-
Matatizo Yanayowakabili WanawakeMnara wa Mlinzi—2012 | Septemba 1
-
-
Matatizo Yanayowakabili Wanawake
“Ninapoona jinsi wanawake wanavyotendewa, kwa kweli singependa kuwa mmoja wao.”—ZAHRA, MWENYE UMRI WA MIAKA 15, aliyenukuliwa katika gazeti la GEO, toleo la Kifaransa.
MANENO ya msichana huyo mdogo, yaliyo upande wa kulia, yanafunua ukweli wenye kuhuzunisha ulio ulimwenguni pote, jeuri na ubaguzi kuelekea wasichana na wanawake katika maisha yao yote. Fikiria mambo yafuatayo.
Ubaguzi wa kijinsia. Barani Asia, wazazi wengi wanapendelea wavulana kuliko wasichana. Ripoti ya mwaka wa 2011 ya Umoja wa Mataifa inakadiria kwamba katika bara hilo, karibu wanawake milioni 134 wamekufa kwa sababu ya utoaji mimba, mauaji ya watoto, na kupuuzwa.
Elimu. Ulimwenguni pote, asilimia 67 ya watu ambao hawajaenda shuleni hata kidogo au wameenda shuleni kwa miaka isiyozidi minne ni wanawake.
Kusumbuliwa kingono. Zaidi ya wanawake bilioni 2.6 wanaishi katika nchi ambazo bado hazioni ubakaji katika ndoa kuwa hatia.
Afya. Katika nchi zinazoendelea, karibu kila dakika mbili, mwanamke hufa kutokana na matatizo ya mimba au kujifungua yanayosababishwa na kukosa huduma za msingi za kitiba.
Haki za kumiliki mali. Ingawa wanawake hukuza zaidi ya nusu ya vyakula ulimwenguni, katika nchi nyingi hawana haki za kisheria za kumiliki mali au kurithi mashamba.
Kwa nini wanawake wamenyimwa haki kama hizo za kimsingi? Jamii fulani hufuata itikadi za kidini na mazoea ambayo huendeleza au hata kutetea jeuri dhidi ya wanawake. Gazeti fulani la Kifaransa lilimnukuu mwanasheria wa India Chandra Rami Chopra ambaye alisema: “Sheria zote za kidini zinapatana katika jambo hili: Zinaunga mkono ubaguzi dhidi ya wanawake.”
Je, una maoni kama hayo? Je, unafikiri Biblia inafundisha kwamba wanawake ni duni, kama vitabu vingine vingi vya kidini vinavyofundisha? Watu fulani wanafikiri kwamba baadhi ya maandiko katika Biblia yanaunga mkono jambo hilo. Lakini kwa kweli Mungu aliyetunga Biblia anawaonaje wanawake? Ingawa hili linaweza kuwa jambo lenye kuchochea sana hisia, kuchunguza kwa makini na kwa unyoofu mambo ambayo Biblia inasema kutatusaidia kupata jibu.
-
-
Je, Kweli Mungu Anawajali Wanawake?Mnara wa Mlinzi—2012 | Septemba 1
-
-
Je, Kweli Mungu Anawajali Wanawake?
“Dhambi ilianza na mwanamke, na kwa sababu ya mwanamke lazima sote tufe.”—KITABU CHA KIAPOKRIFA KINACHOITWA ECCLESIASTICUS, KARNE YA PILI K.W.K.
“Wewe ni lango la ibilisi: uliufunua ule mti uliokatazwa: wewe ndiye wa kwanza kuasi sheria za Mungu . . . Uliharibu kwa urahisi mfano wa Mungu, yaani, mwanamume.”—TERTULLIAN, KATIKA KITABU ON THE APPAREL OF WOMEN, KARNE YA PILI W.K.
MANENO hayo yaliyoandikwa kale hayapatikani katika Biblia. Kwa karne nyingi, yametumiwa kutetea ubaguzi dhidi ya wanawake. Hata leo, watu fulani wenye msimamo mkali bado wananukuu maandishi ya kidini ili kutetea ukandamizaji wa wanawake, wakidai kwamba wanawake ndio chanzo cha matatizo yanayowapata wanadamu. Je, Mungu alikusudia wanawake wadharauliwe na kutendewa vibaya na wanaume? Biblia inasema nini? Acheni tuone.
Je, wanawake wamelaaniwa na Mungu?
Hapana. Badala yake “yule nyoka wa zamani, yeye anayeitwa Ibilisi,” ndiye ‘aliyelaaniwa’ na Mungu. (Ufunuo 12:9; Mwanzo 3:14) Mungu aliposema kwamba Adamu ‘angemtawala’ mke wake, Mungu hakuwa akimruhusu mwanamume amkandamize mwanamke. (Mwanzo 3:16) Alikuwa tu akitabiri matokeo mabaya ya dhambi ambayo yangewapata wenzi wawili wa kwanza.
Hivyo, kutendwa vibaya kwa wanawake ni matokeo ya moja kwa moja ya dhambi ambayo wanadamu walirithi, bali si mapenzi ya Mungu. Biblia haiungi mkono wazo la kwamba ni lazima wanaume wawakandamize wanawake ili kulipia ile dhambi ya kwanza.—Waroma 5:12.
Je, Mungu alimuumba mwanamke akiwa duni kuliko mwanamume?
Hapana. Andiko la Mwanzo 1:27 linasema: “Mungu akamuumba mtu kwa mfano wake, kwa mfano wa Mungu alimuumba; mwanamume na mwanamke aliwaumba.” Hivyo, tangu mwanzoni, wanadamu wote—wanaume na wanawake—waliumbwa wakiwa na uwezo wa kuonyesha sifa za Mungu. Ingawa Adamu na Hawa waliumbwa kwa njia iliyotofautiana kihisia na kimwili, wote walipokea mgawo uleule na walifurahia mapendeleo yaleyale kutoka kwa Muumba wao.—Mwanzo 1:28-31.
Kabla ya kumuumba Hawa, Mungu alisema hivi: “Nitamfanyia [Adamu] msaidizi, awe kikamilisho chake.” (Mwanzo 2:18) Je, neno “kikamilisho” linamaanisha kwamba mwanamke alikuwa duni kuliko mwanaume? Hapana, kwa sababu neno hilo la Kiebrania linaweza pia kutafsiriwa kuwa “mshirika” au “msaada unaolingana na” mwanamume. Fikiria majukumu ya daktari mpasuaji na ya mtaalamu wa dawa za kupunguza maumivu wakati wa upasuaji. Je, mmoja anaweza kufanya kazi bila mwenzake? Huenda asiweze! Ingawa daktari mpasuaji ndiye hufanya upasuaji, je, yeye ni wa maana zaidi? Hatuwezi kusema hivyo. Vivyo hivyo, Mungu alimuumba mwanamume na mwanamke ili washirikiane kwa ukaribu, bali si kushindana.—Mwanzo 2:24.
Ni nini kinachoonyesha kwamba Mungu anawajali wanawake?
Huku akijua kimbele jinsi ambavyo wanaume wasio wakamilifu wangetenda, tangu zamani Mungu alionyesha kwamba alikusudia kuwalinda wanawake. Akizungumza kuhusu Sheria ya Musa ambayo ilianza kutumika katika karne ya 16 K.W.K., katika kitabu chake La Bible au féminin (Biblia Katika Jinsia ya Kike) mwandishi Laure Aynard, aliandika hivi: “Mara nyingi, agano la Sheria linawatetea wanawake linapozungumza kuwahusu.”
Kwa mfano, Sheria iliagiza Waisraeli wamheshimu baba na pia mama. (Kutoka 20:12; 21:15, 17) Vilevile, Sheria iliagiza kwamba mwanamke mwenye mimba atendewe kwa ufikirio. (Kutoka 21:22) Hata leo, ulinzi uliotolewa na sheria hizo za Mungu ni kinyume kabisa na ukosefu wa haki za kisheria ambao wanawake wengi wanakabiliana nao katika sehemu nyingi ulimwenguni. Lakini kuna mambo mengine yanayoonyesha kwamba Mungu anawajali.
Sheria Inayoonyesha Maoni ya Mungu Kuwaelekea Wanawake
Sheria ambayo Yehova Mungu aliwapa Waisraeli iliwapa wote, wanaume na wanawake, faida nyingi sana za kimwili, kiadili, na kiroho. Kama taifa hilo lingeendelea kusikiliza na kutii, lingekuwa “juu ya mataifa mengine yote ya dunia.” (Kumbukumbu la Torati 28:1, 2) Mwanamke alikuwa na daraka gani chini ya Sheria? Fikiria mambo yafuatayo.
1. Walikuwa na uhuru wa kibinafsi. Tofauti na wanawake katika mataifa mengine mengi ya zamani, wanawake Waisraeli walifurahia uhuru mwingi sana. Ingawa mume alipewa daraka la kuwa kichwa cha familia, mke, akiwa na kibali cha mume wake, ‘angefikiria shamba na kulinunua’ na ‘kupanda shamba la mizabibu.’ Ikiwa alikuwa na ujuzi wa kusokota na kufuma, angeweza hata kufanya biashara yake. (Methali 31:11, 16-19) Chini ya Sheria ya Musa, wanawake walionwa kuwa watu wenye haki za kibinafsi.
Katika Israeli la kale, wanawake walikuwa pia na uhuru wa kuwa na uhusiano wa kibinafsi pamoja na Mungu. Biblia inazungumza kumhusu Hana, ambaye alisali kwa Mungu kuhusu jambo la kibinafsi na akaweka nadhiri kisiri. (1 Samweli 1:11, 24-28) Mwanamke fulani katika jiji la Shunemu alikuwa akizungumza na nabii Elisha siku za Sabato. (2 Wafalme 4:22-25) Mungu aliwatumia wanawake, kama vile Debora na Hulda ili wamwakilishe. Inapendeza kuona kwamba wanaume wenye vyeo na makuhani walikuwa tayari kutafuta mashauri kutoka kwa wanawake hao.—Waamuzi 4:4-8; 2 Wafalme 22:14-16, 20.
2. Waliruhusiwa kupata elimu. Kwa sababu walikuwa sehemu ya agano la Sheria, wanawake walikaribishwa kusikiliza Sheria iliposomwa, na hilo liliwapa fursa za kujifunza. (Kumbukumbu la Torati 31:12; Nehemia 8:2, 8) Pia, walizoezwa kushiriki katika migawo fulani ya ibada ya hadharani. Kwa mfano, inaelekea wanawake fulani walifanya “utumishi uliopangwa” kwenye hema la kukutania, huku wengine wakishiriki katika kikundi cha waimbaji kilichokuwa pia na wanaume.—Kutoka 38:8; 1 Mambo ya Nyakati 25:5, 6.
Wanawake wengi walikuwa na ujuzi na ustadi uliohitajiwa ili kufanya biashara na kupata faida. (Methali 31:24) Kinyume na tamaduni katika mataifa mengine siku hizo, ambako baba peke yake ndiye aliyewafundisha wanawe, akina mama Waisraeli walishiriki kuwafundisha watoto wao wa kiume mpaka walipokuwa watu wazima. (Methali 31:1) Bila shaka, wanawake katika Israeli la kale walikuwa wenye elimu.
3. Walistahiwa na kuheshimiwa. Zile Amri Kumi zilisema hivi waziwazi: “Mheshimu baba yako na mama yako.” (Kutoka 20:12) Katika methali za Mfalme Solomoni mwenye hekima, tunasoma hivi: “Mwanangu, sikiliza nidhamu ya baba yako, wala usiiache sheria ya mama yako.”—Methali 1:8.
Sheria ilitia ndani maagizo mengi kuhusu jinsi watu ambao hawajaoana walipaswa kutendeana, na hivyo kuwaheshimu wanawake. (Mambo ya Walawi 18:6, 9; Kumbukumbu la Torati 22:25, 26) Mume mzuri alipaswa kufikiria uwezo wa kimwili na kimaumbile wa mke wake.—Mambo ya Walawi 18:19.
4. Haki ya kulindwa. Katika Neno lake, Yehova anajirejelea kuwa “baba ya wavulana wasio na baba na mwamuzi wa wajane.” Kwa maneno mengine, alikuwa Mlinzi wa wale ambao haki zao hazikulindwa na baba au mume. (Zaburi 68:5; Kumbukumbu la Torati 10:17, 18) Hivyo, pindi moja mjane fulani wa nabii alipotendewa isivyo haki na mkopeshaji, Yehova aliingilia kati na kufanya muujiza ili yule mjane alipe deni lake na kudumisha heshima yake.—2 Wafalme 4:1-7.
Kabla ya Waisraeli kuingia katika ile Nchi ya Ahadi, kichwa cha familia aliyeitwa Selofehadi alikufa bila kuacha mwana. Hivyo, binti zake watano wakamwomba Musa awape “miliki” katika Nchi ya Ahadi. Yehova alifanya mengi zaidi ya yale waliyoomba. Alimwambia hivi Musa: “Wape miliki ya urithi katikati ya ndugu za baba yao, nawe utaupitisha urithi wa baba yao kwao.” Tangu wakati huo na kuendelea, wanawake katika Israeli wangepewa urithi na baba zao na wangewaachia watoto wao urithi huo.—Hesabu 27:1-8.
Maoni ya Mungu Kuhusu Wanawake Yapotoshwa
Chini ya Sheria ya Musa, wanawake walitendewa kwa heshima na haki zao ziliheshimiwa. Hata hivyo, kuanzia karne ya nne K.W.K., dini ya Kiyahudi ilianza kuiga tamaduni za Wagiriki, ambao waliwaona wanawake kuwa duni.—Ona sanduku lenye kichwa “Ubaguzi Dhidi ya Wanawake Katika Maandishi ya Kale.”
Kwa mfano, mtunga-mashairi Mgiriki Hesiod (aliyeishi karne ya nane K.W.K.) aliwalaumu wanawake kwa sababu ya matatizo yote yanayowapata wanadamu. Katika shairi lake linaloitwa Theogony, alizungumza kuhusu “jamii na kabila hatari la wanawake ambao wanaishi katikati ya wanaume na kuwasababishia matatizo mengi.” Wazo hilo liliingizwa katika dini ya Kiyahudi mwanzoni mwa karne ya pili K.W.K. Talmud, ambayo ilianza kuandikwa katika karne ya pili W.K. na kuendelea, iliwaonya wanaume hivi: “Msizungumze sana na wanawake, kwa sababu hilo litawaingiza katika upotovu wa maadili.”
Kwa karne nyingi, maoni hayo yaliyopotoka yameathiri sana daraka la wanawake katika jamii ya Wayahudi. Katika siku za Yesu, tayari wanawake walikuwa wamewekewa mipaka kwenye eneo la hekalu na waliruhusiwa tu kuingia kwenye Ua wa Wanawake. Wanaume tu ndio waliopokea elimu ya kidini, na inaelekea wanawake walitengwa na wanaume kwenye masinagogi. Talmud inanukuu maneno haya ya Rabi mmoja: “Yeyote anayemfundisha binti yake Torati [Sheria] anamfundisha mambo machafu.” Kwa kupotosha maoni ya Mungu, viongozi wa kidini Wayahudi waliwafanya wanaume wengi wawadharau wanawake.
Alipokuwa duniani, Yesu aliona ubaguzi kama huo ambao ulikuwa umekita mizizi katika mapokeo. (Mathayo 15:6, 9; 26:7-11) Je, Yesu alifuata mapokeo hayo alipokuwa akishughulika na wanawake? Tunaweza kujifunza nini kutokana na tabia na mtazamo wake? Je, Ukristo wa kweli umewaletea wanawake kitulizo? Makala inayofuata itajibu maswali hayo.
-
-
Heshima na Staha Chini ya Utunzaji wa MunguMnara wa Mlinzi—2012 | Septemba 1
-
-
Heshima na Staha Chini ya Utunzaji wa Mungu
ALIPOKUWA duniani, Yesu alionyesha kwa ukamili utu wa Baba yake na njia yake ya kufanya mambo. Alisema hivi: “Sifanyi jambo lolote kwa uamuzi wangu mwenyewe; bali kama vile Baba alivyonifundisha, ndivyo ninavyosema . . . sikuzote mimi hufanya mambo yanayompendeza.” (Yohana 8:28, 29; Wakolosai 1:15) Hivyo, kwa kuchunguza jinsi Yesu alivyowatendea wanawake na mtazamo wake kuwaelekea, tunaweza kuelewa maoni ya Mungu kuwahusu na mambo anayotazamia wafanye.
Kulingana na mambo yaliyoandikwa katika masimulizi ya Injili, wasomi fulani wamekubali kwamba maoni ya Yesu kuwaelekea wanawake yalikuwa tofauti sana na maoni ya watu wengi. Jinsi gani? Na jambo la muhimu zaidi ni, je, mafundisho yake bado yanawapa wanawake uhuru leo?
Jinsi Yesu Alivyowatendea Wanawake
Yesu hakuwaona tu kuwa vyombo vya kutosheleza tamaa za ngono. Kulingana na viongozi fulani wa dini ya Kiyahudi, kushirikiana na watu wa jinsia tofauti kungetokeza tu tamaa zisizofaa. Kwa kuwa wanawake walionwa kuwa chanzo cha majaribu, hawakuruhusiwa kuzungumza na wanaume hadharani wala kutembea nje bila kuwa na ushungi. Kwa upande mwingine, Yesu aliwashauri wanaume wazuie tamaa zao wenyewe za kimwili na kuwatendea wanawake kwa heshima badala ya kuwatenga na watu wengine.—Mathayo 5:28.
Pia, Yesu alisema: “Yeyote anayemtaliki mke wake na kumwoa mwingine anafanya uzinzi dhidi [ya mke wake].” (Marko 10:11, 12) Hivyo, alipinga fundisho la kirabi lililofuatwa wakati huo ambalo liliwaruhusu wanaume wawataliki wake zao “kwa kila sababu.” (Mathayo 19:3, 9) Wayahudi wengi hawakuamini kwamba mtu angeweza kufanya uzinzi dhidi ya mke wake. Marabi wao walifundisha kwamba mume hangeweza kamwe kumtendea mke wake uzinzi, mwanamke tu ndiye angekosa kuwa mwaminifu! Kama vile kitabu kimoja kinachofafanua Biblia kinavyosema, “Yesu alipowawekea waume na wake matakwa yaleyale ya kimaadili, aliwastahi na kuwaheshimu wanawake.”
Matokeo ya mafundisho yake leo: Katika kutaniko la Kikristo la Mashahidi wa Yehova, wanawake hushirikiana kwa uhuru pamoja na wanaume kwenye mikutano. Hata hivyo, wanawake hawahitaji kuogopa kwamba wanaume watawaangalia na kuwatamani au kuwatongoza isivyofaa, kwa sababu wanaume Wakristo wanajitahidi kuwatendea “wanawake wazee kama mama, wanawake vijana kama dada kwa usafi wote wa kiadili.”—1 Timotheo 5:2.
Yesu alitumia muda wake kuwafundisha wanawake. Kinyume na maoni ya kirabi ya kutowaelimisha wanawake yaliyoenea sana siku hizo, Yesu aliwafundisha na kuwatia moyo wajieleze. Kwa kutomnyima Maria shangwe ya kufundishwa, Yesu alionyesha kwamba mwanamke hapaswi tu kukaa jikoni. (Luka 10:38-42) Martha dada ya Maria, alifaidika pia kutokana na mafundisho ya Yesu, kama inavyoonyeshwa na jinsi alivyomjibu Yesu kwa hekima baada ya Lazaro kufa.—Yohana 11:21-27.
Yesu alisikiliza maoni ya wanawake. Nyakati hizo, wanawake wengi Wayahudi waliamini kwamba ili mtu apate furaha alipaswa kuwa na mwana mwenye kuheshimika, ikiwezekana mwana huyo awe nabii. Mwanamke fulani aliposema hivi kwa sauti: “Lenye furaha ni tumbo la uzazi lililokuchukua!” Yesu alitumia nafasi hiyo kumfundisha jambo bora zaidi. (Luka 11:27, 28) Kwa kumfundisha kwamba kumtii Mungu ni jambo muhimu zaidi, Yesu alimwonyesha jambo bora kuliko daraka la kidesturi ambalo wanawake walipewa.—Yohana 8:32.
Matokeo ya mafundisho yake leo: Walimu katika kutaniko la Kikristo leo huwakaribisha wanawake watoe maelezo kwenye mikutano ya kutaniko. Wanawaheshimu wanawake wakomavu kwa kuwa “walimu wa yaliyo mema,” faraghani na kwa kuweka mfano mzuri. (Tito 2:3) Pia, wanawategemea wanawake hao katika kutangaza hadharani habari njema kuhusu Ufalme wa Mungu.—Zaburi 68:11; ona sanduku “Je, Mtume Paulo Aliwakataza Wanawake Kuzungumza?” kwenye ukurasa wa 9.
Yesu aliwajali wanawake. Katika nyakati za Biblia, wasichana hawakuthaminiwa sana kama wavulana. Talmud inaonyesha jambo hilo inaposema hivi: “Mwenye furaha ni mtu ambaye watoto wake ni wavulana, na ole kwake yule ambaye watoto wake ni wasichana.” Wazazi fulani walimwona msichana kuwa mzigo mkubwa sana, walilazimika kumtafutia mwenzi na kumlipia mahari, na hawangemtegemea awasaidie walipozeeka.
Yesu alionyesha kwamba uhai wa msichana mdogo ni muhimu kama vile tu uhai wa mvulana, alipomfufua binti ya Yairo, kama tu alivyomfufua mwana wa yule mjane wa Naini. (Marko 5:35, 41, 42; Luka 7:11-15) Baada ya kumponya mwanamke aliyekuwa akisumbuliwa na “roho ya udhaifu kwa miaka kumi na minane,” Yesu alimwita “binti ya Abrahamu,” usemi ambao inaelekea haukuwepo katika maandishi ya Kiyahudi. (Luka 13:10-16) Kwa kutumia usemi huo wenye kuheshimika na wa fadhili, hakumwona tu kuwa mshiriki kamili wa jamii, bali pia alitambua imani yake kubwa.—Luka 19:9; Wagalatia 3:7.
Matokeo ya mafundisho yake leo: Msemo fulani wa huko Asia unasema hivi: “Kumlea binti ni kama kunyunyizia maji shamba la jirani.” Badala ya kuongozwa na mawazo kama hayo, kwa upendo akina baba Wakristo wanawatunza vizuri watoto wao wote, wa kiume na pia wa kike. Wazazi Wakristo wanahakikisha kwamba watoto wao wote wanapokea matibabu na elimu nzuri.
Yesu aliwaamini wanawake. Katika mahakama za Kiyahudi, ushahidi wa mwanamke ulionwa kuwa sawa na wa mtumwa. Yosefo, mwanahistoria wa karne ya kwanza alitoa ushauri huu: “Ushahidi wowote kutoka kwa mwanamke usikubaliwe, kwa sababu ya mwelekeo wao wa kutochukua mambo kwa uzito na ujasiri wao wa kike.”
Kinyume na hilo, Yesu aliwachagua wanawake watoe ushahidi kuhusu ufufuo wake. (Mathayo 28:1, 8-10) Ingawa wanawake hao waaminifu walijionea Bwana wao akiuawa na kuzikwa, ilikuwa vigumu kwa mitume kuamini maneno ya wanawake hao. (Mathayo 27:55, 56, 61; Luka 24:10, 11) Hata hivyo, kwa kuwatokea kwanza wanawake, Kristo aliyefufuliwa alionyesha kwamba walistahili kutoa ushahidi kama vile tu wanafunzi wake wengine walivyostahili.—Matendo 1:8, 14.
Matokeo ya mafundisho yake leo: Katika kutaniko la Mashahidi wa Yehova, wanaume wenye madaraka wanaonyesha kwamba wanawajali wanawake kwa kusikiliza maoni yao. Nao waume Wakristo ‘wanawapa heshima’ wake zao kwa kuwasikiliza kwa makini.—1 Petro 3:7; Mwanzo 21:12.
Kanuni za Biblia Huchangia Wanawake Kuwa na Furaha
Wanaume wanapomwiga Kristo, wanawake wanaheshimiwa na kupewa uhuru ambao Mungu alikusudia wawe nao mwanzoni. (Mwanzo 1:27, 28) Badala ya kuunga mkono tabia ya wanaume kuwadharau wanawake, waume Wakristo wanaruhusu waongozwe na kanuni za Biblia, na hivyo kuwaletea wake zao furaha.—Waefeso 5:28, 29.
Yelena alipoanza kujifunza Biblia, alikuwa akiumia kimyakimya kwa sababu ya kutendewa kikatili na mumewe. Mume huyo alikuwa amelelewa katika jamii yenye jeuri ambako ilikuwa jambo la kawaida kwa mtu kumteka nyara msichana ili awe mke wake na kumtendea vibaya. “Mambo niliyojifunza katika Biblia yalinitia nguvu,” anasema Yelena. “Nilielewa kwamba kuna mtu aliyenipenda sana na ambaye alinithamini na kunijali. Pia, nilielewa kwamba ikiwa mume wangu angejifunza Biblia, angebadili mtazamo wake kunielekea.” Mwishowe, matumaini yake yalitimia mume wake alipokubali kujifunza Biblia na akabatizwa na kuwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova. “Mume wangu akawa mfano mzuri wa kujizuia,” asema Yelena. “Tulijifunza kusameheana kwa hiari.” Yelena alifikia mkataa gani? “Kwa kweli kanuni za Biblia zimenisaidia nijihisi ninahitajiwa na kwamba niko salama katika ndoa yangu.”—Wakolosai 3:13, 18, 19.
Si Yelena tu aliyejionea jambo hilo. Mamilioni ya wanawake Wakristo wana furaha kwa sababu wao na waume zao wanajitahidi kufuata kanuni za Biblia katika ndoa zao. Wanaheshimiwa, wanafarijiwa, na kupata uhuru wanaposhirikiana na Wakristo wenzao.—Yohana 13:34, 35.
Wanaume na wanawake Wakristo wanatambua kwamba wakiwa wanadamu wenye dhambi na wasio wakamilifu, wao ni sehemu ya uumbaji wa Mungu ambao ‘umetiishwa chini ya ubatili.’ Hata hivyo, kwa kuwa na uhusiano wa karibu na Baba na Mungu wao mwenye upendo, Yehova, wanatumaini la ‘kuwekwa huru kutoka katika utumwa wa uharibifu’ na kufurahia “uhuru wenye utukufu wa watoto wa Mungu.” Ni tumaini zuri kama nini kwa wanaume na wanawake chini ya utunzaji wa Mungu!—Waroma 8:20, 21.
-