-
Jambo Kuu Maishani Mwako Ni Nini?Mnara wa Mlinzi—1996 | Desemba 15
-
-
Jambo Kuu Maishani Mwako Ni Nini?
“Unijulishe njia nitakayoiendea.”—ZABURI 143:8.
1. Mfalme Solomoni alifikia mkataa gani juu ya ufuatiaji mbalimbali wa kibinadamu na mambo yanayotimizwa?
LABDA wewe wafahamu kwamba maisha yamejaa utendaji mbalimbali na mahangaiko. Uyafikiriapo, waweza kuona kwamba baadhi yayo si muhimu. Utendaji na mahangaiko mengine si ya maana sana au hata huwa ya ubatili. Jambo la kwamba unatambua hilo lamaanisha una upatano na mmoja wa watu wenye hekima zaidi, Mfalme Solomoni. Baada ya kupitia kwa ukamili utendaji mbalimbali wa maisha, yeye alifikia mkataa huu: “Mche Mungu, nawe uzishike amri zake, maana kwa jumla ndiyo impasayo mtu.” (Mhubiri 2:4-9, 11; 12:13) Hilo lina umaana gani kwetu leo?
2. Watu wenye kumhofu Mungu wapaswa kujiuliza swali gani la msingi, hilo likiongoza kwenye maswali gani yanayohusiana na hilo?
2 Ikiwa wataka ‘kumcha Mungu na kuzishika amri zake,’ jiulize swali hili lenye kuvutia, ‘Jambo kuu maishani mwangu ni nini?’ Ni kweli, huenda usilifikirie kwa uzito swali hilo kila siku, lakini kwa nini usilifikirie sasa? Kwa hakika, hilo lakumbusha maswali fulani yanayohusiana na hilo, kama, ‘Je, huenda nikawa nakaza fikira isivyofaa juu ya kazi yangu au maishilio yangu au vitu vya kimwili? Nyumba yangu, familia yangu, na wapendwa wangu wana umaana gani maishani mwangu?’ Huenda kijana akauliza hivi, ‘Elimu huvuta uangalifu na wakati wangu kadiri gani? Kwa kweli, je, napendezwa hasa na hobi, mchezo, au namna fulani ya vitumbuizo au tekinolojia?’ Na hata umri wetu au hali yetu iwe ni nini, twapaswa kujiuliza kwa kufaa, ‘Kumtumikia Mungu kuna sehemu gani maishani mwangu?’ Yamkini ungekubali uhitaji wa kupanga mambo ya kutangulizwa. Lakini ni jinsi gani na ni wapi tuwezapo kupata msaada ili kuyapanga kwa hekima?
3. Kupanga mambo ya kutangulizwa kwahusisha nini kwa Wakristo?
3 “Kuu” lina maana ya msingi ya jambo linalotangulia mambo yote mengine au linalohitaji kufikiriwa kwanza. Kama wewe ni mmoja wa Mashahidi wa Yehova au wewe umo miongoni mwa wale mamilioni ya wanafunzi wenye moyo mweupe wa Neno la Mungu wanaoshirikiana nao, fikiria kweli hii: “Kwa kila jambo, kuna majira yake, na wakati kwa kila kusudi chini ya mbingu.” (Mhubiri 3:1) Kwa haki, hilo latia ndani kuonyesha kwako hangaiko lenye upendo kuelekea mahusiano ya familia. (Wakolosai 3:18-21) Lahusisha kufanya uandalizi wa haki kwa ajili ya watu wa nyumbani kwako kwa kufanya kazi ya kimwili. (2 Wathesalonike 3:10-12; 1 Timotheo 5:8) Na ili kuubadili mwendo wa kawaida waweza kutumia wakati wa kushughulikia hobi au vitumbuizo au tafrija za pindi kwa pindi. (Linganisha Marko 6:31.) Lakini, baada ya kufikiria kwa uzito, je, huoni kwamba hakuna lolote kati ya mambo hayo lililo kuu maishani? Jambo jingine ni la maana zaidi.
4. Wafilipi 1:9, 10 (NW), huhusianaje na kupanga kwetu mambo ya kutangulizwa?
4 Labda watambua kwamba kanuni zenye kuongoza za Biblia ni misaada yenye thamani katika kupanga mambo ya kutangulizwa na kufanya maamuzi yenye hekima. Kwa kielelezo, kwenye Wafilipi 1:9, 10 (NW), Wakristo wanasihiwa sana “kuzidi bado hata zaidi na zaidi pamoja na ujuzi sahihi na ufahamu kamili.” Kwa kusudi jipi? Mtume Paulo aliongeza hivi: “Mpate kuhakikisha mambo yaliyo ya maana zaidi.” Je, hilo halipatani na akili? Kwa msingi wa ujuzi sahihi, Mkristo mwenye utambuzi aweza kuamua ni jambo gani lipasalo kuwa lenye upendezi wa kwanza—kuwa kuu—maishani.
Kigezo Kionyeshacho Jambo Kuu
5. Katika kufafanua kigezo walichoachiwa Wakristo, Maandiko huonyeshaje jambo lililokuwa kuu maishani mwa Yesu?
5 Twaona upande wenye thamani wa ujuzi, katika maneno haya ya mtume Petro: “Kwa sababu ndio mlioitiwa; maana Kristo naye aliteswa kwa ajili yenu, akawaachia kielelezo, mfuate nyayo zake.” (1 Petro 2:21) Ndiyo, ili kupata vidokezi vionyeshavyo jambo kuu maishani ni gani, twaweza kuchunguza maoni ya Yesu Kristo kuhusu jambo hilo. Zaburi 40:8 ilisema hivi kiunabii juu yake: “Kuyafanya mapenzi yako, Ee Mungu wangu, ndiyo furaha yangu; naam, sheria yako imo moyoni mwangu.” Hivyo ndivyo alivyotoa wazo lilo hilo: “Chakula changu ndicho hiki, niyatende mapenzi yake aliyenipeleka, nikaimalize kazi yake.”—Yohana 4:34; Waebrania 12:2.
6. Twaweza kuwaje na matokeo yaleyale ambayo Yesu alikuwa nayo katika kuweka mapenzi ya Mungu kwanza?
6 Kazia uangalifu ufunguo huo—kuyatenda mapenzi ya Mungu. Kielelezo cha Yesu chakazia jambo ambalo wanafunzi wake wapaswa kwa kufaa, kulifanya liwe kuu maishani mwao, kwa maana alisema kwamba “kila mtu ambaye amehitimu hulingana na mwalimu wake.” (Luka 6:40) Na Yesu alipokuwa akitembea katika njia ambayo Baba yake alikusudia, alionyesha kwamba kulikuwa na “furaha tele” katika kuweka mapenzi ya Mungu kuwa jambo kuu. (Zaburi 16:11; Matendo 2:28) Je, waona kinachodokezwa na hilo? Wafuasi wa Yesu wachaguapo kule kuyatenda mapenzi ya Mungu kuwa jambo kuu maishani mwao, wao watakuwa na “furaha tele” na uhai ulio halisi. (1 Timotheo 6:19) Kwa hiyo kuna sababu zaidi ya moja ifanyayo kule kuyatenda mapenzi ya Mungu kuwa jambo la kutangulizwa maishani mwetu.
7, 8. Yesu alikabili majaribu gani, nasi twaweza kujifunza nini kutokana na hilo?
7 Mara baada ya Yesu kuonyesha kujitoa kwake ili kuyatenda mapenzi ya Mungu, Ibilisi alijaribu kumkengeusha. Jinsi gani? Kwa kumshawishi katika mambo matatu. Kila mara Yesu alijibu kwa maneno ya Kimaandiko, yaliyo wazi. (Mathayo 4:1-10) Lakini majaribu zaidi yalimngojea—mnyanyaso, dhihaka, kusalitiwa na Yudasi, mashtaka yasiyo ya kweli, kisha kifo juu ya mti wa mateso. Bado, hakuna mojawapo ya majaribu hayo yaliyomfanya Mwana mwaminifu-mshikamanifu wa Mungu ageuze njia yake. Katika hali ya hatari, Yesu alisali hivi: “Si kama nitakavyo mimi, bali kama utakavyo. . . . Mapenzi yako yatimizwe.” (Mathayo 26:39, 42) Je, kila moja wetu hapaswi kusukumwa kwa kina kirefu na sehemu hii ya kigezo tulichoachiwa, ikitufanya ‘tudumu katika kusali’?—Warumi 12:12.
8 Ndiyo, tupangapo mambo yetu ya kutangulizwa maishani, mwongozo wa kimungu ni wenye kusaidia sana, hasa ikiwa twakabili maadui wa ile kweli na wapinzani wa mapenzi ya Mungu. Kumbuka kule kusihi kwa Mfalme Daudi akiomba mwongozo alipopatwa na upinzani wa adui. Tutaona hilo tuchunguzapo sehemu ya Zaburi 143. Hiyo yapaswa kutusaidia tutambue jinsi tuwezavyo kuimarisha uhusiano wetu wa kibinafsi pamoja na Yehova na kutiwa nguvu ili kuweka kule kuyatenda mapenzi ya Mungu kuwa jambo la kwanza maishani mwetu.
Yehova Husikia na Kujibu Sala Zetu
9. (a) Ingawa Daudi alikuwa mtenda-dhambi, maneno na vitendo vyake vyafunua nini? (b) Kwa nini tusikate tamaa katika kufanya lililo sawa?
9 Ingawa alikuwa binadamu mwenye dhambi awezaye kufa, Daudi alikuwa na imani kwamba Yehova angesikia kusihi kwake. Aliomba hivi kwa unyenyekevu: “Ee BWANA, uisikie sala yangu, uzisikilize dua zangu, kwa uaminifu wako unijibu kwa haki yako [“uadilifu wako,” NW]. Wala usimhukumu mtumishi wako, maana kwako hakuna aliye hai mwenye haki.” (Zaburi 143:1, 2) Daudi alitambua kutokamilika kwake, hata hivyo moyo wake ulikuwa kamili kumwelekea Mungu. Hivyo, alikuwa na uhakika kwamba angepokea jibu katika uadilifu. Je, hilo halitutii moyo? Ingawa twapungukiwa na uadilifu wa Mungu, twaweza kuwa na uhakika kwamba yeye hutusikia ikiwa mioyo yetu ni kamili kumwelekea yeye. (Mhubiri 7:20; 1 Yohana 5:14) Huku tukidumu katika kusali, ni lazima tuazimie ‘kuushinda ubaya kwa wema’ katika siku hizi zenye uovu.—Warumi 12:20, 21; Yakobo 4:7.
10. Kwa nini Daudi alikuwa na vipindi vyenye hangaiko?
10 Daudi alikuwa na maadui, sawa na tulivyo nao. Alipokuwa mtoro kutoka kwa Sauli, aliyelazimika kutafuta kimbilio katika mahali pasipo na watu, pasipofikika, au alipokuwa mfalme aliyesumbuliwa na maadui, Daudi alikuwa na vipindi vyake vyenye hangaiko. Alifafanua jinsi hilo lilivyomwathiri: “Adui ameifuatia nafsi yangu . . . Amenikalisha mahali penye giza . . . Na roho yangu imezimia ndani yangu, moyo wangu ndani yangu umesituka [“umejionyesha kuwa wenye kutiwa ganzi,” NW].” (Zaburi 143:3, 4) Je, umekuwa na sababu ya kuhisi vivyo hivyo?
11. Watumishi wa siku ya kisasa wa Mungu wamekabili vipindi vipi vyenye hangaiko?
11 Msongo wa adui, majaribu kwa sababu ya ugumu mkali wa kiuchumi, ugonjwa mbaya, au matatizo mengine yenye kusababisha hangaiko yamewafanya watu fulani wa Mungu wahisi kwamba roho yao ingekata tamaa. Pindi fulani mioyo yao pia imekuwa kana kwamba imetiwa ganzi. Ni kana kwamba wao mmoja-mmoja wamelia hivi: “Wewe, uliyetuonyesha mateso mengi, mabaya, utatuhuisha tena . . . Urejee tena na kunifariji moyo.” (Zaburi 71:20, 21) Wao wamesaidiwaje?
Jinsi ya Kukabili Jitihada za Adui
12. Mfalme Daudi alikabilianaje na hatari na majaribu?
12 Zaburi 143:5 yaonyesha kile Daudi alichofanya alipokabiliwa na hatari na majaribu makubwa: “Nimezikumbuka siku za kale, nimeyatafakari matendo yako yote, naziwaza kazi za mikono yako.” Daudi alikumbuka jinsi Mungu alivyoshughulika na watumishi Wake na jinsi yeye mwenyewe alivyokuwa amepata ukombozi. Aliyatafakari yale ambayo Yehova alikuwa amefanya kwa ajili ya jina Lake kuu. Ndiyo, Daudi alifuliza kujishughulisha na kazi za Mungu.
13. Tukabilipo majaribu, kufikiria kwetu vielelezo vya kale na vya kisasa vya watumishi waaminifu kutatusaidiaje kuvumilia?
13 Je, sisi hatujakumbuka mara nyingi jinsi ambavyo Mungu ameshughulika na watu wake? Bila shaka tumefanya hivyo! Hilo latia ndani rekodi iliyowekwa na lile “wingu kubwa la mashahidi” katika nyakati za kabla ya Ukristo. (Waebrania 11:32-38; 12:1) Wakristo watiwa-mafuta katika karne ya kwanza walitiwa moyo pia ‘kuzikumbuka siku za kwanza’ na yale waliyokuwa wamevumilia. (Waebrania 10:32-34) Namna gani yale mambo yaliyoonwa na watumishi wa Mungu katika nyakati za kisasa, kama yale yaliyosimuliwa katika Jehovah’s Witnesses—Proclaimers of God’s Kingdom?a Masimulizi yaliyoandikwa humo na kwingineko hutuwezesha tukumbuke jinsi ambavyo Yehova amewasaidia watu wake wavumilie marufuku, vifungo vya gerezani, utendaji wa vikundi vya wafanya-ghasia, na kambi za mateso na za kazi ya kulazimishwa. Kumekuwa na majaribu katika nchi zilizogawanywa na vita, kama vile Burundi, Liberia, Rwanda, na iliyokuwa Yugoslavia. Upinzani ulipojidhihirisha, watumishi wa Mungu walivumilia kwa sababu ya kudumisha uhusiano wenye nguvu pamoja na Yehova. Mkono wake ulitegemeza wale waliofanya kule kuyatenda mapenzi yake kuwa jambo kuu maishani mwao.
14. (a) Ni kipi kimojawapo vielelezo vionyeshavyo jinsi Mungu amemtegemeza mtu akiwa katika hali ambayo huenda ikafanana na yetu? (b) Unajifunza nini kutokana na kielelezo hicho?
14 Hata hivyo, huenda ukaitikia kwamba hujapata kutendwa kinyama jinsi hiyo, na huenda ukahisi kwamba si yamkini kwamba utapatwa kutendwa hivyo wakati wowote. Lakini, kutegemeza kwa Mungu watu wake, hakujafanywa sikuzote katika hali ambazo wengine huenda wakaziona kuwa zenye kutokeza sana. Yeye amewategemeza watu wengi mmoja-mmoja waonwao kuwa wa “wastani” katika hali za “kawaida.” Hapa pana kimojawapo tu cha vielelezo vingi: Mnara wa Mlinzi la Desemba 1, 1996, lilikuwa na simulizi la Penelope Makris? Ni kielelezo bora sana kama nini cha uaminifu-maadili wa Kikristo! Je, waweza kukumbuka kile alichovumilia kutoka kwa majirani, jinsi alivyopambana na magonjwa mabaya, na jitihada alizotia ili kukaa katika huduma ya wakati wote? Namna gani lile jambo lenye kuthawabisha aliloona katika Mytilene? Hoja ni, Je, wewe huona vielelezo hivyo kuwa msaada kwetu sote katika kupanga mambo ya kutangulizwa, tukiweka kule kuyatenda mapenzi ya Mungu kuwa jambo la kwanza maishani mwetu?
15. Ni yapi baadhi ya matendo ya Yehova tupaswayo kuyatafakari?
15 Kuutafakari utendaji mbalimbali wa Yehova, kwatuimarisha kama kulivyomwimarisha Daudi. Katika kulitimiza kusudi lake, Yehova alifanya uandalizi kwa ajili ya wokovu kupitia kifo, ufufuo, na utukuzo wa Mwana wake. (1 Timotheo 3:16) Ameusimamisha Ufalme wake wa kimbingu, akaondolea mbali Shetani na roho zake waovu kutoka mbinguni, na kurudisha ibada ya kweli duniani. (Ufunuo 12:7-12) Amejenga paradiso ya kiroho na amewabariki watu wake kwa kuwapa ongezeko. (Isaya 35:1-10; 60:22) Sasa watu wake wanatoa ushahidi wa mwisho kabla ya dhiki kubwa kutokea kwa ghafula. (Ufunuo 14:6, 7) Ndiyo, tuna mengi ya kutafakari.
16. Twatiwa moyo kujishughulisha na nini, na kufanya hivyo kutatia nini moyoni mwetu?
16 Kufuliza kujishughulisha na kazi ya mikono ya Mungu badala ya kujishughulisha sana na jitihada za kibinadamu kwatia moyoni mwetu kwamba nguvu anazotumia Yehova haziwezi kuzuiwa na mtu. Lakini kazi hizo hazihusishi tu zile kazi za kimwili za ajabu za uumbaji huko mbinguni na hapa duniani. (Ayubu 37:14; Zaburi 19:1; 104:24) Kazi zake za ajabu zatia ndani matendo ya ukombozi kwa ajili ya watu wake kutoka kwa wapinzani walio adui, kama ilivyoonyeshwa katika mambo yaliyoonwa na watu wake wachaguliwa wa kale.—Kutoka 14:31; 15:6.
Kujua Njia ya Kuiendea
17. Yehova alikuwa halisi kwa Daudi kadiri gani, na twaweza kuhakikishiwaje na hilo?
17 Daudi alisali akiomba msaada ili unyevunyevu wa uhai ulio ndani yake usipate kukauka: “Nakunyoshea mikono yangu; nafsi yangu inakuonea kiu kama nchi kame. Ee BWANA, unijibu hima, roho yangu imelegea, usinifiche uso wako, nisifanane nao washukao shimoni.” (Zaburi 143:6, 7) Daudi, aliyekuwa mtenda-dhambi, alijua kwamba Mungu aliifahamu hali yake. (Zaburi 31:7) Nyakati nyingine huenda sisi pia tukahisi kwamba hali yetu ya kiroho imefikia kiwango cha chini. Lakini hali si bila tumaini. Yehova, asikiaye sala zetu, aweza kuharakisha kurudi kwetu kwa kutuburudisha kupitia wazee wenye upendo, makala katika Mnara wa Mlinzi, au sehemu za mkutano zionekanazo kuwa zimekusudiwa sisi hasa.—Isaya 32:1, 2.
18, 19. (a) Twapaswa kumsihi Yehova kwa bidii tukimwomba nini? (b) Twaweza kuwa na uhakika juu ya nini?
18 Kumtumaini kwetu Yehova hutusukuma tumsihi hivi: “Unifanye kusikia fadhili zako asubuhi, kwa maana nimekutumaini wewe. Unijulishe njia nitakayoiendea.” (Zaburi 143:8) Je, yeye alimtamausha Dada Makris, aliyekuwa mbali na wengine akiwa katika kisiwa cha Kigiriki? Basi je, atakutamausha ufanyapo kule kuyatenda mapenzi yake kuwa jambo kuu maishani mwako? Ibilisi na mawakili wake wangependa kuizuia au kuikomesha kabisa kazi yetu ya kupiga mbiu ya Ufalme wa Mungu. Tuwe twatumikia katika nchi ambamo ibada ya kweli huruhusiwa kwa ujumla au twatumikia mahali ambapo imekandamizwa, sala zetu zenye muungano zapatana na ombi hili la unyenyekevu la Daudi: “Ee BWANA, uniponye na adui zangu; nimekukimbilia Wewe.” (Zaburi 143:9) Usalama wetu dhidi ya kupatwa na afa la kiroho wategemea kukaa katika mahali pa siri pa Aliye Juu Zaidi Sana.—Zaburi 91:1.
19 Usadikisho wetu juu ya jambo lililo kuu una msingi thabiti. (Warumi 12:1, 2) Basi, kinza jitihada za ulimwengu za kukulazimisha ufuate yale ambayo huo wafikiri kuwa ya maana katika taratibu ya mambo ya kibinadamu. Endelea kuruhusu kila sehemu ya maisha yako ionyeshe jambo unalojua kuwa ndilo kuu—kule kuyatenda mapenzi ya Mungu.—Mathayo 6:9, 10; 7:21.
20. (a) Tumejifunza nini juu ya Daudi kwenye Zaburi 143:1-9? (b) Wakristo leo huonyeshaje roho ya Daudi?
20 Mistari tisa ya kwanza ya Zaburi 143 hukazia uhusiano wa kibinafsi wa karibu wa Daudi pamoja na Yehova. Alipozingiwa na maadui, alimsihi Mungu kwa uhuru ili kupata mwongozo. Aliumwaga moyo wake, akitafuta msaada wa kujua njia iliyo sawa ya kuendea. Ndivyo ilivyo leo kwa habari ya mabaki ya watiwa-mafuta kwa roho walio duniani pamoja na waandamani wao. Wao huona uhusiano wao pamoja na Yehova kuwa wenye thamani wamsihipo wakiomba mwongozo. Wanaweka kwanza kule kuyatenda mapenzi ya Mungu, ijapokuwa misongo kutoka kwa Ibilisi na ulimwengu.
21. Kwa nini ni jambo la maana kwetu kuweka kielelezo chema ikiwa tutawafundisha wengine jambo lipaswalo kuwa kuu maishani mwao?
21 Mamilioni wanaojifunza Biblia pamoja na Mashahidi wa Yehova wanahitaji kutambua kwamba kule kuyatenda mapenzi ya Mungu ndilo jambo kuu. Twaweza kuwasaidia kuelewa hilo tunapozungumzia sura ya 13 ya kitabu Ujuzi Uongozao Kwenye Uhai Udumuo Milele, inayokazia kanuni zinazohusika katika kuwa watiifu kwa Neno.b Bila shaka, wao wapaswa kuona kielelezo chema cha yale tunayowafundisha katika maisha yetu. Baada ya kipindi kifupi kwa kulinganishwa, wao pia watakuja kujua njia wapaswayo kuiendea. Mamilioni hao watambuapo kibinafsi jambo lipaswalo kuwa lenye umaana zaidi maishani mwao, wengi watasukumwa kuchukua hatua za kujiweka wakfu na kubatizwa. Baadaye, kutaniko laweza kuwasaidia waendelee kufuliza kuenenda katika njia ya uhai.
22. Ni maswali gani yatakayochunguzwa katika makala inayofuata?
22 Wengi hukiri kwa utayari kwamba mapenzi ya Mungu yapaswa kuwa yenye umaana zaidi maishani mwao. Lakini, Yehova huwafundishaje watumishi wake kwa kuendelea kufanya mapenzi yake? Hilo huwaletea manufaa zipi? Maswali hayo yatachunguzwa, pamoja na mazungumzo juu ya mstari wa msingi, Zaburi 143:10, katika makala ifuatayo.
-
-
Kufundishwa Kuyatenda Mapenzi ya YehovaMnara wa Mlinzi—1996 | Desemba 15
-
-
Kufundishwa Kuyatenda Mapenzi ya Yehova
“Unifundishe kuyatenda mapenzi yako, kwa maana ndiwe mungu wangu.”—Zaburi 143:10.
1, 2.(a) Inatupasa kufundishwa wakati gani, na kukiwa na maoni gani ya kihalisi? (b) Kwa nini kufundishwa na Yehova ni muhimu sana?
KILA siku ambayo mtu yu hai na mwenye kutenda, yeye aweza kufundishwa jambo lenye kufaa. Ndivyo ilivyo kwa habari yako, na ndivyo ilivyo kwa habari ya wengine. Lakini inakuwaje wakati wa kifo? Haiwezekani kufundishwa jambo lolote lile wala kujifunza mtu akiwa katika hali hiyo. Biblia husema wazi kwamba wafu “hawajui neno lo lote.” Hamna ujuzi katika Sheoli, kaburi la ujumla la wanadamu. (Mhubiri 9:5, 10) Je, hilo lamaanisha kwamba kufundishwa kwetu, kukusanya ujuzi, ni kwa ubatili? Hilo lategemea yale tufundishwayo na jinsi tuutumiavyo ujuzi huo.
2 Ikiwa twafundishwa mambo ya kilimwengu tu, hatuna wakati ujao udumuo. Lakini, kwa furaha, mamilioni ya watu katika mataifa yote wanafundishwa mapenzi ya kimungu kukiwa na taraja la uhai udumuo milele. Msingi wa tumaini hilo wategemea kule kufundishwa na Yehova, aliye Chanzo cha ujuzi upao uhai.—Zaburi 94:9-12.
3. (a) Kwa nini yaweza kusemwa kwamba Yesu alikuwa mwanafunzi wa kwanza wa Mungu? (b) Tuna uhakikishio gani kwamba wanadamu wangefundishwa na Yehova, na tokeo likiwa nini?
3 Mwana mzaliwa wa kwanza wa Mungu, akiwa mwanafunzi Wake wa kwanza, alifundishwa kuyatenda mapenzi ya Baba yake. (Mithali 8:22-30; Yohana 8:28) Kisha, Yesu alionyesha kwamba makumi ya maelfu ya wanadamu wangefundishwa na Baba yake. Matazamio ya mbele ya wale kati yetu wajifunzao kutoka kwa Mungu ni nini? Yesu alisema hivi: “Imeandikwa katika manabii, Na wote watakuwa wamefundishwa na Mungu. Basi kila aliyesikia na kujifunza kwa Baba huja kwangu. . . . Amin, amin, nawaambia, Yeye aaminiye yuna uzima wa milele.”—Yohana 6:45-47.
4. Mamilioni ya watu wanaathiriwaje na ufundishaji wa kimungu, nao wana matazamio gani ya mbele?
4 Yesu alikuwa akinukuu kutoka Isaya 54:13, lililoelekezwa kwa mwanamke wa ufananisho wa Mungu, Zayoni wa kimbingu. Unabii huo unawahusu hasa wana wa mwanamke huyo, wale wanafunzi wazaliwa-roho 144,000 wa Yesu Kristo. Mabaki ya hao wana wa kiroho ni wenye kutenda leo, wakiongoza programu ya ufundishaji ya tufeni pote. Likiwa tokeo, mamilioni ya wengine wafanyizao “umati mkubwa” hunufaika pia kutokana na kufundishwa na Yehova. Wana tazamio la mbele la kipekee la kujifunza bila kupatwa kamwe na kifo. Jinsi gani? Wamo katika mstari wa kuokoka ile ‘dhiki kubwa’ inayokaribia upesi na kufurahia uhai udumuo milele juu ya dunia iliyo paradiso.—Ufunuo 7:9, 10, 13-17.
Kukazia Zaidi Kuyatenda Mapenzi ya Mungu
5. (a) Andiko la mwaka la 1997 ni jipi? (b) Tuhisije juu ya kuhudhuria mikutano ya Kikristo?
5 Mwaka wa 1997, katika makutaniko zaidi ya 80,000 ulimwenguni pote, Mashahidi wa Yehova watazingatia maneno ya ufunguzi ya Zaburi 143:10: “Unifundishe kuyatenda mapenzi yako.” Hilo litakuwa andiko la mwaka la 1997. Maneno hayo yakiwa yameonyeshwa kwa wazi katika Majumba ya Ufalme, yatatumika yakiwa kikumbusha cha kwamba mahali penye kutokeza pa kupokea elimu ya kimungu ni kwenye mikutano ya kutaniko, tuwezapo kushiriki katika programu ya mafunzo inayoendelea. Tujiungapo na ndugu zetu kwenye mikutano ili tupate kufundishwa na Mfunzi Mtukufu wetu, twaweza kuhisi sawa na alivyohisi yule mtunga-zaburi, aliyeandika hivi: “Nalifurahi waliponiambia, Na twende nyumbani kwa BWANA.”—Zaburi 122:1; Isaya 30:20.
6. Katika maneno ya Daudi, sisi twakiri nini?
6 Ndiyo, twatamani kufundishwa kuyatenda mapenzi ya Mungu badala ya mapenzi ya mpinzani wetu Ibilisi au mapenzi ya wanadamu wasio wakamilifu. Kwa hiyo, sawa na Daudi, sisi twamkiri hivi, yule Mungu tunayemwabudu na kumtumikia: “Kwa maana wewe ndiwe Mungu wangu. Roho yako ni njema; na iniongoze katika nchi ya unyoofu.” (Zaburi 143:10, NW) Badala ya kutaka kuchangamana na watu wasiosema kweli, Daudi alipendelea kuwa mahali ambapo ibada ya Yehova iliendeshwa. (Zaburi 26:4-6) Akiwa na roho ya Mungu ikielekeza hatua zake, Daudi aliweza kutembea katika njia za uadilifu.—Zaburi 17:5; 23:3.
7. Roho ya Mungu imetendaje juu ya kutaniko la Kikristo?
7 Yule Daudi Mkubwa Zaidi, Yesu Kristo, aliwahakikishia mitume kwamba roho takatifu ingewafundisha mambo yote na kuwakumbusha mambo yote aliyokuwa amewaambia. (Yohana 14:26) Tangu Pentekoste na kuendelea, Yehova amekuwa akiyafunua kiendelevu “mafumbo ya Mungu” yaliyomo katika Neno lake lililoandikwa. (1 Wakorintho 2:10-13) Amefanya hivyo kupitia njia ionekanayo ambayo Yesu aliiita “mtumwa mwaminifu mwenye akili.” Hiyo huandaa chakula cha kiroho kinachochunguzwa katika programu ya ufundishaji kwa ajili ya makutaniko ya watu wa Mungu ulimwenguni pote.—Mathayo 24:45-47.
Kufundishwa Mapenzi ya Yehova Kwenye Mikutano Yetu
8. Kwa nini kushiriki katika Funzo la Mnara wa Mlinzi ni jambo lenye thamani sana?
8 Mara nyingi habari katika funzo la Mnara wa Mlinzi la kutaniko la kila juma hushughulikia matumizi ya kanuni za Biblia. Hilo bila shaka hutusaidia tukabiliane na mahangaiko ya maisha. Katika mafunzo mengine kweli za kiroho zenye kina au unabii mbalimbali wa Biblia huchunguzwa. Tunafundishwa mengi kama nini katika mafunzo hayo! Katika nchi nyingi Majumba ya Ufalme hujaa pomoni kwa ajili ya mikutano hiyo. Hata hivyo katika nchi kadhaa, hudhurio la mikutano limepunguka. Wadhani ni kwa nini iko hivyo? Je, yawezekana kwamba wengine wanaruhusu kazi ya kimwili izuie kukusanyika kwao pamoja kwa ukawaida ili “kuhimizana katika upendo na kazi nzuri”? Au je, yawezekana kwamba muda mwingi wa wakati unatumiwa katika ushirika wa kijamii au katika kutazama televisheni, na kufanya ratiba ionekane kuwa na vitu vingi mno wasiweze kwenda kwenye mikutano yote? Kumbuka ile amri yenye kupuliziwa kwenye Waebrania 10:23-25. Je, kukusanyika pamoja ili kupata mafunzo ya kimungu si jambo la maana hata zaidi sasa ‘tuonavyo siku ile kuwa inakaribia’?
9. (a) Mkutano wa Utumishi waweza kutuandaliaje vifaa kwa ajili ya huduma? (b) Mtazamo wetu uwe nini kuhusu kutoa ushahidi?
9 Mojawapo ya madaraka yetu ya kwanza kabisa ni lile la kutumikia tukiwa wahudumu wa Mungu. Mkutano wa Utumishi umekusudiwa kutufundisha jinsi tuwezavyo kutimiliza hilo kwa mafanikio. Twajifunza jinsi ya kuwafikia watu, mambo ya kusema, njia ya kuitikia kunapokuwa na itikio zuri, na hata jambo la kufanya watu wakataapo ujumbe wetu. (Luka 10:1-11) Njia zenye matokeo zinapozungumziwa na kufanyiwa maonyesho katika mkutano huo wa kila juma, tunatayarishwa vizuri zaidi ili kuwafikia watu si wakati tu twendapo nyumba hadi nyumba bali pia tuhubiripo barabarani, kwenye maegesho ya magari, katika usafiri wa umma, kwenye wanja za ndege, kwenye mahali pa biashara, au shuleni. Kwa kupatana na ombi letu, “Unifundishe kuyatenda mapenzi yako,” tutataka kutumia kila fursa ili kutenda sawa na vile Bwana-Mkubwa wetu alivyosihi: ‘Nuru yenu na iangaze mbele ya watu wapate kumtukuza Baba yenu aliye mbinguni.’—Mathayo 5:16.
10. Twaweza kuwasaidiaje kikweli ‘wale wanaostahili’?
10 Kwenye mikutano hiyo ya kutaniko, tunafundishwa pia kufanya wengine wawe wanafunzi. Mara kupendezwa kunapopatikana au fasihi inapoangushwa, lengo letu tunapofanya ziara za kurudia ni kuanzisha mafunzo ya Biblia nyumbani. Katika maana fulani, hilo lafanana na vile wanafunzi ‘walivyokaa pamoja na wanaostahili’ ili kuwafundisha mambo ambayo Yesu alikuwa ameamuru. (Mathayo 10:11; 28:19, 20) Tukiwa na misaada bora zaidi, kama kitabu Ujuzi Uongozao Kwenye Uhai Udumuo Milele, kwa kweli tumeandaliwa vifaa vizuri ili tupate kuitimiza huduma yetu kikamili. (2 Timotheo 4:5) Kila juma uhudhuriapo Mkutano wa Utumishi na Shule ya Huduma ya Kitheokrasi, jitahidi kuelewa kisha kuyatumia mambo yenye kusaidia yatakayokupendekeza kuwa mmoja wa wahudumu wa Mungu wenye sifa za ustahili wa kutosha, wanaotenda mapenzi yake.—2 Wakorintho 3:3, 5; 4:1, 2.
11. Watu fulani wameonyeshaje imani katika maneno yanayopatikana kwenye Mathayo 6:33?
11 Ni mapenzi ya Mungu kwamba ‘tufulize kutafuta kwanza ufalme na uadilifu wake.’ (Mathayo 6:33, NW) Jiulize mwenyewe, ‘Ningetumiaje kanuni hiyo ikiwa madai katika kazi yangu [au ya mwenzi wangu] ya kimwili yangenizuia nisihudhurie mikutano?’ Wengi walio wakomavu kiroho wangechukua hatua za kuongea na waajiri wao kuhusu jambo hilo. Mhudumu mmoja wa wakati wote alimjulisha mwajiri wake kwamba alihitaji kuchukua wakati fulani kila juma ili kuhudhuria mikutano ya kutaniko. Mwajiri alimpa ruhusa. Lakini kwa sababu ya kuwa na udadisi kuhusu kile kinachotendeka mikutanoni, yeye aliomba aweze kuhudhuria. Akiwa huko alisikia tangazo lililohusu mkusanyiko wa wilaya uliokuwa ukikaribia. Likiwa tokeo, mwajiri huyo alipanga kupisha siku nzima kwenye huo mkusanyiko. Unapata somo gani kutokana na kielelezo hicho?
Kufundishwa Mapenzi ya Yehova na Wazazi wa Kimungu
12. Ili watoto wafundishwe mapenzi ya Yehova, wazazi Wakristo wafanye nini kwa subira na uthabiti?
12 Lakini mikutano ya kutaniko na mikusanyiko si uandalizi pekee wa kufundishwa kuyatenda mapenzi ya kimungu. Wazazi wa kimungu Mungu wanaamuriwa kuzoeza, kutia nidhamu, na kuwalea watoto wao ili wapate kumsifu Yehova na kuyatenda mapenzi yake. (Zaburi 148:12, 13; Mithali 22:6, 15) Kufanya hivyo kwataka kwamba tuwapeleke “watoto” wetu mikutanoni ambako wanaweza ‘kusikiliza na kujifunza,’ lakini ni vipi juu ya kuwafundisha kutokana na maandishi matakatifu nyumbani? (Kumbukumbu la Torati 31:12; 2 Timotheo 3:15, linganisha NW.) Kwa bidii ya kufanya mema, familia nyingi zimeanza programu za funzo la Biblia la familia la ukawaida, lakini upesi zimeruhusu mafunzo hayo yafifie au kupuuzwa kabisa. Je, umepatwa na jambo hilo? Je, utakata kauli kwamba lile pendekezo la kuwa na funzo la ukawaida halifai au kwamba familia yako ina hali tofauti sana hivi kwamba hilo halitawezekana hata kidogo katika hali yenu? Hali iweje, nyinyi wazazi tafadhali pitieni zile makala nzuri “Urithi Wetu wa Kiroho Wenye Thamani Kubwa” na “Thawabu za Udumifu” katika Mnara wa Mlinzi la Agosti 1, 1995.
13. Familia zaweza kunufaikaje kutokana na kulichunguza andiko la kila siku?
13 Familia zinatiwa moyo kufanya zoea la kuchunguza andiko la kila siku kutoka katika kijitabu Kuyachunguza Maandiko Kila Siku. Kusoma tu andiko na maelezo ni jambo jema, lakini kuzungumzia andiko hilo na kulitumia ni jambo lenye manufaa zaidi. Kwa kielelezo, ikiwa wanachunguza Waefeso 5:15-17, washiriki wa familia wangeweza kusababu juu ya jinsi ya ‘kuukomboa wakati’ kwa ajili ya funzo la kibinafsi, kushiriki katika namna fulani ya huduma ya wakati wote, na kushughulikia migawo mingine ya kitheokrasi. Ndiyo, mazungumzo ya familia juu ya andiko la kila siku yangeweza kumwongoza mtu mmoja au wengi ‘wafahamu kikamili zaidi ni nini yaliyo mapenzi ya Bwana.’
14. Kumbukumbu la Torati 6:6, 7 laonyesha kwamba wazazi wapaswa kuwa walimu wa aina gani, hilo likitaka nini?
14 Ni lazima wazazi wawe walimu wenye bidii ya uendelevu wa watoto wao. (Kumbukumbu la Torati 6:6, 7) Lakini si jambo tu la kuwakemea au kuwaamuru wazao wao. Baba na mama wahitaji pia kusikiliza, na kwa njia hiyo waweze vizuri zaidi kujua ni mambo gani yanayohitaji kuelezwa, kufafanuliwa, kutolewa kielezi, au kurudiwa. Katika familia moja ya Kikristo, wazazi huchochea uwasiliano wa waziwazi kwa kuwatia moyo watoto wao waulize maswali juu ya mambo ambayo hawaelewi au yanayohangaisha. Hivyo walipata kujua kwamba mwana aliye tineja aliona vigumu kuelewa kwamba Yehova hana mwanzo. Hao wazazi waliweza kutumia habari kutoka katika vichapo vya Watch Tower Society inayoonyesha kwamba wakati na anga zinakubaliwa kuwa hazina mwanzo. Hilo liliweza kutolea kielezi jambo hilo, na lilimridhisha mwana wao. Kwa hiyo chukueni wakati wa kuyajibu maswali ya watoto wenu kwa wazi na kutokana na Maandiko, mkiwasaidia waone kwamba kujifunza kuyatenda mapenzi ya Mungu kwaweza kuwa jambo lenye kuridhisha sana. Watu wa Mungu—vijana kwa wazee—wanafundishwa nini kingine leo?
Kufundishwa Kupenda na Kupiga Vita
15. Uhalisi wa upendo wetu wa kidugu huenda ukajaribiwa wakati upi?
15 Kwa kupatana na amri mpya ya Yesu, ‘tunafundishwa na Mungu kupendana.’ (1 Wathesalonike 4:9) Mambo yanapokuwa matulivu na bila matata, huenda tukahisi kwamba twawapenda ndugu zetu wote. Hata hiyo inakuwaje wakati tofauti za kibinafsi zinapotokea au tunapoudhika kwa sababu ya kile ambacho Mkristo mwingine asema au kutenda? Wakati huo ndipo uhalisi wa upendo wetu huenda ukajaribiwa. (Linganisha 2 Wakorintho 8:8.) Biblia hutufundisha tutendeje katika hali hizo? Jambo moja ni kujitahidi kuonyesha upendo kikamili zaidi. (1 Petro 4:8) Badala ya kujitafutia masilahi yetu wenyewe, kuchokozeka juu ya kasoro ndogo-ndogo, au kuweka hesabu ya ubaya fulani, twapaswa kujitahidi kuruhusu upendo ufunike wingi wa dhambi. (1 Wakorintho 13:5) Twajua hayo ni mapenzi ya Mungu, kwa maana ndivyo Neno lake hufundisha.
16. (a) Wakristo wanafundishwa kushiriki katika aina gani ya vita? (b) Tunaandaliwaje vifaa?
16 Ingawa watu wengi wasingefungamanisha upendo pamoja na vita, vita ni jambo jingine tunalofundishwa, lakini twafundishwa vita ya aina tofauti. Daudi aling’amua kumtegemea kwake Yehova ili afundishwe naye jinsi ya kupiga vita, ingawa katika wakati wake, huko kulitia ndani kupigana kihalisi dhidi ya maadui wa Israeli. (1 Samweli 17:45-51; 19:8; 1 Wafalme 5:3; Zaburi 144:1) Namna gani pigano letu leo? Silaha zetu si za kimwili. (2 Wakorintho 10:4) Pigano letu ni la kiroho, ambalo lahitaji tuandaliwe vifaa vya silaha za kiroho. (Waefeso 6:10-13) Kupitia Neno lake na watu wake waliokutanika, Yehova hutufundisha tupige vita ya kiroho yenye mafanikio.
17. (a) Ibilisi hutumia mbinu zipi ili kutugeuza upande? (b) Tuepuke nini kwa hekima?
17 Mara nyingi katika njia za udanganyifu, zenye hila, Ibilisi hutumia vishawishi vya kilimwengu, waasi-imani, na wengine waipingao kweli katika jitihada ya kutugeuza upande kwenye mambo yasiyo ya maana. (1 Timotheo 6:3-5, 11; Tito 3:9-11) Ni kana kwamba anaona hana uwezo mwingi wa kutushinda kwa shambulio la moja kwa moja, kwa hiyo anajaribu kutukwaza kwa kutufanya tudhihirishe malalamiko yetu ya kawaida na maswali-maswali ya kipumbavu, ambayo hayana thamani ya kiroho. Tukiwa wapiga-vita wenye bidii, twapaswa kuwa macho kuona hatari hizo sawa na vile tulivyo macho kuona mashambulio ya moja kwa moja.—1 Timotheo 1:3, 4.
18. Kutoishi tena kwa ajili yetu wenyewe kwahusisha nini kwa kweli?
18 Sisi hatuendelezi tamaa za wanadamu au mapenzi ya mataifa. Yehova ametufundisha kupitia kielelezo cha Yesu kwamba hatupaswi kuishi tena kwa ajili yetu wenyewe; badala ya hivyo twapaswa tuwe na mwelekeo uleule wa akilini aliokuwa nao Kristo Yesu na kuishi kwa ajili ya mapenzi ya Mungu. (2 Wakorintho 5:14, 15) Katika wakati uliopita, huenda tukawa tuliishi maisha yasiyo na kiasi kabisa, na yenye kukosa adili, tukitumia vibaya wakati wenye thamani. Karamu za ulevi na ulafi, mashindano ya kunywa, na ukosefu wa adili ni tabia zinazoutambulisha ulimwengu huu mwovu. Sasa kwa kuwa tunafundishwa kuyatenda mapenzi ya Mungu, je, hatushukuru kuwa tumetenganishwa na ulimwengu huu mfisadi? Basi acheni tupige vita kali kwa njia ya kiroho ili tuepuke kuhusika katika mazoea ya kilimwengu yenye kutia unajisi.—1 Petro 4:1-3.
Kufundishwa Tupate Kujinufaisha
19. Kufundishwa mapenzi ya Yehova kisha kuyatenda kutaongoza kwenye manufaa zipi?
19 Ni lazima kabisa tutambue kwamba kufundishwa kuyatenda mapenzi ya Yehova kwatunufaisha sana. Kwa kueleweka, hatuna budi kufanya sehemu yetu kwa kukazia uangalifu sana ili tupate kujifunza kisha kufuata mafunzo tunayopata kupitia Mwana wake na pia kupitia Neno lake na watu Wake waliokutanika. (Isaya 48:17, 18; Waebrania 2:1) Tukifanya hivyo, tutatiwa nguvu ili kusimama imara katika nyakati hizi zenye msiba na kukabiliana na dhoruba zilizo mbele. (Mathayo 7:24-27) Hata sasa, tutampendeza Mungu kwa kuyatenda mapenzi yake na tutakuwa tukihakikisha kwamba sala zetu zinajibiwa. (Yohana 9:31; 1 Yohana 3:22) Nasi tutakuwa na furaha halisi.—Yohana 13:17.
20. Ingekuwa vema kutafakari nini uonapo andiko la mwaka muda wote wa 1997?
20 Katika mwaka wa 1997, tutakuwa na fursa mara nyingi ya kusoma na kuchunguza andiko la mwaka, Zaburi 143:10: “Unifundishe kuyatenda mapenzi yako.” Tufanyapo hivyo, acheni tuzitumie baadhi ya fursa za kufikiria maandalizi ambayo Mungu ametufanyia ili tupate kufundishwa, kama yalivyoonyeshwa juu. Na acheni tutumie kutafakari kwa jinsi hii juu ya maneno hayo kuwa kichocheo cha kutenda kwa upatano na kusihi huko, tukijua kwamba ‘yeye atendaye mapenzi ya Mungu adumu hata milele.’—1 Yohana 2:17.
-