-
Undugu Wenye UmojaTengenezo Linalofanya Mapenzi ya Yehova
-
-
KUBADILI MTAZAMO
3 Ikiwa wengine wanaona ni vigumu kushinda ubaguzi wa rangi, wa kisiasa, wa kitabaka, au ubaguzi wa aina nyingine yoyote, wanaweza kuwafikiria Wakristo Wayahudi wa karne ya kwanza, ambao walihitaji kufanya juu chini ili waache kuwabagua watu wengine ambao hawakuwa wa dini ya Kiyahudi. Petro alipoagizwa aende nyumbani kwa Kornelio, ofisa wa jeshi wa kikosi cha Roma, Yehova alimtayarisha Petro kwa ajili ya mgawo huo kwa njia ya fadhili.—Matendo sura ya 10.
4 Katika maono, Petro aliambiwa achinje na kula wanyama fulani waliokuwa najisi kulingana na desturi za Wayahudi. Petro alipokataa, sauti kutoka mbinguni ilimwambia: “Acha kuviita najisi vitu ambavyo Mungu amevitakasa.” (Mdo. 10:15) Mungu alihitaji kuingilia kati ili Petro abadili mtazamo wake kuhusu mgawo ambao angepewa wa kwenda kumtembelea mtu wa mataifa. Alipotii mwelekezo wa Yehova, Petro aliwatangazia hivi wale waliokusanyika: “Mnajua jinsi ilivyo kinyume cha sheria kwa Myahudi kushirikiana au kumkaribia mtu wa jamii nyingine, lakini Mungu amenionyesha kwamba sipaswi kumwita mtu yeyote najisi au asiye safi. Basi nilipoitwa nilikuja bila kupinga.” (Mdo. 10:28, 29) Baadaye, Petro alijionea uthibitisho wa kwamba Yehova alikuwa amemkubali Kornelio na watu wa nyumbani mwake.
5 Sauli wa Tarso, Farisayo mwenye elimu ya juu, alihitaji kujinyenyekeza ili kushirikiana na watu wa jamii ambayo hapo zamani hangekubali kushirikiana nao. Hata alihitaji kukubali mwongozo kutoka kwao. (Mdo. 4:13; Gal. 1:13-20; Flp. 3:4-11) Ni wazi kwamba watu kama vile Sergio Paulo, Dionisio, Damari, Filemoni, Onesimo, na wengine walihitaji kubadili kabisa mtazamo wao walipokubali habari njema na kuwa wanafunzi wa Yesu Kristo.—Mdo. 13:6-12; 17:22, 33, 34; Flm. 8-20.
KUDUMISHA UMOJA WETU WA ULIMWENGUNI POTE
6 Bila shaka upendo wa ndugu na dada katika kutaniko lenu ulikusaidia umkaribie Yehova na tengenezo lake. Uliona alama ya pekee ya upendo na umoja ambayo inawatambulisha wanafunzi wa kweli wa Yesu Kristo, kama alivyosema: “Ninawapa ninyi amri mpya, kwamba mpendane; kama vile ambavyo nimewapenda, nanyi mpendane vivyo hivyo. Kwa jambo hili wote watajua kwamba ninyi ni wanafunzi wangu—mkiwa na upendo miongoni mwenu.” (Yoh. 13:34, 35) Ulimthamini zaidi Yehova na tengenezo lake ulipotambua kwamba upendo unaoonyeshwa kutanikoni ni kionjo tu cha upendo unaoonyeshwa na ushirika wa ulimwenguni pote wa watu wa Yehova. Unajionea utimizo wa unabii wa Biblia wa kukusanywa kwa watu katika siku za mwisho ili wamwabudu Yehova kwa amani na umoja.—Mika 4:1-5.
7 Kwa kuwa kuna mambo mengi leo yanayosababisha migawanyiko, ni nani angefikiri kwamba ingewezekana kuwaunganisha watu “kutoka mataifa yote na makabila na jamii na lugha”? (Ufu. 7:9) Fikiria tofauti zilizopo kati ya jamii ya watu wenye elimu ya kisasa na wale wanaoshikilia desturi za kale za kikabila. Hebu fikiria mizozo ya kidini kati ya watu wa kabila na taifa moja. Kwa sababu ya uzalendo, watu wamegawanyika zaidi kisiasa kuliko wakati mwingine wowote. Pia, unapofikiria tofauti kubwa za kiuchumi na mambo mengine mengi yanayosababisha migawanyiko, kuwaunganisha watu wa mataifa, lugha, vikundi, na tabaka mbalimbali katika kifungo kisichoweza kuvunjika cha upendo na amani, ni muujiza ambao unaweza kufanywa tu na Mungu Mweza-Yote.—Zek. 4:6.
8 Lakini umoja huo ni halisi, na ulipojiweka wakfu na kubatizwa na kuwa Shahidi wa Yehova, ulijiunga na undugu huo. Ili ufaidike na umoja huo, una jukumu la kuudumisha. Unaweza kufanya hivyo kwa kutii maneno ya mtume Paulo katika Wagalatia 6:10: “Tukiwa bado na nafasi, acheni tuwatendee watu wote mema, na hasa wale ambao ni ndugu zetu katika imani.” Pia, tunafuata ushauri huu: “Msifanye jambo lolote kwa ugomvi au kwa kujisifu, bali kwa unyenyekevu mwaone wengine kuwa bora kuliko ninyi, huku mkiangalia, si faida zenu wenyewe, bali pia faida za wengine.” (Flp. 2:3, 4) Maadamu tunajizoeza kuwaona ndugu na dada zetu kama Yehova anavyowaona, wala si kulingana na wanavyoonekana kwa nje, tutaendelea kufurahia uhusiano wenye amani pamoja nao.—Efe. 4:23, 24.
KUTUNZANA
9 Kama mtume Paulo alivyofafanua, wote kutanikoni hawana mgawanyiko, bali ni viungo vya mwili mmoja vinavyotunzana kwa njia ileile. (1 Kor. 12:14-26) Huenda tukawa mbali sana na baadhi ya ndugu zetu, lakini bado tunawahangaikia. Baadhi ya ndugu zetu wakiteswa, sisi huhuzunika sana. Ikiwa baadhi ya akina ndugu wana uhitaji fulani au wamekumbwa na msiba, vita, au mizozo ya kikabila, sisi sote hujitahidi sana kutafuta njia za kuwasaidia kiroho na vilevile kimwili.—2 Kor. 1:8-11.
10 Kila siku sisi sote tunapaswa kusali kwa ajili ya ndugu zetu. Kuna ndugu wanaoshawishiwa kufanya mambo mabaya. Huenda mateso ya baadhi ya ndugu zetu yanajulikana. Hata hivyo huenda tusijue upinzani ambao wengine wanakabili kila siku kutoka kwa wafanyakazi wenzao na familia zilizogawanyika kidini. (Mt. 10:35, 36; 1 The. 2:14) Sote tunahangaishwa na hali hizo kwa sababu sisi ni undugu wa ulimwenguni pote. (1 Pet. 5:9) Pia, miongoni mwetu tuna wale wanaofanya utumishi wa Yehova kwa bidii, wakiongoza katika kazi ya kuhubiri na kusimamia makutaniko. Na kuna wale wanaosimamia kazi ya ulimwenguni pote. Wote wanahitaji sala zetu, na kupitia sala, tunaonyesha kwamba tunawajali na kuwapenda ndugu zetu kikweli hata wakati ambapo hakuna lolote ambalo sisi wenyewe tunaweza kufanya ili kuwasaidia.—Efe. 1:16; 1 The. 1:2, 3; 5:25.
11 Kwa sababu ya misukosuko ya siku hizi za mwisho, watu wa Yehova wanapaswa kuwa tayari kusaidiana. Wakati mwingine, majanga kama vile matetemeko ya nchi na mafuriko yanapotokea, huenda tukahitaji kukusanya na kutuma misaada mingi ya kimwili. Wakristo wa karne ya kwanza waliweka mfano mzuri katika jambo hilo. Wakikumbuka ushauri wa Yesu, wanafunzi huko Antiokia walifurahi kutuma msaada kwa ndugu zao waliokuwa Yudea. (Mdo. 11:27-30; 20:35) Baadaye, mtume Paulo aliwatia moyo Wakorintho waunge mkono mipango ya kutoa msaada kwa utaratibu. (2 Kor. 9:1-15) Leo, ndugu zetu wanapopatwa na hali ngumu na kuhitaji msaada, tengenezo na Wakristo mmoja-mmoja hutenda haraka na kuandaa msaada unaohitajika.
WAMECHAGULIWA ILI KUFANYA MAPENZI YA YEHOVA
12 Undugu wetu wenye umoja wa ulimwenguni pote umepangwa ili kufanya mapenzi ya Yehova. Wakati huu, mapenzi yake ni kwamba habari njema ya Ufalme ihubiriwe katika dunia yote ili kuwa ushahidi kwa mataifa yote. (Mt. 24:14) Tunapofanya kazi hiyo, ni mapenzi ya Yehova kwamba sikuzote mwenendo wetu upatane na viwango vyake vya juu vya maadili. (1 Pet. 1:14-16) Ili kutimiza kazi ya Yehova, sote tunapaswa kuwa tayari kujitiisha kila mmoja kwa mwenzake na kuunga mkono kazi ya kuhubiri habari njema. (Efe. 5:21) Huu si wakati wa kutafuta mapendezi yetu bali ni wakati wa kujitahidi kabisa kutanguliza Ufalme wa Mungu maishani mwetu. (Mt. 6:33) Tunapozingatia jambo hilo na kufanya kazi pamoja kwa umoja kwa ajili ya habari njema, tunaridhika na kupata shangwe sasa na kutazamia baraka za milele.
13 Tukiwa Mashahidi wa Yehova, sisi ni watu wa pekee, watu waliochaguliwa kutoka kwa wanadamu wengine wakiwa watu safi ili tumtumikie Mungu wetu kwa bidii. (Tito 2:14) Ibada yetu kwa Yehova inatufanya tuwe tofauti. Mbali na kufanya kazi bega kwa bega na ndugu zetu duniani pote, tunazungumza lugha moja ya kweli na kutenda kupatana na kweli tunayozungumza. Hilo lilitabiriwa Yehova alipotangaza hivi kupitia nabii Sefania: “Nitabadili lugha ya mataifa iwe lugha safi, ili wote waweze kuliitia jina la Yehova, wamtumikie bega kwa bega.”—Sef. 3:9.
14 Kisha, kupitia roho takatifu, Yehova alimwongoza Sefania kufafanua undugu wa ulimwenguni pote ambao ni halisi leo: “Waisraeli watakaobaki hawatatenda mambo yasiyo ya uadilifu; hawatasema uwongo, wala hawatakuwa na ndimi za udanganyifu vinywani mwao; watakula na kulala, na hakuna yeyote atakayewaogopesha.” (Sef. 3:13) Baada ya kuelewa Neno la Yehova la kweli, kufanya upya akili zetu, na kupatanisha maisha yetu na viwango vya Yehova, tunaweza kufanya kazi kwa umoja. Tunatimiza mambo ambayo wale walio na mtazamo wa kimwili wanafikiri kwamba haiwezekani kuyatimiza. Kwa kweli, sisi ni watu tofauti, watu wa Mungu, tunaomletea heshima duniani pote.—Mika 2:12.
-
-
Shikamana na Tengenezo la YehovaTengenezo Linalofanya Mapenzi ya Yehova
-
-
SURA YA 17
Shikamana na Tengenezo la Yehova
MWANAFUNZI Yakobo aliandika hivi: “Mkaribieni Mungu, naye atawakaribia ninyi.” (Yak. 4:8) Ijapokuwa sisi si wakamilifu, Yehova hayuko juu sana au mbali sana asiweze kusikia sala zetu. (Mdo. 17:27) Tunawezaje kumkaribia Mungu? Kwa kusitawisha uhusiano wa karibu pamoja na Yehova unaotia ndani kusali kwa bidii. (Zab. 39:12) Pia, tunaweza kusitawisha uhusiano wa karibu pamoja na Mungu kwa kujifunza kwa ukawaida Neno lake, Biblia. Tunapofanya hivyo, tunazidi kumjua Yehova Mungu, makusudi yake, na mapenzi yake. (2 Tim. 3:16, 17) Kwa njia hiyo, tunajifunza kumpenda Yehova, tunasitawisha woga unaofaa na kuepuka kumchukiza.—Zab. 25:14.
2 Hata hivyo, njia pekee ya kumkaribia Yehova ni kupitia Mwana wake, Yesu. (Yoh. 17:3; Rom. 5:10) Hakuna mwanadamu anayeweza kutusaidia kufahamu maoni na hisia za Yehova kama alivyofanya Yesu. Alikuwa na uhusiano wa karibu sana na Baba yake hivi kwamba alisema hivi: “Hakuna mtu anayemjua Mwana isipokuwa Baba, wala hakuna anayemjua Baba isipokuwa Mwana, na yeyote ambaye Mwana anapenda kumfunulia.” (Luka 10:22) Kwa hiyo, tunapojifunza mambo ambayo Injili zinafunua kuhusu maoni na hisia za Yesu, kwa kweli tunajifunza maoni na hisia za Yehova. Ujuzi huo unatuwezesha kumkaribia zaidi Mungu wetu.
3 Chini ya ukichwa wa Mwana wa Mungu, tunasitawisha uhusiano wa karibu sana pamoja na Yehova kwa kushikamana na sehemu inayoonekana ya tengenezo la Yehova linalotufundisha kufanya mapenzi ya Mungu. Kama ilivyotabiriwa kwenye Mathayo 24:45-47, Bwana, Yesu Kristo, amemweka rasmi “mtumwa mwaminifu na mwenye busara,” ili aliandalie kutaniko ‘chakula kwa wakati unaofaa.’ Leo, mtumwa mwaminifu hutuandalia chakula kingi cha kiroho. Kupitia mtumwa huyo, Yehova hutushauri tusome Neno lake kila siku, tuhudhurie mikutano ya Kikristo kwa ukawaida, na kushiriki kwa bidii katika kazi ya kuhubiri “habari njema ya Ufalme.” (Mt. 24:14; 28:19, 20; Yos. 1:8; Zab. 1:1-3) Hatutaki kamwe kuwa na maoni yasiyofaa kuelekea mtumwa huyo. Tunapaswa kujitahidi kushikamana na sehemu inayoonekana ya tengenezo la Yehova na kufuata mwelekezo wake. Hilo litatufanya tumkaribie zaidi Mungu wetu, Yehova, na litatuimarisha na kutulinda licha ya majaribu.
KWA NINI MAJARIBU YANAONGEZEKA?
4 Labda umekuwa katika kweli kwa miaka mingi. Ikiwa ndivyo, bila shaka unajua changamoto za kuvumilia utimilifu wetu unapojaribiwa. Hata ikiwa umeanza kumjua Yehova na kushirikiana na watu wake hivi karibuni, bila shaka unajua kwamba Shetani Ibilisi humpinga mtu yeyote anayejitiisha chini ya enzi kuu ya Yehova. (2 Tim. 3:12) Hivyo, iwe umevumilia machache au mengi, usiogope wala kuvunjika moyo. Yehova anaahidi kwamba atakutegemeza na kukuthawabisha kwa kukukomboa na kukupa uzima wakati ujao.—Ebr. 13:5, 6; Ufu. 2:10.
-