Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Mtegemee Yehova—Hakika Atakusaidia
    Mnara wa Mlinzi—2010 | Septemba 1
    • Mnamo Septemba (Mwezi wa 9) 1939, Vita vya Pili vya Ulimwengu vilikuwa vimeanza huko Ulaya, na wasiwasi kuhusu vita hivyo uliikumba Marekani yote. Vijana na vilevile watu wazima mbao hawakuelewa msimamo wetu wa kutounga mkono vita, waliwapiga na kuwatesa vijana Mashahidi. Iliripotiwa kwamba kuanzia mwaka wa 1940 hadi 1944, Mashahidi wa Yehova nchini Marekani walishambuliwa mara zaidi ya 2,500 na umati wa watu wenye jeuri. Mateso yaliongezeka hata zaidi wakati Japani iliposhambulia Pearl Harbor mnamo Desemba 7, 1941 (7/12/1941).

  • Mtegemee Yehova—Hakika Atakusaidia
    Mnara wa Mlinzi—2010 | Septemba 1
    • Mateso Kusini mwa Marekani

      Wakaaji wa eneo hilo walituruhusu kuegesha gari letu katika shamba fulani la matunda karibu na jiji la Jeanerette. Jumamosi moja tuliamua kufanya mahubiri ya barabarani, lakini mkuu wa polisi akawatuma askari wake waje kutukamata na kutufungia katika ukumbi wa jiji. Kundi la watu wapatao 200 hivi lilikusanyika nje, na polisi wakatuachilia bila ulinzi wowote. Tulifurahi kundi hilo lilipofungua njia na kuturuhusu kupita. Siku iliyofuata, tulienda Baton Rouge, jiji kubwa lililokuwa karibu, kuwaeleza Mashahidi wenzetu kile kilichotokea.

      Tuliporudi Jeanerette, tulikuta ujumbe umebandikwa kwenye mlango wa gari letu uliosema: “Tafadhali, naomba tukutane katika kambi ya wafanyakazi wa mafuta.” Ujumbe huo ulikuwa na jina, “E. M. Vaughn.” Tulikutana na Bw. Vaughn, naye akatukaribisha kula mlo pamoja naye na mke wake. Alisema kwamba alikuwa kati ya umati wa watu uliokuwa umekusanyika siku ya Jumamosi, na kwamba kama kungalikuwa na tatizo angalitutetea tusishambuliwe na umati huo. Tulimshukuru kwa kututia moyo na kututegemeza.

      Siku iliyofuata, askari polisi wakiwa na silaha walitukamata na kuharibu vitabu vyetu. Walichukua ufunguo wa nyumba yetu iliyokokotwa na gari na kunifunga kifungo cha upweke kwa siku 17. Nilipewa chakula kidogo sana. Bw. Vaughn alijitahidi kutusaidia, lakini hakufanikiwa. Tulipokuwa tumefungwa, kundi la watu lilipora vitu vyetu na kuteketeza kila kitu tulichokuwa nacho kutia ndani nyumba yetu ya kukokotwa na gari. Wakati huo, sikujua kwamba Yehova alikuwa akinitayarisha kwa ajili ya yale ambayo muda si mrefu ningeyakabili.

      Nafungwa Kaskazini mwa Marekani

      Mwezi mmoja baada ya kurudi kaskazini, niliwekwa rasmi kuwa painia wa pekee ili nitumike pamoja na Mashahidi wengine huko Olean, New York. Nikiwa huko, serikali ilitaka nijiandikishe kwa ajili ya utumishi wa kijeshi, lakini niliruhusiwa kutojiandikisha kwa msingi wa dhamiri yangu. Hata hivyo, baada ya kuchunguzwa afya ya mwili na akili, karatasi yangu ilipigwa muhuri ulioonyesha kwamba nilifaa kupata mafunzo ya kijeshi.

      Niliendelea na utumishi wa painia kwa mwaka mwingine mmoja hivi. Kisha, mnamo 1943, kwa sababu nilikataa kuacha huduma yangu na kujiunga na mafunzo ya kijeshi, Shirika la Upelelezi la Marekani (FBI) lilinikamata na kuniagiza niripoti mahakamani huko Syracuse, New York, wiki iliyofuata ili nijibu mashtaka. Nilishtakiwa na kesi yangu ikapangwa kusikilizwa baada ya siku mbili.

      Nilijitetea mwenyewe mahakamani. Katika mikutano yetu ya Kikristo, sisi vijana tulipata mazoezi ya jinsi tunavyoweza kutetea haki zetu za kisheria mahakamani na jinsi ya kujiendesha vizuri tukiwa huko. Nilikumbuka vizuri ushauri uliotajwa mwanzoni mwa makala haya. Hata waendesha mashtaka fulani walilalamika kwamba Mashahidi walijua mengi zaidi kuhusu sheria kuliko wao! Hata hivyo, hakimu alisema nina hatia. Hakimu aliponiuliza ikiwa nina jambo lingine zaidi la kusema, nilisema tu, “Leo taifa linahukumiwa mbele ya Mungu kutokana na jinsi linavyowatendea watumishi wake.”

      Nilihukumiwa kifungo cha miaka minne katika gereza la Chillicothe, Ohio. Huko nilipewa kazi ya kuwa mwandishi wa ofisa wa gereza. Baada ya majuma machache, mpelelezi maalumu kutoka Washington D.C. alikuja ofisini kwetu na kusema kwamba walikuwa wakimchunguza Hayden Covington. Ndugu Covington alikuwa mwanasheria aliyewawakilisha Mashahidi wa Yehova, na alijulikana kuwa mmoja kati ya wanasheria bora nchini Marekani.

      Mpelelezi huyo alisema kwamba anahitaji mafaili ya wafungwa wawili—Danny Hurtado na Edmund Schmidt. Mkubwa wangu akajibu: “Hata Bw. Schmidt mwenyewe ndiye huyu hapa.” Mpelelezi huyo alikuwa ametumwa kisiri, lakini mara moja akatambua kwamba siri hiyo imefichuka. Hivyo, muda si muda nikabadilishiwa kazi na kupelekwa jikoni.

  • Mtegemee Yehova—Hakika Atakusaidia
    Mnara wa Mlinzi—2010 | Septemba 1
    • Maisha Yenye Kuridhisha Sana

      Watu fulani wameniuliza kama nimewahi kujuta kwa sababu ya kupigwa na kufungwa kwa ajili ya kumtumikia Mungu. Kinyume cha hilo, ninamshukuru Yehova kwamba nilipata pendeleo la kumtumikia nikiwa pamoja na wengi wa watumishi wake waaminifu. Ninatumaini kwamba mambo ambayo nimejionea yatawatia moyo wengine wamkaribie Mungu hata zaidi na kutomwacha kamwe.

      Watumishi wengi wa Mungu wameteswa sana kwa sababu ya kumtumikia. Lakini, je, hatukuambiwa tutazamie mambo hayo? Biblia inasema, “wote wanaotamani kuishi kwa ujitoaji-kimungu katika ushirika na Kristo Yesu watateswa pia.” (2 Timotheo 3:12) Hata hivyo, maneno ya Zaburi 34:19 yamethibitika kuwa kweli: “Mwadilifu ana misiba mingi, lakini Yehova humkomboa kutoka katika yote hiyo”!

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki