Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Ni Nani Atakayeutawala Ulimwengu?
    Sikiliza Unabii wa Danieli!
    • MZEE WA SIKU AHUKUMU

      33. (a) Mzee wa Siku ni nani? (b) Ni ‘vitabu gani vilivyofunuliwa’ katika Mahakama ya kimbingu?

      33 Baada ya kuwatambulisha wale wanyama wanne, Danieli aacha kumwangalia mnyama wa nne na kuona kikao mbinguni. Aona Mzee wa Siku ameketi katika kiti chake chenye utukufu akiwa Hakimu. Mzee wa Siku si mwingine ila Yehova Mungu. (Zaburi 90:2) Mahakama ya kimbingu iketipo, Danieli aona ‘vitabu vikifunuliwa.’ (Danieli 7:9, 10) Kwa kuwa Yehova ni wa tangu milele, anajua historia yote ya binadamu kana kwamba imeandikwa katika kitabu. Amewaangalia wanyama wote hao wanne naye aweza kuwahukumu kulingana na mambo ajuayo yeye mwenyewe.

      34, 35. Ile pembe “ndogo” na serikali nyingine za mnyama zitapatwa na nini?

      34 Danieli aendelea kusema hivi: “Nikatazama wakati huo; kwa sababu ya sauti ya yale maneno makubwa iliyoyasema ile pembe; nalitazama hata mnyama yule akauawa, mwili wake ukaharibiwa, akatolewa ateketezwe kwa moto. Na kwa habari za wale wanyama wengine, walinyang’anywa mamlaka yao; walakini maisha yao yalidumishwa kwa wakati na majira.” (Danieli 7:11, 12) Malaika amwambia Danieli hivi: “Hukumu itawekwa, nao watamwondolea mamlaka yake, kuyapoteza na kuyaangamiza, hata milele.”—Danieli 7:26.

      35 Kwa amri ya Hakimu Mkuu, Yehova Mungu, pembe iliyomkufuru Mungu na kuwasumbua “watakatifu” wake itapatwa na jambo lilelile lililoipata Milki ya Roma, ambayo iliwanyanyasa Wakristo wa mapema. Utawala wake hautaendelea. Hata wale “wafalme” wadogo walio kama pembe waliotokana na Milki ya Roma hawataendelea. Hata hivyo, vipi juu ya tawala zilizotokana na serikali za awali zilizofananishwa na mnyama? Kama ilivyotabiriwa, maisha yao yalidumishwa “kwa wakati na majira.” Maeneo yao yameendelea kuwa na watu hadi leo. Kwa mfano, Iraki iko kwenye eneo la Babiloni ya Kale. Uajemi (Iran) na Ugiriki zingaliko. Mabaki ya serikali hizo za ulimwengu ni sehemu ya Umoja wa Mataifa. Falme hizo pia zitaangamia serikali ya ulimwengu ya mwisho itakapoangamizwa. Serikali zote za kibinadamu zitafutiliwa mbali kwenye “vita ya siku kubwa ya Mungu Mweza-Yote.” (Ufunuo 16:14, 16) Lakini, ni nani basi atakayeutawala ulimwengu?

      UTAWALA WENYE KUDUMU U KARIBU!

      36, 37. (a) ‘Mmoja aliye mfano wa mwana wa binadamu’ ni nani, naye alitokea kwenye Mahakama ya kimbingu lini na kwa kusudi gani? (b) Ni nini kilichosimamishwa mwaka wa 1914 W.K.?

      36 “Nikaona katika njozi za usiku, na tazama,” akasema Danieli kwa mshangao. “Mmoja aliye mfano wa mwanadamu [“mwana wa binadamu,” NW] akaja pamoja na mawingu ya mbingu akamkaribia huyo mzee wa siku, wakamleta karibu naye.” (Danieli 7:13) Alipokuwa duniani, Yesu Kristo alijiita “Mwana wa binadamu,” akionyesha uhusiano wake na wanadamu. (Mathayo 16:13; 25:31) Yesu aliiambia Sanhedrini, au mahakama kuu ya Kiyahudi hivi: “Mtaona Mwana wa binadamu ameketi kwenye mkono wa kuume wa nguvu na akija juu ya mawingu ya mbinguni.” (Mathayo 26:64) Kwa hiyo, katika ono la Danieli, yule ajaye, asiyeonekana kwa macho ya kibinadamu, na kumwendea Yehova Mungu alikuwa Yesu Kristo aliyefufuliwa na kutukuzwa. Hilo lilitukia lini?

      37 Mungu amefanya agano na Yesu Kristo kwa ajili ya Ufalme, kama vile tu alivyokuwa amefanya agano na Mfalme Daudi. (2 Samweli 7:11-16; Luka 22:28-30) “Nyakati zilizowekwa rasmi za mataifa” zilipoisha mwaka wa 1914 W.K., Yesu Kristo, akiwa mrithi wa ufalme wa Daudi, alikuwa na haki ya kupokea utawala wa Ufalme. Rekodi ya kiunabii ya Danieli yasema hivi: “Naye akapewa mamlaka, na utukufu, na ufalme, ili watu wa kabila zote, na taifa zote, na lugha zote, wamtumikie; mamlaka yake ni mamlaka ya milele, ambayo hayatapita kamwe, na ufalme wake ni ufalme usioweza kuangamizwa.” (Danieli 7:14) Kwa hiyo, Ufalme wa Kimesiya ulisimamishwa mbinguni mwaka wa 1914. Hata hivyo, wengine pia wanapewa utawala huo.

      38, 39. Ni nani watakaopokea utawala udumuo milele juu ya dunia?

      38 “Watakatifu wake Aliye juu wataupokea ufalme,” akasema malaika. (Danieli 7:18, 22, 27) Yesu Kristo ndiye mtakatifu mkuu. (Matendo 3:14; 4:27, 30) Wale “watakatifu” wengine ambao watatawala naye ni wale Wakristo waaminifu watiwa-mafuta kwa roho 144,000, ambao ni warithi wa Ufalme pamoja na Kristo. (Waroma 1:7; 8:17; 2 Wathesalonike 1:5; 1 Petro 2:9) Wanafufuliwa wakiwa roho zisizoweza kufa ili watawale pamoja na Kristo katika Mlima Zayoni wa kimbingu. (Ufunuo 2:10; 14:1; 20:6) Kwa hiyo, Kristo Yesu na Wakristo watiwa-mafuta waliofufuliwa watautawala ulimwengu wa wanadamu.

      39 Kuhusu utawala wa Mwana wa binadamu na wale “watakatifu” wengine waliofufuliwa, malaika wa Mungu alisema hivi: “Ufalme, na mamlaka, na ukuu wa ufalme, chini ya mbingu zote, watapewa watu wa watakatifu wake Aliye juu; ufalme wake ni ufalme wa milele, na wote wenye mamlaka watamtumikia na kumtii.” (Danieli 7:27) Wanadamu watiifu watabarikiwa kama nini chini ya Ufalme huo!

  • Ni Nani Atakayeutawala Ulimwengu?
    Sikiliza Unabii wa Danieli!
    • [Picha katika ukurasa wa 147]

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki