-
Samoa2009 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
-
-
Kisha, kuanzia mwaka wa 1974, familia kadhaa zilihamia Savaii ili kuchochea tena kazi hiyo. Waliohamia huko ni kutia ndani Risati na Mareta Segi, Happy na Maota Goeldner-Barnett, Faigaai Tu,
-
-
Samoa2009 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
-
-
[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 113, 114]
“Yehova Amejibu Sala Zangu”
FAIGAAI TU
ALIZALIWA 1932
ALIBATIZWA 1964
MAELEZO MAFUPI KUMHUSU Alikuwa painia katika visiwa vya Upolu na Savaii tangu mwaka wa 1965 mpaka 1980. Sasa anaishi Savaii.
NILIZALIWA nikiwa na miguu iliyojipinda vibaya na kwa sababu hiyo ilikuwa vigumu sana kwangu kutembea.
Nilipoisikia kweli kwa mara ya kwanza, ilipenya moyoni mwangu. Nilitamani kuhudhuria mikutano ya kutaniko lakini ilikuwa vigumu kwangu kutembea kwa miguu mitupu katika barabara yenye mawe ili kufika huko. Mwishowe nikawa stadi wa kujitengenezea viatu vyangu mwenyewe kutokana na malapa nami ningeweza kutembea bila shida.
Nilianza upainia baada tu ya kubatizwa. Kisha baada ya kufanya upainia kwa miaka tisa katika kisiwa cha Upolu, mimi na dada yangu na mume wake tulihamia Savaii, palipokuwa na uhitaji wa wahubiri wa Ufalme. Mimi na mpwa wangu, Kumi Falema‘a, tulitumikia tukiwa mapainia wa pekee katika eneo hili.
Nikiwa pamoja na Kumi, tulisafiri kwa basi kila juma kutoka Faga mpaka Lata, kijiji kidogo kilicho upande wa pwani ya magharibi ya Savaii. Baada ya kujifunza na mwanamke mmoja kijijini Lata, tulitembea kilomita nane kwenda Taga kujifunza na mwanamke mwingine. Tulilala kwa mwanamke huyo na kurudi Faga siku iliyofuata kwa basi la asubuhi. Tulifanya hivyo kwa miaka miwili hivi. Inafurahisha kwamba wanawake hao wawili pamoja na familia zao ni Mashahidi wenye bidii.
Familia yetu ilipoondoka Savaii, nilibaki ili kushughulikia kikundi kidogo cha akina dada na wanawake fulani wenye kupendezwa kijijini Faga. Niliongoza Funzo la Mnara wa Mlinzi na Funzo la Kitabu la Kutaniko na kuhubiri pamoja na akina dada hao katika huduma ya nyumba kwa nyumba. Mara moja kila mwezi mzee mmoja kutoka Apia alikuja kuongoza mikutano ya Jumapili. Kwa kuwa chifu wa kijiji alitukataza kuimba nyimbo za Ufalme katika mikutano yetu, tulisoma maneno ya nyimbo hizo kwa sauti. Miaka mitano baadaye, wamishonari wawili, Leva na Tenisia Faai‘u, walikuja kutoka New Zealand kusaidia kikundi chetu kidogo. Wengine wakafuata. Leo, kisiwa cha Savaii kina makutaniko mawili yenye maendeleo, moja liko Faga na lingine Taga.
Ingawa sikuwahi kuolewa, ninapenda watoto na kila wakati ninakuwa karibu nao. Watoto wengine hata waliishi nami kwa muda. Kuona “watoto” wangu wa kiroho wakifanya maendeleo na kubaki waaminifu kwa Yehova kunanipa shangwe.
Sasa nimezeeka na siwezi tena kutembea kutoka nyumba moja hadi nyingi. Mimi huongoza mafunzo ya Biblia nyumbani kwangu na kuwahubiria watu ninaokutana nao hospitalini. Hata hivyo, hali yangu ilinitamausha, nami nilisali kwa Yehova na kumwomba anisaidie nifanye mengi zaidi. Kisha, wamishonari katika kutaniko letu wakanifundisha jinsi ya kuhubiri kwa kutumia simu. Ninapotazama maisha yangu, ninaona kwamba kwa kweli Yehova amejibu sala zangu.
-