Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Kwa Nini Ulimwengu Hauna Umoja?
    Mnara wa Mlinzi—2005 | Juni 1
    • Kwa Nini Ulimwengu Hauna Umoja?

      “Hii ndiyo mara ya kwanza kwa jumuiya ya kimataifa kuungana tangu Vita vya Pili vya Ulimwengu. . . . Hivyo, ulimwengu unaweza kutumia nafasi hii kutimiza ahadi ya muda mrefu ya kutokeza ulimwengu mpya.”

      HIVYO ndivyo alivyosema rais mmoja wa Marekani mwishoni mwa karne ya 20. Wakati huo, matukio katika nchi mbalimbali yalionyesha kwamba muda si muda ulimwengu ungekuwa wenye umoja. Serikali za kimabavu zilianguka, moja baada ya nyingine. Ukuta wa Berlin uliporomoka, na huo ukawa mwanzo wa enzi mpya barani Ulaya. Muungano wa Sovieti, ambao watu wengi katika nchi za Magharibi waliuona kuwa kisababishi cha mizozo ya kimataifa, ulitoweka na watu wengi ulimwenguni wakashangaa. Vita Baridi vilikwisha, na ilitazamiwa kwamba silaha zingepunguzwa, kutia ndani zile za nyuklia. Ni kweli kwamba vita vilitokea katika Ghuba ya Uajemi, lakini vita hivyo vilionwa kuwa tatizo la muda mfupi tu, na watu wengi ulimwenguni waliendelea kujitahidi kutafuta amani.

      Zaidi ya kutazamia mabadiliko ya kisiasa, watu walitarajia maendeleo katika sehemu nyingine za maisha. Hali ya maisha ilikuwa ikiboreka katika maeneo mengi ya ulimwengu. Maendeleo ya kitiba yaliwawezesha madaktari kufanya mambo ambayo hayangewezekana miaka kadhaa mapema. Uchumi ulisitawi haraka katika nchi nyingi hivi kwamba ilitarajiwa kungekuwa na ufanisi ulimwenguni pote. Ilionekana kwamba mambo yako shwari.

      Leo, miaka kadhaa baadaye, tunajiuliza maswali haya: ‘Ni nini kilichotukia? Kwa nini ulimwengu hauna umoja kama ilivyokuwa imeahidiwa?’ Kinyume cha ilivyotarajiwa, inaonekana kwamba mambo yanakwenda kombo. Mara nyingi vyombo vya habari huripoti visa vya milipuko inayosababishwa na wapiganaji wa kujilipua kwa mabomu, mashambulizi ya kigaidi, ongezeko la silaha za maangamizi, na mambo mengine yenye kuhuzunisha. Matukio hayo yanazidi kugawanya ulimwengu. Hivi majuzi, mtaalamu mmoja mashuhuri wa uchumi alisema: “Tumenaswa katika ulimwengu uliojaa jeuri kwa sababu ya matendo ya watu ya kulipiza kisasi.”

      Je, Ulimwengu Una Umoja au Umegawanyika?

      Umoja wa Mataifa ulipoanzishwa, mojawapo ya malengo yake yalikuwa “kusitawisha uhusiano wa kirafiki kati ya mataifa kwa kuheshimu kanuni ya usawa baina ya watu na haki yao ya kujitawala.” Baada ya miaka 60 hivi, je, lengo hilo zuri limefikiwa? La hasha! Inaonekana mataifa yanafikiria “kujitawala” hasa badala ya kuwa na “uhusiano wa kirafiki.” Watu wa jamii na makabila mbalimbali ambao wanajitahidi juu chini kutambuliwa na kujitawala wamesababisha mgawanyiko mwingi ulimwenguni. Umoja wa Mataifa ulipoanzishwa ulikuwa na mataifa 51. Leo una mataifa 191.

      Kama tulivyoona, mwishoni mwa karne ya 20, kulikuwa na matumaini makubwa ya kuwa na umoja ulimwenguni. Tangu wakati huo, matumaini hayo yamedidimia huku wanadamu wakishuhudia kugawanyika kwa ulimwengu hatua kwa hatua. Mgawanyiko na jeuri huko Yugoslavia, mapambano kati ya Chechnya na Urusi, vita vya Iraq, na mauaji makubwa yanayoendelea katika Mashariki ya Kati, yanaonyesha kwamba kuna utengano mkubwa.

      Hakuna shaka kwamba jitihada nyingi za kuleta amani zimefanywa kwa nia njema. Hata hivyo, ni kana kwamba ulimwengu hauwezi kuwa na umoja. Basi, watu wengi wanajiuliza: ‘Kwa nini ni vigumu sana kuwa na umoja ulimwenguni? Ulimwengu unaelekea wapi?’

  • Ulimwengu Unaelekea Wapi?
    Mnara wa Mlinzi—2005 | Juni 1
    • Ulimwengu Unaelekea Wapi?

      ULIMWENGU WENYE UMOJA. Maneno hayo yanavutia sana. Bila shaka, kila mtu angependa ulimwengu uwe na umoja. Naam, watu wamezungumzia sana umoja. Viongozi wa ulimwengu wameuzungumzia mara nyingi katika mikutano yao. Mnamo Agosti 2000, zaidi ya viongozi wa dini 1,000 walihudhuria Mkutano wa Milenia Kuhusu Amani ya Ulimwengu kwenye jengo la shirika la Umoja wa Mataifa huko New York. Walizungumzia masuluhisho ya mizozo ya ulimwengu. Lakini hata mkutano wenyewe ulikuwa na mizozo kama tu ilivyo ulimwenguni. Mtaalamu mmoja wa sheria za Kiislamu kutoka Jerusalem alikataa kuuhudhuria eti kwa sababu rabi Myahudi alikuwepo. Wengine waliudhika kwa sababu Dalai Lama hakukaribishwa kuhudhuria siku mbili za kwanza eti kwa sababu hilo lingekasirisha China.

      Mnamo Oktoba 2003, mkutano wa Ushirikiano wa Kiuchumi wa Mataifa ya Asia na Pasifiki ulifanywa huko Thailand. Mataifa 21 yaliyohudhuria mkutano huo yalizungumzia masuala ya usalama ulimwenguni. Yaliazimia kuvunja makundi ya magaidi na kukubaliana kuhusu njia za kufanya ulimwengu uwe salama zaidi. Lakini mkutano huo ulipokuwa ukiendelea, baadhi ya wawakilishi waliteta kuhusu maelezo ya waziri mkuu mmoja ambayo yalitajwa kuwa mashtaka yaliyojaa chuki kuwaelekea Wayahudi.

      Kwa Nini Hakuna Umoja?

      Ijapokuwa jitihada za kuleta umoja ulimwenguni zimezungumziwa sana, hatujaona mabadiliko makubwa. Licha ya jitihada za watu wengi wenye nia nzuri, kwa nini wanadamu wameshindwa kuleta umoja ulimwenguni hata katika karne ya 21?

      Swali hilo lilijibiwa kwa sehemu na mmoja kati ya mawaziri wakuu waliohudhuria ule mkutano wa ushirikiano wa kiuchumi. Alisema hivi, “Kuna jambo hili linaloitwa utaifa.” Naam, wanadamu wamelewa utaifa. Kila taifa na kabila linachochewa na tamaa ya kujitawala. Hali ya mataifa kutaka kujitawala na roho ya mashindano na pupa hufanya mambo yawe mabaya zaidi. Mara nyingi, masilahi ya taifa yasipopatana na masilahi ya watu ulimwenguni pote, masilahi ya taifa ndiyo hutangulizwa.

      Maneno ya mtunga-zaburi, “tauni inayosababisha shida,” yanaufafanua vizuri utaifa. (Zaburi 91:3) Utaifa umekuwa kama tauni inayowakumba wanadamu, na umesababisha mateso makubwa sana. Utaifa umekuwepo kwa karne nyingi, nao umetokeza chuki kuelekea watu wengine. Leo, utaifa unaendelea kusababisha migawanyiko, na viongozi hawajafaulu kuukomesha.

      Viongozi wengi wanatambua kwamba utaifa na ubinafsi ndivyo visababishi vya matatizo ya ulimwengu. Kwa mfano, U Thant, aliyekuwa Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa, alisema: “Matatizo mengi tunayokabili leo yamesababishwa na maoni yenye kasoro . . . Mojawapo ya maoni hayo ni kushikilia sana utaifa, yaani, ‘vyovyote vile, taifa langu ndilo bora.’” Hata hivyo, leo mataifa yenye ubinafsi mwingi yanazidi kung’ang’ania utawala. Mataifa yenye nguvu hayataki kupunguza mamlaka yake hata kidogo. Kwa mfano, gazeti International Herald Tribune lilisema hivi kuhusu Jumuiya ya Ulaya: “Bado mashindano na kutoaminiana ndicho kiini cha siasa za Ulaya. Mataifa mengi ya Jumuiya ya Ulaya yangali yanaona kwamba haifai kwa taifa lingine katika jumuiya hiyo kuwa na mamlaka zaidi na kuongoza mambo.”

      Neno la Mungu, Biblia, linafafanua kwa usahihi matokeo ya utawala wote wa wanadamu, kwa kusema: “Mwanadamu amemtawala mwanadamu kwa kumuumiza.” (Mhubiri 8:9) Kwa kuugawanya ulimwengu katika mataifa mbalimbali, wanadamu wameona kanuni hii ya Biblia ikitimia wakiwa vikundi au mtu mmoja-mmoja: “Mtu anayejitenga na wengine atatafuta mapendezi yake mwenyewe; atashindana na hekima yote inayotumika.”—Methali 18:1.

      Muumba wetu, ambaye anajua tunachohitaji, hakukusudia kamwe wanadamu waanzishe serikali zao na kujitawala. Kwa kuanzisha serikali zao, wanadamu wamepuuza kusudi la Mungu nao hawatambui kwamba vitu vyote ni vyake. Zaburi 95:3-5 inasema: “Yehova ni Mungu mkuu na Mfalme mkuu juu ya miungu mingine yote, yeye ambaye mkononi mwake mna vina vya ndani sana vya dunia na ambaye vilele vya milima ni vyake; ambaye bahari, aliyoiumba yeye mwenyewe, ni yake na ambaye mikono yake mwenyewe iliifanyiza nchi kavu.” Mungu ndiye ana haki ya kutawala, na watu wote wanapaswa kujitiisha kwake. Mataifa yanapinga mapenzi ya Mungu kwa kuendelea kutetea serikali zao.—Zaburi 2:2.

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki