Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Uzuri Mwingi Mno wa Kiti cha Ufalme cha Yehova cha Kimbingu
    Ufunuo—Upeo Wao Mtukufu U Karibu!
    • Sura ya 14

      Uzuri Mwingi Mno wa Kiti cha Ufalme cha Yehova cha Kimbingu

      Njozi ya 2—Ufunuo 4:1–5:14

      Habari: Matukio yenye kutia hofu mbele ya kiti cha ufalme cha Mungu cha hukumu

      Wakati wa utimizo: Njozi hii huonyesha matukio ya tangu 1914 mpaka mwisho wa Mileani na ng’ambo yayo, wakati kila kiumbe mbinguni na duniani kitamsifu Yehova.—Ufunuo 5:13

      1. Ni kwa nini imetupasa tupendezwe sana na njozi ambazo Yohana anashiriki nasi?

      YOHANA anaanza kushiriki pamoja nasi njozi zaidi zenye kuchochea nafsi. Kwa kuvuviwa yeye angali yumo katika siku ya Bwana. Kwa hiyo, mambo anayoeleza yana maana kubwa sana kwetu sisi ambao tunaishi kikweli katika hiyo siku. Kwa njia ya njozi hizi, Yehova anainua kisetiri cha kutoonekana juu ya mambo halisi ya kimbingu na kutupa mwono wake mwenyewe wa hukumu zake ambazo zitatekelezwa duniani. Zaidi ya hilo, tuwe tuna tumaini la kimbingu au la kidunia, mafunuo haya hutusaidia tuone mahali petu katika kusudi la Yehova. Kwa hiyo, sisi sote, inatupasa tuendelee kupendezwa sana sana na usemi wa Yohana: “Mwenye furaha ni yeye ambaye husoma kwa sauti kubwa na wale ambao husikia maneno ya unabii huu, na ambao hushika vitu vilivyoandikwa katika huo.”—Ufunuo 1:3, NW.

      2. Sasa Yohana anapata ono gani?

      2 Kitu ambacho Yohana anaona halafu kinapita kitu chochote ambacho kimetolewa na vidio kwa binadamu wa leo! Yeye aandika hivi: “Baada ya vitu hivi mimi nikaona, na, tazama! mlango uliofunguliwa katika mbingu, na sauti ya kwanza ambayo mimi nilisikia ilikuwa kama ya tarumbeta, ikinena na mimi, ikisema: ‘Njoo juu huku, na mimi nitaonyesha wewe vitu ambavyo ni lazima vitukie.’” (Ufunuo 4:1, NW) Yohana katika njozi anapenya zile mbingu zisizoonekana za kuwapo kwa Yehova, mwenye kukwezwa juu sana zaidi ya anga za juu zaidi kama zinavyovumbuliwa na wanaanga, hata juu zaidi ya magalaksi ya ulimwengu wote mzima wa kimwili. Kana kwamba kwa kuingia mlango uliofunguliwa, Yohana anaalikwa alishe macho yake karamu ya mandhari nzuri sana ya kustaajabisha ya mbingu za kiroho zilizo za mwisho kabisa kabisa ambako Yehova mwenyewe anakalia kiti cha ufalme. (Zaburi 11:4; Isaya 66:1) Lo! ni pendeleo lililoje!

      3. Ile sauti “kama ya tarumbeta” inarudisha nini akilini, na bila shaka ni nani aliye Chanzo chayo?

      3 Biblia haitambulishi hii “sauti ya kwanza.” Kama ile sauti ya Yesu yenye nguvu iliyosikiwa mapema zaidi, ina mlio wenye kuamrisha kama tarumbeta. (Ufunuo 1:10, 11) Inakumbusha ule mlio wa pembe wenye kupenya ambao uliashiria kuwapo kwa Yehova kwenye Mlima Sinai. (Kutoka 19:18-20) Bila shaka, Yehova ndiye Chanzo adhimu cha mialiko hiyo. (Ufunuo 1:1) Yeye amefungua mlango ili Yohana, katika njozi, aweze kuingia mahali patakatifu zaidi sana katika milki yote iliyo kubwa mno ya enzi kuu ya Yehova.

      Kuwapo Kwenye Fahari kwa Yehova

      4. (a) Njozi ya Yohana ina maana gani kwa Wakristo wapakwa-mafuta? (b) Njozi hiyo ina maana gani kwa wale ambao tumaini lao ni kuishi milele duniani?

      4 Yohana aona nini? Sikiliza, ashirikipo pamoja nasi ono lake bora sana: “Baada ya vitu hivi mimi nikaja kuwa katika nguvu ya roho: na, tazama! kiti cha ufalme kimoja kilikuwa katika mahali pacho katika mbingu, na kuna mmoja aliyeketi juu ya hicho kiti cha ufalme.” (Ufunuo 4:2, NW) Papo hapo, Yohana anasafirishwa kiroho kwa kani-tendaji ya Mungu mpaka kwenye kiti cha ufalme chenyewe cha Yehova. Inasisimua kama nini kwa Yohana! Huko yeye anapewa mwono wa kimbele wenye kutia kiwi wa mbingu hizo zenyewe ambamo yeye na Wakristo wengine wapakwa-mafuta wamewekewa “urithi usiofisidika na usiochafuliwa na usionyauka.” (1 Petro 1:3-5, NW; Wafilipi 3:20) Kwa wale ambao tumaini lao ni kuishi milele duniani, njozi ya Yohana ina maana kubwa sana pia. Inawasaidia wafahamu utukufu wa kuwapo kwa Yehova na wa ule muundo wa kutawala wa kimbingu anaotumia Yehova katika kuhukumu mataifa na baadaye katika kuongoza maisha za binadamu duniani. Kweli kweli Yehova ndiye Mungu wa tengenezo zuri ajabu!

      5. Ni kitu halisi gani kilichofananishwa na kifuniko cha ile arka ya agano anachoona Yohana?

      5 Vingi vya vitu ambavyo Yohana anaona huko juu katika mbingu vinafanana na vitu mbalimbali vya ile tabenakulo (hema) katika jangwa. Hiyo ilijengwa yapata miaka 1,600 mapema zaidi iwe patakatifu pa ibada ya kweli kwa ajili ya Waisraeli. Katika Patakatifu pa Patakatifu Pote pa tabenakulo hiyo ilikuwamo ile arka ya agano, na ilikuwa kutoka juu ya kifuniko cha dhahabu halisi cha hiyo arka kwamba Yehova mwenyewe alisema. (Kutoka 25:17-22; Waebrania 9:5) Kwa sababu hiyo, kifuniko cha arka hiyo kilitumika kuwa ufananisho wa kiti cha ufalme cha Yehova. Sasa Yohana anaona uhalisi wa kiwakilisho hicho cha kufananisha: Yehova Bwana Mwenye Enzi Kuu mwenyewe ameketi kwa adhama bora sana juu ya kiti cha ufalme chake cha kimbingu chenye kuinuliwa juu!

      6. Ni chapa gani juu ya Yehova anayotupa Yohana, na ni kwa sababu gani hii inafaa?

      6 Tofauti na wale manabii wa mapema zaidi waliopata njozi za kiti cha ufalme cha Yehova, Yohana hatoi habari zaidi juu ya yule Mmoja Mtakatifu anayekikalia. (Ezekieli 1:26, 27; Danieli 7:9, 10) Lakini Yohana anatupa chapa yake kuhusu yule Mmoja anayekalia kiti cha ufalme hicho kwa maneno haya: “Na yule mmoja anayeketi chini, katika kuonekana, ni kama jiwe la yaspa na jiwe lenye thamani ya juu rangi-nyekundu, na kuzunguka kiti cha ufalme kuna upinde-mvua kama emeraldi katika kuonekana.” (Ufunuo 4:3, NW) Lo-o-o! ni uzuri mwingi mno usiolinganika kama nini! Yohana anaona akilini uzuri mtulivu, wenye kumetameta kama ule wa mawe yenye thamani yenye kung’aa, yenye kumetameta. Jinsi hili linavyopatana na elezo la mwanafunzi Yakobo kuhusu Yehova kuwa “Baba wa mianga ya kimbingu”! (Yakobo 1:17, NW) Muda mfupi baada ya kuandika Ufunuo, Yohana mwenyewe alitaarifu hivi: “Mungu ni nuru na hamna giza hata kidogo katika muungano pamoja na yeye.” (1 Yohana 1:5, NW) Yehova ni Mtu mashuhuri mwenye utukufu unaopita ubora kweli kweli!

      7. Tunaweza kujifunza nini kutokana na uhakika wa kwamba kuna upinde-mvua kuzunguka kiti cha ufalme cha Yehova?

      7 Angalia kwamba Yohana anaona kuzunguka kiti cha ufalme upinde-mvua, rangi-emeraldi chanikiwiti. Neno la Kigiriki linalotafsiriwa hapa kuwa upinde-mvua (irʹis) hudokeza umbile la duara kabisa. Upinde-mvua unatajwa kwa mara ya kwanza katika Biblia kuhusiana na siku ya Noa. Baada ya yale maji ya Gharika kutindika, Yehova alitokeza upinde-mvua katika wingu, naye akaeleza kwa maneno haya ulichofananisha: “Upinde-mvua wangu mimi natoa katika wingu, na huo lazima utumike kuwa ishara ya agano kati ya mimi na dunia. Na mimi kwa hakika nitakumbuka agano langu ambalo liko kati ya mimi na nyinyi na kila nafsi iliyo hai miongoni mwa mnofu wote; na maji hayatakuwa tena gharika kuleta mnofu wote kwenye angamio.” (Mwanzo 9:13, 15, NW) Basi, ile njozi ya kimbingu ingeleta jambo gani akilini mwa Yohana? Ule upinde-mvua alioona lazima uwe ulimkumbusha uhitaji wa uhusiano wenye amani pamoja na Yehova, kama ule unaofurahiwa na jamii ya Yohana leo. Pia ingepiga chapa akilini ule utulivu na amani ya kuwapo kwa Yehova, utulivu ambao utaenea kwa binadamu wote wenye kutii wakati Yehova atandapo hema yake juu ya aina ya binadamu katika ile jamii ya dunia mpya.—Zaburi 119:165; Wafilipi 4:7; Ufunuo 21:1-4.

      Kutambulisha Wale Wazee 24

      8. Ni nani ambao Yohana anaona kuzunguka kiti cha ufalme cha Yehova, na hao wanawakilisha nani?

      8 Yohana alijua kwamba makuhani waliwekwa rasmi watumikie katika ile tabenakulo ya kale. Kwa hiyo huenda akawa alishangaa alipoona anachofuata kueleza: “Na kuzunguka kiti cha ufalme kuna viti vya ufalme ishirini na vinne, na juu ya viti vya ufalme hivi mimi niliona wameketi wazee ishirini na wanne wamevalia mavazi ya nje meupe, na juu ya vichwa vyao mataji ya dhahabu.” (Ufunuo 4:4, NW) Ndiyo, badala ya makuhani, kuna wazee 24, wameketishwa katika viti vya ufalme na kuvikwa mataji kama wafalme. Wazee hawa ni akina nani? Wao si wengine ila wapakwa-mafuta wa kundi la Kikristo, wamefufuliwa na kuchukua cheo cha kimbingu ambacho Yehova aliwaahidi. Sisi twajuaje hilo?

      9, 10. Sisi twajuaje kwamba wazee 24 huwakilisha kundi la Kikiristo lililopakwa mafuta katika cheo kitukufu chalo cha kimbingu?

      9 Kwanza kabisa wao wanavaa taji. Biblia husema juu ya Wakristo wapakwa-mafuta kuwa wakipata ‘taji lisilofisidika’ na wakifikia uhai usio na mwisho—usioweza kufa. (1 Wakorintho 9:25; 15:53, 54, NW) Lakini kwa kuwa wazee hawa 24 wanakalia viti vya ufalme, yale mataji katika maana hii huwakilisha mamlaka ya kifalme. (Linga Ufunuo 6:2; 14:14.) Hilo linaunga mkono wazo la kwamba wazee hao 24 hutaswiri wafuasi wa nyayo za Yesu wapakwa-mafuta katika cheo chao cha kimbingu, maana Yesu alifanya agano pamoja nao la kukalia viti vya ufalme katika Ufalme wake. (Luka 22:28-30) Ni Yesu na hawa wazee 24 tu—hata si malaika—ndio wanaoelezwa kuwa wakitawala katika mbingu katika kuwapo kwa Yehova.

      10 Hili lapatana na ile ahadi ambayo Yesu alifanya kwa kundi la Laodikia: “Yeye ambaye hushinda mimi nitaruhusu kuketi chini pamoja na mimi juu ya kiti cha ufalme changu.” (Ufunuo 3:21, NW) Lakini mgawo wa kimbingu wa hawa wazee 24 si wa utawala wa kiserikali tu. Katika utangulizi wa kitabu cha Ufunuo, Yohana alisema hivi kwa habari ya Yesu: “Yeye alifanya sisi kuwa ufalme, makuhani kwa Mungu na Baba yake.” (Ufunuo 1:5, 6, NW) Hawa ni wafalme na makuhani pia. “Wao watakuwa makuhani wa Mungu na wa Kristo, na watatawala wakiwa wafalme pamoja na yeye kwa miaka elfu.”—Ufunuo 20:6, NW.

      11. Ni kwa nini inafaa kwamba nambari ya wale wazee ni 24, na nambari hiyo inamaanisha nini?

      11 Ni nini lililo la maana kwa habari ya nambari 24, kwa kuwa Yohana anaona wazee 24 kuzunguka kiti cha ufalme? Katika njia nyingi, hawa walitangulia kufananishwa na wale makuhani waaminifu wa Israeli wa kale. Mtume Petro aliandikia Wakristo wapakwa-mafuta hivi: “Nyinyi ni ‘jamii iliyochaguliwa, ukuhani wa kifalme, taifa takatifu, watu kwa ajili ya mali ya pekee.’” (1 Petro 2:9, NW) Kwa kupendeza, ukuhani huo wa kale wa Kiyahudi, ulikuja kugawanywa ukawa migawanyo 24. Kila mgawanyo ulipewa mgawo wa majuma yao wenyewe katika mwaka wa kutumikia mbele za Yehova, hivi kwamba utumishi mtakatifu ulitolewa bila kukatizwa. (1 Nyakati 24:5-19) Basi, inafaa kwamba wako wazee 24 wakionyeshwa katika njozi ya Yohana ya ule ukuhani wa kimbingu kwa sababu huu ukuhani unatumikia Yehova kwa kuendelea, bila kukoma. Utakapokamilishwa, itakuwako migawanyo 24, kila mmoja ukiwa na washindi 6,000, kwa kuwa Ufunuo 14:1-4 hutuambia kwamba 144,000 (24 x 6,000) ‘wananunuliwa miongoni mwa aina ya binadamu’ wakasimame juu ya Mlima Sayuni wa kimbingu pamoja na Mwana-Kondoo, Yesu Kristo. Kwa kuwa nambari 12 huashiria tengenezo la kimungu lenye usawaziko, 24 hurudufisha—au huimarisha—mpango kama huo.

      Meme, Sauti, na Ngurumo

      12. Ni nini kinachofuata kuonwa na kusikiwa na Yohana, na “meme na sauti na ngurumo” huleta nini akilini?

      12 Ni nini kinachofuata kuonwa na kusikiwa na Yohana? “Na katika kiti cha ufalme zinatoka meme na sauti na ngurumo.” (Ufunuo 4:5a, NW) Lo! jinsi inavyokumbusha madhihirisho mengine yenye kutia hofu ya uwezo wa kimbingu wa Yehova! Mathalani, wakati Yehova ‘aliposhuka’ juu ya Mlima Sinai, Musa aliripoti hivi: “Katika siku ya tatu wakati ilipokuwa asubuhi, ikawa kwamba ngurumo na meme zikaanza kutukia, na wingu zito juu ya mlima na sauti kubwa sana ya pembe. . . . Wakati sauti ya pembe iliendelea kuwa kubwa zaidi na zaidi, Musa akaanza kunena, na Mungu wa kweli akaanza kujibu yeye kwa sauti.”—Kutoka 19:16-19, NW.

      13. Ni nini kinachoonyeshwa na picha ya meme zinazotoka katika kiti cha ufalme cha Yehova?

      13 Katika kipindi cha siku ya Bwana, Yehova hufanya nguvu na kuwapo kwake vidhihirike kwa njia yenye ukwezo mkubwa mno. La, si kwa umeme halisi, kwa kuwa Yohana anaona ishara. Basi, meme hizo zinawakilisha nini? Basi, mimeto ya umeme inaweza kunurisha, lakini inaweza pia kumpiga mtu mpaka kufa. Kwa hiyo, meme hizi zinazotoka kwenye kiti cha ufalme cha Yehova hufananisha kwa kufaa ile mimeto ya nuru ya elimu ambayo yeye amekuwa akiwapa watu wake kwa kuendelea na, hata la maana zaidi, jumbe zake za hukumu zenye moto.—Linga Zaburi 18:14; 144:5, 6; Mathayo 4:14-17; 24:27.

      14. Sauti zimevumaje leo?

      14 Namna gani zile sauti? Wakati wa kushuka kwa Yehova juu ya Mlima Sinai, sauti ilinena kwa Musa. (Kutoka 19:19) Sauti kutoka mbinguni zilitoa nyingi za zile amri na mbiu katika kitabu cha Ufunuo. (Ufunuo 4:1; 10:4, 8; 11:12; 12:10; 14:13; 16:1, 17; 18:4; 19:5; 21:3) Leo, Yehova ametoa pia amri na mbiu kwa watu wake, akimulikia kuelewa kwao unabii na kanuni za Biblia. Habari yenye kutoa nuru ya elimu mara nyingi imejulishwa kwenye mikusanyiko ya kimataifa, kisha, mbiu ya kweli hizo za Biblia imepigwa ulimwenguni pote. Mtume Paulo alisema hivi juu ya wahubiri waaminifu wa habari njema: “Kwani, kwa hakika, ‘katika dunia yote mvumo wao ulitoka ukaenda, na kwenye ncha za dunia inayokaliwa matamko yao.’”—Warumi 10:18, NW.

      15. Ni ngurumo gani ambazo zimetoka katika kiti cha ufalme katika sehemu hii ya siku ya Bwana?

      15 Kwa kawaida ngurumo hufuatana na umeme. Daudi alirejezea ngurumo halisi kuwa “sauti ya Yehova.” (Zaburi 29:3, 4, NW) Wakati Yehova alipopigania Daudi dhidi ya adui zake, ngurumo ilisemekana kuwa ilitoka kwa Yeye. (2 Samweli 22:14; Zaburi 18:13) Elihu alimwambia Ayubu kwamba sauti ya Yehova ilivuma kama ngurumo, Yeye anapofanya “vitu vikubwa ambavyo sisi hatuwezi kujua.” (Ayubu 37:4, 5, NW) Wakati wa sehemu hii ya siku ya Bwana, Yehova ‘amenguruma,’ akionya juu ya matendo makubwa ambayo atafanya dhidi ya adui zake. Hii milio ya ufananisho ya ngurumo imetoa mwangwi na ikatoa mwangwi tena na tena katika dunia yote. Wewe ni mwenye furaha ikiwa umesikiliza matangazo haya yenye ngurumo na unatumia ulimi wako katika kuongezea ukubwa wayo!—Isaya 50:4, 5; 61:1, 2.

      Taa za Moto na Bahari ya Kioo

      16. Ni jambo gani linalomaanishwa na zile “taa saba za moto”?

      16 Yohana anaona nini zaidi? Hiki: “Na kuna taa saba za moto zikiwaka mbele ya kiti cha ufalme, na hizi humaanisha roho saba za Mungu. Na mbele ya kiti cha ufalme kuna, kana kwamba, ni bahari ya kioo kama fuwele.” (Ufunuo 4:5b, 6a, NW) Yohana mwenyewe anatuambia maana ya hizo taa saba: “Hizi humaanisha roho saba za Mungu.” Nambari saba hufananisha utimilifu wa kimungu; kwa hiyo taa saba lazima ziwakilishe ule ujazo wa kani ya roho takatifu yenye kutoa nuru ya elimu. Jinsi ile jamii ya Yohana ilivyo yenye kushukuru leo kwa vile imeaminishwa hii nuru ya elimu, pamoja na lile daraka la kuipitisha kwenye vikundi vya watu wa dunia wenye njaa ya kiroho! Jinsi tunavyoterema kwamba kila mwaka mamilioni ya nakala za gazeti Mnara wa Mlinzi yanaendelea kuangaza nuru katika lugha zipatazo 150!—Zaburi 43:3.

      17. Ile “bahari ya kioo kama fuwele” inafananisha nini?

      17 Pia Yohana anaona “bahari ya kioo kama fuwele.” Hii ingefananisha nini kwa wale walioalikwa waingie ndani ya kitala cha kimbingu? Paulo alisema juu ya njia ambayo katika hiyo Yesu alitakasa kundi, “akilisafisha kwa mwosho wa maji kwa njia ya neno.” (Waefeso 5:26, NW) Kabla ya kifo chake, Yesu aliwaambia wanafunzi wake hivi: “Nyinyi mmekwisha kuwa safi kwa sababu ya neno ambalo mimi nimesema kwa nyinyi.” (Yohana 15:3, NW) Kwa sababu hiyo, hii bahari ya kioo kama fuwele lazima iwakilishe Neno la Mungu lenye kusafisha, lililorekodiwa. Wale wa ukuhani wa kifalme ambao wanakuja ndani ya kuwapo kwa Yehova lazima wawe wamekwisha safishwa kikamili kwa Neno lake.

      Ona—“Viumbe Hai Wanne”!

      18. Yohana anaona nini katikati na kuzunguka kiti cha ufalme?

      18 Sasa Yohana anaona sura nyingine. Yeye anaandika: “Na katikati ya kiti cha ufalme na kuzunguka kiti cha ufalme kuna viumbe hai wanne ambao wanajaa macho mbele na nyuma.”—Ufunuo 4:6b, NW.

      19. Viumbe hai wanne hawa ni picha ya nini, na sisi tunajuaje hili?

      19 Viumbe hawa ni picha ya nini? Njozi iliyoripotiwa na nabii mwingine, Ezekieli, husaidia sisi tupate jibu. Ezekieli alimwona Yehova amekalia kiti cha ufalme katika gari la kimbingu, lililoandamanwa na viumbe hai waliokuwa na miili yenye sifa kama zile alizoeleza Yohana. (Ezekieli 1:5-11, 22-28) Baadaye, Ezekieli aliona tena viumbe hai wakiandamana na hilo gari-kiti cha ufalme. Hata hivyo, wakati huu yeye aliita hao viumbe hai makerubi. (Ezekieli 10:9-15) Viumbe hai wanne anaoona Yohana lazima wawakilishe wale makerubi wengi wa Mungu—viumbe wa cheo cha juu katika tengenezo Lake la roho. Yohana hangefikiri ni jambo lisilo la kawaida kuona makerubi wakikaa karibu sana hivyo na utu wa Yehova, kwa kuwa katika ule mpango wa tabenakulo wa kale, makerubi wawili wa dhahabu walionyeshwa juu ya kifuniko cha ile arka ya agano, ambayo iliwakilisha kiti cha ufalme cha Yehova. Kutoka katikati ya makerubi hao, sauti ya Yehova ilitoa amri kulipa taifa.—Kutoka 25:22; Zaburi 80:1.

      20. Ni katika njia gani inaweza kusemwa kwamba wale viumbe hai wanne wako “katikati ya kiti cha ufalme na kuzunguka kiti cha ufalme”?

      20 Viumbe hai wanne hawa wako “katikati ya kiti cha ufalme na kuzunguka kiti cha ufalme.” Hii humaanisha nini hasa? Ingeweza kumaanisha kwamba wamewekwa kuzunguka kiti cha ufalme katika njia ya kwamba mmoja anasimama katikati ya kila upande. Hivyo, watafsiri wa Today’s English Version walifasili-fasili tu usemi asilia wa Kigiriki kwa njia hii: “kuzunguka kiti cha ufalme kila upande wacho.” Kwa njia nyingine, huo usemi ungeweza kumaanisha kwamba wale viumbe hai wanne wako mahali pa kitovu katika mbingu kilipo kile kiti cha ufalme. Inaelekea, ndiyo sababu The Jerusalem Bible hutafsiri fungu hilo la maneno hivi: “katika kitovu, wakipangwa kikundi kuzunguka kiti cha ufalme chenyewe.” Jambo la maana ni ule ukaribu wa makerubi hao kwenye kiti cha ufalme cha Yehova, ikilinganishwa na wale makerubi ambao Ezekieli aliona kwenye kila kona ya gari la kitengenezo la Yehova. (Ezekieli 1:15-22) Yote haya yanapatana na maneno ya Zaburi 99:1, NW: “Yehova mwenyewe amekuwa mfalme. . . . Yeye anakaa juu ya makerubi.”

      21, 22. (a) Yohana anasimuliaje habari ya wale viumbe hai wanne? (b) Ni nini kinachowakilishwa na kuonekana kwa kila mmoja wa hao viumbe hai wanne?

      21 Yohana anaendelea: “Na kiumbe hai wa kwanza ni kama simba, na kiumbe hai wa pili ni kama fahali mchanga, na kiumbe hai wa tatu ana uso kama wa mwanadamu, na kiumbe hai wa nne ni kama tai arukaye.” (Ufunuo 4:7, NW) Ni kwa nini hawa viumbe hai wanne wanaonekana tofauti sana hivyo, mmoja na mwingine? Hawa viumbe hai mashuhuri kwa wazi wanakazia sifa za kimungu mahususi. Kwanza, kuna simba mwenyewe. Simba anatumiwa katika Biblia kuwa ufananisho wa ujasiri, hasa katika kufuatilia haki na uadilifu. (2 Samweli 17:10; Mithali 28:1) Hivyo, simba anawakilisha vizuri ile sifa ya kimungu ya haki yenye ujasiri. (Kumbukumbu 32:4; Zaburi 89:14) Yule kiumbe hai wa pili anafanana na fahali (ng’ombe) mchanga. Ni sifa gani anayoleta fahali akilini mwako? Kwa Waisraeli fahali alikuwa miliki yenye thamani kwa sababu ya nguvu zake. (Mithali 14:4; ona pia Ayubu 39:9-11, NW.) Basi, huyo fahali mchanga anawakilisha nguvu, nishati-msukumo kama inayotolewa na Yehova.—Zaburi 62:11; Isaya 40:26, NW.

      22 Kiumbe hai wa tatu ana uso kama wa mwanadamu. Huyo lazima awakilishe upendo wa kimungu, kwa kuwa duniani mwanadamu pekee ndiye aliumbwa katika mfano wa Mungu, akiwa na sifa bora sana ya upendo. (Mwanzo 1:26-28; Mathayo 22:36-40; 1 Yohana 4:8, 16) Bila shaka, makerubi hao huonyesha sifa hii wanapotumikia kuzunguka kiti cha ufalme cha Yehova. Namna gani sasa yule kiumbe hai wa nne? Huyo anaonekana kama tai arukaye. Yehova mwenyewe anavuta fikira kwenye uwezo mkubwa wa kuona wa tai: “Mbali katika masafa marefu jicho lake hufuliza kutazama.” (Ayubu 39:29, NW) Kwa sababu hiyo, tai huyo anafananisha vizuri hekima yenye kuona mbali. Yehova ndiye Chanzo cha hekima. Makerubi wake hutumia hekima ya kimungu wanapotii amri zake.—Mithali 2:6; Yakobo 3:17.

      Sifa kwa Yehova Zasikika

      23. Ni nini kinachofananishwa na uhakika wa kwamba hao viumbe hai wanne “wanajaa macho,” na ni jambo gani linalokaziwa na kuwa kwao na jozi tatu za mabawa?

      23 Yohana anaendelea na simulio lake: “Na kwa habari ya hawa viumbe hai wanne, kila mmoja wao pekee ana mabawa sita; kuzunguka na chinichini wanajaa macho. Na wao hawana pumziko mchana na usiku wanaposema: ‘Mtakatifu, mtakatifu, mtakatifu ni Yehova Mungu, Mweza Yote, ambaye alikuwako na ambaye yuko na ambaye anakuja.’” (Ufunuo 4:8, NW) Huu ujazo wa macho unadokeza uwezo wa kuona mbali na ulio kamili. Hao viumbe hai wanne huutumia huu bila kukoma, kwa kuwa wao hawana uhitaji wa kulala usingizi. Wao wanaiga yule Mmoja ambaye kwa habari yake imeandikwa: “Kwa habari ya Yehova, macho yake yanaenda huku na huku katika dunia yote ili kuonyesha nguvu zake kwa niaba ya wale ambao moyo wao ni kamili kuelekea yeye.” (2 Nyakati 16:9, NW) Wakiwa na hesabu kubwa hivyo ya macho, makerubi hao wanaweza kuona kila mahali. Hakuna kitu kinachoponyoka uangalifu wao. Hivyo wametayarishwa vizuri watumikie Mungu katika kazi yake ya kuhukumu. Kwa habari yake imesemwa: “Macho ya Yehova yako kila mahali, ili kushika lindo juu ya wabaya na wema.” (Mithali 15:3, NW) Na wakiwa na jozi tatu za mabawa—nambari tatu ikiwa inatumiwa katika Biblia kutilia mkazo—makerubi hao wanaweza kwenda kwa wepesi wa umeme wakapeleke habari za hukumu za Yehova na kuzitekeleza.

      24. Hao makerubi wanamsifuje Yehova, na kukiwa na maana gani?

      24 Sikiliza! Wa kimelodia, wenye kuchochea nafsi, ni wimbo wa sifa ambao makerubi wanamwimbia Yehova: “Mtakatifu, mtakatifu, mtakatifu ni Yehova Mungu, Mweza Yote, ambaye alikuwako na ambaye yuko na ambaye anakuja.” Kwa mara nyingine tena, huo utatu huonyesha mkazo. Makerubi hao wanathibitisha kwa nguvu utakatifu wa Yehova Mungu. Yeye ndiye Chanzo na Kiwango cha hali ya juu kabisa cha utakatifu. Yeye pia ndiye “Mfalme wa umilele,” sikuzote yeye ndiye “Alfa na Omega, wa kwanza na wa mwisho, mwanzo na mwisho.” (1 Timotheo 1:17; Ufunuo 22:13, NW) Makerubi hao hawachukui vipindi vya kupumzika wanapopiga mbiu ya sifa za Yehova zisizo na kifani mbele ya uumbaji wote.

      25. Viumbe hai wanne na wale wazee 24 wanaunganaje katika kusujudia Yehova?

      25 Mbingu ya mbingu zote inavuma kwa sifa anazoimbiwa Yehova! Elezo la Yohana laendelea: “Na wakati wowote viumbe hai wanapotoa utukufu na heshima na utoaji-shukrani kwa yule Mmoja aketiye juu ya kiti cha ufalme, Mmoja ambaye huishi milele na milele, wazee ishirini na wanne huanguka chini mbele ya Mmoja aketiye juu ya kiti cha ufalme na huabudu Mmoja ambaye huishi milele na milele, nao hutupa mataji yao mbele ya kiti cha ufalme, kusema: ‘Wewe wastahiki, Yehova, hata Mungu wetu, kupokea utukufu na heshima na nguvu, kwa sababu wewe uliumba vitu vyote, na kwa sababu ya penzi lako hivyo vilikuwako na vikaumbwa.’” (Ufunuo 4:9-11, NW) Katika Andiko lote, hili ndilo mojapo majulisho-wazi matukufu zaidi ya kumpa Yehova shikamoo, Mungu wetu na Bwana Mwenye Enzi Kuu!

      26. Ni kwa nini wazee 24 wanatupa mataji yao mbele ya Yehova?

      26 Wazee 24 wana mwelekeo wa akili ule ule ambao Yesu anaonyesha, hata wanatupa mataji yao chini mbele ya Yehova. Wazo la kujikweza wenyewe katika kuwapo kwa Mungu liko mbali zaidi sana na akili zao. Wao wanatambua kwa unyenyekevu kwamba kusudi pekee la umaliki wao ni kumletea yeye heshima na utukufu, kama afanyavyo Yesu sikuzote. (Wafilipi 2:5, 6, 9-11) Kwa unyenyekeo, wanakubali udhalili wao wenyewe na kukiri kwamba utawala wao unategemea enzi kuu ya Yehova. Hivyo, wako katika upatani wa moyo wote na wale makerubi na ule uumbaji mwingine wote wenye uaminifu katika kumpa sifa na utukufu Mungu ambaye aliumba vitu vyote.—Zaburi 150:1-6.

      27, 28. (a) Elezo la Yohana la njozi hii linapasa lituathirije? (b) Ni maswali gani huzuka kwa habari ya ambacho Yohana anafuata kuona na kusikia?

      27 Ni nani anaweza kubaki bila kuchochewa hisia zake anaposoma simulizi la Yohana la njozi hii? Ni nzuri mno na tukufu! Lakini kitu halisi lazima kiweje? Fahari yenyewe ya Yehova lazima ihuishe yeyote aliye na moyo wenye uthamini ajiunge na wale viumbe hai wanne na wale wazee 24 katika kumsifu Yeye, katika sala na pia kwa kutangaza peupe jina Lake. Huyu ndiye Mungu ambaye kwa ajili yake Wakristo wana pendeleo la kuwa mashahidi leo. (Isaya 43:10) Kumbuka kwamba njozi ya Yohana inahusu ile siku ya Bwana, tulimo sisi sasa. “Zile roho saba” sikuzote ziko karibu kutuongoza na kututia imara. (Wagalatia 5:16-18) Neno la Mungu linapatikana leo kutusaidia tuwe watakatifu katika kutumikia Mungu mtakatifu. (1 Petro 1:14-16) Kwa hakika, sisi tu wenye furaha kusoma kwa sauti kubwa maneno ya unabii huu. (Ufunuo 1:3, NW) Yanaandaa kishawishi kama nini tuwe waaminifu kwa Yehova na tusiruhusu ulimwengu utukengeushe kutoka kuimba kwa utendaji sifa zake!—1 Yohana 2:15-17.

      28 Kufikia hapo, Yohana ameeleza anachoona wakati anapoalikwa akaribie kupitia mlango huo uliofunguliwa katika mbingu. Kwa kutokeza zaidi sana, yeye anaripoti kwamba Yehova, akiwa katika uzuri wote wa fahari Yake na adhama, ameketi juu ya kiti cha ufalme Chake cha kimbingu. Yeye anazungukwa na tengenezo lenye nguvu zaidi ya matengenezo yote—liking’aa kwa umaridadi mwingi na ushikamanifu walo. Mahakama ya kimungu i kikaoni. (Danieli 7:9, 10, 18) Jukwaa limewekwa kwa ajili ya kitu kisicho cha kawaida kitukie. Ni nini, na kinatuathirije sisi leo? Acheni tutazame kadiri mandhari ifungukavyo!

  • Uzuri Mwingi Mno wa Kiti cha Ufalme cha Yehova cha Kimbingu
    Ufunuo—Upeo Wao Mtukufu U Karibu!
    • [Picha ya ukurasa mzima katika ukurasa wa 75]

      [Picha ya ukurasa mzima katika ukurasa wa 78]

  • “Ni Nani Ambaye Anastahili Kufungua Hati-Kunjo?”
    Ufunuo—Upeo Wao Mtukufu U Karibu!
    • Sura ya 15

      “Ni Nani Ambaye Anastahili Kufungua Hati-Kunjo?”

      1. Ni nini kinachotukia sasa katika ile njozi ya Yohana?

      YA HALI YA JUU MNO! YENYE KUVUVIA HOFU MNO! Ndivyo ilivyo ile njozi yenye kuchochea ya kiti cha ufalme cha Yehova katika mazingira yacho katikati ya taa za moto, makerubi, wazee 24, na bahari ya kioo. Lakini Yohana, ni kitu gani unachofuata kuona? Yohana anakaza macho yake juu ya kitovu chenyewe cha mandhari hii ya kimbingu, akituambia hivi: “Na mimi nikaona katika mkono wa kulia wa Mmoja aketiye juu ya kiti cha ufalme hati-kunjo iliyoandikwa ndani na kwenye upande-pindu, imefungwa kikiki kwa vifungo saba. Na mimi nikaona malaika kabambe akipiga mbiu kwa sauti kubwa: ‘Ni nani ambaye anastahili kufungua hati-kunjo na kulegeza vifungo vyayo?’ Lakini wala katika mbingu wala juu ya dunia wala chini ya dunia hakukupatikana hata mmoja anayeweza kufungua hati-kunjo hiyo au kutazama ndani yayo. Na mimi nikabubujisha machozi mengi kwa sababu hakuna mmoja aliyepatikana kuwa anastahili kufungua hati-kunjo hiyo au kutazama ndani yayo.”—Ufunuo 5:1-4, NW.

      2, 3. (a) Ni kwa nini Yohana ana hamu nyingi kwamba mtu fulani apatikane wa kufungua hati-kunjo, lakini ni nini linaloonekana kuwa tazamio la jambo hilo? (b) Watu wa Mungu wamengojea nini kwa hamu nyingi katika wakati wetu?

      2 Yehova mwenyewe, Bwana Mwenye Enzi Kuu wa uumbaji wote, ndiye anayetoa hati-kunjo hiyo. Ni lazima iwe imejaa habari za muhimu, kwa kuwa ina maandishi mbele na nyuma. Udadisi wetu unaamshwa. Hati-kunjo hiyo ina nini ndani? Tunakumbuka mwaliko wa Yehova kwa Yohana: “Njoo juu huku, na mimi nitakuonyesha wewe vitu ambavyo lazima vitukie.” (Ufunuo 4:1, NW) Tukiwa na taraja lenye kuwasha-washa, sisi tunatazama mbele ili tujifunze juu ya vitu hivyo. Lakini ole, hati-kunjo imeshindikwa ndi, ikafungwa kwa vifungo saba!

      3 Je! yule malaika kabambe atapata mtu anayestahili kufungua hiyo hati-kunjo? Kulingana na Kingdom Interlinear, hati-kunjo iko “juu ya mkono wa kulia” wa Yehova. Hii hudokeza kwamba yeye anaitoa juu ya kiganja chake kilichofunguliwa. Lakini inaonekana kwamba hakuna mmoja katika mbingu au juu ya dunia anayestahili kupokea na kufungua hati-kunjo hiyo. Wala hata chini ya dunia, miongoni mwa watumishi wa Mungu ambao wamekufa, hakuna yeyote aliye na sifa zinazofaa kupokea heshima hii ya juu sana. Si ajabu kwamba Yohana anaonekana amefadhaika! Pengine yeye hatajifunza kamwe vile “vitu ambavyo lazima vitukie.” Vilevile katika siku yetu, watu wa Mungu waliopakwa mafuta wamengojea kwa hamu sana Yehova apeleke nuru yake na ukweli juu ya Ufunuo. Hili angefanya kwa mwendeleo katika wakati uliowekwa wa utimizo wa unabii huo, ili aongoze watu wake katika njia ya “wokovu mtukufu.”—Zaburi 43:3, 5, NW.

      Mmoja Ambaye Anastahili

      4. (a) Ni nani ambaye amepatikana anayestahili kufungua hati-kunjo na vifungo vyayo? (b) Wale wa jamii ya Yohana na waandamani wayo sasa wanashiriki katika thawabu na pendeleo gani?

      4 Ndiyo kuna mtu fulani ambaye anaweza kufungua hati-kunjo! Yohana asimulia hivi: “Lakini mmoja wa wale wazee asema kwangu mimi: ‘Acha kutoa machozi. Tazama! Simba ambaye ni wa kabila la Yuda, mzizi wa Daudi, ameshinda ili kufungua hati-kunjo na vifungo saba vyayo.’” (Ufunuo 5:5, NW) Kwa hiyo Yohana, kausha machozi hayo! Ile jamii ya Yohana na waandamani wayo washikamanifu leo wamevumilia pia makumi ya miaka ya majaribu makali huku wakingojea kwa saburi nuru ya elimu. Lo! ni thawabu yenye kufariji kama nini tuliyo nayo sasa katika kuelewa ile njozi, na ni pendeleo kama nini kushiriki katika utimizo wayo kwa kupiga mbiu ya ujumbe wayo kwa wengine!

      5. (a) Ni unabii gani uliosemwa kuhusu Yuda, na wazao wa Yuda walitawala wapi? (b) Shilo ni nani?

      5 Aha, “Simba ambaye ni wa kabila la Yuda”! Yohana anazoelea unabii ambao Yakobo, babu ya jamii ya Kiyahudi, alitangaza kuhusu mwana wake wa nne, Yuda: “Mwana-simba ni Yuda. Kutoka windo, mwana wangu, wewe utapanda hakika. Yeye aliinama, yeye alijinyoosha mwenyewe kama simba na, kama simba, ni nani ambaye huthubutu kuamsha yeye? Fimbo ya kifalme haitageuka kando kutoka Yuda, wala gongo la kamanda kutoka katikati ya nyayo zake, mpaka Shilo aje; na kwa yeye utii wa vikundi vya watu utakuwa.” (Mwanzo 49:9, 10, NW) Mstari wa kifalme wa watu wa Mungu ulikuwa na shina katika Yuda. Kuanzia na Daudi, wafalme wote waliotawala katika Yerusalemu mpaka wakati Wababuloni walipoharibu jiji hilo walikuwa wazao wa Yuda. Lakini hakuna mmoja wao aliyekuwa ndiye Shilo aliyetabiriwa na Yakobo. Shilo humaanisha “Yeye Ambaye [Haki] Ni Yake.” Kiunabii, jina hilo lilielekeza kwa Yesu, mmoja ambaye sasa Ufalme wa Kidaudi ni wake daima.—Ezekieli 21:25-27; Luka 1:32, 33; Ufunuo 19:16.

      6. Ni katika njia gani Yesu alikuwa “kitawi” cha Yese na pia “mzizi wa Daudi”?

      6 Kwa haraka Yohana anatambua lile rejezo kwa “mzizi wa Daudi.” Mesiya aliyeahidiwa anaitwa kiunabii “kitawi kutoka kisiki cha Yese [baba ya Mfalme Daudi] . . . chipukizi” na pia “mzizi wa Yese ambao utakuwa unasimama kuwa ishara kwa vikundi vya watu.” (Isaya 11:1, 10, NW) Yesu alikuwa kitawi cha Yese, akizaliwa katika mstari wa kifalme wa Daudi, mwana wa Yese. Na zaidi, akiwa mzizi wa Yese, ndiye yule Mmoja ambaye alifanya nasaba ya kifalme ya Kidaudi ichipuke tena, akiipa uhai na lisho milele.—2 Samweli 7:16.

      7. Ni nini kinachomstahilisha Yesu kuchukua hati-kunjo kutoka mkono wa Mmoja anayeketi juu ya kiti cha ufalme?

      7 Yesu ndiye mmoja ambaye kwa kutokeza sana, akiwa binadamu mkamilifu, alitumikia Yehova katika ukamilifu na chini ya majaribu yenye maumivu makali sana. Yeye alitoa jawabu kamili kwa dai la Shetani. (Mithali 27:11) Hivyo, yeye angeweza kusema kama alivyosema katika ule usiku kabla ya kifo chake cha dhabihu, “mimi nimeshinda ulimwengu.” (Yohana 16:33, NW) Kwa sababu hiyo, Yehova alimwaminisha Yesu aliyefufuliwa “mamlaka yote katika mbingu na juu ya dunia.” Yeye pekee kati ya watumishi wote wa Mungu ndiye aliye na sifa zinazofaa kupokea hati-kunjo, akitazamia kujulisha ujumbe wayo wenye maana kubwa.—Mathayo 28:18, NW.

      8. (a) Kwa habari ya Ufalme, ni jambo gani linaloonyesha ustahili wa Yesu? (b) Ni kwa nini inafaa kwamba mmoja wa wale wazee 24 afunulie Yohana yule mtu ambaye anastahili kufungua hati-kunjo?

      8 Inafaa kweli kweli kwamba yapasa Yesu afungue hati-kunjo. Tangu 1914 yeye ameketishwa juu ya kiti cha ufalme akiwa Mfalme wa Ufalme wa Kimesiya, na hati-kunjo inafunua mengi sana kuhusu ule Ufalme na utakachotimiza. Kwa uaminifu Yesu alitoa ushuhuda kwa ukweli wa Ufalme alipokuwa hapa duniani. (Yohana 18:36, 37) Yeye alifundisha wafuasi wake wasali juu ya kuja kwa Ufalme huo. (Mathayo 6:9, 10) Yeye alianzisha kuhubiriwa kwa habari njema za Ufalme mwanzoni mwa wakati wa Kikristo na akatoa unabii juu ya kukamilishwa kwa kazi hiyo ya kuhubiri katika pindi ya wakati wa mwisho. (Mathayo 4:23; Marko 13:10) Hali kadhalika, inafaa kwamba yapasa mmoja wa wazee 24 afunulie Yohana kwamba Yesu ndiye mmoja atakayefungua vile vifungo. Kwa nini? Kwa sababu wazee hawa wanakalia viti vya ufalme na huvaa mataji, wakiwa warithi washirika pamoja na Kristo katika Ufalme wake.—Warumi 8:17; Ufunuo 4:4.

      ‘Mwana-Kondoo Ambaye Alichinjwa’

      9. Badala ya simba, Yohana anaona nini kikisimama “katikati ya kiti cha ufalme,” naye alielezaje habari zacho?

      9 Yohana anatazama aone huyu “Simba ambaye ni wa kabila la Yuda.” Lakini inashangaza kama nini! Umbo la ufananisho lililo tofauti kabisa latokea: “Na mimi nikaona akisimama katikati ya kiti cha ufalme na ya viumbe hai wanne na katikati ya wazee mwana-kondoo kana kwamba alikuwa amechinjwa, akiwa na pembe saba na macho saba, macho ambayo humaanisha roho saba za Mungu ambazo zimepelekwa katika dunia kwa ujumla.”—Ufunuo 5:6, NW.

      10. Ni nani aliye “mwana-kondoo” ambaye Yohana aliona, na ni kwa nini jina hilo linafaa?

      10 Katika kitovu kabisa, kando ya kile kiti cha ufalme, ndani ya duara zilizofanyizwa na wale viumbe hai wanne na wale wazee 24, kuna mwana-kondoo! Bila shaka Yohana anashirikisha kwa haraka huyu mwana-kondoo na “Simba ambaye ni wa kabila la Yuda” na “mzizi wa Daudi.” Yeye anajua kwamba, zaidi ya miaka 60 mapema, Yohana Mbatizaji alimjulisha Yesu kwa Wayahudi watazamaji kuwa “Mwana-Kondoo wa Mungu ambaye huondolea mbali dhambi ya ulimwengu.” (Yohana 1:29, NW) Wakati wote wa maisha yake duniani, Yesu alibaki bila kutiwa waa na ulimwengu—kama vile mwana-kondoo asiye na ila—ili aweze kutoa uhai wake usio na lawama uwe dhabihu kwa ajili ya aina ya binadamu.—1 Wakorintho 5:7; Waebrania 7:26.

      11. Ni kwa nini si utovu wa adhama kumwakilisha Yesu aliyetukuzwa kuwa “mwana-kondoo kana kwamba alikuwa amechinjwa”?

      11 Je! kwa vyovyote ni kumfanya mdogo au utovu wa adhama kuwakilisha Yesu aliyetukuzwa kuwa “mwana-kondoo kana kwamba alikuwa amechinjwa”? Sivyo kabisa! Ule uhakika wa kwamba Yesu alibaki akiwa mwaminifu mpaka kifo ulikuwa ushinde mkuu kwa Shetani na ushindi mkubwa wenye shangwe kwa Yehova Mungu. Kumwakilisha Yesu katika njia hii huonyesha waziwazi ushindi wake juu ya ulimwengu wa Shetani na ni kikumbusho cha ule upendo wenye kina walio nao Yehova na Yesu kwa aina ya binadamu. (Yohana 3:16; 15:13; linga Wakolosai 2:15.) Hivyo Yesu anaonyeshwa kuwa ile Mbegu iliyoahidiwa, akiwa na sifa zinazofaa zenye kutokeza kufungua ile hati-kunjo.—Mwanzo 3:15.

      12. Zile pembe saba za Mwana-Kondoo hufananisha nini?

      12 Ni kitu gani kingine kinachoongeza uthamini wetu kwa huyu “mwana-kondoo”? Ana pembe saba. Pembe katika Biblia mara nyingi huwa ni ufananisho wa nguvu au mamlaka, na saba ingeonyesha utimilifu. (Linga 1 Samweli 2:1, 10; Zaburi 112:9; 148:14.) Kwa sababu hiyo, zile pembe saba za Mwana-Kondoo zawakilisha utimilifu wa nguvu ambazo Yehova ameaminisha Yesu. Yeye yuko “juu sana juu ya kila serikali na mamlaka na nguvu na ubwana na kila jina linaloitwa jina, si katika huu mfumo wa mambo tu, bali pia katika ule unaopasa kuja.” (Waefeso 1:20-23; 1 Petro 3:22, NW) Hasa Yesu ametumia nguvu, nguvu za kiserikali, tangu 1914 wakati Yehova alipomketisha juu ya kiti cha ufalme akiwa Mfalme wa kimbingu.—Zaburi 2:6.

      13. (a) Macho saba ya Mwana-Kondoo yanafananisha nini? (b) Mwana-Kondoo anaanza kufanya nini?

      13 Zaidi ya hilo, Yesu amejazwa roho takatifu kwa utimilifu, kama inavyofananishwa na yale macho saba ya Mwana-Kondoo, ambayo “humaanisha roho saba za Mungu.” Yesu ni mfereji ambao kupitia huo utimilifu wa kani-tendaji ya Mungu hutiririkia watumishi Wake wa kidunia. (Tito 3:6) Kwa udhahiri, ni kupitia roho ii hii kwamba yeye huona kutoka mbinguni yanayotendeka hapa duniani. Kama Baba yake, Yesu ana utambuzi mkamilifu. Hakuna kitu kinachoponyoka asikione. (Linga Zaburi 11:4; Zekaria 4:10.) Kwa wazi, Mwana huyu—yule mshika ukamilifu aliyeshinda ulimwengu; yule Simba wa kabila la Yuda; ule mzizi wa Daudi; yule mmoja aliyetoa uhai wake kwa ajili ya aina ya binadamu; yule mmoja aliye na mamlaka kamili, utimilifu wa roho takatifu, na utambuzi mkamilifu kutoka kwa Yehova Mungu—ndiyo, huyu mmoja anastahili kwa kutokeza sana kutwaa hati-kunjo kutoka mkono wa Yehova. Je! yeye anasitasita kukubali utume huu wa utumishi katika tengenezo tukufu la Yehova? Hapana! Badala yake, “yeye alienda na mara hiyo akaitwaa [hati-kunjo] kutoka mkono wa kulia wa Mmoja aketiye juu ya kiti cha ufalme.” (Ufunuo 5:7, NW) Ni kielelezo kilichoje cha utii wa moyo wa kupenda!

      Nyimbo za Sifa

      14. (a) Wale viumbe hai wanne na wazee 24 wanatendaje kwa kuitikia kutwaa kwa Yesu hati-kunjo? (b) Ile habari ambayo Yohana anapokea kuhusu wale wazee 24 inathibitishaje utambulisho na cheo chao?

      14 Wale wengine mbele ya kiti cha ufalme cha Yehova wanatendaje kwa kuitikia? “Na wakati alipotwaa ile hati-kunjo, wale viumbe hai wanne na wale wazee ishirini na wanne walianguka chini mbele ya Mwana-Kondoo, kila mmoja akiwa na kinubi na mabakuli ya dhahabu yaliyokuwa yamejaa uvumba, na huo uvumba humaanisha sala za watakatifu.” (Ufunuo 5:8, NW) Kama wale viumbe hai wanne wa kikerubi mbele ya kiti cha ufalme cha Mungu, wazee 24 wanainamia Yesu katika kukiri mamlaka yake. Lakini hao wazee wako peke yao katika kuwa na vinubi na mabakuli ya uvumba.a Na wao peke yao sasa waimba wimbo mpya. (Ufunuo 5:9) Hivyo wanafanana na wale 144,000 wa “Israeli wa Mungu” watakatifu, ambao pia wanabeba vinubi na kuimba wimbo mpya. (Wagalatia 6:16; Wakolosai 1:12; Ufunuo 7:3-8; 14:1-4) Na zaidi, wale wazee 24 wanaonyeshwa wakitimiza utendaji wa kikuhani wa kimbingu, uliofananishwa na ule wa makuhani katika Israeli wa kale ambao walimchomea Yehova uvumba katika ile tabenakulo—utendaji ambao ulikwisha wakati Yehova alipoioondolea mbali ile Sheria ya Musa, akiigongomelea penye nguzo ya mateso ya Yesu. (Wakolosai 2:14) Tunakata neno gani kutokana na haya yote? Kwamba hapa wale washindi wapakwa-mafuta wanaonekana wakiwa katika mgawo wao wa mwisho kabisa wakiwa ‘makuhani wa Mungu na wa Kristo, wakitawala wakiwa wafalme pamoja naye kwa miaka elfu.’—Ufunuo 20:6, NW.

      15. (a) Katika Israeli, ni nani pekee aliyependelewa kuingia ndani ya Patakatifu Zaidi Sana pa ile tabenakulo? (b) Ni kwa nini ilikuwa ni uhai au kifo kwamba kuhani mkuu achome uvumba mbele ya kuingia ndani ya Patakatifu Zaidi Sana?

      15 Katika Israeli wa kale, kuhani mkuu pekee ndiye aliyeruhusiwa kuingia Patakatifu Zaidi Sana mbele za kuwapo kwa ufananisho kwa Yehova. Kwake yeye, kupeleka uvumba kulikuwa ni uhai au kifo. Sheria ya Yehova ilisema: “Ni lazima [Haruni] achukue kishika-moto kilichojaa makaa-mawe yenye kuwaka moto kutoka madhabahu mbele za Yehova, na mavungu mawili ya mikono yake yakiwa yamejaa uvumba mzuri uliotiwa manukato, na yeye lazima avilete ndani ya pazia. Ni lazima pia atie uvumba juu ya moto mbele za Yehova, na wingu la uvumba lazima litande juu ya funiko la Arka, lililo juu ya Agano, ili asije akafa.” (Walawi 16:12, 13, NW) Haikuwezekana kuhani mkuu apenye kwa kufaulu ndani ya Patakatifu Zaidi Sana isipokuwa yeye alichoma uvumba.

      16. (a) Katika mfumo wa mambo wa Kikristo, ni nani wanaopenya ndani ya Patakatifu Zaidi Sana palipofananishwa? (b) Ni kwa nini Wakristo wapakwa-mafuta sharti ‘wachome uvumba’?

      16 Katika mfumo wa mambo wa Kikristo, anayepata kuingia Patakatifu Zaidi Sana palipofananishwa, mahali pa kuwapo kwa Yehova katika mbingu, si Kuhani Mkuu tu aliyefananishwa, yaani, Yesu Kristo, bali hatimaye kila mmoja wa makuhani wa chini 144,000 pia hupata kupaingia. (Waebrania 10:19-23) Mwingio ndani wa hapa Patakatifu Zaidi Sana hauwezekani kwa makuhani hawa, kama wanavyowakilishwa hapa na wale wazee 24, isipokuwa wao ‘wachome uvumba,’ yaani, watoe sala na dua kwa Yehova kwa kuendelea.—Waebrania 5:7; Yuda 20, 21; linga Zaburi 141:2.

      Wimbo Mpya

      17. (a) Ni wimbo gani mpya wanaoimba wale wazee 24? (b) Usemi huo “wimbo mpya” hutumiwaje kwa kawaida katika Biblia?

      17 Sasa wimbo wa kimelodia wasikika. Anaimbiwa Mwana-Kondoo na washiriki wenzake wa kikuhani, wale wazee 24: “Na wao huimba wimbo mpya, kusema: ‘Wewe wastahili kuchukua hati-kunjo na kufungua vifungo vyayo, kwa sababu wewe ulichinjwa na kwa damu yako wewe ulinunua watu kwa ajili ya Mungu kutoka kila kabila na ulimi na kikundi cha watu na taifa.’” (Ufunuo 5:9, NW) Usemi “wimbo mpya” huonekana mara kadhaa katika Biblia na kwa kawaida hurejezea kumsifu Yehova kwa ajili ya tendo fulani hodari la ukombozi. (Zaburi 96:1; 98:1; 144:9) Hivyo, wimbo ni mpya kwa sababu yule mwimbaji sasa anaweza kupiga mbiu za kazi zaidi za ajabu za Yehova na aonyeshe uthamini uliofanywa upya kwa ajili ya jina Lake tukufu.

      18. Ni kwa ajili ya nini wazee 24 wanamsifu Yesu wakiwa na wimbo wao mpya?

      18 Ingawa hivyo, hapa, wale wazee 24 wanaimba wimbo mpya mbele ya Yesu badala ya mbele za Yehova. Lakini kanuni ni ile ile. Wao wanamsifu Yesu kwa ajili ya vitu vipya ambavyo yeye, akiwa Mwana wa Mungu, amewafanyia. Kwa njia ya damu yake, yeye alipatanisha agano jipya na hivyo akafanya kuwezekane kule kutokezwa kwa taifa jipya likiwa miliki ya pekee ya Yehova. (Warumi 2:28, 29; 1 Wakorintho 11:25; Waebrania 7:18-25) Washiriki wa hili taifa jipya la kiroho walitoka kwa mataifa mengi ya kimnofu, lakini Yesu aliwaunganisha kuwa kundi moja wawe taifa moja.—Isaya 26:2; 1 Petro 2:9, 10.

      19. (a) Ni baraka gani ambazo Israeli wa kimnofu walishindwa kupata kwa sababu ya kutoaminika kwao? (b) Taifa jipya la Yehova linapata kufurahia baraka gani?

      19 Wakati Yehova alipofanyiza Waisraeli wa kale kuwa taifa huko nyuma katika siku za Musa, yeye alifanya agano pamoja nao na akaahidi kwamba ikiwa wao wangebaki wakiwa waaminifu kwa agano hilo, wao wangekuwa ufalme wa makuhani mbele zake. (Kutoka 19:5, 6) Waisraeli hawakuwa waaminifu na kwa hiyo hawakupata kamwe utimizo wa ahadi hiyo. Kwa upande mwingine, taifa jipya, lililofanyizwa kwa thamani ya agano jipya lenye kupatanishwa na Yesu, limebaki likiwa jaminifu. Basi washiriki walo wanapata kutawala juu ya dunia wakiwa wafalme na pia wanatumikia wakiwa makuhani, wakisaidia wale wenye mioyo inayofaa miongoni mwa aina ya binadamu wapatanishwe kwa Yehova. (Wakolosai 1:20) Ni kama vile ule wimbo mpya unavyoonyesha hilo: “Na wewe ulifanya wao kuwa ufalme na makuhani kwa Mungu wetu, nao wanapaswa kutawala wakiwa wafalme juu ya dunia.” (Ufunuo 5:10, NW) Hao wazee 24 wana shangwe kama nini katika kuimba huu wimbo mpya wa sifa kwa Yesu Kristo aliyetukuzwa!

      Korasi ya Kimbingu

      20. Ni wimbo gani wa kusifu Mwana-Kondoo unaovumishwa sasa?

      20 Wale wengine wa lile jeshi kubwa mno la kimbingu la tengenezo la Yehova wanaitikiaje huu wimbo mpya: Yohana anasisimuka kuona upatani wao wa kuhisi moyoni: “Na mimi nikaona, na mimi nikasikia sauti ya malaika wengi kuzunguka kiti cha ufalme na viumbe hai na wazee, na nambari yao ilikuwa mamiriadi ya mamiriadi na maelfu ya maelfu, wakisema kwa sauti kubwa: ‘Mwana-Kondoo ambaye alichinjwa anastahili kupokea nguvu na utajiri na hekima na imara na heshima na utukufu na baraka.’” (Ufunuo 5:11, 12, NW) Ni wimbo wa sifa wenye kuvutia kama nini!

      21. Je! kusifiwa kwa Mwana-Kondoo kunapunguza enzi kuu au cheo cha Yehova?

      21 Je! hii inamaanisha kwamba sasa Yesu amechukua mahali pa Yehova Mungu na kwamba sasa uumbaji wote umegeuka ukaanza kumsifu yeye badala ya Baba yake? Mbali sana na hilo! Badala ya hivyo, huu wimbo wa sifa unapatana na yale aliyoandika mtume Paulo: “Mungu alikweza yeye [Yesu] kwenye cheo cha juu sana na kwa fadhili akampa yeye jina ambalo liko juu ya kila jina jingine, ili kwamba kwa jina la Yesu kila goti lipaswe kupigwa la wale walio katika mbingu na wale walio juu ya dunia na wale walio chinichini ya dunia, na kila ulimi upaswe kukiri waziwazi kwamba Yesu Kristo ni Bwana kwa utukufu wa Mungu Baba.” (Wafilipi 2:9-11, NW) Yesu anasifiwa hapa kwa sababu ya sehemu yake katika kumaliza lile suala la msingi lililo mbele ya uumbaji wote—kutetewa kwa uhalali wa enzi kuu ya Yehova. Kweli kweli, ni utukufu ulioje hilo limeletea Baba yake!

      Wimbo wa Utukuzo Unaokua

      22. Sauti kutoka milki ya kidunia zinajiunga katika wimbo gani wa utukuzo?

      22 Katika ile mandhari aliyoieleza Yohana, majeshi ya kimbingu yanamtolea Yesu kigelegele cha kimelodia katika ukiri wa uaminifu wake na mamlaka yake ya kimbingu. Katika hili, wanaungwa na sauti kutoka milki ya kidunia hizo nazo zinaposhiriki kusifu Baba na Mwana pia. Kama vile mambo aliyotimiza mwana wa kibinadamu yanavyoweza kuwaletea sifa wazazi, ndivyo na mwendo wa ushikamanifu wa Yesu unavyotokeza sifa miongoni mwa uumbaji wote “kwa utukufu wa Mungu Baba.” Hivyo, Yohana anaendelea kuripoti hivi: “Na kila kiumbe ambacho kimo katika mbingu na juu ya dunia na chini-chini ya dunia na juu ya bahari, na vitu vyote vilivyo ndani yavyo, mimi nilisikia vikisema: ‘Kwake yule Mmoja aketiye juu ya kiti cha ufalme na kwa Mwana-Kondoo kuwe baraka na heshima na utukufu na uweza milele na milele.’”—Ufunuo 5:13, NW.

      23, 24. (a) Ni nini kinachoonyesha ni wakati gani wimbo wa utukuzo ungeanza katika mbingu, na wakati gani juu ya dunia? (b) Wimbo wa utukuzo unazidije kukua kadiri miaka inavyopita?

      23 Ni wakati gani huu wimbo wa utukuzo unaopita ubora wote unapovuma? Ulianza mapema katika ile siku ya Bwana. Baada ya Shetani na roho waovu wake kutupwa nje ya zile mbingu, “kila kiumbe ambacho kimo katika mbingu” kingeweza kuungana katika huu wimbo wa sifa. Na, kama vile maandishi yanavyoonyesha, tangu 1919 umayamaya unaoendelea kukua duniani umeunganisha sauti zao katika kusifu Yehova, ukiongezeka kutoka maelfu machache mpaka zaidi ya milioni sita kufikia mwaka wa 2005.b Baada ya mfumo wa Shetani wa kidunia kuangamizwa, “kila kiumbe . . . juu ya dunia” kitakuwa kikiimba juu ya sifa za Yehova na Mwana wake. Katika wakati wa Yehova mwenyewe, ufufuo wa yale mamilioni yasiyohesabika ya wafu utaanza, na ndipo “kila kiumbe . . . chinichini ya dunia” ambacho kimo katika kumbukumbu la Mungu kitakuwa na fursa ya kujiunga katika kuimba wimbo wa utukuzo.

      24 Tayari, “kutoka miisho ya dunia . . . bahari na . . . visiwa,” mamilioni ya binadamu wanaimba wimbo mpya katika ushirika na tengenezo la Yehova la tufe lote. (Isaya 42:10, Zaburi 150:1-6, NW) Sifa hii yenye shangwe itafikia uvumo wenye sauti kubwa kwenye mwisho wa ile Mileani, wakati aina ya binadamu itakuwa imeinuliwa kufikia ukamilifu. Yule nyoka wa zamani, mdanganyaji mkuu, Shetani mwenyewe, ataangamizwa baada ya hapo katika utimizo kamili wa Mwanzo 3:15, na katika upeo wenye shangwe yenye ushindi, uumbaji wote ulio hai, wa kiroho na wa kibinadamu, utaimba kwa sauti moja: “Kwake yule Mmoja aketiye juu ya kiti cha ufalme na kwa Mwana-Kondoo kuwe baraka na heshima na utukufu na uweza milele na milele.” Hakutakuwa na sauti yenye kukaidi katika ulimwengu wote mzima.

      25. (a) Kusoma simulizi la Yohana kuhusu wimbo wa utukuzo wa ulimwengu wote mzima kunatuhimiza sisi tufanye nini? (b) Ni kielelezo gani kizuri sana tunachowekewa na viumbe hai wanne na wazee 24 wakati njozi inapoisha?

      25 Huo utakuwa wakati wenye shangwe kama nini! Hakika, yale ambayo Yohana anaeleza hapa yanafanya mioyo yetu ifure kwa furaha na yanachochea sisi tujiunge na majeshi ya kimbingu katika kuimbia Yehova Mungu na Yesu Kristo sifa za kuhisi moyoni. Je! sisi hatuazimii zaidi ya wakati mwingine wowote kuvumilia katika kazi zinazofaa? Tukifanya hivyo, sisi tunaweza kutazamia kwamba, kwa msaada wa Yehova, sisi mmoja mmoja tutakuwapo kwenye huo upeo wenye furaha, tukiongeza sauti zetu kwenye korasi hiyo ya sifa ya ulimwengu wote mzima. Kwa hakika, wale viumbe hai wanne wa kikerubi na wale Wakristo wapakwa-mafuta waliofufuliwa wanapatana kabisa, kwa kuwa ile njozi inamalizia kwa maneno haya: “Na viumbe hai wanne wakaenda wakisema: ‘Ameni!’ na wazee wakaanguka chini na wakaabudu.”—Ufunuo 5:14, NW.

      26. Inatupasa sisi tuzoee imani katika nini, naye Mwana-Kondoo anajitayarisha kufanya nini?

      26 Wewe msomaji mpendwa, na uzoee imani katika dhabihu ya Mwana-Kondoo—‘mmoja anayestahili’—na ubarikiwe katika jitihada zako za unyenyekevu za kumwabudu na kumtumikia Yehova—“yule Mmoja aketiye juu ya kiti cha ufalme.” Acha jamii ya Yohana ikusaidie leo iandaapo “kipimo cha ugavi wa chakula [cha kiroho kinachohitajiwa] kwenye wakati unaofaa.” (Luka 12:42, NW) Lakini tazama! Yule Mwana-Kondoo anajitayarisha kufungua vile vifungo saba. Kuna mafumbuo gani yenye kusisimua katika akiba sasa kwa ajili yetu?

      [Maelezo ya Chini]

      a Kusema kisarufi, usemi “kila mmoja akiwa na kinubi na mabakuli ya dhahabu yaliyokuwa yamejaa uvumba” ungeweza kurejezea wazee na viumbe hai wanne pia. Hata hivyo, muktadha hudhihirisha kwamba usemi huo unarejezea wazee 24 pekee.

      b Ona chati kwenye ukurasa 64.

  • “Ni Nani Ambaye Anastahili Kufungua Hati-Kunjo?”
    Ufunuo—Upeo Wao Mtukufu U Karibu!
    • [Picha ya ukurasa mzima katika ukurasa wa 86]

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki