-
Samoa2009 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
-
-
KISIWA CHA SAVAII CHAPOKEA HABARI NJEMA
Sasa, acheni tuzungumzie kisiwa kikubwa zaidi cha Samoa, ambacho kwa kiasi kikubwa mazingira yake yangali yalivyokuwa kiasili. Sehemu kubwa ya kisiwa hicho haikaliwi nacho kina milima mirefu, magenge ya volkano, na mabonde yapatayo 450 ya volkano, misitu mikubwa isiyopenyeka kwa urahisi, na nyanda zenye mawe-mawe ya lava. Wenyeji wengi hukaa katika vijiji vidogo-vidogo vilivyo kando ya bahari. Mwaka wa 1955 ndipo habari njema ilipofika Savaii. Len Helberg na kikundi cha wahubiri kutoka katika kisiwa cha Upolu walizuru kwa siku chache na kuonyesha ile filamu ya The New World Society in Action.
Miaka sita baadaye, dada wawili wamishonari—Tia Aluni, Msamoa wa kwanza kuhudhuria Shule ya Gileadi, na mwenzake Ivy Kawhe—waliombwa wahame kutoka Samoa ya Marekani na kwenda Savaii. Walipofika mwaka wa 1961, dada hao waliishi na mume na mke waliokuwa wazee kwa umri huko Fogapoa, kijiji kilicho upande wa mashariki wa kisiwa hicho. Baadaye, dada mwingine painia wa pekee, ambaye wakati mmoja alikuwa akiishi Savaii, akajiunga nao kwa muda. Ili kukitia moyo na kukitegemeza kikundi hicho kipya cha watu sita hadi nane hivi, akina ndugu kutoka Apia walizuru mara moja kwa mwezi na kutoa hotuba ya watu wote. Mikutano hiyo ilifanyiwa katika nyumba ndogo huko Fogapoa.
Tia na Ivy waliendelea kukaa Savaii hadi 1964, walipopewa mgawo wa kuhamia kisiwa kingine. Kwa miaka kumi iliyofuata, kazi ya kuhubiri katika kisiwa hicho cha Savaii ilifanywa kwa kiwango kidogo. Kisha, kuanzia mwaka wa 1974, familia kadhaa zilihamia Savaii ili kuchochea tena kazi hiyo. Waliohamia huko ni kutia ndani Risati na Mareta Segi, Happy na Maota Goeldner-Barnett, Faigaai Tu, Palota Alagi, Kumi Falema‘a (aliyeitwa Thompson baadaye), na Ron na Dolly Sellars, waliohama kutoka Samoa ya Marekani. Kikundi kidogo kilichoanzishwa Fogapoa kilikuwa kikikutanikia katika nyumba ya akina Segi, iliyokuwa kando ya bahari. Baadaye makao ya wamishonari na Jumba la Ufalme lilijengwa karibu na mahali hapo. Baada ya muda, kikundi kingine kikaanzishwa Taga, kijiji kilicho pwani, upande wa magharibi wa Savaii.
Kuanzia 1979, wamishonari zaidi walipewa mgawo wa kwenda Savaii kuwaunga mkono wahubiri wenyeji. Walitia ndani Robert na Betty Boies, John na Helen Rhodes, Leva na Tenisia Faai‘u, Fred na Tami Holmes, Brian na Sue Mulcahy, Matthew na Debbie Kurtz, na Jack na Mary Jane Weiser. Wamishonari hao walitoa mwongozo unaohitajika nayo kazi kisiwani Savaii ilisonga mbele.
Hata hivyo, katika kisiwa cha Savaii, utamaduni na masuala ya familia yalikuwa yamewafunga sana watu. Karibu theluthi moja ya vijiji vilikuwa vimewapiga marufuku Mashahidi wa Yehova wasihubiri katika jamii zao, vijiji fulani hata vikitangaza kupitia redio. Kwa hiyo, kuwasaidia wapya wafanye maendeleo kulihitaji wakati na subira. Hata hivyo, wengi, kutia ndani wengine waliokuwa na matatizo makubwa ya afya, walijifunza kweli.
KUSHINDA MATATIZO YA AFYA ILI KUMTUMIKIA YEHOVA
Mmoja wao ni Metusela Neru. Alipokuwa na umri wa miaka 12, alianguka alipokuwa akiendesha farasi na kuvunjika mgongo. “Baada ya kuanguka,” akumbuka mmishonari mmoja, “alitembea kana kwamba ana kibiongo, naye alikuwa na maumivu daima.” Metusela alipoanza kujifunza Biblia akiwa na umri wa miaka 19, aliamua kabisa kuvumilia upinzani wa familia yake. Kwa sababu ya ulemavu wake, safari ya kwenda kwenye mikutano ambayo kwa kawaida ingechukua dakika tano, ilimchukua dakika 45, tena kwa shida. Hata hivyo, Metusela alifanya maendeleo, akabatizwa mwaka wa 1990. Baadaye akawa painia wa kawaida na kustahili kuwa mzee kutanikoni. Tangu wakati huo, watu zaidi ya 30 kutoka katika familia yao wamehudhuria mikutano huko faga, na baadhi yao wamebatizwa. Leo, licha ya matatizo yake ya afya, Metusela anajulikana kuwa mtu mwenye tabasamu na furaha sikuzote.
Mwingine aliyeshinda matatizo makubwa ya afya na kufanya maendeleo ya kiroho ni Saumalu Taua‘anae. Saumalu alikuwa na sura isiyo ya kawaida kwa sababu ya ukoma, naye alikuwa akiishi katika kijiji cha Aopo. Kwa sababu kijiji alichoishi kilikuwa mbali, mwanzoni alijifunza Biblia kupitia barua walizokuwa wakiandikiana na Ivan Thompson. Kisha Asa Coe, painia wa pekee, akahamia Savaii na kuendeleza funzo hilo. Saumalu alipohudhuria mkutano wake wa kwanza mwaka wa 1991, alisafiri kwa gari kwa saa mbili hadi Taga, kijiji kilichokuwa upande wa pili wa kisiwa hicho.
Saumalu hakuwa huru kuchangamana na watu kwa sababu ya sura yake. Hivyo, alipohudhuria kusanyiko la pekee, alisikiliza programu akiwa ndani ya gari lake. Hata hivyo, aliguswa moyo sana kwamba wakati wa mapumziko ya mchana, ndugu na dada walimjia kwa upendo na kumkaribisha kwa moyo mkunjufu. Alikubali mwaliko wao na kusikiliza programu iliyosalia akiwa ameketi pamoja na wasikilizaji wengine.
Punde si punde, Saumalu na mke wake, Torise, wakaanza kuhudhuria mikutano katika kijiji cha Faga, wakisafiri umbali wa zaidi ya saa moja. Saumalu alibatizwa mwaka wa 1993, na baada ya muda akastahili kutumikia akiwa mtumishi wa huduma. Baadaye, hata madaktari walipoukata mguu wake, bado alikuwa akiendesha gari lake kwenda kwenye mikutano. Kijiji chao kimepiga marufuku kazi ya kuhubiri inayofanywa na Mashahidi wa Yehova; kwa hiyo, Saumalu na Torise huwahubiria wengine kwa njia zisizo rasmi na kupitia simu.
Leo, wanaishi Apia, ambapo Saumalu hupata matibabu mbalimbali anayohitaji mara kwa mara. Badala ya kuwa na uchungu moyoni, anajulikana kuwa mtu mwenye matumaini na shangwe maishani. Yeye na mke wake wanaheshimiwa sana kwa sababu ya imani yao yenye nguvu.
-
-
Samoa2009 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
-
-
“Yehova Amejibu Sala Zangu”
FAIGAAI TU
ALIZALIWA 1932
ALIBATIZWA 1964
MAELEZO MAFUPI KUMHUSU Alikuwa painia katika visiwa vya Upolu na Savaii tangu mwaka wa 1965 mpaka 1980. Sasa anaishi Savaii.
NILIZALIWA nikiwa na miguu iliyojipinda vibaya na kwa sababu hiyo ilikuwa vigumu sana kwangu kutembea.
Nilipoisikia kweli kwa mara ya kwanza, ilipenya moyoni mwangu. Nilitamani kuhudhuria mikutano ya kutaniko lakini ilikuwa vigumu kwangu kutembea kwa miguu mitupu katika barabara yenye mawe ili kufika huko. Mwishowe nikawa stadi wa kujitengenezea viatu vyangu mwenyewe kutokana na malapa nami ningeweza kutembea bila shida.
Nilianza upainia baada tu ya kubatizwa. Kisha baada ya kufanya upainia kwa miaka tisa katika kisiwa cha Upolu, mimi na dada yangu na mume wake tulihamia Savaii, palipokuwa na uhitaji wa wahubiri wa Ufalme. Mimi na mpwa wangu, Kumi Falema‘a, tulitumikia tukiwa mapainia wa pekee katika eneo hili.
Nikiwa pamoja na Kumi, tulisafiri kwa basi kila juma kutoka Faga mpaka Lata, kijiji kidogo kilicho upande wa pwani ya magharibi ya Savaii. Baada ya kujifunza na mwanamke mmoja kijijini Lata, tulitembea kilomita nane kwenda Taga kujifunza na mwanamke mwingine. Tulilala kwa mwanamke huyo na kurudi Faga siku iliyofuata kwa basi la asubuhi. Tulifanya hivyo kwa miaka miwili hivi. Inafurahisha kwamba wanawake hao wawili pamoja na familia zao ni Mashahidi wenye bidii.
Familia yetu ilipoondoka Savaii, nilibaki ili kushughulikia kikundi kidogo cha akina dada na wanawake fulani wenye kupendezwa kijijini Faga. Niliongoza Funzo la Mnara wa Mlinzi na Funzo la Kitabu la Kutaniko na kuhubiri pamoja na akina dada hao katika huduma ya nyumba kwa nyumba. Mara moja kila mwezi mzee mmoja kutoka Apia alikuja kuongoza mikutano ya Jumapili. Kwa kuwa chifu wa kijiji alitukataza kuimba nyimbo za Ufalme katika mikutano yetu, tulisoma maneno ya nyimbo hizo kwa sauti. Miaka mitano baadaye, wamishonari wawili, Leva na Tenisia Faai‘u, walikuja kutoka New Zealand kusaidia kikundi chetu kidogo. Wengine wakafuata. Leo, kisiwa cha Savaii kina makutaniko mawili yenye maendeleo, moja liko Faga na lingine Taga.
Ingawa sikuwahi kuolewa, ninapenda watoto na kila wakati ninakuwa karibu nao. Watoto wengine hata waliishi nami kwa muda. Kuona “watoto” wangu wa kiroho wakifanya maendeleo na kubaki waaminifu kwa Yehova kunanipa shangwe.
Sasa nimezeeka na siwezi tena kutembea kutoka nyumba moja hadi nyingi. Mimi huongoza mafunzo ya Biblia nyumbani kwangu na kuwahubiria watu ninaokutana nao hospitalini. Hata hivyo, hali yangu ilinitamausha, nami nilisali kwa Yehova na kumwomba anisaidie nifanye mengi zaidi. Kisha, wamishonari katika kutaniko letu wakanifundisha jinsi ya kuhubiri kwa kutumia simu. Ninapotazama maisha yangu, ninaona kwamba kwa kweli Yehova amejibu sala zangu.
-