-
Jinsi Baraza Linaloongoza Linavyotofautiana na Shirika la KisheriaMnara wa Mlinzi—2001 | Januari 15
-
-
MIKUTANO ya kila mwaka ya shirika la Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania imekuwa ikifanywa tangu Januari mwaka wa 1885. Kukusanywa kwa Wakristo watiwa-mafuta kulipokuwa kunaendelea mwishoni mwa karne ya 19, waelekezi na wasimamizi wa shirika hilo walikuwa na tumaini la kimbingu. Kusema kweli, mambo yamekuwa hivyo karibu sikuzote.
Lakini kuna wakati ambapo mambo yalikuwa tofauti. Mwaka 1940, Hayden C. Covington—ambaye wakati huo alikuwa wakili wa Sosaiti na mmoja wa “kondoo wengine,” mwenye tumaini la kidunia—alichaguliwa kuwa mwelekezi wa Sosaiti. (Yohana 10:16) Alitumikia akiwa makamu-msimamizi wa Sosaiti kuanzia 1942 hadi 1945. Wakati huo, Ndugu Covington alijiuzulu kazi ya uelekezi ili kutimiza yale ambayo wakati huo yalionekana kuwa mapenzi ya Yehova—kwamba waelekezi na wasimamizi wote wa shirika la Pennsylvania wawe Wakristo watiwa-mafuta. Lyman A. Swingle alichukua mahali pa Hayden C. Covington kwenye baraza la waelekezi, naye Frederick W. Franz akachaguliwa kuwa makamu-msimamizi.
Kwa nini watumishi wa Yehova waliamini kwamba waelekezi na wasimamizi wote wa shirika la Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania walipasa kuwa Wakristo watiwa-mafuta? Kwa sababu wakati huo, baraza la waelekezi na wasimamizi wa shirika la Pennsylvania lilihusiana kwa ukaribu na Baraza Linaloongoza la Mashahidi wa Yehova, ambalo sikuzote limefanyizwa na wanaume watiwa-mafuta pekee.
-
-
Jinsi Baraza Linaloongoza Linavyotofautiana na Shirika la KisheriaMnara wa Mlinzi—2001 | Januari 15
-
-
Hata hivyo, baada ya mkutano huo muhimu wa kila mwaka uliofanywa mwaka wa 1944, swali muhimu lilibaki. Kwa kuwa wakati huo Baraza Linaloongoza lilihusiana kwa ukaribu na shirika la Pennsylvania lenye baraza la waelekezi saba, je, hilo lilimaanisha kwamba Baraza Linaloongoza halingeweza kamwe kufanyizwa na Wakristo watiwa-mafuta zaidi ya saba? Isitoshe, kwa kuwa waelekezi hao wanachaguliwa na washiriki wa shirika hilo, je, washiriki hao walikuwa wakichagua washiriki wa Baraza Linaloongoza kwenye mikutano hiyo kila mwaka? Je, waelekezi na wasimamizi wa shirika la Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania na washiriki wa Baraza Linaloongoza ni kitu kimoja au kuna tofauti?
Mkutano Mwingine wa Kila Mwaka Usioweza Kusahaulika
Maswali hayo yalijibiwa kwenye mkutano wa kila mwaka uliofanywa Oktoba 1, 1971. Pindi hiyo, mmoja wa wasemaji alitaja kwamba baraza linaloongoza la “mtumwa mwaminifu na mwenye busara” lilitangulia shirika la Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania kwa mamia ya miaka. (Mathayo 24:45-47) Baraza linaloongoza lilianzishwa siku ya Pentekoste mwaka wa 33 W.K., zaidi ya karne 18 kabla ya shirika la Pennsylvania kuanzishwa. Mwanzoni, baraza linaloongoza lilikuwa na mitume 12 wala si wanaume 7. Ni dhahiri kwamba idadi yake iliongezeka baadaye, kwa kuwa “mitume na wanaume wazee katika Yerusalemu” walikuwa wanaongoza.—Matendo 15:2.
Mwaka wa 1971, msemaji huyohuyo alieleza kwamba washiriki wa shirika la Watch Tower Society hawangeweza kuwachagua washiriki waliotiwa-mafuta wa Baraza Linaloongoza. Kwa nini? “Kwa sababu,” akasema, “baraza linaloongoza la jamii ya ‘mtumwa’ haliwekwi rasmi na mwanadamu yeyote. Linawekwa rasmi na . . . Yesu Kristo, aliye Kichwa cha kutaniko la kweli la Kikristo na Bwana na Bwana-Mkubwa wa jamii ya ‘mtumwa mwaminifu na mwenye busara.’” Basi, ni wazi kwamba washiriki wa Baraza Linaloongoza hawawezi kuchaguliwa kwenye nyadhifa zao na washiriki wa shirika lolote la kisheria.
Akiendelea na mazungumzo yake, msemaji alitoa taarifa hii muhimu sana: “Baraza linaloongoza halina wasimamizi kama Baraza la Waelekezi wa Sosaiti, yaani, msimamizi, makamu-msimamizi, mwandishi-mweka-hazina na msaidizi wa mwandishi-mweka-hazina. Lina mwenyekiti tu.” Kwa miaka mingi, msimamizi wa shirika la Pennsylvania alikuwa pia mshiriki muhimu wa Baraza Linaloongoza. Hali zingebadilika. Wajibu wa washiriki wa Baraza Linaloongoza ungekuwa sawa japo hawangekuwa na uzoefu na uwezo sawa. Msemaji aliongezea hivi: “Mshiriki yeyote wa baraza linaloongoza anaweza kuwa mwenyekiti wake bila wakati huohuo kuwa msimamizi wa . . . Sosaiti . . . Inategemea utaratibu wa baraza linaloongoza ambao wadhifa wa mwenyekiti huchukuliwa kwa zamu.”
Kwenye mkutano huo wa kila mwaka usioweza kusahaulika mwaka wa 1971, tofauti kati ya washiriki watiwa-mafuta kwa roho wa Baraza Linaloongoza na waelekezi wa shirika la Pennsylvania ilionyeshwa waziwazi. Lakini, washiriki wa Baraza Linaloongoza waliendelea kutumikia wakiwa waelekezi na wasimamizi wa Sosaiti. Hata hivyo, leo swali hili lazuka: Je, kuna sababu yoyote ya Kimaandiko inayoonyesha kwamba ni lazima waelekezi wa shirika la Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania wawe washiriki wa Baraza Linaloongoza?
Jibu ni la. Kuna mashirika mengine ya kisheria, mbali na shirika la Pennsylvania, ambayo hutumiwa na Mashahidi wa Yehova. Mojawapo ni shirika la Watchtower Bible and Tract Society of New York, Incorporated. Shirika hilo hurahisisha kazi yetu huko Marekani. Ni wazi kwamba Yehova amebariki shirika hilo, ingawa wengi wa waelekezi na wasimamizi wake wamekuwa wa “kondoo wengine.” Shirika la International Bible Students Association linatumiwa huko Uingereza. Mashirika mengine ya kisheria yanatumiwa kuendeleza masilahi ya Ufalme katika nchi nyinginezo. Yote husaidia kwa upatano na hutimiza jukumu fulani katika kuhubiriwa kwa habari njema duniani kote. Bila kujali yako wapi au waelekezi na wasimamizi ni nani, mashirika hayo yanaelekezwa kitheokrasi nayo hutumiwa na Baraza Linaloongoza. Hivyo, mashirika hayo yamegawiwa kazi ya kufanya ili kuendeleza masilahi ya Ufalme.
-