-
Tembea Pamoja na Mungu Nyakati Hizi za MisukosukoMnara wa Mlinzi—2005 | Septemba 1
-
-
Tembea Pamoja na Mungu Nyakati Hizi za Misukosuko
“Enoko akaendelea kutembea pamoja na Mungu wa kweli. Kisha hakuwapo tena, kwa maana Mungu alimchukua.”—MWANZO 5:24.
1. Ni baadhi ya mambo gani katika nyakati zetu yanayofanya maisha yawe magumu sana?
NYAKATI za misukosuko! Maneno hayo hufafanua vema miaka yenye misukosuko na jeuri ambayo wanadamu wameona tangu Ufalme wa Kimasihi ulipozaliwa mwaka wa 1914. Kwa muda huo wote, wanadamu wamekuwa wakiishi katika “siku za mwisho.” Misiba kama vile njaa, magonjwa, matetemeko ya nchi, na vita, imewakumba kwa kiwango kikubwa zaidi. (2 Timotheo 3:1; Ufunuo 6:1-8) Waabudu wa Yehova wamepatwa na misiba hiyo pia. Kwa kadiri fulani, leo sote hukabili matatizo na hali zinazosababisha wasiwasi. Matatizo ya kiuchumi, misukosuko ya kisiasa, uhalifu, na magonjwa ni baadhi ya mambo yanayofanya maisha yawe magumu sana.
2. Watumishi wa Yehova wamekabili matatizo gani?
2 Isitoshe, watumishi wengi wa Yehova wamevumilia mateso mengi makali kwa kuwa Shetani anaendelea kupigana vita na wale “wanaoshika amri za Mungu na walio na kazi ya kutoa ushahidi kumhusu Yesu.” (Ufunuo 12:17) Ijapokuwa sisi sote hatujateswa moja kwa moja, Wakristo wote wa kweli wanahitaji kupambana na Shetani Ibilisi na ile roho anayoeneza miongoni mwa wanadamu. (Waefeso 2:2; 6:12) Tunahitaji kuwa macho kila wakati ili tusiathiriwe na roho hiyo, kwa kuwa tunaikabili kazini, shuleni, na mahali popote ambapo tunakutana na watu wasiopendezwa na ibada safi.
Tembea Pamoja na Mungu, Si na Mataifa
3, 4. Ni kwa njia gani Wakristo ni tofauti na ulimwengu?
3 Katika karne ya kwanza, Wakristo pia walipigana vikali na roho ya ulimwengu huu, na jambo hilo liliwafanya wawe tofauti sana na wale waliokuwa nje ya kutaniko la Kikristo. Paulo alieleza kuhusu tofauti hiyo alipoandika hivi: “Kwa hiyo, nasema hili na kulitolea ushahidi katika Bwana, kwamba msiendelee tena kutembea kama vile mataifa wanavyotembea pia katika ubatili wa akili zao, huku wakiwa katika giza kiakili, na kutenganishwa mbali na uzima ambao ni wa Mungu, kwa sababu ya kule kutojua ambako kumo ndani yao, kwa sababu ya ugumu wa mioyo yao. Wakiisha kuishiwa na ufahamu wote wa maadili, walijitoa wenyewe ili kuwa na mwenendo mpotovu na kufanya ukosefu wa usafi wa kila namna kwa pupa.”—Waefeso 4:17-19.
4 Maneno hayo yanafafanua waziwazi giza zito la kiroho na la kiadili lililopo katika ulimwengu wa leo, sawa na ilivyokuwa katika siku za Paulo! Kama ilivyokuwa katika karne ya kwanza, leo Wakristo ‘hawaendelei kutembea kama vile mataifa wanavyotembea.’ Badala yake, wanafurahia pendeleo la pekee la kutembea pamoja na Mungu. Naam, huenda watu fulani wakatilia shaka ikiwa ni sawa kusema kwamba wanadamu duni wasio wakamilifu wanaweza kutembea pamoja na Yehova. Hata hivyo, Biblia inaonyesha kuwa inawezekana. Isitoshe, Yehova anataka wafanye hivyo. Katika karne ya nane kabla ya Wakati Wetu wa Kawaida, nabii Mika aliandika maneno haya kwa mwongozo wa roho ya Mungu: “Yehova anataka nini kutoka kwako ila kutenda haki na kupenda fadhili na kuwa na kiasi katika kutembea na Mungu wako?”—Mika 6:8.
Tunawezaje Kutembea na Mungu na kwa Nini Tufanye Hivyo?
5. Mwanadamu asiye mkamilifu anawezaje kutembea pamoja na Mungu?
5 Tunawezaje kutembea pamoja na Mungu mwenye nguvu zote ambaye haonekani? Ni wazi kwamba hatuwezi kutembea pamoja naye kama tunavyotembea na wanadamu wenzetu. Katika Biblia, neno “kutembea” linaweza kumaanisha “kufuata mwendo fulani.”a Basi, yule anayetembea pamoja na Mungu anafuata mwendo wa maisha ulioagizwa na Mungu na unaompendeza. Kufuata mwendo huo hutufanya tuwe tofauti na watu wengi. Lakini, huo tu ndio mwendo unaomfaa Mkristo. Kwa nini? Kuna sababu nyingi.
6, 7. Kwa nini kutembea pamoja na Mungu ndiyo njia bora kabisa ya maisha?
6 Kwanza, Yehova ndiye Muumba wetu, Chanzo cha uhai wetu, na Mwandalizi wa vitu vyote tunavyohitaji ili tuendelee kuwa hai. (Ufunuo 4:11) Hivyo, ni yeye tu aliye na haki ya kutuambia jinsi tunavyopaswa kutembea. Zaidi ya hayo, kutembea pamoja na Mungu ndiyo njia ya maisha yenye faida zaidi. Yehova amefanya maandalizi ili wale wanaotembea pamoja naye wapate msamaha wa dhambi na tumaini hakika la uzima wa milele. Pia, Baba yetu mwenye upendo mwingi sana hutoa mashauri yenye hekima yanayowasaidia wale wanaotembea pamoja naye kufanikiwa maishani sasa, licha ya kwamba wao si wakamilifu na wanaishi katika ulimwengu unaotawaliwa na Shetani. (Yohana 3:16; 2 Timotheo 3:15, 16; 1 Yohana 1:8; 2:25; 5:19) Sababu nyingine inayotufanya tutembee pamoja na Mungu ni kwamba utayari wetu wa kufanya hivyo huchangia amani na umoja katika kutaniko.—Wakolosai 3:15, 16.
7 Mwishowe, sababu ya maana zaidi ni kwamba tunapotembea pamoja na Mungu tunaonyesha msimamo wetu kuhusiana na lile suala kuu lililotokezwa katika bustani ya Edeni, yaani, suala la enzi kuu. (Mwanzo 3:1-6) Kupitia maisha yetu, tunaonyesha kwamba tunamuunga Yehova mkono kabisa, na tunatangaza bila woga kwamba ni yeye tu aliye na haki ya kuwa Mwenye Enzi Kuu. (Zaburi 83:18) Hivyo, tunatenda kupatana na sala yetu kwamba jina la Mungu litakaswe na mapenzi yake yatendeke. (Mathayo 6:9, 10) Wale wanaochagua kutembea pamoja na Mungu wana hekima iliyoje! Wanaweza kuwa na uhakika kwamba wanafuata njia inayofaa kwa sababu Yehova ndiye “mwenye hekima peke yake.” Hawezi kamwe kukosea.—Waroma 16:27.
8. Nyakati za Enoko na za Noa zilifananaje na nyakati zetu?
8 Hata hivyo, je, inawezekana kuishi kama Wakristo wakati ambapo kuna misukosuko mingi na watu wengi hawataki kumtumikia Yehova? Tunapata jibu la swali hilo tunapochunguza mifano ya waaminifu wa kale ambao walidumisha utimilifu wao licha ya kuishi nyakati ngumu sana. Wawili kati yao ni Enoko na Noa. Wote waliishi nyakati kama zetu. Uovu ulikuwa umezidi. Katika siku za Noa, dunia ilijaa jeuri na ukosefu wa adili. Hata hivyo, Enoko na Noa walipinga roho ya ulimwengu wa siku zao, nao wakatembea pamoja na Yehova. Waliwezaje kufanya hivyo? Ili tujibu swali hilo, katika makala hii tutachunguza mfano wa Enoko. Katika makala inayofuata tutamkazia fikira Noa.
Enoko Alitembea na Mungu Nyakati za Misukosuko
9. Tuna habari zipi kumhusu Enoko?
9 Enoko ndiye mtu wa kwanza ambaye Maandiko yanamtaja kuwa alitembea pamoja na Mungu. Simulizi la Biblia linasema: “Baada ya kumzaa Methusela, Enoko akaendelea kutembea pamoja na Mungu wa kweli.” (Mwanzo 5:22) Simulizi hilo linaendelea kutaja miaka ambayo Enoko aliishi. Ingawa aliishi kwa muda mrefu kwa kulinganisha na muda ambao watu katika siku zetu huishi, bado ulikuwa mfupi katika siku zake. Kisha simulizi hilo linasema: “Enoko akaendelea kutembea pamoja na Mungu wa kweli. Kisha hakuwapo tena, kwa maana Mungu alimchukua.” (Mwanzo 5:24) Inaonekana kwamba Yehova alimhamisha Enoko kutoka katika nchi ya walio hai hadi katika usingizi wa kifo kabla ya wapinzani kumwangamiza. (Waebrania 11:5, 13) Zaidi ya kutajwa katika mistari hiyo mifupi, Enoko ametajwa katika sehemu nyingine chache za Biblia. Hata hivyo, kutokana na habari tulizo nazo na kwa kutegemea mambo mengine, tunaweza kusema kwamba Enoko aliishi nyakati za misukosuko.
10, 11. (a) Uovu ulieneaje baada ya Adamu na Hawa kuasi? (b) Enoko alihubiri ujumbe gani wa kinabii, na watu waliitikiaje?
10 Kwa mfano, fikiria jinsi ambavyo uovu ulienea haraka katika jamii ya wanadamu baada ya Adamu kutenda dhambi. Biblia inatueleza kwamba mwana mzaliwa wa kwanza wa Adamu, Kaini, ndiye aliyekuwa mwanadamu wa kwanza kuua alipomuua ndugu yake Abeli. (Mwanzo 4:8-10) Baada ya Abeli kuuawa kikatili, Adamu na Hawa walipata mwana mwingine, nao wakamwita Sethi. Tunasoma hivi kumhusu: “Sethi akazaa mwana pia naye akamwita jina lake Enoshi. Wakati huo watu wakaanza kuliitia jina la Yehova.” (Mwanzo 4:25, 26) Inasikitisha kwamba huko “kuliitia jina la Yehova” kulifanywa kwa njia ya kumwasi Yehova.b Miaka mingi baada ya Enoshi kuzaliwa, mzao fulani wa Kaini aliyeitwa Lameki alitunga wimbo kwa ajili ya wake zake wawili na kutangaza kwamba alikuwa amemuua kijana aliyemtia jeraha. Kisha Lameki akaonya hivi: “Ikiwa Kaini atalipizwa kisasi mara 7, basi Lameki ni mara 77.”—Mwanzo 4:10, 19, 23, 24.
11 Maelezo hayo mafupi yanaonyesha kwamba uasi ulioanzishwa na Shetani katika bustani ya Edeni ulisababisha uovu uenee haraka kati ya wazao wa Adamu. Enoko alikuwa nabii wa Yehova katika ulimwengu huo, na maneno yake yenye nguvu yaliyoongozwa kwa roho ya Mungu yanahusu nyakati zetu pia. Yuda aliandika unabii huu wa Enoko: “Tazama! Yehova alikuja pamoja na watakatifu wake makumi ya maelfu, ili kufanya hukumu juu ya wote, na kuwathibitisha kuwa ni wenye hatia wote wasiomwogopa Mungu kuhusu matendo yao yote ya kutomwogopa Mungu ambayo walitenda kwa njia ya kutomwogopa Mungu, na kuhusu mambo yote ya kushtua ambayo watenda-dhambi wasiomwogopa Mungu walisema juu yake.” (Yuda 14, 15) Maneno hayo yatatimia kwa ukamili wakati wa Har–Magedoni. (Ufunuo 16:14, 16) Hata hivyo, tuna uhakika kwamba hata katika siku za Enoko, “watenda-dhambi [wengi] wasiomwogopa Mungu” waliudhika waliposikia unabii wa Enoko. Yehova alionyesha upendo ulioje kwa kumhamisha Enoko ili wasimuumize!
Ni Nini Kilichomwimarisha Enoko Kutembea na Mungu?
12. Ni nini kilichofanya Enoko awe tofauti na watu wa nyakati zake?
12 Katika bustani ya Edeni, Adamu na Hawa walimsikiliza Shetani, naye Adamu akamwasi Yehova. (Mwanzo 3:1-6) Mwana wao Abeli hakutenda kama wao, naye Yehova akamtazama kwa kibali. (Mwanzo 4:3, 4) Kwa kusikitisha, wazao wengi wa Adamu hawakuwa kama Abeli. Hata hivyo, Enoko, aliyezaliwa mamia ya miaka baadaye, alikuwa kama Abeli. Kulikuwa na tofauti gani kati ya Enoko na wazao wengi wa Adamu? Mtume Paulo alijibu swali hilo alipoandika hivi: “Kwa imani Enoko alihamishwa ili asione kifo, naye hakupatikana popote kwa sababu Mungu alikuwa amemhamisha; kwa maana kabla ya kuhamishwa kwake alikuwa ametolewa ushahidi kwamba amempendeza Mungu vema.” (Waebrania 11:5) Enoko alikuwa sehemu ya ‘wingu kubwa la mashahidi’ wa kabla ya Ukristo ambao walikuwa mifano bora ya imani. (Waebrania 12:1) Imani ndiyo iliyomwezesha Enoko kuendelea kufanya yaliyo sawa katika maisha yake ya zaidi ya miaka 300. Hiyo ni zaidi ya mara tatu ya muda ambao wanadamu wengi leo huishi!
13. Enoko alikuwa na imani ya aina gani?
13 Paulo alieleza kuhusu imani ya Enoko na ya mashahidi wengine alipoandika hivi: “Imani ni tarajio lililohakikishwa la mambo yanayotumainiwa, uthibitisho ulio wazi wa mambo halisi ingawa hayaonekani.” (Waebrania 11:1) Naam, imani ni tarajio hakika, linalotegemea uhakikisho wa kwamba mambo tunayoyatumaini yatatimia. Imani inahusisha tarajio lenye nguvu sana ambalo linabadili maoni yetu kuhusu mambo yaliyo muhimu zaidi maishani mwetu. Imani ya aina hiyo ndiyo iliyomwezesha Enoko kutembea pamoja na Mungu hata ingawa watu wa nyakati zake hawakufanya hivyo.
14. Imani ya Enoko ilitegemea ujuzi gani sahihi?
14 Imani ya kweli inategemea ujuzi sahihi. Enoko alijua mambo gani? (Waroma 10:14, 17; 1 Timotheo 2:4) Bila shaka, alijua mambo yaliyotukia Edeni. Huenda pia alikuwa amesikia jinsi maisha yalivyokuwa katika bustani ya Edeni, ambayo huenda bado ilikuwapo wakati huo, ingawa wanadamu walizuiwa wasiingie ndani. (Mwanzo 3:23, 24) Na alijua kusudi la Mungu kwamba wazao wa Adamu wataijaza dunia na kuifanya iwe kama Paradiso hiyo ya kwanza. (Mwanzo 1:28) Isitoshe, Enoko alithamini kabisa ahadi ya Yehova ya kutokeza Uzao ambao ungeponda kichwa cha Shetani na kukomesha matokeo mabaya ya uwongo wa Shetani. (Mwanzo 3:15) Naam, unabii wa Enoko ulioongozwa kwa roho ya Mungu na kuhifadhiwa katika kitabu cha Yuda, unahusu kuharibiwa kwa uzao wa Shetani. Kwa kuwa Enoko alikuwa na imani, tunajua kwamba alimwabudu Yehova huku akiamini kwamba “yeye huwa mthawabishaji wa wale wanaomtafuta kwa bidii.” (Waebrania 11:6) Hivyo, ingawa Enoko hakujua mambo yote tunayoyajua, ujuzi aliokuwa nao ulitosha kuwa msingi wa imani thabiti. Imani hiyo ilimwezesha kudumisha utimilifu wake nyakati za misukosuko.
Iga Mfano wa Enoko
15, 16. Tunawezaje kuiga mfano wa Enoko?
15 Kwa kuwa, kama Enoko, tunataka kumpendeza Yehova katika nyakati hizi za misukosuko, inafaa tumwige. Tunahitaji kupata na kuendelea kuwa na ujuzi sahihi kumhusu Yehova na kusudi lake. Lakini mengi zaidi yanahitajika. Tunahitaji kukubali ujuzi huo sahihi uongoze maisha yetu. (Zaburi 119:101; 2 Petro 1:19) Tunahitaji kuongozwa na maoni ya Mungu, na kujitahidi sikuzote kumpendeza katika mambo yote tunayofikiria na kutenda.
16 Hatujui ni nani wengine waliomtumikia Yehova nyakati za Enoko, lakini huenda alikuwa peke yake au kulikuwa na wengine wachache. Sisi pia ni wachache ulimwenguni, lakini hilo halituvunji moyo. Yehova atatutegemeza hata nani awe dhidi yetu. (Waroma 8:31) Enoko alionya kwa ujasiri kuhusu uharibifu wa watu wasiomwogopa Mungu uliokuwa ukikaribia. Sisi pia huhubiri kwa ujasiri kuhusu “hii habari njema ya ufalme” licha ya dhihaka, upinzani, na mateso. (Mathayo 24:14) Enoko hakuishi kwa muda mrefu kama watu wengi wa siku zake. Lakini hakuweka tumaini lake katika ulimwengu huo. Alikazia fikira jambo kubwa zaidi. (Waebrania 11:10, 35) Sisi pia tunakazia fikira kutimizwa kwa kusudi la Yehova. Hivyo, hatutumii ulimwengu huu kwa ukamili. (1 Wakorintho 7:31) Badala yake, tunatumia nguvu na mali zetu hasa kumtumikia Yehova.
17. Tunajua mambo gani ambayo Enoko hakujua, nasi tunapaswa kufanya nini?
17 Enoko aliamini kwamba Uzao ulioahidiwa na Mungu ungetokea kwa wakati wa Yehova unaofaa. Sasa karibu miaka 2,000 imepita tangu Uzao huo, Yesu Kristo, kutokea, kuandaa fidia, na kutufungulia njia ili sisi pamoja na mashahidi wengine waaminifu wa zamani kama Enoko tuweze kurithi uzima wa milele. Uzao huo, ambao umetawazwa kuwa Mfalme wa Ufalme wa Mungu, ulimporomosha Shetani kutoka mbinguni hadi duniani, nasi tunaona dhiki inayosababishwa na jambo hilo. (Ufunuo 12:12) Ndiyo, tunajua mambo mengi sana kuliko Enoko. Basi, acheni tuwe na imani thabiti kama yeye. Acheni maisha yetu yote yaongozwe na uhakika wa kwamba ahadi za Mungu zitatimia. Naam, kama Enoko, acheni tutembee pamoja na Mungu japo tunaishi nyakati za misukosuko.
[Maelezo ya Chini]
a Ona Buku la 1 la kitabu Insight on the Scriptures, ukurasa wa 220, fungu la 6 (au Étude Perspicace Des Écritures, ukurasa wa 228, fungu la 4 katika Kifaransa), kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.
b Kabla ya siku za Enoshi, Yehova alizungumza na Adamu. Abeli alimtolea Yehova toleo lililokubalika. Pia, kabla Kaini hajachochewa kuua kwa sababu ya hasira yenye wivu, Mungu alizungumza naye. Hivyo, yaonekana watu walianza “kuliitia jina la Yehova” kwa njia mpya, si katika ibada safi.
-
-
Tutatembea Katika Jina la Yehova Mungu WetuMnara wa Mlinzi—2005 | Septemba 1
-
-
Tutatembea Katika Jina la Yehova Mungu Wetu
“Sisi tutatembea katika jina la Yehova Mungu wetu mpaka wakati usio na kipimo, naam, milele.”—MIKA 4:5.
1. Hali ya maadili ilikuwaje katika siku za Noa, na Noa alikuwa tofauti kwa njia gani?
ENOKO ndiye mtu wa kwanza anayetajwa katika Biblia kuwa alitembea pamoja na Mungu. Wa pili alikuwa Noa. Simulizi linasema: “Noa alikuwa mtu mwadilifu. Alionekana kuwa mtu asiye na kosa kati ya watu wa siku zake. Noa alitembea pamoja na Mungu wa kweli.” (Mwanzo 6:9) Kufikia wakati wa Noa, wanadamu kwa ujumla walikuwa wameiacha ibada safi. Hali hiyo mbaya ilizidishwa na malaika wasio waaminifu waliokuwa na mahusiano yasiyo ya asili pamoja na wanawake, nao wakazaa watoto walioitwa Wanefili, yaani, “watu wenye nguvu” au “wanaume wenye sifa” wa siku hizo. Haishangazi kwamba dunia ilijaa jeuri! (Mwanzo 6:2, 4, 11) Hata hivyo, Noa hakuonekana na kosa, naye alikuwa “mhubiri wa uadilifu.” (2 Petro 2:5) Mungu alipomwamuru ajenge safina ili kuokoa uhai, Noa alitii naye “akafanya kulingana na yote ambayo Mungu alikuwa amemwamuru. Alifanya vivyo hivyo.” (Mwanzo 6:22) Ndiyo, Noa alitembea pamoja na Mungu.
2, 3. Noa alituwekea mfano gani bora?
2 Paulo alimtia Noa katika orodha yake ya mashahidi waaminifu alipoandika hivi: “Kwa imani Noa, baada ya kupewa onyo la kimungu la mambo ambayo yalikuwa bado hayajaonekana, alionyesha woga wa kimungu na kujenga safina kwa ajili ya kuiokoa nyumba yake; na kupitia imani hiyo aliuhukumu ulimwengu kuwa wenye hatia, naye akawa mrithi wa uadilifu unaolingana na imani.” (Waebrania 11:7) Huo ni mfano bora kama nini! Akiwa na uhakika wa kwamba maneno ya Yehova yatatimia, Noa alitumia wakati, nguvu, na mali ili kutimiza amri za Mungu. Vivyo hivyo, wengi leo hukataa kutumia nafasi wanazopata katika ulimwengu huu na badala yake wanatumia wakati wao, nguvu zao, na mali zao ili kutii amri za Yehova. Imani yao inaonekana wazi, nayo itawawezesha wao na wengine pia wapate wokovu.—Luka 16:9; 1 Timotheo 4:16.
3 Inaonekana ilikuwa vigumu kwa Noa na familia yake kuwa na imani, sawa na ilivyokuwa kwa Enoko, babu ya baba ya Noa, ambaye alizungumziwa katika makala iliyotangulia. Kama vile ilivyokuwa katika siku za Enoko, katika siku za Noa pia waabudu wa kweli walikuwa wachache. Ni watu wanane tu waliokuwa waaminifu na waliookoka Gharika. Noa alihubiri uadilifu katika ulimwengu wenye jeuri na ukosefu wa adili. Isitoshe, yeye na familia yake walikuwa wakijenga safina kubwa ya mbao ili kujitayarisha kwa ajili ya gharika ya ulimwenguni pote, ingawa hakuna mtu aliyewahi kuona gharika kama hiyo. Haikosi kwamba watu waliowatazama walishangaa sana.
4. Yesu alikazia kosa gani la watu walioishi siku za Noa?
4 Inafaa kutambua kwamba Yesu alipozungumzia siku za Noa, yeye hakuongea kuhusu jeuri, dini ya uwongo au ukosefu wa adili, ingawa hayo ni mambo mabaya sana. Kosa ambalo Yesu alikazia ni kwamba watu walikataa kutii onyo lililotolewa. Alisema kwamba watu walikuwa “wakila na kunywa, wanaume wakioa na wanawake wakiolewa, mpaka siku ambayo Noa aliingia ndani ya safina.” Je, kulikuwa na ubaya wowote kula, kunywa, kuoa, au kuolewa? Watu hao walikuwa wakiishi maisha ya “kawaida” tu! Lakini gharika ilikuwa karibu kutokea, na Noa alihubiri uadilifu. Maneno yake na mwenendo wake ulipaswa kuwa onyo kwao. Lakini “hawakujali mpaka gharika ikaja na kuwafagilia mbali wote.”—Mathayo 24:38, 39.
5. Noa na familia yake walihitaji sifa zipi?
5 Tunapofikiria nyakati hizo, tunatambua kwamba Noa alifuata njia ya hekima. Hata hivyo, kabla ya Gharika, ujasiri ulihitajiwa ili kuwa tofauti na wengine. Noa na familia yake walihitaji kuwa na usadikisho wenye nguvu ili wajenge safina kubwa na kuijaza wanyama wa kila aina. Je, kuna wakati ambapo watu hao wachache waaminifu walihisi kwamba ni afadhali waishi maisha ya “kawaida” tu na kuepuka kuvuta fikira za watu? Hata ikiwa walifikiri hivyo nyakati nyingine, waliendelea kuwa watimilifu. Baada ya miaka mingi sana—muda mrefu kuliko muda ambao sisi tutavumilia katika mfumo huu wa mambo—imani ya Noa ilimwezesha kuokoka Gharika. Hata hivyo, Yehova aliwahukumu wote walioishi maisha ya “kawaida” na ambao hawakutilia maanani umuhimu wa nyakati walizoishi.
Wanadamu Wakabili Jeuri Tena
6. Hali ilikuwaje baada ya Gharika?
6 Maji ya Gharika yalipopungua, wanadamu walianza maisha mapya. Lakini bado hawakuwa wakamilifu na “mwelekeo wa moyo wa mwanadamu” uliendelea kuwa “mbaya tangu ujana wake na kuendelea.” (Mwanzo 8:21) Isitoshe, ingawa roho waovu hawangejibadilisha na kuvaa tena miili ya wanadamu, bado walikuwa watendaji sana. Baada ya muda mfupi tu, ulimwengu wa wanadamu wasiomwogopa Mungu ulionyesha kwamba ulikuwa “unakaa katika nguvu za yule mwovu,” na kama ilivyo leo, waabudu wa kweli walihitaji kupambana na “hila za Ibilisi.”—1 Yohana 5:19; Waefeso 6:11, 12.
7. Jeuri iliongezekaje duniani baada ya Gharika?
7 Baada ya Gharika, angalau kuanzia wakati wa Nimrodi, wanadamu walianza tena kutenda kwa jeuri. Kwa sababu ya ongezeko la idadi ya watu na maendeleo ya teknolojia, jeuri imeongezeka kadiri ambavyo miaka imepita. Zamani, kulikuwa na upanga, mkuki, upinde, mshale, na magari ya vita yaliyokokotwa na farasi. Baadaye, kukawa na bunduki, mizinga, na silaha nyingine za hali ya juu zilizotengenezwa mwanzoni mwa karne ya 20. Wakati wa Vita vya Kwanza vya Ulimwengu silaha mpya zenye kuogopesha zilitumiwa, kama vile ndege, vifaru, nyambizi, na gesi za sumu. Katika vita hivyo, silaha hizo ziliua mamilioni ya watu. Je, hilo lilitarajiwa? Ndiyo.
8. Andiko la Ufunuo 6:1-4 limetimizwaje?
8 Katika mwaka wa 1914, Yesu alitawazwa kuwa Mfalme wa Ufalme wa Mungu huko mbinguni, na “siku ya Bwana” ikaanza. (Ufunuo 1:10) Katika maono yaliyoandikwa katika kitabu cha Ufunuo, Yesu anaonekana akiwa Mfalme anayeendesha farasi mweupe kwa ushindi. Wapanda-farasi wengine wanamfuata, na kila mmoja wao anawakilisha pigo fulani linalowakumba wanadamu. Mmoja wao anamwendesha farasi mwenye rangi ya moto, naye amepewa ruhusa ya ‘kuondoa amani duniani ili wauane; naye amepewa upanga mkubwa.’ (Ufunuo 6:1-4) Farasi huyo na mpandaji wake wanafananisha vita, na ule upanga mkubwa unafananisha uharibifu mkubwa sana unaosababishwa na vita vya sasa na silaha kali zinazotumiwa. Leo, silaha hizo zinatia ndani silaha za nyuklia, kila moja ikiwa na uwezo wa kuua makumi ya maelfu ya watu; roketi zinazoweza kusafirisha silaha hizo hadi maeneo ya mbali sana; na pia silaha kali za maangamizi makubwa za kemikali na kibiolojia.
Tunatii Maonyo ya Yehova
9. Ulimwengu wa leo unafananaje na ule wa kabla ya Gharika?
9 Katika siku za Noa, Yehova aliwaangamiza wanadamu kwa sababu ya jeuri nyingi sana ya watu waovu iliyochochewa na Wanefili. Namna gani leo? Je, sasa jeuri imepungua duniani kuliko ilivyokuwa wakati huo? Sivyo hata kidogo! Isitoshe, kama ilivyokuwa katika siku za Noa, leo watu wanaendelea kufanya shughuli zao huku wakijaribu kuishi maisha ya “kawaida,” na kukataa kutii maonyo yanayotolewa. (Luka 17:26, 27) Basi, je, kuna sababu yoyote ya kutilia shaka kwamba Yehova atawaangamiza tena wanadamu? Hakuna.
10. (a) Ni onyo gani ambalo linatolewa mara nyingi katika unabii wa Biblia? (b) Ni ipi iliyo njia bora tu tunayoweza kuifuata leo?
10 Mamia ya miaka kabla ya Gharika, Enoko alitabiri kuhusu uharibifu ambao ungetokea katika siku zetu. (Yuda 14, 15) Yesu pia alizungumza kuhusu “dhiki kuu” inayokaribia. (Mathayo 24:21) Manabii wengine walionya kuhusu wakati huo. (Ezekieli 38:18-23; Danieli 12:1; Yoeli 2:31, 32) Na katika kitabu cha Ufunuo, tunasoma maelezo yaliyo wazi kuhusu uharibifu huo wa mwisho. (Ufunuo 19:11-21) Tukiwa mtu mmoja-mmoja tunamwiga Noa na kuwa wahubiri wa uadilifu wenye bidii. Sisi hutii maonyo ya Yehova na kuwasaidia wanadamu wenzetu kwa upendo wafanye hivyo. Hivyo, kama Noa, tunatembea pamoja na Mungu. Naam, ni muhimu wote wale wanaopenda uhai waendelee kutembea pamoja na Mungu. Tunawezaje kufanya hivyo licha ya matatizo tunayokabili kila siku? Tunahitaji kusitawisha imani yenye nguvu kwamba kusudi la Mungu litatimia.—Waebrania 11:6.
Endelea Kutembea Pamoja na Mungu Nyakati za Misukosuko
11. Sisi huwaigaje Wakristo wa karne ya kwanza?
11 Katika karne ya kwanza, Wakristo watiwa-mafuta waliitwa watu wa “Ile Njia.” (Matendo 9:2) Maisha yao yote yalitegemea imani katika Yehova na Yesu Kristo. Walitembea katika njia ambayo Bwana wao alitembea. Leo, Wakristo waaminifu hufanya vivyo hivyo.
12. Ni nini kilichotukia baada ya Yesu kufanya muujiza wa kuulisha umati?
12 Umuhimu wa imani unaonekana katika jambo lililotukia wakati wa huduma ya Yesu. Pindi moja, Yesu alifanya muujiza wa kuulisha umati wa wanaume 5,000 hivi. Watu walishangaa na kufurahi. Lakini ona jambo lililofuata. Tunasoma hivi: “Watu hao walipoona ishara alizofanya, wakaanza kusema: ‘Kwa hakika huyu ndiye nabii aliyepaswa kuja ulimwenguni.’ Kwa hiyo Yesu, akijua walikuwa karibu kuja kumkamata wamfanye kuwa mfalme, akaondoka tena kwenda mlimani akiwa peke yake.” (Yohana 6:10-15) Usiku huo alisafiri akaenda mahali pengine. Inaonekana watu wengi walikata tamaa Yesu alipokataa kuwa mfalme. Alikuwa ameonyesha kwamba ana hekima ya kutosha kuwa mfalme na kwamba ana uwezo wa kutosheleza mahitaji ya kimwili ya watu. Lakini wakati wa Yehova wa kumweka awe Mfalme haukuwa umefika. Zaidi ya hayo, Ufalme wa Yesu ungekuwa mbinguni, si duniani.
13, 14. Watu wengi walikuwa na mtazamo gani, na imani yao ilijaribiwaje?
13 Hata hivyo, kama Yohana anavyosema, watu hao walijitahidi juu chini kumfuata Yesu wakampata “ng’ambo ya bahari.” Kwa nini walimfuata baada ya yeye kukataa jitihada zao za kumfanya awe mfalme? Wengi walikuwa na mtazamo wa kimwili, huku wakitaja waziwazi kuhusu chakula ambacho Yehova aliandaa nyikani katika siku za Musa. Ni kana kwamba walimtaka Yesu aendelee kuwapa chakula. Akitambua nia yao mbaya, Yesu alianza kuwafundisha kweli za kiroho ambazo zingeweza kubadili mawazo yao. (Yohana 6:17, 24, 25, 30, 31, 35-40) Kwa sababu hiyo, wengine walianza kumnung’unikia, hasa alipotoa mfano huu: “Kwa kweli kabisa ninawaambia, Ninyi msipoula mwili wa Mwana wa binadamu na kunywa damu yake, hamna uzima ndani yenu wenyewe. Yule ambaye hula mwili wangu na kunywa damu yangu ana uzima wa milele, nami nitamfufua katika siku ya mwisho.”—Yohana 6:53, 54.
14 Mara nyingi mifano ya Yesu iliwachochea watu kuonyesha ikiwa kweli walitamani kutembea pamoja na Mungu. Mfano huu ulitimiza kusudi hilohilo. Ulichochea hisia kali. Tunasoma hivi: “Wengi kati ya wanafunzi wake, waliposikia hilo, wakasema: ‘Maneno hayo yanashtua; ni nani ambaye anaweza kuyasikiliza?’” Kisha Yesu akawaeleza kwamba wanapaswa kuelewa maneno yake kwa njia ya kiroho. Alisema: “Roho ndiyo inayotokeza uzima; mwili hauna faida hata kidogo. Maneno ambayo nimewaambia ni roho na ni uzima.” Lakini wengi hawakutaka kusikiliza. Simulizi hilo linasema: “Kwa sababu ya hili wengi kati ya wanafunzi wake wakaenda zao kwenye mambo yaliyo nyuma wakawa hawatembei tena pamoja naye.”—Yohana 6:60, 63, 66.
15. Baadhi ya wafuasi wa Yesu walikuwa na mtazamo gani unaofaa?
15 Hata hivyo, baadhi ya wanafunzi wa Yesu walitenda kwa njia tofauti. Ni kweli kwamba wanafunzi hao washikamanifu hawakuelewa kwa ukamili yale ambayo Yesu alisema. Hata hivyo, waliendelea kumwamini kwa uthabiti. Petro, mmoja wa wanafunzi hao washikamanifu, alionyesha maoni ya wanafunzi wote waliobaki, aliposema: “Bwana, tutaenda kwa nani? Wewe una maneno ya uzima wa milele.” (Yohana 6:68) Huo ni mtazamo mzuri sana, mfano bora kwelikweli!
16. Tunaweza kujaribiwaje, na tunapaswa kusitawisha mtazamo gani unaofaa?
16 Leo, sisi pia tunaweza kujaribiwa kama wanafunzi hao wa mapema. Huenda tukakata tamaa kwa sababu ahadi za Yehova hazitimizwi haraka kama tulivyotarajia. Huenda tukaona kwamba ufafanuzi wa Maandiko katika vichapo vyetu vinavyotegemea Biblia ni mgumu kueleweka. Huenda tukavunjwa moyo na mwenendo wa Mkristo mwenzetu. Je, itakuwa sawa kuacha kutembea pamoja na Mungu kwa sababu hizo au nyingine kama hizo? Sivyo! Wanafunzi waliomwacha Yesu walikuwa na maoni ya kimwili. Tunapaswa kuepuka kutenda kama wao.
“Sisi Si Namna ya Watu Wanaorudi Nyuma”
17. Tunaweza kusaidiwaje kuendelea kutembea pamoja na Mungu?
17 Mtume Paulo aliandika hivi: “Andiko lote limeongozwa na roho ya Mungu.” (2 Timotheo 3:16) Kupitia Biblia, Yehova anatuambia hivi waziwazi: “Hii ndiyo njia. Tembeeni ndani yake.” (Isaya 30:21) Kutii Neno la Mungu hutusaidia ‘kuendelea kuangalia sana jinsi tunavyotembea.’ (Waefeso 5:15) Kujifunza Biblia na kutafakari yale tunayojifunza hutuwezesha ‘kuendelea kutembea katika kweli.’ (3 Yohana 3) Naam, kama Yesu alivyosema, “roho ndiyo inayotokeza uzima; mwili hauna faida hata kidogo.” Mwongozo pekee unaotegemeka tunaoweza kufuata ili kuelekeza hatua zetu ni mwongozo wa kiroho, ambao hupatikana kupitia Neno la Yehova, roho yake, na tengenezo lake.
18. (a) Wengine hufanya nini kwa kukosa hekima? (b) Sisi husitawisha imani ya aina gani?
18 Leo, wale wanaoudhika kwa sababu ya maoni ya kimwili au matarajio yasiyotimizwa mara nyingi huanza kujishughulisha sana na mambo ya ulimwengu huu. Kwa kutotambua umuhimu wa nyakati tunazoishi, hawaoni uhitaji wa ‘kuendelea kukesha,’ nao huchagua kufuatia mambo ya ubinafsi badala ya kutanguliza faida za Ufalme. (Mathayo 24:42) Kutembea katika njia hiyo ni kukosa hekima. Ona maneno haya ya mtume Paulo: “Sisi si namna ya watu wanaorudi nyuma kwenye maangamizi, bali sisi ni namna ya watu walio na imani ya kuihifadhi hai nafsi.” (Waebrania 10:39) Kama Enoko na Noa, sisi pia tunaishi nyakati za misukosuko, lakini kama wao, tuna pendeleo la kutembea pamoja na Mungu. Tukifanya hivyo, tuna tarajio lililohakikishwa kwamba tutaona ahadi za Yehova zikitimizwa, uovu ukikomeshwa, na ulimwengu mpya wenye uadilifu ukija. Hilo ni tarajio zuri kama nini!
19. Mika anaelezaje njia ya waabudu wa kweli?
19 Kwa mwongozo wa roho ya Mungu, nabii Mika alisema kwamba mataifa ya ulimwengu ‘yatatembea kila moja katika jina la mungu wake.’ Kisha akasema hivi kujihusu yeye mwenyewe na waabudu wengine waaminifu: “Sisi tutatembea katika jina la Yehova Mungu wetu mpaka wakati usio na kipimo, naam, milele.” (Mika 4:5) Ikiwa azimio lako ni kama la Mika, dumisha uhusiano wa karibu pamoja na Yehova hata nyakati za misukosuko ziwe mbaya namna gani. (Yakobo 4:8) Acheni kila mmoja wetu atamani kutoka moyoni mwake kutembea pamoja na Yehova Mungu wetu sasa na mpaka wakati usio na kipimo, naam, milele!
-