba la sakafu la zege vimwagwe, ilibidi umeme uwe unafanya kazi, ilibidi mabomba ya maji ya chini ya ardhi yawe yamewekwa mahali payo, na ilibidi ifanywe mipango yenye kutegemeka ya kuleta vifaa vya ujenzi. Kisha tarehe ingeweza kuwekwa ya ujenzi wa Jumba la Ufalme lenyewe. Jengo hilo halingekuwa limetangulia kuundwa; lingejengwa toka chini hadi juu mahali papo hapo pa ujenzi.

      Ni nani wangefanya hasa kazi ya ujenzi? Kwa kadiri ilivyowezekana, ilifanywa na wafanyakazi wa kujitolea, wasiolipwa. Familia nzimanzima mara nyingi zilishiriki. Wale wenye kupanga mradi huo waliwasiliana na Mashahidi waliokuwa mafundi na ambao walikuwa wameeleza nia yao ya kushiriki katika miradi hiyo. Wengi wao walitazamia kwa hamu kila mradi mpya wa ujenzi. Mashahidi wengine waliopata kujua juu ya miradi hiyo walitaka kushiriki; mamia kutoka eneo la karibu—na kutoka sehemu za mbali zaidi—walimiminika kwenye mahali pa ujenzi, wakiwa na hamu ya kutoa utumishi wao mbalimbali katika njia yoyote waliyoweza. Walio wengi wao hawakuwa wajenzi stadi, lakini hakika walitoa ithibati kwamba wao walifaana na maelezo ya wale ambao wangekuwa waungaji mkono wa Mfalme wa Kimesiya wa Yehova kama ilivyoandikwa kwenye Zaburi 110:3, ambalo husema: “Watu wako wanajitoa kwa hiari.”

      Alhamisi jioni kabla ya ile jitihada kubwa kuanza, wale waliokuwa wakisimamia ujenzi walikutana ili kupanga mambo madogomadogo ya mwisho. Jioni iliyofuata, wafanyakazi walionyeshwa slaidi juu ya utaratibu ili waelewe jinsi ambavyo kazi ingefanywa. Mkazo ulitiwa juu ya umaana wa sifa za kimungu. Ndugu walitiwa moyo wafanye kazi pamoja kwa upendo, wawe wenye fadhili, na kuonyesha saburi na ufikirio. Kila mtu alitiwa moyo afanye kazi kwa mwendo wa taratibu lakini asiharakishe na asisite kuchukua dakika chache kushiriki pamoja na mwingine jambo lililoonwa lenye kujenga. Mapema asubuhi iliyofuata, ujenzi ulianza.

      Katika wakati uliopangwa mapema Jumamosi asubuhi, kila mtu angeacha kufanya alilokuwa akifanya ili kusikiliza mazungumzo ya Andiko la siku. Sala ilitolewa, maana ilifahamiwa vema kwamba fanikio la mradi wote lilitegemea baraka ya Yehova.—Zab. 127:1.

      Kazi ilipoanza, hiyo ilisonga mbele kasi. Katika muda wa saa moja kuta zilikuwa zimesimama. Farasi za paa zilifuata. Kufunika kuta kukamalizwa. Mafundi wa umeme wakaanza kuzungusha waya. Vitundu vya visawazishahewa vikawekwa. Kabati zikajengwa pahali pazo. Nyakati nyingine kulinyesha mwisho-juma wote, au halihewa iligeuka kuwa baridi sana au joto sana, lakini kazi ilisonga mbele. Hakukuwa na mashindano au ushindani miongoni mwa mafundi.

      Mara nyingi, kabla ya jua kushuka katika siku ya pili, Jumba la Ufalme lilikuwa limekamilishwa—limepambwa vizuri ndani, labda hata kupambwa mandhari ya nje. Ilipofaa zaidi, kazi ziliratibiwa ziendelee kwa siku tatu, au labda miisho-juma miwili. Mwishoni mwa mradi, walio wengi kati ya wafanyakazi wangebaki, wakiwa wamechoka lakini wenye furaha sana, wafurahie mkutano wa kwanza wa kawaida wa kutaniko, funzo la Mnara wa Mlinzi.

      Wakitia shaka kwamba kazi nzuri ingeweza kufanywa kwa haraka sana jinsi hiyo, watu kadhaa katika Guymon, Oklahoma, Marekani, waliita mkaguzi wa ujenzi wa jiji. “Niliwaambia kwamba kama walitaka kuona jambo lililofanywa sawasawa, yawapasa kuzuru jumba hilo!” akasema mkaguzi huyo baadaye alipokuwa akisimulia Mashahidi kisa hicho. “Nyinyi watu hata mnafanya sawasawa yale yaliyofichika na yasiyoonekana!”

  • Kujenga Pamoja Duniani Pote
    Mashahidi wa Yehova—Wapiga-Mbiu wa Ufalme wa Mungu
    • [Sanduku/Picha katika ukurasa wa 320, 321]

      Kufanya Kazi Pamoja ili Kujenga Haraka Majumba ya Ufalme

      Maelfu ya makutaniko mapya huundwa kila mwaka. Katika visa vingi, Majumba ya Ufalme mapya hujengwa na Mashahidi wenyewe. Picha hizi zilipigwa wakati wa ujenzi wa Jumba la Ufalme katika Connecticut, Marekani, katika 1991

      Ijumaa, saa 1:40 asubuhi

      Ijumaa, saa 6 adhuhuri

      Jumamosi, saa 1:41 jioni

      Kazi kubwa yakamilika, Jumapili, saa 12:10 jioni

      Wamtegemea Yehova kwa baraka yake, na huchukua wakati kuzungumzia shauri kutoka Neno lake

      Wote ni wenye kujitolea wasiolipwa, wenye furaha kufanya kazi mmoja kando ya mwenzake

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki