-
Maji Halisi na ya Kiroho Ni Muhimu kwa UhaiAmkeni!—2001 | Juni 22
-
-
ZAIDI ya miaka 2,000 iliyopita, jiji moja mashuhuri lenye wakazi 30,000 lilisitawi katika Jangwa la Arabia. Ijapokuwa jiji hilo la Petra lilikuwa na ukame, na kwa wastani lilipata mvua yenye kipimo cha milimeta 150 kwa mwaka, wakazi wake walizoea kuishi bila maji ya kutosha. Jiji la Petra lilisitawi sana na kuwa na ufanisi.
Wakazi wa Petra (Wanabatea) hawakuwa na mashine za umeme za kupiga maji. Hawakujenga mabwawa makubwa ya maji. Hata hivyo, walijua jinsi ya kuvuta na kuhifadhi maji. Walisambaza maji jijini na kwenye mashamba yao madogo kwa mifereji, mabwawa, na matangi ya kuhifadhia maji. Walihifadhi maji kwa udi na uvumba. Walijenga visima na matangi yao kwa njia nzuri sana hivi kwamba Wabedui wa kisasa bado huyatumia.
“Mfumo wa maji wa Petra unavutia ajabu,” asema mtaalamu mmoja wa maji kwa mshangao. ‘Wakazi wa Petra walikuwa na akili na uwezo usio wa kawaida.’ Hivi karibuni, wataalamu wa Israeli wamejaribu kuiga ustadi wa wakazi hao wa Petra. Wakazi hao walikuza mimea katika Negebu, ambako mvua isiyozidi milimeta 100 hunyesha kila mwaka. Wataalamu wa kilimo wamechunguza maelfu ya mashamba madogo yaliyosalia ya wakazi hao. Wakazi hao walikusanya maji ya mvua kwa ustadi kupitia mifereji na kuyaelekeza kwenye mashamba yao.
Tayari wakulima wanaoishi kwenye nchi zenye ukame katika jangwa la Sahel barani Afrika wanatumia mbinu za wakazi wa Petra. Hata hivyo, mbinu za kisasa za kuhifadhi maji zina matokeo pia. Katika Lanzarote, kimojawapo cha Visiwa vya Canary, kilicho karibu na pwani ya Afrika, wakulima wamejifunza kukuza zabibu na tini kwenye maeneo yasiyopata mvua kabisa. Wao hupanda mizabibu au mitini ndani ya mashimo halafu hutia majivu ya volkano juu ya udongo ili kuzuia maji yasiwe mvuke. Umande wa kutosha hutiririka mizizini na hivyo wanavuna kwa wingi.
Utatuzi kwa Kutumia Mbinu Sahili
Kotekote ulimwenguni watu fulani wamefaulu kuishi kwenye maeneo yenye ukame—kutia ndani Wabishnoi, wanaoishi kwenye Jangwa la Thar huko India; wanawake Waturkana wanaoishi Kenya; na Wahindi wa Navajo wanaoishi Arizona, Marekani. Mbinu wanazotumia kukusanya maji ya mvua, ambazo wamejifunza kwa karne nyingi, zinawasaidia kujiruzuku kupitia kilimo kuliko mbinu za kisasa za tekinolojia.
Mabwawa mengi yalijengwa katika karne ya 20. Watu walitumia maji ya mito mikubwa, na mifumo mikubwa ya umwagiliaji-maji mashamba ilibuniwa. Mwanasayansi mmoja akadiria kwamba asilimia 60 ya mito na vijito vyote ulimwenguni vimedhibitiwa kwa njia fulani. Ijapokuwa miradi hiyo ilileta manufaa fulani, wataalamu wa mazingira na viumbe wanaeleza jinsi ambavyo mazingira yameharibiwa na jinsi ambavyo mamilioni ya watu wameathiriwa baada ya kupoteza makao yao.
Isitoshe, wakulima wanaohitaji maji sana hawafaidiki kutokana na miradi hiyo iliyoanzishwa kwa makusudi mazuri. Aliyekuwa Waziri Mkuu wa India Rajiv Gandhi alisema hivi kuhusiana na miradi ya umwagiliaji-maji mashamba nchini humo: “Kwa miaka 16 tumetumia pesa nyingi. Watu hawajafaidika kwa vyovyote, mashamba hayamwagiliwi maji, hakuna maji, uzalishaji haujaongezeka, maisha ya watu yangali magumu.”
Kwa upande mwingine, mbinu sahili za kilimo ziliboresha hali na hazikuharibu mazingira. Vidimbwi vidogo na mabwawa milioni sita yaliyojengwa na jumuiya yamewasaidia sana watu nchini China. Nchini Israel, watu wamegundua kwamba maji yaliyotumiwa nyumbani yanaweza kutumiwa tena katika kilimo cha umwagiliaji-maji mashamba.
Mbinu nyingine inayofanya kazi ni kudondosha matone ya maji mashambani (drip irrigation). Mbinu hiyo huhifadhi udongo na hutumia asilimia 5 tu ya maji yanayotumiwa katika mbinu za kawaida za kumwagilia maji mashamba. Kutumia maji kwa hekima kwamaanisha pia kupanda mazao ambayo yanasitawi katika maeneo yenye ukame, kama vile mawele au mtama, badala ya mazao yanayohitaji maji mengi, kama vile miwa au mahindi.
Wale walio nyumbani na viwandani wanaweza kujitahidi kupunguza kiasi cha maji wanachotumia. Kwa mfano, kilogramu moja ya karatasi inaweza kutengenezwa kwa lita moja hivi ya maji ikiwa kiwanda kinasafisha na kutumia maji yaleyale—na hivyo kuhifadhi zaidi ya asilimia 99 ya maji. Jiji la Mexico City limeacha kutumia vyoo vya kawaida na badala yake linatumia vyoo vinavyotumia theluthi ya maji waliyotumia mbeleni. Jiji hilo pia lilifadhili kampeni ya kuelimisha watu ili kupunguza matumizi ya maji.
Utatuzi Unategemea Nini?
Utatuzi wa matatizo ya maji—na matatizo mengi ya mazingira—unategemea kubadili mitazamo. Watu wanahitaji kushirikiana badala ya kuwa na ubinafsi, kujidhabihu iwezekanapo, na kuazimia kutunza dunia kwa ajili ya vizazi vijavyo. Kuhusiana na hilo Sandra Postel, aeleza hivi katika kitabu chake Last Oasis—Facing Water Scarcity: “Tunahitaji kuwa na kanuni za maji—ili kutusaidia kutenda ifaavyo tunapokabili maamuzi magumu kuhusu mifumo ya asili ambayo hatuelewi na tusiyoweza kuelewa kikamili.”
Bila shaka, ni lazima hizo “kanuni za maji” zimhusu kila mtu. Nchi zinahitaji kushirikiana na nchi jirani, kwa kuwa mito hutiririka katika nchi mbalimbali. Ismail Serageldin asema hivi katika ripoti yake Beating the Water Crisis (Kutatua Tatizo la Maji): “Sasa ni lazima mahangaiko kuhusu kiasi na hali ya maji—mambo ambayo hapo awali yalionwa kuwa hayahusiani—yaonwe kuwa matatizo yanayoathiri ulimwengu wote.”
Lakini Katibu-Mkuu wa UM Kofi Annan akiri kwamba kuunganisha mataifa ili yashughulikie matatizo yanayoathiri ulimwengu wote si kazi rahisi. Asema hivi: “Mbinu zilizopo leo za kutatua tatizo la maji ulimwenguni pote ni za hali ya chini sana. Huu ndio wakati ufaao wa kuzingatia kwa uzito wazo la ‘jamii ya kimataifa.’”
-
-
Maji Halisi na ya Kiroho Ni Muhimu kwa UhaiAmkeni!—2001 | Juni 22
-
-
[Picha katika ukurasa wa 10]
Juu: Wakazi wa kale wa Petra walijua kuhifadhi maji
Chini: Mfereji wa maji uliojengwa na Wanabatea huko Petra
[Hisani]
Garo Nalbandian
[Picha katika ukurasa wa 10]
Wakulima kwenye kimojawapo cha Visiwa vya Canary wamejifunza kukuza mimea kwenye maeneo yasiyopata mvua kabisa
-