-
Samoa2009 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
-
-
MSAADA KUTOKA NG’AMBO
Mnamo Mei (Mwezi wa 5), 1953, mapainia wawili kutoka Australia, Ronald na Olive (Dolly) Sellars walifika ili kulisaidia Kutaniko la Apia. “Kwa muda fulani, mawasiliano kati ya Kutaniko la Apia na ofisi ya tawi ya Australia yalikuwa yamekatika, nayo ofisi ya tawi ilikuwa na hamu ya kujua hali ya kutaniko hilo,” aandika Ron. “Kwa kuwa tulikuwa tayari kutumikia katika Pasifiki, ofisi ya tawi ilituomba twende Samoa na kutumikia katika kutaniko hilo jipya tukiwa mapainia wa pekee.”
Wakiwa kwenye ndege kuelekea Samoa, Ron na Dolly walijitayarisha kiakili kukabili hali ngumu mbalimbali ambazo kwa kawaida watu hukumbana nazo katika migawo yao ya umishonari sehemu za mbali. “Tulishangaa kama nini,” akumbuka Ron, “kuona miti na mimea mingi kila sehemu ya kisiwa hicho. Kila mahali, tuliona watu wenye furaha, wenye kutabasamu, na wenye afya. Watoto walikuwa wakichezacheza kuzunguka nyumba zilizoezekwa na zenye sakafu nzuri ya matumbawe, ijapokuwa hazikuwa na kuta. Kila kitu kilikuwa kikifanywa polepole, bila haraka yoyote. Ni kana kwamba tulikuwa katika paradiso.”
Baada ya kupewa mahali pa kukaa na familia ya Pele, akina Sellars walianza kazi mara moja. “Nilipanga kukutana na akina ndugu kila jioni ili kuwajibu maswali yao mengi,” asema Ron. “Ijapokuwa walijua mafundisho ya msingi ya Biblia, muda si muda niliona kwamba wanahitaji kufanya mabadiliko mbalimbali ili kupatanisha maisha yao na viwango vya Mungu. Ili kuwasaidia kufanya hivyo, Dolly nami tulijitahidi sana kuwa na subira na kuwaonyesha upendo mwingi sana.” Hata hivyo, kwa kusikitisha, wengine walikataa marekebisho hayo ya upendo yaliyotokana na Maandiko na baada ya muda wakaacha kushirikiana na kutaniko. Lakini, wengine walikuwa wanyenyekevu nao walikubali mafundisho na mahimizo hayo. Baadaye, wakafanya maendeleo ya kiroho, na kwa sababu hiyo, kutaniko likasafishwa na kuimarishwa.
Ron na Dolly waliongoza katika kazi ya kuhubiri nyumba kwa nyumba pia. Kabla ya hapo, ndugu wengi walikuwa wakiwahubiria marafiki na majirani tu. Sasa, walipokuwa wakihubiri nyumba kwa nyumba pamoja na akina Sellars, walipata watu wengi wanaopendezwa. “Pindi moja,” aandika Ron, “tulialikwa kwenda katika kijiji cha chifu anayependezwa, ambaye alitaka kujua mengi zaidi kuhusu habari njema ya Ufalme. Baada ya kula, tukawa na mazungumzo mazuri ya Biblia. Baada ya saa moja hivi, mazungumzo hayo yalikuwa yamebadilika na kuwa hotuba ya watu wote kwa sababu watu walikuwa wameongezeka kufikia 50, nasi hatukuwa tumemwalika yeyote!” Mara nyingi, wahubiri walipoanza kujifunza Biblia na watu 2 au 3, muda si muda kikundi hicho kilivutia watu wengine 10 hadi 40, waliotaka kujua utendaji wa Mashahidi wa Yehova.
Mapadri pia walikuwa wakiona yaliyokuwa yakiendelea. Wenye mamlaka walipokataa kuwaongezea Ron na Dolly muda wa kuendelea kukaa nchini humo, Ron alimwendea kamishna mkuu na kumuuliza ni kwa nini. Ron akumbuka: “Alitujibu kwamba makasisi fulani waliilalamikia serikali kwa sababu ya kazi yetu ya kuhubiri. Kwa hiyo, akasema kwamba tukiahidi kwamba tutaacha kusaidia kutaniko hilo katika kazi ya kuhubiri, atatuongezea muda kwenye vibali vyetu. Nilikataa. Pia, nikamwambia asisahau kamwe kwamba hakuna mtu anayeweza kuzuia kazi ya Mungu. Alicheka na kusema, ‘Tutaona, mkishaondoka!’”
-
-
Samoa2009 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
-
-
[Picha katika ukurasa wa 81]
Ron na Dolly Sellars walihamia Samoa mwaka wa 1953 kutumikia katika eneo lenye uhitaji
-