-
Je, Utafuata Mwongozo wa Yehova Wenye Upendo?Mnara wa Mlinzi—2011 | Julai 15
-
-
Je, Utafuata Mwongozo wa Yehova Wenye Upendo?
“Nimechukia kila njia ya uwongo.”—ZAB. 119:128.
1, 2. (a) Unapotafuta mwongozo wa kukusaidia kufika mahali fulani, ungefurahi kupata maonyo ya aina gani, na kwa nini? (b) Yehova anawapatia maonyo ya aina gani wale wanaomtumikia, na kwa nini?
WAZIA hali hii: Unahitaji kusafiri kwenda mahali fulani. Ili kupata mwongozo, unazungumza na rafiki unayemwamini ambaye anajua njia vizuri. Anapokupatia mwongozo, anaweza kusema hivi: “Uwe mwangalifu kwa sababu ya kona iliyo hapo mbele. Ishara ya barabarani inadanganya watu. Watu wengi ambao wanafuata ishara hiyo wanapotea njia.” Je, ungethamini msaada wake na kutii onyo? Kwa njia fulani, Yehova ni kama rafiki huyo. Anatupatia mwongozo mzuri sana kuhusu jinsi ya kupata uzima wa milele, lakini pia anatuonya kuhusu hatari ambazo zinaweza kutuelekeza kwenye njia mbaya.—Kum. 5:32; Isa. 30:21.
2 Katika habari hii na habari inayofuata, tutazungumzia hatari fulani ambazo Rafiki yetu, Yehova Mungu, anatuonya kuzihusu. Tunapaswa kukumbuka sikuzote kwamba Yehova anatupatia maonyo hayo kwa sababu anatujali na anatupenda. Anataka tufike mahali tunapoelekea. Anaumia moyoni watu wanapofuata njia iliyo hatari na kupotea. (Eze. 33:11) Katika habari hii, tutazungumzia hatari tatu. Hatari ya kwanza inatoka nje, ya pili iko ndani yetu. Hatari ya tatu inasababishwa na kitu ambacho si halisi; hata hivyo, ni mbaya sana. Tunahitaji kujua hatari hizo na jinsi Baba yetu wa mbinguni anavyotufundisha kuziepuka. Mtunga-zaburi mmoja aliyeongozwa na roho takatifu alimwambia Yehova hivi: “Nimechukia kila njia ya uwongo.” (Zab. 119:128) Je, unahisi vivyo hivyo? Acheni tuone jinsi tunavyoweza kuazimia kuchukia “kila njia ya uwongo.”
“Usiufuate Umati”
3. (a) Kwa nini inaweza kuwa hatari kufuata wasafiri wengine tunapokuwa na shaka kuhusu njia tunayopaswa kufuata? (b) Ni kanuni gani ya maana ambayo tunapata katika Kutoka 23:2?
3 Ikiwa ungekuwa unasafiri kwenda mbali, ungefanya nini ikiwa ungekuwa na shaka kuhusu njia unayopaswa kufuata? Huenda ungeshawishiwa kufuata wasafiri wengine, hasa ikiwa ungeona wengi wao wakifanya uamuzi uleule. Ni hatari kufanya hivyo. Kwa kweli, huenda wasafiri hao hawaendi mahali unapoenda, au huenda wao pia wamepotea njia. Kuhusiana na jambo hilo, fikiria kanuni ambayo iliongoza sheria fulani ambayo Waisraeli wa kale walipewa. Wale waliotumika wakiwa waamuzi au mashahidi katika mambo ya kihukumu walionywa kuhusu hatari ya ‘kufuata umati.’ (Soma Kutoka 23:2.) Bila shaka, ni rahisi sana kwa wanadamu wasio wakamilifu kufuata umati, na kupotosha haki. Hata hivyo, je, kanuni kuhusu kutofuata umati inahusu tu mambo ya kihukumu? Hapana.
4, 5. Yoshua na Kalebu walipata mkazo gani wa kufuata umati, lakini ni nini kilichowawezesha kuushinda?
4 Ni kweli kwamba wakati wowote tunaweza kupata mkazo wa ‘kufuata umati.’ Mkazo huo unaweza kutokea kwa ghafula, na inaweza kuwa vigumu sana kuushinda. Kwa mfano, fikiria jinsi Yoshua na Kalebu walivyopata mkazo kutoka kwa Waisraeli wenzao. Walikuwa kati ya wanaume 12 ambao walienda kupeleleza ile Nchi ya Ahadi. Waliporudi, kumi kati ya wanaume hao walileta habari mbaya na yenye kuvunja moyo. Hata walidai kwamba wakaaji fulani wa nchi hiyo walikuwa majitu ambayo yalitokana na Wanefili, wazao wa malaika waasi na wanawake. (Mwa. 6:4) Kwa kweli, dai hilo lilikuwa la uwongo. Wazao hao waovu walikuwa wameangamizwa katika Gharika karne nyingi mapema, na hawakuacha mzao hata mmoja. Lakini hata madai yasiyo na msingi yanaweza kuwashawishi sana wale walio na imani dhaifu. Habari hiyo mbaya kutoka kwa wale wapelelezi kumi ilieneza kwa haraka woga na wasiwasi kati ya watu. Baada ya muda mfupi, wengi wao walikuwa na hakika kwamba lingekuwa kosa kuingia katika ile Nchi ya Ahadi kama walivyokuwa wameagizwa na Yehova. Yoshua na Kalebu walifanya nini katika hali hiyo ngumu?—Hes. 13:25-33.
5 Yoshua na Kalebu hawakufuata umati. Ingawa umati huo wa Waisraeli haukutaka kusikia, wanaume hao wawili walisema ukweli na wakashikamana nao, hata walipotishwa kwamba wangepigwa mawe mpaka kufa! Walipata wapi ujasiri huo? Bila shaka, walipata ujasiri mwingi kutokana na imani yao. Watu wenye imani wanaona waziwazi tofauti kati ya ahadi takatifu za Yehova Mungu na madai ya watu yasiyo na msingi. Baadaye, wanaume hao wawili walieleza namna walivyohisi kuhusu jinsi Yehova alivyotimiza kila moja ya ahadi zake wakati uliopita. (Soma Yoshua 14:6, 8; 23:2, 14.) Yoshua na Kalebu walishikamana na Mungu wao mwaminifu, na hawangeweza hata kuwazia kumuumiza moyoni kwa kufuata umati usio na imani. Kwa hiyo, walisimama imara, na wakatuwekea mfano mzuri sana leo.—Hes. 14:1-10.
6. Ni katika mambo gani tunaweza kusukumwa kufuata umati?
6 Je, nyakati nyingine unasukumwa kufuata umati? Bila shaka, watu ambao wametengwa mbali na Yehova na ambao wanadharau viwango vyake vya maadili ni wengi sana leo. Mara nyingi umati huo unaeneza mawazo yasiyo na msingi kuhusu vitumbuizo na tafrija. Huenda wakasisitiza kwamba hakuna madhara yoyote kutazama upotovu wa maadili, jeuri, na mazoea ya kupashana habari na roho waovu, mambo ambayo yameenea sana katika programu za televisheni, sinema, na katika michezo ya video. (2 Tim. 3:1-5) Unapochagua vitumbuizo kwa ajili yako na familia yako, je, unaruhusu dhamiri dhaifu za watu wengine ziongoze dhamiri yako na kukuchochea kufanya maamuzi? Ikiwa hivyo ndivyo unavyofanya maamuzi, basi unafuata umati.
7, 8. (a) ‘Nguvu zetu za ufahamu’ zinazoezwa jinsi gani, na kwa nini mazoezi hayo ni ya maana kuliko kufuata orodha ya sheria kali? (b) Kwa nini unatiwa moyo na mfano wa vijana wengi Wakristo?
7 Yehova ametupatia zawadi yenye thamani ili kutusaidia kufanya maamuzi, yaani, ‘nguvu zetu za ufahamu.’ Hata hivyo, nguvu hizo zinahitaji kuzoezwa ‘kwa kutumiwa.’ (Ebr. 5:14) Kuufuata umati hakuwezi kuzoeza nguvu zetu za ufahamu wala sheria kali za mambo yanayohusu dhamiri. Hiyo ndiyo sababu watu wa Yehova hawapewi orodha ya sinema, vitabu, na vituo vya Intaneti ambavyo wanapaswa kuepuka. Kwa kuwa ulimwengu huu unabadilika haraka sana, orodha kama hiyo ingehitaji kubadilishwa kila wakati. (1 Kor. 7:31) Lakini jambo baya zaidi ni kwamba orodha kama hiyo ingetuzuia kufanya kazi ya maana zaidi ya kuchunguza kwa makini kanuni za Biblia na kusali na kisha kufanya maamuzi kwa msingi wa kanuni hizo.—Efe. 5:10.
8 Bila shaka, nyakati nyingine huenda maamuzi yetu yanayotegemea Biblia yasiwapendeze watu wengi. Vijana Wakristo wanaweza kusukumwa sana na wanafunzi wenzao shuleni ili waone na kufanya mambo ambayo kila mtu anaona na kufanya. (1 Pet. 4:4) Kwa hiyo, inapendeza kuona Wakristo vijana na waliozeeka wakiiga imani ya Yoshua na Kalebu kwa kukataa kuufuata umati.
Msifuate “Mioyo Yenu na Macho Yenu”
9. (a) Kwa nini inaweza kuwa hatari kufuata maoni na hisia zetu tunapokuwa katika safari? (b) Kwa nini sheria iliyo katika Hesabu 15:37-39 ilikuwa na faida kwa watu wa kale wa Mungu?
9 Hatari ya pili ambayo tutazungumzia iko ndani yetu. Tunaweza kuilinganisha na mfano huu: Kama ungekuwa safarini kuelekea mahali fulani, je, unaweza kuamua kutupa ramani ya njia na kufuata hisia zako, labda kwa kufuata njia yoyote ambayo inaonekana kuwa na maeneo yenye kupendeza? Bila shaka, huwezi kufika mahali unapoenda ukifuata maoni kama hayo. Kuhusiana na jambo hilo, fikiria sheria nyingine ambayo Yehova aliwapa Waisraeli wa kale. Inaweza kuwa vigumu kwa watu wengi leo kuelewa sheria ambayo inawataka watu kuweka pindo na nyuzi za bluu kwenye mavazi yao. (Soma Hesabu 15:37-39.) Hata hivyo, je, unaona faida ya kufanya hivyo? Kutii sheria kama hiyo kuliwasaidia watu wa Mungu kuwa tofauti na kujitenga na mataifa ya kipagani yaliyowazunguka. Walipaswa kufanya hivyo ili waendelee kukubaliwa na Yehova. (Law. 18:24, 25) Hata hivyo, sheria hiyo inafunua hatari nyingine iliyo ndani yetu ambayo inaweza kutukengeusha tusipate uzima wa milele. Jinsi gani?
10. Yehova ameonyesha jinsi gani kwamba anaelewa utu wa mwanadamu?
10 Ona jinsi Yehova alivyoeleza sababu ya kuwapa watu wake sheria hiyo: “Wala hamtaifuata mioyo yenu na macho yenu, ambayo mnayafuata katika uasherati.” Yehova anaelewa vizuri sana utu wa mwanadamu. Anajua jinsi ilivyo rahisi sana kwa moyo wetu, au mtu wetu wa ndani, kudanganywa na mambo tunayotazama kwa macho yetu. Hivyo, Biblia inatuonya hivi: “Moyo ni wenye hila kuliko kitu kingine chochote nao ni hatari. Ni nani anayeweza kuujua?” (Yer. 17:9) Hivyo basi, je, unaona jinsi onyo la Yehova kwa Waisraeli lilivyokuwa lenye kufaa? Alijua vizuri kwamba wangekuwa na mwelekeo wa kuangalia wapagani waliowazunguka na kushawishiwa kufanya mambo waliyoona. Huenda wangeshawishiwa kuwa kama watu hao wasio waamini na kisha kufikiri, kuhisi, na kutenda kama wao.—Met. 13:20.
11. Tunaweza kushawishiwa kwa njia gani na hisia zetu za kimwili?
11 Leo, ni rahisi hata zaidi kwa moyo wetu wenye hila kuongozwa vibaya na hisia zetu za kimwili. Tunaishi katika ulimwengu ambao unachochea watu wafuate tamaa za kimwili. Kwa hiyo, tunaweza kutumia jinsi gani kanuni iliyo katika Hesabu 15:39? Fikiria jambo hili: Ikiwa watu wanaokuzunguka shuleni, kazini, au katika ujirani wenu wanavalia kwa njia yenye kuvutia kingono, je, unaweza kushawishiwa kuvalia hivyo? Je, unaweza kushawishiwa ‘kufuata moyo na macho yako’ na kuchochewa kufanya mambo unayoona? Na je, unaweza kushawishiwa kulegeza viwango vyako mwenyewe na kuvalia kwa njia kama hiyo?—Rom. 12:1, 2.
12, 13. (a) Tunapaswa kufanya nini ikiwa macho yetu yanatanga-tanga na kutazama mambo yasiyofaa? (b) Ni nini kinachoweza kutuchochea kuepuka kuwa chanzo cha kuwashawishi wengine?
12 Tunahitaji kusitawisha kwa haraka sifa ya kujizuia. Ikiwa macho yetu yanatanga-tanga na kutazama mambo yasiyofaa, acheni tukumbuke azimio la Ayubu aliyekuwa mwaminifu, ambaye alifanya agano na macho yake, alikuwa ameazimia kabisa kutomtazama kimapenzi mwanamke ambaye si mke wake. (Ayu. 31:1) Vivyo hivyo, Mfalme Daudi aliazimia hivi: “Sitaweka mbele ya macho yangu kitu chochote kisichofaa.” (Zab. 101:3) Kitu chochote ambacho kinaweza kuchafua dhamiri zetu safi na kuharibu uhusiano wetu pamoja na Yehova ni ‘kitu kisichofaa.’ Kitu kisichofaa kinaweza kuwa kishawishi chochote ambacho kinavutia macho yetu na kujaribu kushawishi moyo wetu ufanye dhambi.
13 Kwa upande mwingine, bila shaka, hatungependa kuwa ‘kitu kisichofaa’ kwa wengine kwa kujaribu kuwashawishi kufanya mambo yasiyofaa. Kwa hiyo, tunachukua kwa uzito shauri la Biblia lililoongozwa na roho ya Mungu kuhusu kuvalia mavazi yenye mpangilio mzuri na yenye kiasi. (1 Tim. 2:9) Kuvalia mavazi yenye kiasi hakumaanishi kuvalia jinsi tunavyopenda. Tunahitaji kujali dhamiri na hisia za watu wanaotuzunguka, na kufikiria kwanza amani yao ya akili na hali yao nzuri badala ya mapendezi yetu wenyewe. (Rom. 15:1, 2) Kutaniko la Kikristo limebarikiwa kwa kuwa na maelfu ya vijana ambao wanaweka mfano mzuri katika jambo hilo. Tunafurahi tunapoona kwamba wanakataa ‘kufuata mioyo yao na macho yao,’ na badala yake wanaamua kumpendeza Yehova katika kila jambo wanalofanya, hata katika njia wanayovalia!
Usifuate “Vitu Visivyo vya Kweli”
14. Samweli alitangaza onyo gani kuhusu kufuatia “vitu visivyo vya kweli”?
14 Wazia kwamba ukiwa safarini unapita katika jangwa kubwa, na kwa mbali unaona kitu kinachofanana na maji, lakini si maji. Ni nini kingetokea ikiwa ungeacha barabara ili kwenda kuona kitu hicho kinachoonekana kama maji? Unaweza kupoteza uhai wako ukifuata kitu hicho ambacho si cha kweli! Yehova anajua vizuri hatari hiyo. Fikiria mfano fulani. Waisraeli walitaka kuwa kama mataifa yaliyowazunguka, ambayo yalitawaliwa na wafalme wa kibinadamu. Kwa kweli, tamaa hiyo ilikuwa dhambi kubwa kwa sababu ilikuwa sawa na kumkataa Yehova kuwa Mfalme wao. Ingawa Yehova aliwaruhusu kuwa na mfalme wa kibinadamu, alimwongoza nabii wake Samweli kutangaza onyo kuhusu kufuata “vitu visivyo vya kweli.”—Soma 1 Samweli 12:21.
15. Waisraeli walifuata jinsi gani vitu visivyo vya kweli?
15 Je, watu hao walifikiria kwamba kwa njia fulani mfalme wa kibinadamu angekuwa halisi zaidi, mwenye kutegemeka zaidi, kuliko Yehova? Ikiwa ndivyo, kwa kweli walikuwa wakifuatia vitu visivyo vya kweli! Na walikuwa katika hatari ya kufuatia vitu vingine vingi vya kishetani visivyo vya kweli. Wafalme wa kibinadamu wangewaongoza kwa urahisi kuabudu sanamu. Watu wanaoabudu sanamu wanakosea kwa kufikiria kwamba vitu vinavyoonekana, yaani, miungu iliyotengenezwa kwa mbao au mawe, kwa njia fulani ni halisi zaidi, ni yenye kutegemeka zaidi kuliko Yehova, Mungu asiyeonekana ambaye aliumba vitu vyote. Lakini kama mtume Paulo alivyosema, sanamu “si kitu.” (1 Kor. 8:4) Haziwezi kuona, kusikia, kuzungumza, au kutenda. Unaweza kuziona na kuzigusa, lakini ikiwa ungeabudu sanamu, kwa kweli ungekuwa ukifuatia kitu kisicho cha kweli, jambo lisilo halisi ambalo lingeleta msiba tu.—Zab. 115:4-8.
16. (a) Shetani anawashawishi jinsi gani watu wengi wafuatie vitu visivyo vya kweli? (b) Kwa nini tunaweza kusema kwamba vitu vya kimwili ni vitu visivyo vya kweli, hasa vikilinganishwa na Yehova Mungu?
16 Bado Shetani ni fundi katika kuwasadikisha watu wafuatie vitu ambavyo si vya kweli. Kwa mfano, amewashawishi watu wengi sana wafuatie vitu vya kimwili ili kupata usalama. Inaweza kuonekana kwamba pesa, mali, na kazi zenye mishahara mikubwa zinaleta faida. Hata hivyo, vitu vya kimwili vina faida gani wakati afya ya mtu inapodhoofika, wakati mfumo wa kiuchumi unapoporomoka, au wakati msiba wa kiasili unapotokea? Vitu vya kimwili vina faida gani watu wanapoona kwamba hawafai chochote, wanapokosa kusudi, mwongozo, na majibu ya maswali au maulizo ya maana zaidi maishani? Vinaweza kuwa na faida gani mtu anapokaribia kufa? Tukitazamia kwamba vitu vya kimwili vitatimiza uhitaji wetu wa kiroho, tutavunjika moyo. Vitu vya kimwili haviwezi kuleta furaha wala kuondoa matatizo yote; ni vitu visivyo vya kweli. Mwishowe, haviwezi kuleta usalama wa kimwili, kwa kuwa haviwezi kuongeza urefu wa maisha ya mwanadamu, au kuondoa magonjwa na kifo. (Met. 23:4, 5) Lakini Mungu wetu Yehova ni halisi kabisa! Tunaweza tu kupata usalama wa kweli tukiwa na uhusiano wa karibu zaidi pamoja naye. Hiyo ni baraka yenye thamani kama nini! Na tusimwache kamwe kwa kufuatia vitu visivyo vya kweli.
17. Umeazimia kufanya nini kuhusiana na hatari ambazo tumezungumzia?
17 Je, si ni kweli kwamba tumebarikiwa kwa sababu Yehova ni Rafiki yetu na Kiongozi wetu katika safari ya kupata uzima? Tukiendelea kutii maonyo yake kuhusu hatari tatu, yaani, umati, mioyo yetu, na vitu visivyo vya kweli, inaelekea kwamba tutafanikiwa kufika mwisho wa safari yetu, yaani, kupata uzima wa milele. Katika habari inayofuata tutazungumzia maonyo mengine matatu ambayo Yehova anatupatia ili kutusaidia kuchukia na kuepuka njia za uwongo ambazo zinawapoteza watu wengi sana.—Zab. 119:128.
-
-
Je, Utatii Maonyo Yaliyo Wazi Kutoka Kwa Yehova?Mnara wa Mlinzi—2011 | Julai 15
-
-
Je, Utatii Maonyo Yaliyo Wazi Kutoka Kwa Yehova?
“Hii ndiyo njia. Tembeeni ndani yake.”—ISA. 30:21.
1, 2. Shetani ameazimia kufanya nini, na Neno la Mungu linatusaidia jinsi gani?
ISHARA ya barabarani ambayo inaelekeza upande usiofaa inapotosha na pia inaweza kusababisha hatari. Wazia kwamba rafiki anakuonya kuwa mtu fulani mwovu amebadili kimakusudi ishara ya barabarani kwa sababu anataka kuwaumiza wasafiri ambao hawajui njia. Bila shaka, utatii onyo la rafiki yako.
2 Kwa kweli, Shetani ni adui mwovu ambaye ameazimia kutudanganya. (Ufu. 12:9) Shetani ndiye anayesababisha hatari zote ambazo tumezungumzia katika habari iliyotangulia na hatari hizo zinakusudiwa kutufanya tuache barabara inayoongoza kwenye uzima wa milele. (Mt. 7:13, 14) Tunashukuru kwamba Mungu wetu mwenye upendo anatuonya ili tusifuate ‘ishara za barabarani’ zenye kupotosha ambazo Shetani anatumia ili kutudanganya. Acheni sasa tuzungumzie hatari nyingine tatu ambazo Shetani anatumia ili kutudanganya. Tunapochunguza jinsi Neno la Mungu linavyotusaidia kuepuka kudanganywa, tunaweza kuwazia Yehova akitembea nyuma yetu na kutuelekeza upande unaofaa, akisema hivi: “Hii ndiyo njia. Tembeeni ndani yake.” (Isa. 30:21) Kutafakari kuhusu maonyo yaliyo wazi ya Yehova kutatusaidia kuazimia zaidi kuyatii.
Usiwafuate “Walimu wa Uwongo”
3, 4. (a) Kwa nini walimu wa uwongo ni kama visima ambavyo vimekauka? (b) Walimu wengi wa uwongo wanatoka wapi, na wanataka nini?
3 Wazia kwamba unasafiri katika jangwa. Kwa mbali, unaona kisima, na unaenda kwenye kisima hicho kwa sababu unafikiri kwamba utapata maji ya kumaliza kiu chako. Lakini unapofika kwenye kisima hicho, unaona kwamba kimekauka. Unavunjika moyo kama nini! Walimu wa uwongo ni kama visima ambavyo vimekauka. Mtu yeyote ambaye anaenda kutafuta maji ya kweli kutoka kwao atavunjika moyo kabisa. Kupitia mtume Paulo na Petro, Yehova anatuonya kuhusu walimu wa uwongo. (Soma Matendo 20:29, 30; 2 Petro 2:1-3.) Walimu hao wa uwongo ni nani? Maneno ya mitume hao wawili yaliyoongozwa na roho ya Mungu yanatusaidia kutambua walimu wa uwongo wanatoka wapi na jinsi wanavyowadanganya watu.
4 Paulo aliwaambia hivi wazee wa kutaniko la Efeso: “Kutoka katikati yenu ninyi wenyewe watu watasimama na kusema mambo yaliyopotoka.” Naye Petro alisema hivi katika barua ambayo aliwaandikia Wakristo wenzake: ‘Kutakuwa na walimu wa uwongo katikati yenu.’ Kwa hiyo, walimu wa uwongo wanatoka wapi? Wanaweza kutoka ndani ya kutaniko. Walimu hao wa uwongo ni waasi-imani.a Wanataka nini? Hawatosheki tu kuacha tengenezo ambalo huenda mwanzoni walilipenda. Paulo alieleza kwamba kusudi lao ni “kuwavuta wanafunzi wawafuate wao wenyewe.” Wanafunzi ambao Paulo anazungumzia ni wanafunzi wa Yesu Kristo. Badala ya kwenda kutafuta wanafunzi wao wenyewe, waasi-imani wanajaribu kuchukua au kuiba wanafunzi wa Kristo. Yesu alisema kwamba walimu wa uwongo ni kama “mbwa-mwitu wenye kunyafua” ambao wanatafuta kuwameza washiriki wa kutaniko wanaowafuata na hivyo kuharibu imani yao na kuwafanya waache kweli.—Mt. 7:15; 2 Tim. 2:18.
5. Walimu wa uwongo wanatumia njia gani mbalimbali?
5 Walimu wa uwongo wanawadanganya watu jinsi gani? Njia wanazotumia zinaonyesha kwamba ni wajanja sana. Waasi-imani ‘wanaingiza kimya-kimya’ mawazo yenye kupotosha ndani ya kutaniko. Kama watu wanaofanya biashara ya magendo, wanaingiza kisiri-siri maoni ya uasi-imani kwa njia ya ujanja. Na kama vile mhalifu mjanja anavyojaribu kufanya vyeti vya uwongo vionekane kuwa ni vya kweli, ndivyo waasi-imani wanavyotumia “maneno yasiyo ya kweli,” au mawazo ya uwongo, kujaribu kufanya maoni yao ya uwongo yaonekane kuwa ya kweli. Wanaeneza ‘mafundisho ya udanganyifu,’ ‘wakiyapotosha Maandiko’ ili yalingane na mawazo yao wenyewe. (2 Pet. 2:1, 3, 13; 3:16) Ni wazi kwamba waasi-imani hawatujali hata kidogo. Tukiwafuata, tutaacha tu barabara inayoongoza kwenye uzima wa milele.
6. Biblia inatupatia onyo gani lililo wazi kuhusu walimu wa uwongo?
6 Tunaweza kujilinda wenyewe jinsi gani kutokana na walimu wa uwongo? Biblia inatupatia mashauri yaliyo wazi kuhusu jinsi ya kushughulika nao. (Soma Waroma 16:17; 2 Yohana 9-11.) Neno la Mungu linasema hivi: “Mjiepushe nao.” Hilo linamaanisha kwamba tunapaswa kukaa mbali nao! Shauri hilo ambalo liliongozwa na roho ya Mungu liko wazi kabisa. Tuseme kwamba daktari anakuambia uepuke kumkaribia mtu ambaye ana ugonjwa hatari wenye kuambukiza. Utaelewa kile ambacho daktari huyo anamaanisha, na utatii kabisa onyo lake. Kwa kweli, waasi-imani ni ‘wagonjwa kiakili,’ na wanajaribu kuwaambukiza wengine mafundisho yao ya uwongo. (1 Tim. 6:3, 4) Yehova, ambaye ndiye Daktari Mkuu, anatuambia tuwaepuke kabisa waasi-imani. Tunajua hilo linamaanisha nini, lakini je, tumeazimia kutii onyo lake katika kila njia?
7, 8. (a) Ni lazima tufanye nini ili tuwaepuke walimu wa uwongo? (b) Kwa nini umeazimia kuwaepuka kabisa walimu wa uwongo?
7 Ni lazima tufanye nini ili tuwaepuke walimu wa uwongo? Hatuwasalimu au kuwakaribisha katika nyumba zetu. Pia, tunakataa kusoma vitabu vyao, kutazama vipindi vyao kwenye televisheni, kuchunguza vituo vyao katika Intaneti, au kutoa maoni yetu kuhusu habari ambazo wanaandika katika Intaneti. Kwa nini tumeazimia kabisa kuwaepuka? Kwa sababu tunampenda “Mungu wa ukweli.” Kwa hiyo, hatutaki kusikiliza mafundisho yaliyopotoshwa ambayo yanapingana na Neno lake la kweli. (Zab. 31:5; Yoh. 17:17) Pia, tunapenda tengenezo la Yehova, ambalo ametumia kutufundisha kweli zenye kusisimua, kama vile jina la Yehova na maana yake, kusudi la Mungu kwa ajili ya dunia, hali ya wafu, na tumaini la ufufuo. Je, unakumbuka jinsi ulivyofurahi sana ulipojifunza kwa mara ya kwanza kweli hizo na kweli nyingine zenye thamani? Basi, kwa nini ukubali kudanganywa na mtu yeyote ambaye anadharau tengenezo ambalo lilikufundisha kweli hizo?—Yoh. 6:66-69.
8 Hata walimu wa uwongo waseme nini, hatutawafuata! Kwa nini twende kwenye visima hivyo ambavyo vimekauka ili kudanganywa tu na kukatishwa tamaa? Badala yake, acheni tuazimie kubaki washikamanifu kwa Yehova na kwa tengenezo lake ambalo kwa muda mrefu limekuwa likitupatia maji safi yenye kuburudisha ya kweli kutoka katika Neno la Mungu lililoongozwa na roho yake ambayo yanamaliza kiu chetu.—Isa. 55:1-3; Mt. 24:45-47.
Usifuate “Hadithi za Uwongo”
9, 10. Paulo alimpa Timotheo onyo gani kuhusu “hadithi za uwongo,” na huenda Paulo alikuwa akifikiria nini? (Ona pia maelezo ya chini.)
9 Nyakati fulani, si rahisi kutambua kwamba ishara ya barabarani imebadilishwa na inaelekeza upande usiofaa. Nyakati nyingine, inaweza kuwa vigumu kutambua uwongo. Ndivyo ilivyo na uwongo wa Shetani; tusipokuwa waangalifu, anaweza kutudanganya kwa urahisi na mambo fulani ya uwongo. Mtume Paulo anatuonya kuhusu moja ya njia au mbinu za werevu za Shetani, “hadithi za uwongo.” (Soma 1 Timotheo 1:3, 4.) Ili tusipotoshwe kutoka kwenye barabara inayoongoza kwenye uzima, tunahitaji kujua hadithi za uwongo ni nini, na jinsi tunavyoweza kuepuka kuzisikiliza.
10 Onyo la Paulo kuhusu hadithi za uwongo liko katika barua yake ya kwanza kwa Timotheo, mwangalizi Mkristo ambaye alipewa daraka la kulinda usafi wa kutaniko na kuwasaidia waamini wenzake kubaki waaminifu. (1 Tim. 1:18, 19) Paulo anatumia neno la Kigiriki ambalo linamaanisha hadithi ya kutungwa, au uwongo. Kitabu kimoja (The International Standard Bible Encyclopaedia) kinasema kwamba neno hilo linahusu “hadithi (ya kidini) ambayo haina uhusiano wowote na mambo halisi.” Labda Paulo alikuwa akifikiria kuhusu uwongo wa kidini ambao ulienezwa na hadithi za zamani zenye kusisimua ambazo watu walitunga au kuwazia tu.b Hadithi kama hizo ‘zinatokeza tu maswali ya utafiti,’ yaani, zinatokeza maswali au maulizo ambayo yanawafanya watu wafanye utafiti usio na maana yoyote. Hadithi za uwongo zinatumiwa na Shetani, yule mwongo mkubwa, ambaye anatumia uwongo wa kidini na hadithi ambazo hazimpendezi Mungu ili kuwapotosha watu wasiojua. Shauri la Paulo liko wazi: Usisikilize hadithi za uwongo!
11. Shetani ametumia jinsi gani dini ya uwongo kwa werevu ili kuwadanganya watu, na tunapaswa kutii onyo gani ili tusidanganywe?
11 Ni hadithi gani za uwongo ambazo zinaweza kutudanganya tusipokuwa waangalifu? Tunaweza kusema kwamba “hadithi za uwongo” ni fundisho lolote la kidini au hadithi ya kutungwa ya kidini ambayo inaweza kugeuza masikio yetu “kutoka kwenye kweli.” (2 Tim. 4:3, 4) Shetani, ambaye anajifanya kuwa “malaika wa nuru,” amekuwa akitumia kwa werevu dini ya uwongo ili kuwadanganya watu. (2 Kor. 11:14) Dini zinazodai kuwa za Kikristo zinasema kwamba zinamfuata Kristo, lakini zinafundisha mafundisho ya uwongo ambayo yanategemea hadithi za uwongo, kama vile Utatu, moto wa mateso, na kutokufa kwa nafsi. Dini hizo pia zinaendeleza sikukuu kama vile Krismasi na Ista, ambazo zinaonekana kuwa desturi nzuri lakini kwa kweli zinatokana na upagani na hadithi za kutungwa. Hatutadanganywa na hadithi za uwongo ikiwa tutatii onyo la Mungu la kujitenga na ‘kuacha kugusa kitu kilicho najisi.’—2 Kor. 6:14-17.
12, 13. (a) Shetani ameeneza uwongo gani mbalimbali, na ukweli ni nini kuhusu kila moja ya uwongo huo? (b) Ni lazima tufanye nini ikiwa hatutaki kudanganywa na hadithi za uwongo za Shetani?
12 Shetani ameeneza uwongo mwingine mwingi ambao unaweza kutupotosha tusipokuwa waangalifu. Fikiria mifano mitatu. Uwongo wa kwanza ni huu: Unaweza kufanya jambo lolote unalotaka; amua mwenyewe mambo yanayofaa na yale yasiyofaa. Mara nyingi tunasikia hivyo katika televisheni, sinema, vitabu, magazeti, na katika Intaneti. Kwa kuwa tunasikia uwongo huo kila wakati, ni rahisi kwetu kuanza kufikiri kwa njia hiyo na kufuata mawazo ya ulimwengu yaliyopotoka kimaadili. Lakini ukweli ni kwamba tunahitaji sana mwongozo kutoka kwa Mungu kuhusu mambo yanayofaa na yale yasiyofaa. (Yer. 10:23) Uwongo wa pili ni huu: Mungu hatabadili kamwe jambo lolote duniani. Tukianza kufuata maoni hayo ya kuishi tu kwa ajili ya leo tunaweza kuwa “wasiotenda au wasiozaa matunda” katika utumishi wetu kwa Mungu. (2 Pet. 1:8) Ukweli ni kwamba siku ya Yehova inakaribia haraka, na ni lazima tuendelee kuitazamia. (Mt. 24:44) Uwongo wa tatu ni huu: Mungu hakujali wewe binafsi. Tukiamini uwongo huo wa Shetani tunaweza kukata tamaa, na kuhisi kwamba hatustahili kamwe kupendwa na Mungu. Ukweli ni kwamba Yehova anampenda na kumthamini kila mtu anayemwabudu.—Mt. 10:29-31.
13 Ni lazima sikuzote tujilinde kwa sababu mawazo na mitazamo ya ulimwengu wa Shetani inaweza kuonekana kwa nje kuwa inafaa. Hata hivyo, kumbuka kwamba Shetani ni hodari katika kudanganya. Tunaweza kuepuka kudanganywa na ‘hadithi za uwongo za Shetani zilizotungwa kwa ufundi [“hadithi zilizotungwa kwa werevu,” The New American Bible],’ kwa kutii tu mashauri na vikumbusho vya Neno la Mungu.—2 Pet. 1:16.
‘Usimfuate Shetani’
14. Paulo aliwapa wajane fulani vijana onyo gani, na kwa nini sisi sote tunahitaji kutii maneno yake?
14 Wazia kwamba kuna ishara ya barabarani inayosema, “Njia Hii Inaongoza kwa Shetani.” Ni nani kati yetu anayeweza kufuata ishara hiyo? Hata hivyo, Paulo anatuonya kuhusu njia mbalimbali ambazo Wakristo waliojiweka wakfu wanaweza ‘kugeuzwa kando na kumfuata Shetani.’ (Soma 1 Timotheo 5:11-15.) Paulo aliwaandikia maneno hayo ‘wajane fulani vijana,’ lakini kanuni ambazo anataja zinatuhusu sisi sote. Huenda Wakristo hao wanawake katika karne ya kwanza hawakufikiri kwamba walikuwa wakimfuata Shetani, lakini matendo yao yalionyesha kwamba kwa kweli walikuwa wakimfuata. Tunaweza jinsi gani kuepuka kumfuata Shetani bila kujua? Acheni tuchunguze onyo la Paulo kuhusu porojo zenye kuumiza.
15. Shetani anataka nini, na Paulo anafunua jinsi gani mbinu au njia za Shetani?
15 Shetani anataka kutunyamazisha ili tusizungumze kuhusu imani yetu. Anataka tuache kuhubiri habari njema. (Ufu. 12:17) Hivyo, anajaribu kutushawishi tufuatie mambo ambayo yanapoteza wakati au kusababisha migawanyiko kati yetu. Ona jinsi Paulo anavyofunua mbinu au njia za Shetani. Paulo alisema kwamba wale wajane wa siku zake ‘hawakuwa na kazi, na walizunguka-zunguka nyumba kwa nyumba.’ Wajane hao walitumia wakati wao mwingi kuwatembelea marafiki wao na kuzungumza kuhusu mambo ambayo hayakuwa na maana. Tunahitaji kuwa waangalifu ili tusifanye hivyo. Kwa mfano, tunaweza kutumia wakati wetu mwingi na wa watu wengine tukisoma na kutuma barua-pepe (e-mail) kuhusu mambo ambayo si ya maana na hata huenda si ya kweli. Paulo alisema pia kwamba wajane hao walikuwa “wenye kupiga porojo.” Porojo zenye kuumiza zinaweza kugeuka na kuwa uchongezi, yaani, kusema uwongo kuhusu watu wengine. Mara nyingi uwongo huo unasababisha ugomvi. (Met. 26:20) Iwe wanajua au hawajui, wale ambao wanaeneza uwongo wenye kuumiza kuhusu wengine wanamwiga Shetani Ibilisi.c Kisha, Paulo alisema kwamba wajane hao ‘walijiingiza katika mambo ya watu wengine.’ Hatuna haki ya kuwaambia wengine jinsi ya kufanya mambo yao ya kibinafsi. Tabia hiyo isiyofaa na inayosababisha matatizo inaweza kutukengeusha kuacha kazi ambayo tumepewa na Mungu ya kuhubiri kuhusu Ufalme. Tukiacha kufanya kazi ya Yehova kwa bidii, basi tunaanza kumfuata Shetani. Ni lazima kila mmoja wetu achague upande ambao ataunga mkono.—Mt. 12:30.
16. Tunaweza kuepuka ‘kugeuzwa kando kumfuata Shetani’ tukitii shauri gani?
16 Kutii mashauri ya Biblia kunaweza kutusaidia kuepuka ‘kugeuzwa kando na kumfuata Shetani.’ Fikiria mashauri fulani yenye hekima ambayo Paulo alitoa. Alisema kwamba tunapaswa kuwa “na mengi ya kufanya katika kazi ya Bwana.” (1 Kor. 15:58) Kuwa na mengi ya kufanya katika kazi ya Ufalme kutatulinda tuepuke hatari za kufanya mambo ambayo si ya maana na ambayo yanatupotezea wakati. (Mt. 6:33) Paulo anatuambia pia tuzungumze mambo ‘mema kwa ajili ya kujenga.’ (Efe. 4:29) Azimia kutosikiliza na kutoeneza porojo zenye kuumiza.d Jifunze kuwaamini na kuwaheshimu ndugu na dada zako. Tukifanya hivyo, sikuzote tutasema maneno yenye kujenga badala ya kubomoa. ‘Uwe na shabaha ya kukazia akili mambo yako mwenyewe.’ (1 The. 4:11) Waonyeshe watu kwamba unawajali, lakini fanya hivyo kwa heshima. Kumbuka kwamba huenda kukawa na mambo ya kibinafsi ambayo hawataki kuzungumzia na ambayo hawataki wengine wajue. Pia, kumbuka kwamba hatupaswi kuwalazimisha wengine wafuate maoni yetu katika maamuzi yao ya kibinafsi.—Gal. 6:5.
17. (a) Kwa nini Yehova anatuonya kuhusu mambo ambayo hatupaswi kufuata? (b) Umeazimia kufanya nini kuhusu njia ambayo Yehova anataka tufuate?
17 Tunamshukuru sana Yehova kwa sababu anatuambia waziwazi mambo ambayo hatupaswi kufuata! Hata hivyo, usisahau kamwe kwamba Yehova anatupatia maonyo ambayo tumezungumzia katika habari hii na ile iliyotangulia kwa sababu anatupenda sana. Anataka tuepuke maumivu na taabu ambayo inawapata wale ambao wanafuata ‘ishara za barabarani’ za Shetani ambazo zinapotosha. Huenda njia ambayo Yehova anataka tufuate ina nafasi ndogo, lakini inaongoza mahali bora kabisa, kwenye uzima wa milele. (Mt. 7:14) Ni lazima sikuzote tuazimie kutii shauri hili la Yehova: “Hii ndiyo njia. Tembeeni ndani yake.”—Isa. 30:21.
[Maelezo ya Chini]
a “Uasi-imani” ni hali ya kujitenga na ibada ya kweli, kuanguka, kuasi, na kuacha ibada hiyo.
b Kwa mfano, kitabu cha Tobiti, au Tobia, ambacho kiliandikwa katika karne ya tatu hivi K.W.K. na ambacho kilikuwapo katika siku za Paulo, kimejaa ushirikina na hadithi za ajabu za uchawi ambazo zinaonyeshwa kana kwamba ni za kweli.—Ona Insight on the Scriptures, Buku la 1, ukurasa wa 122 au Étude perspicace des Écritures, Buku la 1, ukurasa wa 135.
c Neno la Kigiriki ambalo limetafsiriwa kuwa “ibilisi” (di·aʹbo·los), linamaanisha “mchongezi.” Neno hilo linatumiwa kama jina lingine la cheo la Shetani, ambaye ni mchongezi mkuu kuliko wote.—Yoh. 8:44; Ufu. 12:9, 10.
-