Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Umoja Unatambulisha Ibada ya Kweli
    Mnara wa Mlinzi—2010 | Septemba 15
    • Umoja Unatambulisha Ibada ya Kweli

      “Nitawaunganisha, kama kundi zizini.”—MIKA 2:12.

      1. Uumbaji unaonyesha jinsi gani hekima ya Mungu?

      MTUNGA-ZABURI mmoja alisema hivi: “Jinsi kazi zako zilivyo nyingi, Ee Yehova! Zote umezifanya kwa hekima. Dunia imejaa vitu ulivyotokeza.” (Zab. 104:24) Hekima ya Mungu inaonekana wazi katika ushirikiano uliopo kati ya mamilioni ya jamii mbalimbali za mimea, wadudu, wanyama, na bakteria katika mfumo wenye kustaajabisha sana wa viumbe duniani. Pia, katika mwili wako, kuna maelfu ya mifumo mbalimbali, inayotia ndani viungo vikubwa na pia mashini ndogondogo za molekuli katika chembe zako. Vitu hivyo vyote vinafanya kazi pamoja ili kukuwezesha kuwa mtu mzima mwenye afya nzuri.

      2. Kama picha iliyo kwenye ukurasa wa 13 inavyoonyesha, kwa nini umoja wa Wakristo ulionekana kuwa muujiza?

      2 Yehova aliwaumba wanadamu ili wategemeane. Jamii ya wanadamu ina sura, nyutu, na ustadi mbalimbali. Zaidi ya hayo, aliwaumba wanadamu wa kwanza wakiwa na sifa za kimungu ambazo zingewawezesha kushirikiana na kutegemeana. (Mwa. 1:27; 2:18) Hata hivyo, leo ulimwengu wa wanadamu kwa ujumla umetenganishwa mbali na Mungu na ulimwengu wote haujawahi kamwe kutenda kwa umoja. (1 Yoh. 5:19) Kwa hiyo, tukikumbuka kwamba kutaniko la Kikristo la karne ya kwanza lilikuwa na watu wa kila aina kama vile watumwa Waefeso, wanawake mashuhuri Wagiriki, wanaume Wayahudi wenye elimu, na watu ambao zamani waliabudu sanamu, ni wazi kwamba umoja wao ulionekana kuwa muujiza.—Mdo. 13:1; 17:4; 1 The. 1:9; 1 Tim. 6:1.

      3. Biblia inaeleza jinsi gani umoja wa Wakristo, na tutazungumzia nini katika habari hii?

      3 Ibada ya kweli inawawezesha watu kushirikiana kwa umoja wakiwa viungo vya mwili wetu mmoja. (Soma 1 Wakorintho 12:12, 13.) Tutazungumzia mambo yafuatayo katika habari hii: Ibada ya kweli inawaunganisha watu jinsi gani? Kwa nini Yehova peke yake ndiye anayeweza kuwaunganisha mamilioni ya watu kutoka katika mataifa yote? Yehova anatusaidia kushinda mambo gani ambayo yanawazuia wanadamu kuwa na umoja? Na kuhusu umoja, Ukristo wa kweli unatofautiana namna gani na dini zinazodai kuwa za Kikristo?

      Ibada ya Kweli Inawaunganisha Watu Jinsi Gani?

      4. Ibada ya kweli inawaunganisha watu jinsi gani?

      4 Watu ambao wanaishi kupatana na ibada ya kweli wanatambua kwamba Yehova ndiye aliye na haki ya kuwa Mwenye Enzi Kuu ya ulimwengu wote kwa sababu yeye ndiye aliyeumba vitu vyote. (Ufu. 4:11) Kwa hiyo, ingawa Wakristo wa kweli wanaishi katika jamii mbalimbali chini ya hali tofauti-tofauti, wote wanatii sheria zilezile za Mungu na wanaishi kupatana na kanuni zilezile za Biblia. Kwa kufaa, waabudu wote wa kweli wanamwita Yehova, “Baba.” (Isa. 64:8; Mt. 6:9) Hivyo, wote ni ndugu wa kiroho na wanaweza kufurahia umoja wenye kuvutia ambao unafafanuliwa hivi na mtunga-zaburi: “Tazama! Jinsi ilivyo vyema na jinsi inavyopendeza ndugu kukaa pamoja kwa umoja!”—Zab. 133:1.

      5. Ni sifa gani inayochangia umoja wa waabudu wa kweli?

      5 Ingawa Wakristo wa kweli si wakamilifu, wanaabudu pamoja kwa umoja kwa sababu wamejifunza kupendana. Yehova anawafundisha kupendana kwa njia ambayo mtu mwingine yeyote hawezi. (Soma 1 Yohana 4:7, 8.) Neno lake linasema hivi: “Jivikeni upendo mwororo wenye huruma, fadhili, unyenyekevu wa akili, upole, na ustahimilivu. Endeleeni kuvumiliana na kusameheana kwa hiari ikiwa yeyote ana sababu ya kulalamika juu ya mwingine. Kama vile Yehova alivyowasamehe ninyi kwa hiari, nanyi fanyeni vivyo hivyo pia. Lakini, zaidi ya mambo haya yote, jivikeni upendo, kwa maana huo ni kifungo kikamilifu cha muungano.” (Kol. 3:12-14) Kifungo hicho kikamilifu cha muungano, yaani, upendo, ni sifa ambayo hasa inawatambulisha Wakristo wa kweli. Je, wewe binafsi umejionea kwamba umoja ni sifa inayotofautisha ibada ya kweli?—Yoh. 13:35.

      6. Tumaini la Ufalme linatusaidia jinsi gani kuwa na umoja?

      6 Pia, waabudu wa kweli wana umoja kwa sababu wanautazamia Ufalme wa Mungu ambao ndio tumaini pekee la wanadamu. Wanajua kwamba hivi karibuni Ufalme wa Mungu utachukua mahali pa serikali za wanadamu na kuwabariki wanadamu watiifu kwa kuwaletea amani ya kweli yenye kudumu. (Isa. 11:4-9; Dan. 2:44) Hivyo, Wakristo wanatii maneno haya ambayo Yesu alisema kuhusu wafuasi wake: “Wao si sehemu ya ulimwengu, kama vile ambavyo mimi si sehemu ya ulimwengu.” (Yoh. 17:16) Wakristo wa kweli hawaungi mkono upande wowote katika mapambano ya ulimwengu; hivyo, wanakuwa na umoja hata watu wengine wanapopigana.

      Chanzo Kikuu cha Maagizo ya Kiroho

      7, 8. Maagizo ya Biblia yanachangia umoja wetu kwa njia gani?

      7 Wakristo wa karne ya kwanza walikuwa na umoja kwa sababu wote walipata kitia-moyo kutoka chanzo kilekile. Walitambua kwamba Yesu alikuwa akilifundisha na kuliongoza kutaniko kupitia baraza linaloongoza, ambalo lilifanyizwa na mitume na wanaume wazee huko Yerusalemu. Wanaume hao waliojitolea walifanya maamuzi kwa kutegemea Neno la Mungu na waliwatuma waangalizi wanaosafiri wapeleke maagizo yao kwenye makutaniko katika nchi nyingi. Kuhusu waangalizi fulani kama hao, Biblia inasema hivi: “Walipoendelea kusafiri kupitia katika majiji walikuwa wakiwapa wale waliokuwa huko maagizo yaliyokuwa yameamuliwa na mitume na wanaume wazee waliokuwa katika Yerusalemu ili wayashike.”—Mdo. 15:6, 19-22; 16:4.

      8 Vivyo hivyo leo, Baraza Linaloongoza ambalo linafanyizwa na Wakristo waliotiwa mafuta kwa roho linachangia umoja katika kutaniko la ulimwenguni pote. Baraza Linaloongoza linachapisha vichapo vya lugha nyingi vinavyotutia moyo kiroho. Chakula hicho cha kiroho kinategemea Neno la Mungu. Hivyo basi, mambo yanayofundishwa hayatoki kwa wanadamu bali kwa Yehova.—Isa. 54:13.

      9. Kazi yetu tuliyopewa na Mungu inatusaidia jinsi gani kuwa na umoja?

      9 Pia, waangalizi Wakristo wanadumisha umoja kwa kuongoza katika kazi ya kuhubiri. Roho ya kushirikiana ambayo inawaunganisha wale wanaofanya kazi pamoja katika utumishi wa Mungu ni yenye nguvu zaidi kuliko roho ambayo inawaunganisha wengine katika ulimwengu ambao wanakutana katika shughuli za kijamii tu. Kutaniko la Kikristo halikuanzishwa kwa kusudi la kuwa chama cha kijamii bali lilianzishwa ili limheshimu Yehova na kutimiza kazi fulani, yaani, kazi ya kuhubiri habari njema, kufanya wanafunzi, na kulijenga kutaniko. (Rom. 1:11, 12; 1 The. 5:11; Ebr. 10:24, 25) Hivyo, mtume Paulo aliwaambia hivi Wakristo: “Mnasimama imara katika roho moja, kwa nafsi moja mkikazana pamoja kwa ajili ya imani ya habari njema.”—Flp. 1:27.

      10. Ni mambo gani mbalimbali yanayotuunganisha tukiwa watu wa Mungu?

      10 Kwa hiyo, tukiwa watu wa Yehova, tuna umoja kwa sababu tunakubali enzi kuu ya Yehova, tunawapenda ndugu zetu, tunatumaini Ufalme wa Mungu, na tunawaheshimu wale ambao Mungu anatumia kutuongoza. Yehova anatusaidia kushinda mitazamo fulani ambayo inaweza kuharibu umoja wetu kwa sababu ya hali yetu ya kutokamilika.—Rom. 12:2.

      Kushinda Kiburi na Wivu

      11. Kwa nini kiburi kinawatenganisha watu, na Yehova anatusaidia jinsi gani kukishinda?

      11 Kiburi kinawatenganisha watu. Mtu mwenye kiburi anapenda kujiona kuwa bora zaidi kuliko wengine na kwa kawaida anapata furaha ya kichoyo kwa kujigamba. Lakini mara nyingi mtazamo huo unazuia umoja, wale wanaomsikia mtu huyo akijigamba wanaweza kuona wivu. Mwanafunzi Yakobo anatuambia hivi waziwazi: “Majivuno yote ya namna hiyo ni maovu.” (Yak. 4:16) Si jambo la upendo kuwatendea wengine kana kwamba wao ni watu wasiofaa. Kwa kweli, Yehova anaweka mfano katika kuonyesha unyenyekevu kwa sababu anashughulika na watu wasio wakamilifu kama sisi. Daudi aliandika hivi: “Unyenyekevu wako [Mungu] ndio hunifanya niwe mkuu.” (2 Sam. 22:36) Neno la Mungu linatusaidia kushinda kiburi kwa kutufundisha kufikiri kwa njia inayofaa. Paulo aliongozwa na roho ya Mungu kuuliza hivi: “Ni nani anayekufanya wewe kuwa tofauti na mwingine? Kwa kweli, una nini ambacho hukupokea? Basi, ikiwa kwa kweli ulikipokea, kwa nini unajisifu kana kwamba hukukipokea?”—1 Kor. 4:7.

      12, 13. (a) Kwa nini ni rahisi kuwaonea wengine wivu? (b) Matokeo yanakuwa nini tunapowaona wengine kama Yehova anavyowaona?

      12 Jambo lingine ambalo linawazuia watu kuwa na umoja ni wivu. Kwa sababu ya hali ya kutokamilika ambayo tumerithi, sisi sote tuna “mwelekeo wa kuona wivu,” na mara kwa mara hata Wakristo wa miaka mingi wanawaonea wengine wivu kwa sababu ya hali zao, mali, mapendeleo, au uwezo wao. (Yak. 4:5) Kwa mfano, ndugu mwenye familia anaweza kumwonea wivu mhudumu wa wakati wote kwa sababu ya mapendeleo yake, bila kutambua kwamba huenda pia mhudumu huyo wa wakati wote akamwonea wivu kidogo mwanamume huyo mwenye familia ambaye ana watoto. Tunaweza jinsi gani kuuzuia wivu usivuruge umoja wetu?

      13 Ili kutusaidia kuepuka wivu, kumbuka kwamba Biblia inawalinganisha washiriki wa kutaniko la Kikristo ambao ni watiwa-mafuta na sehemu za mwili wa mwanadamu. (Soma 1 Wakorintho 12:14-18.) Kwa mfano, ingawa huenda jicho lako linaonekana kuwa la maana zaidi kuliko moyo wako, je, viungo vyote viwili si vyenye thamani kwako? Vivyo hivyo, Yehova anawathamini washiriki wote wa kutaniko hata ingawa huenda wengine wakawa mashuhuri zaidi kuliko wengine kwa muda fulani. Basi, acheni tuwaone ndugu zetu kama Yehova anavyowaona. Badala ya kuwaonea wengine wivu, tunaweza kuonyesha kwamba tunawajali na kupendezwa nao kibinafsi. Kwa kufanya hivyo, tunawasaidia wengine waone tofauti iliyopo kati ya Wakristo wa kweli na washiriki wa makanisa ya dini zinazodai kuwa za Kikristo.

      Dini Zinazodai Kuwa za Kikristo Zina Migawanyiko

      14, 15. Ukristo wa waasi-imani uligawanyika jinsi gani?

      14 Umoja wa Wakristo wa kweli ni tofauti kabisa na mizozano ambayo iko katika makanisa ya dini zinazodai kuwa za Kikristo. Kufikia karne ya nne, Ukristo wa waasi-imani ulikuwa umeenea sana hivi kwamba maliki mpagani wa Roma akaanza kuongoza Ukristo huo, na hilo lilifanya dini zinazodai kuwa za Kikristo zisitawi. Kisha, falme nyingi ziligawanyika haraka kutoka Roma na kuanzisha makanisa yake ya Kitaifa.

      15 Nyingi kati ya falme hizo zilipigana zenyewe kwa karne nyingi. Katika karne ya 17 na 18, watu huko Marekani, Ufaransa, na Uingereza waliwachochea wengine wajitoe kwa ajili ya Taifa lao, na hivyo utaifa au uzalendo, ukawa kama dini. Katika karne ya 19 na 20, uzalendo ulianza kutawala fikira za wanadamu wengi. Mwishowe, makanisa yanayodai kuwa ya Kikristo yaligawanyika na kuanzisha madhehebu mengi sana, na idadi kubwa ya madhehebu hayo inaunga mkono uzalendo. Wafuasi wa makanisa hata wameenda vitani na kupigana na waamini wenzao wa taifa lingine. Leo, dini zinazodai kuwa za Kikristo zimegawanyika kwa sababu ya imani mbalimbali za madhehebu na uzalendo.

      16. Ni mambo gani ambayo yanasababisha migawanyiko katika dini zinazodai kuwa za Kikristo?

      16 Katika karne ya 20, mamia ya madhehebu fulani ya dini zinazodai kuwa za Kikristo yalijaribu kuleta umoja kwa kuanzisha muungano wa madhehebu ya Kikristo. Lakini baada ya kujitahidi kwa miaka mingi sana, ni makanisa machache ambayo yameungana, na watu wanaoenda kanisani bado wamegawanyika kwa sababu ya masuala yanayohusu mageuzi, kutoa mimba, ngono kati ya watu wa jinsia moja, na wanawake kuwekwa rasmi kuwa makasisi. Katika dini fulani zinazodai kuwa za Kikristo, viongozi wa makanisa wanajaribu kuwaunganisha watu kutoka katika madhehebu mbalimbali na kutotilia maanani mafundisho ambayo yalisababisha migawanyiko zamani. Hata hivyo, kutotilia maanani mafundisho hayo kunawaacha watu wakiwa na imani dhaifu na bila shaka hakuunganishi dini zinazodai kuwa za Kikristo ambazo zimegawanyika.

      Ibada ya Kweli Inashinda Uzalendo

      17. Ilitabiriwa kwamba ibada ya kweli ingewaunganisha watu jinsi gani “katika siku za mwisho”?

      17 Ingawa sasa wanadamu wamegawanyika kabisa kuliko wakati mwingine wowote, waabudu wa kweli wanaendelea kuwa tofauti kwa sababu ya umoja wao. Mika, nabii wa Mungu alitabiri hivi: “Nitawaunganisha, kama kundi zizini.” (Mika 2:12) Mika alitabiri kwamba ibada ya kweli ingeinuliwa juu ya aina nyingine zote za ibada, iwe ni ibada za miungu ya uwongo au ni kuabudu Taifa kama mungu. Aliandika hivi: “Itatukia katika siku za mwisho kwamba mlima wa nyumba ya Yehova utawekwa imara juu ya kilele cha milima, nao utainuliwa juu ya vilima; na vikundi vya watu vitamiminika huko. Kwa maana vikundi vyote vya watu vitatembea kila kimoja katika jina la mungu wake; bali sisi tutatembea katika jina la Yehova Mungu wetu.”—Mika 4:1, 5.

      18. Ibada ya kweli imetusaidia kufanya mabadiliko gani?

      18 Pia, Mika alieleza jinsi ambavyo ibada ya kweli ingewaunganisha watu ambao walikuwa maadui mwanzoni. ‘Watu kutoka mataifa mengi hakika watakwenda na kusema: “Njooni, twendeni juu kwenye mlima wa Yehova na kwenye nyumba ya Mungu wa Yakobo; naye atatufundisha njia zake, nasi tutatembea katika mapito yake.”. . . Nao watafua panga zao ziwe majembe na mikuki yao iwe miundu. Hawatainua upanga, taifa juu ya taifa, wala hawatajifunza vita tena.’ (Mika 4:2, 3) Wale wanaoacha ibada ya miungu iliyotengenezwa na wanadamu au ibada ya mataifa na kufuata ibada ya Yehova wanakuwa na umoja duniani pote. Mungu anawafundisha katika njia za upendo.

      19. Kuunganishwa kwa mamilioni ya watu katika ibada ya kweli kunaonyesha nini waziwazi?

      19 Umoja wa duniani pote wa Wakristo wa kweli leo ni wa pekee na unaonyesha wazi kwamba Yehova anaendelea kuwaongoza watu wake kupitia roho yake. Watu mmoja-mmoja kutoka katika mataifa yote wanaunganishwa kwa wingi zaidi kuliko wakati mwingine wowote katika historia ya wanadamu. Jambo hilo linatimiza kwa njia ya pekee maneno ya Ufunuo 7:9, 14, na linaonyesha kwamba hivi karibuni malaika wa Mungu wataziachilia zile “pepo” ambazo zitaharibu mfumo huu mwovu wa mambo. (Soma Ufunuo 7:1-4, 9, 10, 14.) Je, si ni pendeleo kuunganishwa katika undugu wa ulimwenguni pote? Kila mmoja wetu anaweza kuchangia jinsi gani umoja huo? Mambo hayo yatazungumziwa katika habari inayofuata.

  • Umoja wa Kikristo Unamletea Mungu Utukufu
    Mnara wa Mlinzi—2010 | Septemba 15
    • Umoja wa Kikristo Unamletea Mungu Utukufu

      ‘Mjitahidi sana kuushika umoja wa roho.’—EFE. 4:3.

      1. Wakristo wa karne ya kwanza huko Efeso walimletea Mungu utukufu jinsi gani?

      UMOJA wa kutaniko la Kikristo katika jiji la kale la Efeso ulimletea utukufu Mungu wa kweli, Yehova. Inaonekana kwamba ndugu fulani Wakristo katika kituo hicho cha kibiashara chenye utajiri walikuwa matajiri waliomiliki watumwa, na wengine walikuwa watumwa na labda maskini sana. (Efe. 6:5, 9) Wengine walikuwa Wayahudi ambao walijifunza kweli katika muda wa miezi mitatu ambayo mtume Paulo alikuwa akitoa hotuba katika sinagogi lao. Zamani, wengine wao walikuwa wakiabudu Artemi na walikuwa na zoea la kufanya ufundi wa uchawi. (Mdo. 19:8, 19, 26) Ni wazi kwamba Ukristo wa kweli uliwaunganisha watu wa malezi mbalimbali. Paulo alitambua kwamba umoja wa kutaniko ulimletea Yehova utukufu. Mtume huyo aliandika hivi: “Kwake kuwe na utukufu kwa njia ya kutaniko.”—Efe. 3:21.

      2. Ni nini kilichohatarisha umoja wa Wakristo huko Efeso?

      2 Hata hivyo, umoja uliobarikiwa wa kutaniko la Efeso ulikabili hatari. Paulo aliwaonya hivi wazee: “Kutoka katikati yenu ninyi wenyewe watu watasimama na kusema mambo yaliyopotoka ili kuwavuta wanafunzi wawafuate wao wenyewe.” (Mdo. 20:30) Pia, ndugu fulani hawakuwa wameacha kabisa roho inayosababisha migawanyiko ambayo Paulo alionya kwamba ‘inatenda katika wana wa kutotii.’—Efe. 2:2; 4:22.

      Barua Inayokazia Umoja

      3, 4. Barua ya Paulo kwa Waefeso inakazia jinsi gani umoja?

      3 Paulo alitambua kwamba ili Wakristo waendelee kushirikiana kwa upatano, ni lazima kila mmoja wao ajitahidi kabisa kudumisha umoja. Mungu alimwongoza Paulo kupitia roho takatifu kuwaandikia Waefeso barua ambayo ilikazia umoja. Kwa mfano, Paulo aliandika kuhusu kusudi la Mungu la “kukusanya tena pamoja vitu vyote katika Kristo.” (Efe. 1:10) Pia, aliwafananisha Wakristo na mawe mbalimbali yanayotumiwa kujenga jengo. “Jengo lote likiunganishwa pamoja kwa upatano, linakua liwe hekalu takatifu kwa ajili ya Yehova.” (Efe. 2:20, 21) Zaidi ya hayo, Paulo alikazia umoja wa Wakristo Wayahudi na wasio Wayahudi na pia akawakumbusha ndugu hao kwamba wote waliumbwa na Mungu. Alimwita Yehova, ‘Baba, ambaye kila familia mbinguni na duniani hupata jina kutokana naye.’—Efe. 3:5, 6, 14, 15.

      4 Tunapochunguza sura ya 4 ya Waefeso, tutaona kwa nini jitihada zinahitajiwa ili kudumisha umoja, jinsi Yehova anavyotusaidia kuungana, na mitazamo ambayo itatusaidia kudumisha umoja wetu. Kwa nini usisome sura nzima ili ufaidike zaidi na funzo hili?

      Kwa Nini Umoja Unahitaji Jitihada Nyingi?

      5. Kwa nini malaika wa Mungu wanamtumikia kwa umoja, lakini kwa nini ni vigumu zaidi kwetu kudumisha umoja?

      5 Paulo aliwasihi ndugu zake Waefeso ‘wajitahidi sana kuushika umoja wa roho.’ (Efe. 4:3) Ili kuelewa kwa nini jitihada zinahitajiwa katika jambo hilo, fikiria hali ya malaika wa Mungu. Hakuna vitu viwili vilivyo hai duniani ambavyo vinafanana kabisa, kwa hiyo tunaweza kukata kauli kwamba Yehova amembariki kila mmoja kati ya mamilioni ya malaika wake kwa kumuumba akiwa na utu wa kipekee. (Dan. 7:10) Hata hivyo, wanaweza kumtumikia Yehova kwa umoja kwa sababu wote wanamsikiliza na kufanya mapenzi yake. (Soma Zaburi 103:20, 21.) Malaika waaminifu wana sifa tofauti-tofauti kama Wakristo walivyo na sifa tofauti-tofauti, lakini Wakristo wana udhaifu mbalimbali pia. Udhaifu huo unaweza kufanya iwe vigumu zaidi kudumisha umoja.

      6. Ni mitazamo gani itakayotusaidia kufurahia kushirikiana na ndugu ambao wana udhaifu tofauti na wetu?

      6 Ni rahisi kwa watu wasio wakamilifu kukosana wanapojaribu kushirikiana. Kwa mfano, namna gani ikiwa ndugu mpole ambaye mara nyingi anachelewa kufika anamtumikia Yehova akishirikiana na ndugu ambaye hachelewi lakini ambaye anakasirika haraka? Huenda kila mmoja wao akahisi kwamba mwenzake anajiendesha kwa njia isiyofaa lakini labda anasahau kwamba yeye pia anajiendesha kwa njia fulani isiyofaa. Ndugu wawili kama hao wanaweza kutumika pamoja jinsi gani kwa umoja? Ona jinsi mitazamo ambayo Paulo alipendekeza katika maneno yake yanayofuata inavyoweza kuwasaidia. Kisha ufikirie jinsi tunavyoweza kudumisha umoja kwa kusitawisha mitazamo hiyo. Paulo aliandika hivi: “[Mimi] nawasihi ninyi mtembee kwa kuustahili . . . mkiwa na unyenyekevu kamili wa akili na upole, mkiwa na ustahimilivu, mkivumiliana katika upendo, mkijitahidi sana kuushika umoja wa roho katika kifungo chenye kuunganisha cha amani.”—Efe. 4:1-3.

      7. Kwa nini ni jambo la maana kujitahidi kuwa na umoja na Wakristo wengine wasio wakamilifu?

      7 Kujifunza kumtumikia Mungu kwa umoja pamoja na watu wengine wasio wakamilifu ni jambo la maana kwa sababu kuna kikundi au mwili mmoja tu wa waabudu wa kweli. “Kuna mwili mmoja, na roho moja, kama vile mlivyoitwa katika tumaini moja mliloitiwa; Bwana mmoja, imani moja, ubatizo mmoja; Mungu mmoja na Baba wa watu wote.” (Efe. 4:4-6) Roho ya Yehova na baraka zake ziko juu ya ule ushirika mmoja wa ndugu ambao Mungu anatumia. Hata ikiwa mtu fulani katika kutaniko anatukasirisha, tunaweza kwenda mahali gani pengine? Hatuwezi kusikia maneno ya uzima wa milele mahali pengine popote.—Yoh. 6:68.

      Wale Ambao Ni “Zawadi Katika Wanadamu” Wanadumisha Umoja

      8. Kristo anatumia nani ili kutusaidia kupata nguvu za kushinda uvutano unaosababisha migawanyiko?

      8 Akitumia zoea fulani ambalo askari-jeshi walikuwa nalo nyakati za kale, Paulo alionyesha jinsi Yesu alivyotoa “zawadi katika wanadamu” ili kusaidia kuunganisha kutaniko. Askari-jeshi aliyeshinda vitani angeweza kumchukua mtu mateka kutoka nchi nyingine na kumleta nyumbani ili awe mtumwa wake na kumsaidia mke wake kazi. (Zab. 68:1, 12, 18) Vivyo hivyo, ushindi wa Yesu juu ya ulimwengu ulimsaidia kupata watumwa wengi walio tayari kumtumikia. (Soma Waefeso 4:7, 8.) Aliwatumia jinsi gani mateka hao wa mfano? “Alitoa wengine kuwa mitume, wengine kuwa manabii, wengine kuwa waeneza-injili, wengine kuwa wachungaji na walimu, kwa kusudi la kuwarekebisha upya watakatifu, kwa ajili ya kazi ya huduma, kwa ajili ya kuujenga mwili wa Kristo, mpaka sisi sote tuufikie umoja katika imani.”—Efe. 4:11-13.

      9. (a) Wale ambao ni “zawadi katika wanadamu” wanasaidia jinsi gani kudumisha umoja wetu? (b) Kwa nini kila mshiriki wa kutaniko anapaswa kuchangia umoja wa kutaniko?

      9 Wakiwa wachungaji wenye upendo, wazee hao ambao ni “zawadi katika wanadamu” wanasaidia kudumisha umoja wetu. Kwa mfano, mzee wa kutaniko akiona ndugu wawili ‘wakichochea mashindano juu ya mtu na mwenzake,’ anaweza kusaidia sana kudumisha umoja katika kutaniko kwa kuwapa shauri la faragha, ili ‘kuwarekebisha upya katika roho ya upole.’ (Gal. 5:26–6:1) Wakiwa walimu, wazee hao ambao ni “zawadi katika wanadamu” wanatusaidia kujenga imani yenye nguvu inayotegemea mafundisho ya Biblia. Hivyo, wanadumisha umoja na kutusaidia kufikia ukomavu wa Kikristo. Paulo aliandika kwamba kusudi ni “ili tusiwe tena watoto wachanga, tukirushwa huku na huku kama kwa mawimbi na kuchukuliwa huku na huku na kila upepo wa fundisho kupitia udanganyifu wa watu, kwa njia ya ujanja katika kutunga kosa.” (Efe. 4:13, 14) Kila Mkristo anapaswa kuchangia umoja wa undugu wetu, kama vile tu ambavyo kila kiungo cha mwili wetu kinavyojenga viungo vingine kwa kuandaa kile kinachohitajiwa.—Soma Waefeso 4:15, 16.

      Sitawisha Mitazamo Mipya

      10. Mwenendo mpotovu unaweza kuhatarisha umoja wetu namna gani?

      10 Je, uliona kwamba sura ya nne ya barua ya Paulo kwa Waefeso inaonyesha kwamba kuonyesha upendo kwa matendo ndio ufunguo wa kupata umoja tukiwa Wakristo wakomavu? Kisha, inataja mambo ambayo yanahusika katika kuonyesha upendo. Kwanza, ili mtu afuate njia ya upendo ni lazima aepuke kabisa uasherati na mwenendo mpotovu. Paulo aliwahimiza ndugu zake ‘wasiendelee tena kutembea kama vile mataifa wanavyotembea pia.’ Watu hao walikuwa ‘wameishiwa na ufahamu wote wa maadili,’ na “walijitoa wenyewe ili kuwa na mwenendo mpotovu.” (Efe. 4:17-19) Ulimwengu wenye maadili mapotovu ambamo tunaishi unahatarisha umoja wetu. Watu wanafanya mizaha kuhusu uasherati, wanaimba nyimbo kuhusu uasherati, wanatazama uasherati ili kujiburudisha, na wanafanya uasherati katika siri au waziwazi. Lakini, hata kuchezeana kimapenzi, yaani, kutenda kana kwamba unavutiwa kingono na mtu mwingine ambaye hukusudii kumuoa, kunaweza kukutenganisha na Yehova na kutaniko. Kwa nini? Kwa sababu kufanya hivyo kunaongoza kwa urahisi sana katika uasherati. Pia, kuchezeana kimapenzi ambako kunamwongoza mtu aliyefunga ndoa kutumbukia katika uzinzi kunaweza kuwatenganisha kikatili watoto na wazazi wao na wenzi wasio na hatia na wenzi wao wa ndoa. Kwa kweli, zoea hilo linatenganisha watu! Si ajabu kwamba Paulo aliandika hivi: “Ninyi hamkujifunza Kristo kuwa hivyo”!—Efe. 4:20, 21.

      11. Biblia inawatia moyo Wakristo wafanye badiliko gani?

      11 Paulo alikazia kwamba tunapaswa kuacha njia za kufikiri zinazovuruga umoja na badala yake tusitawishe mitazamo ambayo inatuwezesha kuishi kwa upatano na wengine. Alisema hivi: “Mnapaswa kuuondolea mbali utu wa zamani unaolingana na mwenendo wenu wa kwanza na ambao unaharibiwa kulingana na tamaa zake [za utu wa zamani] za udanganyifu; . . . mnapaswa kufanywa upya katika nguvu zinazoendesha akili yenu, na mnapaswa kuvaa utu mpya ulioumbwa kulingana na mapenzi ya Mungu katika uadilifu wa kweli na ushikamanifu.” (Efe. 4:22-24) Tunaweza jinsi gani ‘kufanywa upya katika nguvu zinazoendesha akili yetu’? Tukitafakari na kuthamini mambo tunayojifunza kutoka katika Neno la Mungu na kutokana na mifano mizuri ya Wakristo wakomavu, na tukijitahidi sana, tunaweza kuvaa utu mpya “ulioumbwa kulingana na mapenzi ya Mungu.”

      Sitawisha Njia Mpya za Kuzungumza

      12. Kusema kweli kunadumisha umoja jinsi gani, na kwa nini ni vigumu kwa wengine kusema kweli?

      12 Ni jambo la maana kwa wale ambao ni mwili mmoja katika familia au katika kutaniko kusema kweli. Kuongea kwa unyoofu, kwa fadhili, na waziwazi, kunaweza kuwaunganisha watu. (Yoh. 15:15) Lakini namna gani ikiwa mtu anamdanganya ndugu yake? Ndugu yake akitambua hilo, kifungo cha kuaminiana kati yao kitadhoofika. Basi, unaweza kuelewa kwa nini Paulo aliandika hivi: “Semeni kweli kila mmoja wenu na jirani yake, kwa sababu sisi ni viungo vya mtu na mwenzake.” (Efe. 4:25) Inaweza kuwa vigumu kwa mtu kuanza kusema kweli ikiwa amezoea kusema uwongo, na labda alianza kusema uwongo akiwa mtoto. Lakini Yehova anathamini jitihada za mtu huyo za kubadilika na atamsaidia.

      13. Kuondolea mbali matukano kunahusisha nini?

      13 Yehova anatufundisha kudumisha heshima na umoja katika kutaniko na katika familia kwa kuweka mipaka thabiti kuhusiana na njia yetu ya kusema. “Neno lililooza na lisitoke kinywani mwenu . . . Uchungu wote wenye uovu na hasira na ghadhabu na kupiga kelele na matukano na viondolewe mbali kutoka kwenu pamoja na ubaya wote.” (Efe. 4:29, 31) Njia moja ya kuepuka kusema maneno yenye kuudhi ni kusitawisha mtazamo wenye heshima zaidi kuelekea wengine. Kwa mfano, mtu anayemtukana mke wake anapaswa kujitahidi kubadili mtazamo wake kumwelekea, hasa anapojifunza jinsi Yehova anavyowaheshimu wanawake. Mungu hata anawatia mafuta kwa roho takatifu wanawake fulani, na kuwapa tumaini la kutawala wakiwa wafalme pamoja na Kristo. (Gal. 3:28; 1 Pet. 3:7) Vivyo hivyo, mwanamke ambaye ana tabia ya kumpigia kelele mume wake anapaswa kuchochewa kubadilika anapojifunza jinsi Yesu alivyojizuia alipochokozwa.—1 Pet. 2:21-23.

      14. Kwa nini kuonyesha hasira ni hatari?

      14 Matukano yanahusiana sana na kutozuia hasira. Jambo hilo pia linaweza kuwatenganisha watu ambao ni viungo vya mwili mmoja. Hasira ni kama moto. Inaweza kwa urahisi kupita mipaka na kusababisha msiba. (Met. 29:22) Ni lazima mtu ambaye ana sababu nzuri ya kukasirika azuie hasira yake kwa uangalifu ili aepuke kuharibu mahusiano yenye thamani. Wakristo wanapaswa kujitahidi kuwa wenye kusamehe, na hawapaswi kuweka kinyongo moyoni na kuzungumza tena kuhusu jambo hilo. (Zab. 37:8; 103:8, 9; Met. 17:9) Paulo aliwashauri hivi Waefeso: “Iweni na ghadhabu, lakini msitende dhambi; jua lisitue mkiwa katika hali ya kuchokozeka, wala msimpe Ibilisi nafasi.” (Efe. 4:26, 27) Kutozuia hasira kunaweza kumpa Ibilisi nafasi ya kusababisha migawanyiko na hata mizozano ndani ya kutaniko.

      15. Kuchukua kitu ambacho si chetu kunaweza kuwa na matokeo gani?

      15 Kuheshimu mali ya wengine kunachangia umoja katika kutaniko. Tunasoma hivi: “Mwizi asiibe tena.” (Efe. 4:28) Kwa ujumla, watu wa Yehova wamesitawisha hali ya kuaminiana. Ikiwa Mkristo angetumia vibaya hali hiyo ya kuaminiana kwa kuchukua kitu ambacho si chake, angeharibu umoja huo unaoleta furaha.

      Kumpenda Mungu Kunatuunganisha

      16. Tunaweza kutumia jinsi gani usemi wenye kujenga ili kutia nguvu umoja wetu?

      16 Kuna umoja katika kutaniko la Kikristo kwa sababu wote wanachochewa kumpenda Mungu kwa kuwatendea wengine kwa njia ya upendo. Kuthamini fadhili za Yehova kunatuchochea kujitahidi kabisa kufuata shauri hili: “[Semeni] neno lolote ambalo ni jema kwa ajili ya kujenga kulingana na uhitaji, ili liwape wasikiaji lile linalofaa. . . . Iweni wenye fadhili ninyi kwa ninyi, wenye huruma nyororo, mkisameheana kwa hiari kama vile Mungu pia kupitia Kristo alivyowasamehe ninyi kwa hiari.” (Efe. 4:29, 32) Yehova anawasamehe kwa fadhili watu wasio wakamilifu kama sisi. Je, sisi pia hatupaswi kuwasamehe wengine tunapoona udhaifu wao?

      17. Kwa nini tunapaswa kujitahidi kabisa kudumisha umoja?

      17 Umoja wa watu wa Mungu unamletea Yehova utukufu. Roho yake inatuchochea kwa njia mbalimbali kudumisha umoja. Bila shaka, hatungependa kukataa mwongozo wa roho. Paulo aliandika hivi: “Msiwe mkiihuzunisha roho takatifu ya Mungu.” (Efe. 4:30) Umoja ni hazina ambayo inastahili kulindwa. Unawaletea shangwe wote ambao wana umoja na unamletea Yehova utukufu. “Kwa hiyo, iweni waigaji wa Mungu, kama watoto wapendwa, na endeleeni kutembea katika upendo.”—Efe. 5:1, 2.

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki