Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Nimethawabishwa kwa Kufanya Mabadiliko
    Mnara wa Mlinzi—2011 | Desemba 15
    • Mwezi wa Agosti mwaka huo, mimi na Gerri tulipokea mwaliko wa kuhudhuria darasa la 20 la Gileadi, ambalo lilianza Septemba. Tukiwa katika shule hiyo, tulitarajia kupokea mgawo wa kwenda katika nchi ya kigeni. Dada yangu Doris alikuwa amehitimu katika darasa la 13 la Gileadi na alikuwa akitumikia nchini Brazili. Mimi na Gerri tulishangaa sana tulipopokea mgawo wa kazi ya mzunguko ili kutembelea makutaniko ya watu weusi katika jimbo la kusini la Alabama! Kwa kadiri fulani jambo hilo lilituvunja moyo, kwa kuwa tulikuwa tukitazamia sana kutumikia katika nchi ya kigeni.

      Kutaniko la kwanza tulilotembelea ni kutaniko lililokuwa huko Huntsville. Tulipofika, tulipelekwa nyumbani kwa dada Mkristo ambaye tungekaa naye. Tulipokuwa tukishusha mizigo yetu tulimsikia akisema kwenye simu, “Watoto wamefika.” Tulikuwa na miaka 24 tu na tulionekana kuwa wenye umri mdogo hata zaidi. Tuliitwa “Watoto” muda wote tulipotumikia katika mzunguko huo.

      Mara nyingi eneo la Kusini liliitwa Eneo la Biblia kwa sababu watu wengi katika eneo hilo waliithamini sana Biblia. Hivyo kwa kawaida tulianzisha mazungumzo kwa kutumia mambo haya matatu:

      (1) Maelezo mafupi kuhusu hali ya dunia.

      (2) Suluhisho ambalo Biblia inatoa.

      (3) Mambo ambayo Biblia inasema tunapaswa kufanya.

      Kisha tulitoa kitabu kinachofaa cha kujifunzia Biblia. Kwa sababu tulipata matokeo mazuri kwa kutumia njia hiyo, nilipewa mgawo katika kusanyiko la New World Society mwaka 1953 huko New York. Katika kusanyiko hilo nilionyesha jinsi ya kutumia mambo hayo matatu katika mahubiri.

      Muda si muda, katika kiangazi cha mwaka wa 1953, nilipewa mgawo wa kutumikia katika mzunguko wa watu weusi upande wa Kusini nikiwa mwangalizi wa wilaya. Eneo letu lilianzia Virginia hadi Florida na kuelekea upande wa magharibi kuanzia Alabama hadi Tennessee. Ndiyo, waangalizi wanaosafiri walihitaji kubadilika kulingana na hali. Kwa mfano, mara nyingi tuliishi katika nyumba ambazo hazikuwa na maji ya bomba na tulioga kwa kutumia karai nyuma ya jiko. Hiyo ndiyo sehemu iliyokuwa na joto zaidi katika nyumba hiyo!

      Tatizo la Ubaguzi wa Rangi

      Ili kutumikia katika eneo la Kusini mtu alihitaji kupanga mambo vizuri na kwa ustadi ili aweze kutimiza shughuli mbalimbali. Watu weusi hawakuruhusiwa kutumia mashine za umma za kufua nguo. Hivyo, Gerri angeenda katika sehemu hizo na kueleza kwamba nguo alizonazo ni za “Bi. Thompson.” Wengi walidhani yeye ni mtumishi na “Bi. Thompson” ndiye mama mwenye nyumba. Waangalizi wa wilaya walipokuwa wakionyesha sinema The New World Society in Action, ningepigia simu watu wa duka la vifaa vya sinema na kuwaambia kwamba wamwekee “Bw. Thompson” kitambaa kikubwa cha kuonyeshea sinema. Baadaye, nilienda kwenye duka hilo na kuchukua kitambaa hicho. Sikuzote tulijiendesha kwa adabu na kwa ujumla tulitimiza huduma yetu bila tatizo.

      Kulikuwa pia na ubaguzi mwingine, ubaguzi wa majimbo, watu waliotoka upande wa Kaskazini walibaguliwa. Wakati fulani gazeti moja la eneo hilo liliripoti kuwa James A. Thompson, Jr., wa Watchtower Bible and Tract Society of New York atatoa hotuba kwenye kusanyiko. Wengine waliposoma gazeti hilo walifikiri kwamba ninatoka New York, na hivyo kibali tulichopewa cha kutumia ukumbi wa shule kikafutwa. Hivyo, nikaenda kwenye kamati ya shule na kuwaeleza kwamba nilisomea huko Chattanooga. Hatimaye tukapewa ruhusa ya kufanya kusanyiko letu la mzunguko.

      Chuki kuelekea jamii fulani iliongezeka hata zaidi katikati ya miaka ya 1950, na nyakati nyingine kulikuwa na jeuri. Katika mwaka wa 1954, baadhi ya Mashahidi walikasirika walipoona kwamba hakuna msemaji mweusi kwenye programu za makusanyiko kadhaa ya wilaya. Tuliwatia moyo ndugu zetu weusi wawe na subira. Kusanyiko lililofuata nikapewa mgawo wa kuwa msemaji. Baada ya hapo, ndugu zaidi weusi kutoka eneo la Kusini wakapewa migawo katika makusanyiko.

      Baada ya muda, jeuri dhidi ya jamii fulani katika eneo la Kusini ilipungua, na hatua kwa hatua makutaniko yakaanza kuungana. Hivyo wahubiri walihitaji kupangwa upya katika makutaniko mbalimbali kutia ndani kurekebisha maeneo ya makutaniko na kugawa upya majukumu ya akina ndugu waliokuwa wakisimamia. Baadhi ya ndugu fulani weupe na weusi hawakupendezwa na mpango huo mpya. Hata hivyo, ndugu na dada wengi walikuwa kama Baba yetu wa mbinguni ambaye hana ubaguzi. Kwa kweli, wengi walikuwa marafiki wakubwa licha ya rangi zao. Familia yetu ilishuhudia jambo hilo katika miaka ya 1930 na 1940 nilipokuwa nikikua.

  • Nimethawabishwa kwa Kufanya Mabadiliko
    Mnara wa Mlinzi—2011 | Desemba 15
    • [Picha katika ukurasa wa 5]

      Baada ya kuhudhuria Gileadi, tulipewa mgawo wa kusafiri katika eneo la Kusini

      [Picha katika ukurasa wa 6]

      Waangalizi wanaosafiri na wake zao wakijitayarisha kwa ajili ya kusanyiko la wilaya la mchanganyiko wa watu weupe na weusi, mwaka wa 1966

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki