-
Tangazeni Mfalme na Ufalme! (1919-1941)Mashahidi wa Yehova—Wapiga-Mbiu wa Ufalme wa Mungu
-
-
“Najua Jambo Fulani Kuhusu Sheria ya Waaminifu-Washikamanifu”
Mkusanyiko uliratibiwa katika Pittsburgh, Pennsylvania, Januari 2-5, 1919, wakati ambao Ndugu Rutherford na washirika wake walikuwa gerezani. Lakini huu haukuwa mkusanyiko wa kawaida—uliunganishwa na mkutano wa kila mwaka wa Watch Tower Society, Jumamosi, Januari 4, 1919.
-
-
Tangazeni Mfalme na Ufalme! (1919-1941)Mashahidi wa Yehova—Wapiga-Mbiu wa Ufalme wa Mungu
-
-
Siku hiyo mkutano wenye wasiwasi ulikuwa ukiendelea katika Pittsburgh. “Mvurugo, mgawanyiko, na mabishano yalikuwa mengi kwa kitambo,” akakumbuka Sara C. Kaelin, ambaye alilelewa katika eneo la Pittsburgh. “Wengine walitaka kuahirisha mkutano kwa miezi sita; wengine walitilia shaka uhalali wa kuchagua maofisa waliokuwa gerezani; wengine walidokeza maofisa wapya kabisa.”
Baada ya mazungumzo marefu, W. F. Hudgings, mwelekezi mmoja wa Peoples Pulpit Association,a alisomea wasikilizaji barua kutoka kwa Ndugu Rutherford. Katika barua hiyo alipeleka upendo na salamu kwa wale waliokusanyika. “Silaha kuu za Shetani ni KIBURI, KUTAKA MAKUU na HOFU,” akaonya. Akionyesha tamaa ya kujitiisha kwa mapenzi ya Yehova, hata alidokeza kwa unyenyekevu wanaume wenye kufaa ikiwa wenye hisa wangeamua kuchagua maofisa wapya kwa ajili ya Sosaiti.
Mazungumzo yaliendelea kwa kitambo kidogo zaidi, kisha E. D. Sexton, ambaye alikuwa amewekwa kuwa mwenyekiti wa halmashauri ya kutaja majina ya wachaguliwa, akasema kwa ujasiri hivi:
“Nimewasili sasa hivi. Garimoshi nililosafiria lilichelewa saa arobaini na nane, likiwa limezuiwa na theluji. Nina jambo ambalo ni lazima niliseme na ili nistarehe afadhali niliseme sasa. Ndugu zangu wapendwa, nimekuja hapa, kama vile nyinyi wengine, nikiwa na mawazo fulani akilini—ya kuunga mkono na ya kupinga. . . . Hakuna kizuizi cha kisheria. Tukitaka kuchagua ndugu zetu walioko Kusini kwenye cheo chochote wanachoweza kushika, sioni wala sipati kutoka kwa shauri lolote [la kisheria] nililopokea, jinsi hilo, kwa namna au hali yoyote, litaingilia upande wowote wa kesi yao mbele ya Mahakama ya Serikali Kuu wala mbele ya umma.
“Mimi naamini kwamba pongezi kubwa zaidi ambayo twaweza kumpa ndugu yetu mpendwa Rutherford ingekuwa ni kumchagua tena kuwa msimamizi wa W[atch] T[ower] B[ible] & T[ract] Society. Mimi sifikiri kwamba kuna shaka lolote katika akili za umma kwa habari ya kwamba sisi twasimama wapi katika shauri hili. Ikiwa ndugu zetu kwa njia yoyote walivunja sheria ambayo hawakuelewa, sisi twajua makusudio yao ni mema. Na mbele za [Mungu] Mweza Yote wao hawakuhalifu sheria yoyote ya Mungu wala ya mwanadamu. Tungedhihirisha utumainifu mkubwa zaidi kwa kumchagua tena Ndugu Rutherford kuwa msimamizi wa Shirika.
“Mimi si mwanasheria, lakini inapohusu uhalali wa hali hii najua jambo fulani kuhusu sheria ya waaminifu-washikamanifu. Uaminifu-mshikamanifu ndio ambao Mungu hudai. Mimi siwezi kuwazia utumainifu mkubwa zaidi ambao tungeweza kudhihirisha kuliko kuwa na uchaguzi NA KUMCHAGUA TENA NDUGU RUTHERFORD KUWA MSIMAMIZI.”
Kwa wazi, Ndugu Sexton alieleza hisia za walio wengi kati ya waliohudhuria. Majina yalitajwa; kura ilipigwa; na J. F. Rutherford akachaguliwa kuwa msimamizi, C. A. Wise makamu wa msimamizi, na W. E. Van Amburgh mwandishi-mweka-hazina.
-