-
Afrika Kusini2007 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
-
-
Peter Butt, ambaye ameshiriki ujenzi wa Majumba ya Ufalme kwa zaidi ya miaka 18, ni mwenyekiti wa Halmashauri ya Ujenzi ya Mkoa wa Gauteng. Alisema kwamba ndugu walio katika halmashauri hizo wana familia na wanafanya kazi ya kimwili, hata hivyo, wanatenga wakati mwingi kuwasaidia ndugu zao.
Mshiriki mwingine wa halmashauri ya mkoa, Jakob Rautenbach, alieleza kwamba washiriki wa halmashauri hiyo wanafanya kazi kwenye ujenzi muda wote wa mradi huo. Pia wanashiriki kufanya mipango yote kabla ya ujenzi kuanza. Alisimulia kwa uchangamfu jinsi wafanyakazi wa kujitolea wanavyokuwa na furaha na ushirikiano. Wanasafiri mpaka kwenye eneo la ujenzi kwa gharama yao, na nyakati nyingine wanatoka mbali sana.
Jakob alisema kwamba ndugu wengine wengi wanatenga wakati wao na mali yao kusaidia ujenzi wa Majumba ya Ufalme. Kisha akatoa mfano huu: “Dada wawili wa kimwili wenye kampuni ya usafirishaji hupeleka kontena yetu ya vifaa yenye urefu wa meta 13 kwenye maeneo ya ujenzi kotekote nchini na hata katika nchi jirani, nao wamefanya hivyo tangu mwaka wa 1993. Huo ni mchango mkubwa kwelikweli! Baada ya kuona kazi yetu, makampuni mengi tunayoshughulika nayo yanachochewa kutoa michango au kutupunguzia bei.”
-
-
Afrika Kusini2007 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
-
-
Wafanyakazi wa kujitolea wa rangi mbalimbali walienda katika maeneo ya weusi wakiandamana na ndugu wenyeji. Wengine walishambuliwa na umati wenye hasira. Wakati wa ujenzi wa jumba fulani huko Soweto mwaka wa 1993, umati wenye jeuri uliwarushia mawe ndugu watatu wazungu walipokuwa wakipeleka vifaa kwenye eneo la ujenzi wa Jumba la Ufalme. Madirisha yote ya gari lao yalivunjwa, nao wakajeruhiwa. Waliendelea kuendesha gari mpaka kwenye mahali pa ujenzi. Kisha, ndugu wenyeji wakawapeleka haraka hospitali kupitia njia salama.
Kazi ya ujenzi haikusimama. Akina ndugu walifanya kazi wakiwa macho, na mamia ya akina ndugu wa rangi zote walishiriki ujenzi mwishoni mwa juma lililofuata. Mapainia wenyeji walihubiri barabarani karibu na jumba hilo. Walipoona dalili za matata, waliwaonya ndugu waliokuwa wakijenga. Siku chache baadaye, ndugu waliojeruhiwa walikuwa wamepata nafuu vya kutosha kurudia ujenzi.
Makutaniko yanathamini kazi ngumu na kujidhabihu kwa ndugu wanaojitolea kujenga Majumba ya Ufalme. Kwa miaka 15, Fanie na Elaine Smit wamesaidia makutaniko 46 kujenga Majumba ya Ufalme, na mara nyingi wamesafiri mbali sana kwa gharama yao.
Kutaniko moja mkoani KwaZulu-Natal liliandika barua kwa Halmashauri ya Ujenzi ya Mkoa na kusema: “Mlijinyima usingizi, kuwa na familia zenu, kujifurahisha, na mambo mengine mengi ili mje hapa kutujengea jumba. Isitoshe, tunajua kwamba mlitumia pesa zenu nyingi kwa ajili ya kazi hii. Yehova awakumbuke ‘kwa ajili ya wema.’—Nehemia 13:31.”
-