Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Wanawake Walioufurahisha Moyo wa Yehova
    Mnara wa Mlinzi—2003 | Novemba 1
    • Wanawake Walioufurahisha Moyo wa Yehova

      “Yehova na akupe thawabu kwa sababu ya jinsi unavyotenda, na upate malipo kamili kutoka kwa Yehova.”—RUTHU 2:12.

      1, 2. Tunaweza kunufaikaje kwa kutafakari mifano ya wanawake wanaotajwa katika Biblia ambao waliufurahisha moyo wa Yehova?

      KUMWOGOPA Mungu kuliwachochea wanawake wawili wakatae kumtii Farao. Imani ilimchochea kahaba fulani kuhatarisha maisha yake ili awalinde wapelelezi wawili Waisraeli. Busara na unyenyekevu zilimsaidia mwanamke mmoja wakati wa matatizo kuokoa maisha ya watu wengi na kumzuia mtiwa-mafuta wa Yehova asiwe na hatia ya damu. Imani katika Yehova Mungu pamoja na roho ya ukaribishaji-wageni zilimchochea mama fulani aliyekuwa mjane kumpa nabii wa Mungu chakula alichokuwa amebakisha. Hiyo ni baadhi tu ya mifano mingi katika Biblia kuhusu wanawake walioufurahisha moyo wa Yehova.

      2 Mtazamo wa Yehova kuelekea wanawake hao na baraka alizowapa huonyesha kwamba yeye hufurahishwa sana na sifa za kiroho ambazo ni muhimu zaidi kuliko jinsia ya mtu. Si rahisi watu kutanguliza hali yao ya kiroho kwa sababu ulimwengu wa leo unajishughulisha zaidi na mambo ya kimwili. Lakini inawezekana kufanya hivyo, kama inavyoonyesha na mamilioni ya wanawake wanaomwogopa Mungu ambao ni sehemu kubwa ya watu wa Mungu leo. Wanawake hao Wakristo huiga imani, busara, ukaribishaji-wageni, na sifa nyingine nzuri zilizoonyeshwa na wanawake wanaomwogopa Mungu ambao wanatajwa katika Biblia. Bila shaka, wanaume Wakristo pia wangependa kuiga sifa zilizoonyeshwa na wanawake hao wa kale ambao ni vielelezo vizuri. Ili tuone jinsi tunavyoweza kufanya hivyo kwa ukamili zaidi, acheni tuchunguze kwa undani masimulizi ya Biblia kuhusu wanawake ambao wametajwa katika fungu la kwanza.—Waroma 15:4; Yakobo 4:8.

      Wanawake Waliokataa Kumtii Farao

      3, 4. (a) Kwa nini Shifra na Pua walikataa kumtii Farao alipowaagiza waue kila mtoto wa kiume Mwisraeli? (b) Yehova aliwabarikije wazalishaji wawili kwa sababu ya ujasiri na woga wao wa kimungu?

      3 Katika kesi zilizofanywa huko Nuremberg, Ujerumani baada ya Vita vya Pili vya Ulimwengu, wengi waliopatikana na hatia ya kuua watu wengi walijaribu kujitetea kwa kudai kwamba walifanya hivyo kwa kutii amri tu. Sasa walinganishe watu hao na wazalishaji wawili Waisraeli, Shifra na Pua, walioishi katika Misri ya kale wakati wa utawala wa Farao mmoja mkatili asiyetajwa jina. Akiogopa ongezeko la haraka la idadi ya Waebrania, Farao huyo aliwaamuru wazalishaji hao wahakikishe kwamba wamemwua kila mtoto wa kiume Mwebrania. Wanawake hao waliitikiaje amri hiyo ya kikatili? “Hawakufanya kama vile mfalme wa Misri alivyokuwa amewaambia, bali walikuwa wakiwahifadhi hai watoto wa kiume.” Kwa nini wanawake hao hawakumwogopa mwanadamu? Kwa sababu “walimwogopa Mungu wa kweli.”—Kutoka 1:15, 17; Mwanzo 9:6.

      4 Naam, wazalishaji hao walimfanya Yehova kuwa kimbilio lao, naye akawa “ngao” yao na kuwalinda na hasira ya Farao. (2 Samweli 22:31; Kutoka 1:18-20) Lakini Yehova aliwabariki hata zaidi. Aliwabariki Shifra na Pua kuwa na familia zao wenyewe. Hata aliwaheshimu wanawake hao kwa kufanya majina na matendo yao yaandikwe katika Neno lake lililoongozwa kwa roho ili yasomwe na vizazi vya baadaye, lakini jina la Farao huyo halikumbukwi hata kidogo.—Kutoka 1:21; 1 Samweli 2:30b; Methali 10:7.

      5. Leo wanawake wengi Wakristo huonyeshaje mtazamo kama wa Shifra na Pua, naye Yehova atawabarikije?

      5 Je, leo kuna wanawake walio kama Shifra na Pua? Bila shaka! Kila mwaka, wanawake wengi kama Shifra na Pua huhubiri kwa ujasiri ujumbe wa Biblia unaookoa uhai katika nchi ambako “agizo la mfalme” linakataza kazi hiyo, na hivyo kuhatarisha uhuru wao au hata maisha yao. (Waebrania 11:23; Matendo 5:28, 29) Kwa kuchochewa na upendo kwa Mungu na jirani, wanawake hao wajasiri hawamruhusu yeyote awazuie kuhubiri habari njema za Ufalme wa Mungu. Kwa sababu hiyo, wanawake wengi Wakristo hukabili upinzani na mateso. (Marko 12:30, 31; 13:9-13) Kama vile Yehova alivyoona matendo ya Shifra na Pua, yeye anafahamu kabisa matendo ya wanawake hao wazuri na wajasiri, naye ataonyesha upendo wake kwao kwa kuhifadhi majina yao katika ‘kitabu chake cha uzima,’ ikiwa watavumilia kwa uaminifu mpaka mwisho.—Wafilipi 4:3; Mathayo 24:13.

      Aliyekuwa Kahaba Aufurahisha Moyo wa Yehova

      6, 7. (a) Ni habari gani ambazo Rahabu alijua kumhusu Yehova na watu wake, nazo zilimwathirije? (b) Rahabu anaheshimiwaje katika Neno la Mungu?

      6 Katika mwaka wa 1473 K.W.K., kahaba mmoja aitwaye Rahabu aliishi katika jiji la Kanaani la Yeriko. Yaonekana kwamba Rahabu alikuwa mwanamke aliyejua habari nyingi kuhusu matukio ya wakati huo. Wakati wapelelezi wawili Waisraeli walipokimbilia nyumbani kwake, aliweza kuwasimulia mambo hususa kuhusu jinsi Waisraeli walivyotoka Misri kimuujiza, ingawa jambo hilo lilikuwa limetukia miaka 40 mapema! Pia alifahamu ushindi wa karibuni zaidi wa Waisraeli juu ya Wafalme Waamori, Sihoni na Ogu. Ona jinsi alivyoathiriwa na habari hizo. Aliwaambia hivi wapelelezi hao: “Najua hakika ya kwamba Yehova atawapa nchi hii, . . . kwa kuwa Yehova Mungu wenu ni Mungu juu mbinguni na chini duniani.” (Yoshua 2:1, 9-11) Naam, mambo ambayo Rahabu alijifunza kumhusu Yehova na matendo yake kwa niaba ya Waisraeli yalimgusa moyo na kumfanya amwamini.—Waroma 10:10.

      7 Imani ya Rahabu ilimchochea kutenda. Aliwakaribisha wapelelezi Waisraeli “kwa njia ya amani,” naye alitii maagizo yao yenye kuokoa uhai wakati Waisraeli waliposhambulia Yeriko. (Waebrania 11:31; Yoshua 2:18-21) Hapana shaka kwamba matendo ya imani ya Rahabu yaliufurahisha moyo wa Yehova, kwa kuwa Yehova alimwongoza kwa roho mwanafunzi Mkristo Yakobo aandike jina la Rahabu pamoja na lile la Abrahamu rafiki ya Mungu, ili kuwa mfano wa kuigwa na Wakristo. Yakobo aliandika: “Vivyo hivyo, je, Rahabu yule kahaba hakutangazwa pia kuwa mwadilifu kwa matendo, baada ya kuwakaribisha wale wajumbe na kuwatoa nje kwa njia nyingine?”—Yakobo 2:25.

      8. Yehova alimbarikije Rahabu kwa ajili ya imani na utii wake?

      8 Yehova alimbariki Rahabu katika njia mbalimbali. Kwanza, aliokoa kimuujiza uhai wake pamoja na wa wale waliokimbilia nyumbani kwake, yaani, “nyumba ya baba yake na wote waliokuwa wake.” Kisha akawaruhusu watu hao waishi “katikati ya Israeli,” ambako walipaswa kutendewa kama wenyeji. (Yoshua 2:13; 6:22-25; Mambo ya Walawi 19:33, 34) Na si hayo tu. Yehova pia alimpa Rahabu pendeleo la kuwa nyanya wa Yesu Kristo. Huo ni wonyesho mkubwa sana wa fadhili zenye upendo kwa mwanamke Mkanaani ambaye wakati mmoja alikuwa mwabudu wa sanamu.a—Zaburi 130:3, 4.

      9. Mtazamo wa Yehova kuelekea Rahabu na wanawake fulani Wakristo wa karne ya kwanza unawezaje kuwatia moyo baadhi ya wanawake leo?

      9 Kama Rahabu, wanawake fulani Wakristo, kuanzia karne ya kwanza mpaka leo, wameacha maisha yasiyo ya adili ili kumpendeza Mungu. (1 Wakorintho 6:9-11) Bila shaka, baadhi yao walikulia katika mazingira yanayofanana na ya Wakanaani, ambapo ukosefu wa maadili ulikuwa umeenea sana na hata kuonwa kuwa jambo la kawaida. Hata hivyo, walibadili maisha yao kwa kuchochewa na imani inayotegemea ujuzi sahihi wa Maandiko. (Waroma 10:17) Hivyo, tunaweza pia kusema kuhusu wanawake hao kwamba “Mungu haoni aibu juu yao, kuitwa akiwa Mungu wao.” (Waebrania 11:16) Hiyo ni heshima iliyoje!

      Abarikiwa kwa Busara Yake

      10, 11. Ni hali gani zinazohusu Nabali na Daudi ambazo zilimchochea Abigaili kutenda?

      10 Wanawake wengi waaminifu wa kale walionyesha busara kwa njia ya kipekee na hivyo wakawa wenye thamani sana kwa watu wa Yehova. Mmojawapo wa wanawake hao ni Abigaili, mke wa Nabali, Mwisraeli tajiri mwenye mashamba. Kwa sababu ya busara yake, Abigaili aliokoa maisha ya watu na kumzuia Daudi, ambaye angekuwa mfalme wa Israeli, asiwe na hatia ya damu. Tunaweza kusoma kumhusu Abigaili katika 1 Samweli sura ya 25.

      11 Masimulizi hayo yanaanza kwa kumtaja Daudi na wafuasi wake ambao wamepiga kambi karibu na makundi ya Nabali, ambayo wanalinda mchana na usiku bila malipo kwa sababu ya fadhili yao kwa Nabali, Mwisraeli mwenzao. Vyakula vya Daudi na watu wake vinapoanza kupungua, anawatuma vijana kumi kwenda kwa Nabali wakamwombe chakula. Sasa Nabali ana nafasi ya kumshukuru na kumwonyesha Daudi heshima akiwa mtiwa-mafuta wa Yehova. Lakini Nabali hafanyi hivyo. Kwa hasira kali, Nabali anamtukana Daudi na kuwafukuza wanaume hao mikono mitupu. Daudi anaposikia hayo, anakusanya wanaume 400 wenye silaha na kuondoka kwenda kulipiza kisasi. Abigaili anapata kujua jinsi ambavyo mume wake ametenda kwa ukali naye anachukua hatua ya haraka na ya busara ya kumpelekea Daudi vyakula vingi ili kumtuliza. Kisha yeye mwenyewe anaenda kukutana na Daudi.—Mstari wa 2-20.

      12, 13. (a) Abigaili alionyeshaje kuwa mwenye busara na pia mshikamanifu kwa Yehova na mtiwa-mafuta wake? (b) Abigaili alifanya nini aliporudi nyumbani, na ikawaje kwake?

      12 Abigaili anapokutana na Daudi, anamsihi kwa unyenyekevu amhurumie, jambo linaloonyesha kwamba anamheshimu sana mtiwa-mafuta wa Yehova. Anasema, “Bila shaka Yehova atamfanyia bwana wangu nyumba inayodumu, kwa maana bwana wangu anapigana vita vya Yehova.” Kisha anaongeza kusema kwamba Yehova atamfanya Daudi kuwa kiongozi wa Israeli. (Mstari 28-30) Wakati huohuo, Abigaili anaonyesha ujasiri mwingi anapomwambia Daudi kwamba asipojizuia kulipiza kisasi atakuwa na hatia ya damu. (Mstari 26, 31) Sifa za Abigaili za unyenyekevu, heshima nyingi, na uwezo wa kufikiri vizuri zinafanya Daudi arudiwe na fahamu zake. Anasema: “Abarikiwe Yehova Mungu wa Israeli, aliyekutuma leo unipokee! Busara yako na ibarikiwe, nawe ubarikiwe, ambaye umenizuia leo nisiingie katika hatia ya damu.”—Mstari wa 32, 33.

      13 Anaporudi nyumbani, kwa ujasiri Abigaili anataka kumweleza mume wake kuhusu zawadi aliyompa Daudi. Lakini anapompata, Nabali “amelewa kabisa.” Kwa hiyo, anangoja hadi Nabali anapotokwa na ulevi na kumwambia. Nabali anafanyaje? Anashtuka sana hivi kwamba anapatwa na aina fulani ya ugonjwa wa kupooza. Siku kumi baadaye, anakufa mkononi mwa Mungu. Daudi anaposikia kwamba Nabali amekufa, anamuuliza Abigaili kama atakubali kuwa mke wake. Bila shaka, Daudi anampenda na kumheshimu Abigaili sana naye anakubali kuolewa na Daudi.—Mstari wa 34-42.

      Je, Unaweza Kuwa Kama Abigaili?

      14. Ni sifa gani za Abigaili ambazo tungependa kuzisitawisha kwa kadiri kubwa zaidi?

      14 Je, unaona sifa fulani za Abigaili ambazo wewe—uwe mwanamke au mwanamume—ungependa kusitawisha kwa kadiri kubwa zaidi? Labda ungependa kutenda kwa hekima na busara zaidi matatizo yanapotokea. Au huenda ungependa kuzungumza kwa utulivu na kwa njia inayofaa wakati hisia za wengine zinapopanda. Ikiwa ndivyo, basi sali kwa Yehova kuhusu jambo hilo. Yeye anaahidi kuwapa hekima, utambuzi, na uwezo wa kufikiri wote ambao ‘wanaendelea kuomba kwa imani.’—Yakobo 1:5, 6; Methali 2:1-6, 10, 11.

      15. Ni chini ya hali gani inakuwa muhimu hasa kwa wanawake Wakristo kuonyesha sifa kama zile zilizoonyeshwa na Abigaili?

      15 Sifa hizo ni muhimu hasa kwa mwanamke aliye na mume asiyeamini ambaye hajali sana au hajali kabisa kanuni za Biblia. Labda anakunywa kupita kiasi. Tunatumaini kwamba wanaume hao watabadili mwenendo wao. Wengi wamefanya hivyo, mara nyingi kwa sababu ya kuona upole, heshima nyingi, na mwenendo safi kiadili wa wake zao.—1 Petro 3:1, 2, 4.

      16. Hata hali ziweje nyumbani, dada Mkristo angeonyeshaje kwamba anathamini uhusiano wake na Yehova kuliko kitu kingine chochote?

      16 Hata uwe unalazimika kuvumilia magumu ya aina gani nyumbani, kumbuka kwamba sikuzote Yehova yuko tayari kukusaidia. (1 Petro 3:12) Kwa hiyo, jitahidi kujiimarisha kiroho. Sali upate hekima na moyo mtulivu. Naam, mkaribie Yehova kupitia funzo la Biblia la ukawaida, sala, kutafakari, na kushirikiana na Wakristo wenzako. Upendo wa Abigaili kwa Mungu na mtazamo wake kuelekea mtumishi wake aliyetiwa mafuta hazikuathiriwa na maoni yasiyo ya kiroho ya mume wake. Alitenda kupatana na kanuni za uadilifu. Hata katika familia ambapo mume ni mtumishi wa Mungu mwenye mfano mzuri, mke Mkristo anatambua kwamba anahitaji kujitahidi kuimarisha na kudumisha hali yake mwenyewe ya kiroho. Ni kweli kwamba mume wake ana daraka la Kimaandiko kumtunza kiroho na kimwili, lakini ni lazima mke afanyie kazi ‘wokovu wake mwenyewe kwa kuogopa na kutetemeka.’—Wafilipi 2:12; 1 Timotheo 5:8.

      Alipata “Thawabu ya Nabii”

      17, 18. (a) Mjane wa Sarefathi alikabili jaribu gani la imani lisilo la kawaida? (b) Mjane huyo alifanyaje kuhusiana na ombi la Eliya, naye Yehova alimpa thawabu gani?

      17 Jinsi Yehova alivyomtunza mjane maskini wakati wa nabii Eliya huonyesha kwamba anawathamini sana wale ambao hutegemeza ibada ya kweli kwa kujitoa wenyewe na mali zao. Kwa sababu ya ukame ulioendelea kwa muda mrefu wakati wa Eliya, watu wengi walikabiliwa na njaa, kutia ndani mjane fulani na mwanawe mchanga walioishi Sarefathi. Walipokuwa karibu kula chakula chao cha mwisho, mgeni alifika, ambaye alikuwa nabii Eliya. Aliomba afanyiwe jambo lisilokuwa la kawaida kabisa. Ingawa alijua hali mbaya ya mwanamke huyo, alimwomba amwokee “keki ndogo ya mviringo” akitumia mafuta na unga uliokuwa umebaki. Lakini akaongeza kusema: “Kwa maana Yehova Mungu wa Israeli, amesema hivi, ‘Ule mtungi mkubwa wa unga hautamalizika, na ule mtungi mdogo wa mafuta hautapungua mpaka siku Yehova atakapoleta mvua juu ya uso wa nchi.’”—1 Wafalme 17:8-14.

      18 Wewe ungetendaje kuhusiana na ombi hilo lisilo la kawaida? Yaonekana mjane wa Sarefathi alitambua kwamba Eliya alikuwa nabii wa Yehova, hivyo ‘akafanya kulingana na neno la Eliya.’ Yehova alitendaje kuhusiana na tendo lake la ukaribishaji-wageni? Aliandaa chakula kimuujiza kwa ajili ya mwanamke huyo, mwana wake, na Eliya wakati huo wa ukame. (1 Wafalme 17:15, 16) Naam, Yehova alimpa mjane wa Sarefathi “thawabu ya nabii,” hata ingawa hakuwa Mwisraeli. (Mathayo 10:41) Mwana wa Mungu pia alimsifu mjane huyo alipotaja mfano wake kwa watu wasio na imani wa mji wa nyumbani kwao, Nazareti.—Luka 4:24-26.

      19. Leo wanawake wengi Wakristo huonyeshaje roho ya mjane wa Sarefathi, naye Yehova huhisije kuwahusu?

      19 Leo, wanawake wengi Wakristo huonyesha roho ya mjane wa Sarefathi. Kwa mfano, kila juma, dada Wakristo wasio na ubinafsi—ambao wengi wao ni maskini na wana familia za kutunza—huwakaribisha waangalizi wasafirio na wake zao. Wengine huwakaribisha wahudumu wa wakati wote wa kwao wale chakula pamoja nao, husaidia wenye uhitaji, au kwa njia nyingine kujitoa wenyewe na mali zao kutegemeza kazi ya Ufalme. (Luka 21:4) Je, Yehova huona dhabihu hizo? Bila shaka! “Mungu hakosi kuwa mwadilifu hivi kwamba asahau kazi yenu na upendo mlioonyesha kwa ajili ya jina lake, kwa kuwa mmewahudumia watakatifu nanyi mnaendelea kuhudumu.”—Waebrania 6:10.

      20. Ni nini kitakachozungumziwa katika makala inayofuata?

      20 Katika karne ya kwanza wanawake kadhaa waliomwogopa Mungu walikuwa na pendeleo la kumhudumia Yesu na mitume wake. Katika makala inayofuata, tutazungumzia jinsi wanawake hao walivyoufurahisha moyo wa Yehova, na tutachunguza mfano ambao umewekwa na wanawake wa siku hizi wanaomtumikia Yehova kwa moyo wote, hata katika hali ngumu.

      [Maelezo ya Chini]

      a Ukoo wa Yesu ulioandikwa na Mathayo hutaja majina ya wanawake wanne—Tamari, Rahabu, Ruthu, na Maria. Wote wanaheshimiwa sana katika Neno la Mungu.—Mathayo 1:3, 5, 16.

  • Wanawake Wakristo Waaminifu Ni Waabudu wa Mungu Wenye Thamani
    Mnara wa Mlinzi—2003 | Novemba 1
    • Wanawake Wakristo Waaminifu Ni Waabudu wa Mungu Wenye Thamani

      “Uvutio unaweza kudanganya, nayo sura yenye kupendeza inaweza kuwa ubatili; lakini mwanamke anayemwogopa Yehova ndiye anayejiletea sifa.”—METHALI 31:30.

      1. Maoni ya Yehova kuhusu urembo yanatofautianaje na ya ulimwengu?

      ULIMWENGU hukazia sana sura ya nje, hasa kuhusiana na wanawake. Hata hivyo, Yehova hupendezwa hasa na utu wa ndani, ambao unaweza kuendelea kuwa wenye kuvutia kadiri mtu anavyozeeka. (Methali 16:31) Kwa hiyo, Biblia huwahimiza hivi wanawake: “Kujipamba kwenu kusiwe kule kusuka nywele kwa nje na kule kujivika mapambo ya dhahabu au kuvaa mavazi ya nje, bali kuwe yule mtu wa siri wa moyoni katika vazi lisiloharibika la roho ya utulivu na ya upole, ambayo ni ya thamani kubwa machoni pa Mungu.”—1 Petro 3:3, 4.

      2, 3. Wanawake walichangiaje kuenezwa kwa habari njema katika karne ya kwanza, na jambo hilo lilikuwa limetabiriwaje?

      2 Roho hiyo inayostahili sifa ilionyeshwa na wanawake wengi wanaotajwa katika Biblia. Katika karne ya kwanza, baadhi ya wanawake hao walikuwa na pendeleo la kumhudumia Yesu na mitume wake. (Luka 8:1-3) Baadaye, wanawake Wakristo wakawa waeneza-injili wenye bidii; wengine wakatoa utegemezo muhimu kwa wanaume Wakristo wenye kuongoza, kutia ndani mtume Paulo; nao wengine wakaonyesha ukaribishaji-wageni wa kipekee na hata kutoa nyumba zao kwa ajili ya mikutano ya kutaniko.

      3 Maandiko yalitabiri kwamba Yehova angewatumia wanawake kwa njia kubwa sana katika kutimiza kusudi lake. Kwa mfano, andiko la Yoeli 2:28, 29 lilitabiri kwamba wanaume kwa wanawake, vijana kwa wazee, wangepokea roho takatifu na kushiriki katika kueneza habari njema ya Ufalme. Unabii huo ulianza kutimizwa siku ya Pentekoste 33 W.K. (Matendo 2:1-4, 16-18) Wanawake fulani waliotiwa mafuta kwa roho walipewa zawadi za kufanya miujiza kama vile kutoa unabii. (Matendo 21:8, 9) Kwa sababu ya bidii yao katika huduma, jeshi hilo kubwa la kiroho la dada waaminifu lilichangia kuenea haraka kwa Ukristo katika karne ya kwanza. Kwa kweli, yapata mwaka wa 60 W.K., mtume Paulo aliandika kwamba habari njema ilikuwa ‘imehubiriwa katika uumbaji wote ulio chini ya mbingu.’—Wakolosai 1:23.

      Wapongezwa kwa Ujasiri, Bidii, na Ukaribishaji-Wageni

      4. Kwa nini Paulo alikuwa na sababu nzuri ya kuwapongeza wanawake kadhaa katika kutaniko la Kikristo la karne ya kwanza?

      4 Kwa mfano, mtume Paulo alithamini huduma iliyofanywa na wanawake fulani hususa—kama vile waangalizi Wakristo leo wanavyothamini huduma inayofanywa na wanawake wenye bidii. Kati ya wanawake ambao Paulo aliwataja kwa jina ni “Trifaina na Trifosa, wanawake wanaofanya kazi kwa bidii katika Bwana” na “Persisi mpendwa wetu, kwa maana mwanamke huyo alifanya kazi nyingi katika Bwana.” (Waroma 16:12) Paulo aliandika kwamba Euodia na Sintike walikuwa ‘wamekazana pamoja naye katika habari njema.’ (Wafilipi 4:2, 3) Prisila pamoja na mume wake Akila walitumikia pia pamoja na Paulo. Prisila na Akila hata ‘walihatarisha shingo zao’ kwa ajili ya Paulo, na hivyo kumchochea kuandika: “Si mimi tu bali pia makutaniko yote ya mataifa yanawashukuru.”—Waroma 16:3, 4; Matendo 18:2.

      5, 6. Ni katika njia zipi Prisila aliwawekea dada mfano mzuri leo?

      5 Ni nini kilichofanya Prisila awe mwenye bidii na ujasiri? Tunapata dokezo fulani kwenye Matendo 18:24-26, ambapo tunasoma kwamba alimuunga mkono mume wake kumsaidia Apolo, msemaji mwenye kipawa, afahamu habari za karibuni zaidi kuhusu kweli iliyofunuliwa. Basi, ni wazi kwamba Prisila alikuwa mwanafunzi mwenye bidii wa Neno la Mungu na mafundisho ya mitume. Kwa sababu hiyo, alisitawisha sifa nzuri zilizofanya awe mwenye thamani kwa Mungu na kwa mume wake na pia awe mshiriki mwenye thamani wa kutaniko la mapema. Leo, dada wengi Wakristo wenye bidii ambao hujifunza Biblia kwa bidii na pia kula chakula cha kiroho ambacho Yehova huandaa kupitia “msimamizi-nyumba mwaminifu,” ni wenye thamani pia.—Luka 12:42.

      6 Akila na Prisila walikuwa wakaribishaji-wageni wa kipekee. Paulo alikaa nyumbani kwao alipofanya kazi pamoja nao katika biashara yao ya kutengeneza mahema huko Korintho. (Matendo 18:1-3) Wakati wenzi hao walipohamia Efeso na baadaye Roma, waliendelea kuonyesha sifa ya Kikristo ya ukaribishaji-wageni, na hata wakatoa nyumba yao itumiwe kwa ajili ya mikutano ya kutaniko. (Matendo 18:18, 19; 1 Wakorintho 16:8, 19) Vivyo hivyo, Nimfa na Maria mama ya Yohana Marko walitoa nyumba zao zitumiwe kwa ajili ya mikutano ya kutaniko.—Matendo 12:12; Wakolosai 4:15.

      Ni Wenye Thamani Sana Leo

      7, 8. Leo wanawake wengi Wakristo wana sifa gani nzuri ya utumishi mtakatifu, nao wanaweza kuwa na uhakika wa jambo gani?

      7 Kama ilivyokuwa katika karne ya kwanza, leo wanawake Wakristo waaminifu hutimiza fungu muhimu katika kutimizwa kwa kusudi la Mungu hasa katika kazi ya kueneza injili. Dada hao wana sifa nzuri kama nini! Fikiria mfano wa Gwen, ambaye alimtumikia Yehova kwa uaminifu kwa zaidi ya miaka 50 mpaka alipokufa mwaka wa 2002. Mume wake anasema, “Gwen alijulikana sana katika jiji letu kwa bidii yake ya kueneza injili. Aliwaona watu wote kuwa wanaweza kunufaika na upendo na ahadi za Yehova. Ushikamanifu wake kwa Mungu, tengenezo lake, na kwa familia yetu—pamoja na kitia-moyo chake chenye upendo wakati tulipokuwa tumeshuka moyo—ni mambo yaliyonitegemeza na kutegemeza watoto wetu sana katika kipindi tulichoishi pamoja naye ambacho kilikuwa chenye kuridhisha na kuthawabisha. Tunamkosa sana.” Gwen na mume wake walikuwa wameoana kwa miaka 61.

      8 Wanawake wengi sana Wakristo, waseja na walioolewa, wanatumikia wakiwa wahudumu mapainia na mishonari, nao huridhika na mahitaji ya lazima ya maisha wanapoeneza ujumbe wa Ufalme katika maeneo yanayotia ndani majiji yenye shughuli nyingi na pia maeneo ya mbali. (Matendo 1:8) Wengi wamejinyima kuwa na makao au watoto ili kumtumikia Yehova kwa ukamili zaidi. Kuna wale ambao huwaunga mkono kwa ushikamanifu waume zao wanaotumikia wakiwa waangalizi wasafirio, huku maelfu ya akina dada wengine wakitumika kwenye makao ya Betheli ulimwenguni pote. Bila shaka, wanawake hao wenye kujidhabihu wamo kati ya “vitu vyenye kutamanika vya mataifa yote” ambavyo vinaijaza nyumba ya Yehova utukufu.—Hagai 2:7.

      9, 10. Washiriki fulani wa familia wameonyeshaje kwamba wanathamini kielelezo kizuri kinachowekwa na wake na mama Wakristo?

      9 Bila shaka, wanawake wengi Wakristo wana madaraka ya familia; hata hivyo wanatanguliza mambo ya Ufalme. (Mathayo 6:33) Dada mmoja mseja ambaye ni painia aliandika: “Kielelezo kizuri cha mama na imani yake thabiti vilinisaidia sana kuwa painia wa kawaida. Hata alikuwa mmoja kati ya mapainia bora zaidi niliopata kushirikiana nao.” Mume mmoja anasema hivi kumhusu mke wake, mama ya binti watano ambao sasa ni watu wazima: “Nyumba yetu ilikuwa safi na nadhifu daima. Bonnie hakurundika vitu nyumbani, hivyo familia yetu iliweza kukazia fikira mambo ya kiroho. Kwa sababu alitumia pesa kwa uangalifu, niliweza kufanya kazi isiyo ya wakati wote kwa miaka 32, jambo lililonisaidia kutumia wakati mwingi zaidi pamoja na familia yetu na kushughulikia mambo ya kiroho. Mke wangu pia aliwafunza watoto umuhimu wa kuwa wenye bidii. Ninampongeza sana.” Leo, mume huyo na mke wake wanatumika kwenye makao makuu ya ulimwengu ya Mashahidi wa Yehova.

      10 Mume mmoja anaandika hivi kuhusu mke wake, aliye mama ya watoto ambao sasa ni watu wazima: “Sifa za Susan zinazonivutia zaidi ni upendo wake mwingi kwa Mungu na kwa watu, na vilevile kuelewa hali za watu, huruma, na unyofu. Sikuzote alionelea kwamba tunapaswa kumpa Yehova yaliyo bora zaidi—kanuni ambayo anaifuata akiwa mtumishi wa Mungu na pia mama.” Kwa utegemezo wa mke wake, mume huyo ameweza kukubali mapendeleo kadhaa ya kiroho kutia ndani kutumikia akiwa mzee, painia, mwangalizi wa mzunguko wa badala, na pia mshiriki wa Halmashauri ya Uhusiano na Hospitali. Wanawake hao ni wenye thamani kama nini kwa waume zao, Wakristo wenzao, na zaidi ya yote, kwa Yehova!—Methali 31:28, 30.

      Wanawake Wenye Thamani Wasio na Waume

      11. (a) Yehova ameonyeshaje kwamba anawajali wanawake waaminifu, hasa wajane? (b) Wajane Wakristo na dada wengine waaminifu wasio na mume wanaweza kuwa na uhakika gani?

      11 Mara nyingi Yehova alionyesha jinsi anavyowajali wajane. (Kumbukumbu la Torati 27:19; Zaburi 68:5; Isaya 10:1, 2) Yeye hakubadilika. Bado anawajali sana wajane, mama wasio na wenzi wa ndoa, na pia wanawake ambao wameamua kubaki waseja au wale ambao hawajapata mume Mkristo anayefaa. (Malaki 3:6; Yakobo 1:27) Ikiwa wewe ni mmoja wa wale wanaomtumikia Yehova kwa uaminifu bila utegemezo wa mwenzi Mkristo, unaweza kuwa na hakika kwamba u mwenye thamani machoni pa Mungu.

      12. (a) Dada fulani Wakristo wanaonyeshaje ushikamanifu wao kwa Yehova? (b) Baadhi ya dada zetu wanavumilia hisia za aina gani?

      12 Kwa mfano, fikiria dada zetu Wakristo ambao hawajaolewa kwa sababu wanatii kwa ushikamanifu shauri la Yehova la kuolewa “katika Bwana tu.” (1 Wakorintho 7:39; Methali 3:1) Neno la Mungu linawahakikishia hivi: ‘Kwa mtu mshikamanifu Yehova atatenda kwa ushikamanifu.’ (2 Samweli 22:26) Lakini kwa wengi wao, si rahisi kubaki waseja. Dada mmoja anasema hivi: “Niliazimia kuolewa katika Bwana tu, lakini nimelia mara nyingi ninapoona marafiki wangu wakiolewa na wanaume wazuri Wakristo huku nikibaki mseja.” Dada mwingine anasema: “Nimemtumikia Yehova kwa miaka 25. Nimeazimia kubaki mshikamanifu kwake, lakini mara nyingi mimi huhuzunika kwa sababu ya upweke.” Anaendelea kusema: “Dada kama mimi hutamani sana kutiwa moyo.” Tunaweza kuwasaidiaje dada hao washikamanifu?

      13. (a) Mfano uliowekwa na wale waliomtembelea binti Yeftha unatufunza nini? (b) Ni katika njia gani zaidi tunaweza kuonyesha kwamba tunawajali dada waseja katika kutaniko letu?

      13 Njia moja ni kwa kuiga mfano mmoja wa kale. Wakati binti ya Yeftha alipoachilia mbali nafasi yake ya kuwa na mume, watu walitambua kwamba alikuwa akijinyima. Alitiwaje moyo? “Mwaka baada ya mwaka binti za Israeli wakawa wakienda kumpongeza binti ya Yeftha Mgileadi, siku nne kwa mwaka.” (Waamuzi 11:30-40) Vivyo hivyo, tunapaswa kuwapongeza kutoka moyoni dada waseja wanaotii amri ya Mungu kwa ushikamanifu.a Ni katika njia gani nyingine tunaweza kuonyesha kwamba tunawajali? Tunapotoa sala, tunapaswa kumsihi Yehova awategemeze dada hao wapendwa na waaminifu ili waendelee kumtumikia kwa ushikamanifu. Wanapaswa kuhakikishiwa kwamba wanapendwa na kuthaminiwa sana na Yehova na kutaniko lote la Kikristo.—Zaburi 37:28.

      Wazazi Wasio na Wenzi wa Ndoa Hufanikiwaje?

      14, 15. (a) Kwa nini Wakristo ambao ni mama wasio na wenzi wa ndoa wanapaswa kumwomba Yehova awasaidie? (b) Wazazi wasio na wenzi wanawezaje kutenda kupatana na sala zao?

      14 Wanawake Wakristo ambao ni wazazi wasio na wenzi wa ndoa pia hukabili magumu mengi. Hata hivyo, wanaweza kumwomba Yehova awasaidie kulea watoto wao kupatana na kanuni za Biblia. Ni kweli kwamba ikiwa wewe ni mzazi asiye na mwenzi wa ndoa, huwezi kutimiza kabisa-kabisa daraka la baba na mama. Hata hivyo, Yehova atakusaidia kutimiza majukumu yako mengi ukimwomba msaada wake kwa imani. Kwa mfano: Wazia kwamba unabeba mzigo mzito wa viazi kutoka shambani mwako kurudi nyumbani kwako ambako ni mbali sana. Je, ungeng’ang’ana kuubeba mzigo huo peke yako iwapo rafiki yako mwenye gari kubwa angetokea na kujitolea kukusaidia? La, hungefanya hivyo! Vivyo hivyo, usijaribu kubeba mizigo ya kihisia-moyo peke yako kwa kuwa unaweza kumwomba Yehova akusaidie. Hata anakutia moyo ufanye hivyo. Andiko la Zaburi 68:19 linasema: “Na abarikiwe Yehova, ambaye hutubebea mzigo wetu kila siku.” Vivyo hivyo, andiko la 1 Petro 5:7 linakutia moyo umtupie Yehova mahangaiko yako yote ‘kwa sababu yeye anakujali wewe.’ Kwa hiyo, unapolemewa na matatizo na mahangaiko, mtupie Baba yako wa mbinguni mizigo hiyo, ukifanya hivyo “bila kuacha.”—1 Wathesalonike 5:17; Zaburi 18:6; 55:22.

      15 Kwa mfano, ikiwa wewe ni mama, bila shaka unahangaikia uvutano wa marika juu ya watoto wako shuleni au majaribu ya utimilifu ambayo huenda wakakabili. (1 Wakorintho 15:33) Hayo ni mahangaiko halali. Lakini unaweza pia kusali kuyahusu. Unaweza kusali kuhusu mambo hayo pamoja na watoto wako kabla ya kwenda shuleni, labda baada ya kuchunguza andiko la siku pamoja. Kusali kutoka moyoni na kutaja mambo hususa kunaweza kuwa na matokeo mazuri kwa watoto wako. Zaidi ya yote, Yehova atakubariki ukijitahidi kwa subira kuwafundisha watoto wako Neno lake. (Kumbukumbu la Torati 6:6, 7; Methali 22:6) Kumbuka, “macho ya Yehova yako juu ya waadilifu, na masikio yake yanaielekea dua yao.”—1 Petro 3:12; Wafilipi 4:6, 7.

      16, 17. (a) Mwana mmoja alisema nini kuhusu upendo alioonyeshwa na mama yake? (b) Mtazamo wa kiroho wa mama huyo ulikuwa na matokeo gani juu ya watoto wake?

      16 Fikiria mfano wa Olivia, mama ya watoto sita. Mume wake asiyeamini aliacha familia yake mara tu baada ya kitindamimba kuzaliwa. Lakini mara moja Olivia akachukua daraka la kuwalea watoto wake katika njia za Mungu. Mwana wa Olivia, Darren, ambaye sasa ni painia na mzee Mkristo mwenye umri wa miaka 31, alikuwa na umri wa miaka 5 hivi wakati huo. Mahangaiko ya Olivia yaliongezeka Darren aliposhikwa na ugonjwa mbaya ambao bado unamsumbua. Darren anaandika hivi anapokumbuka mambo yaliyotukia alipokuwa mtoto: “Bado ninakumbuka nikiketi juu ya kitanda changu hospitalini huku nikimsubiri Mama kwa hamu. Yeye angeketi kando yangu na kunisomea Biblia kila siku. Kisha angeimba wimbo wa Ufalme wenye kichwa ‘Asante, Yehova.’b Ningali naupenda sana wimbo huo.”

      17 Olivia alifanikiwa akiwa mama asiye na mwenzi wa ndoa kwa sababu alimtumaini na kumpenda Yehova. (Methali 3:5, 6) Mtazamo wake mzuri ulidhihirishwa katika miradi aliyowawekea watoto wake. “Sikuzote Mama alitutia moyo tufuatie mradi wa kuwa wahudumu wa wakati wote,” asema Darren. “Kwa sababu hiyo, mimi pamoja na wanne kati ya dada zangu watano ni wahudumu wa wakati wote. Hata hivyo, Mama hakuwa akijigamba kwa wengine kuhusu mafanikio hayo. Mimi hujitahidi sana kuiga sifa zake nzuri.” Ni kweli kwamba si watoto wote wanaokua na kumtumikia Mungu kama watoto wa Olivia. Lakini mama anapofanya yote awezayo kuishi kupatana na kanuni za Biblia, anaweza kuwa na hakika kwamba Yehova atamwongoza na kumsaidia kwa upendo.—Zaburi 32:8.

      18. Tunaweza kuonyeshaje kwamba tunathamini uandalizi wa Yehova wa kutaniko la Kikristo?

      18 Mungu hutoa msaada mwingi kupitia kutaniko la Kikristo lenye mpango wa kulisha watu kiroho kwa ukawaida, undugu wa Kikristo, na “zawadi katika wanadamu” ambao wamekomaa kiroho. (Waefeso 4:8) Wazee waaminifu hujitahidi kuwajenga wote kutanikoni, wakiwapa uangalifu wa kipekee “mayatima na wajane katika dhiki yao.” (Yakobo 1:27) Kwa hiyo, kaa karibu na watu wa Mungu na usijitenge kamwe.—Methali 18:1; Waroma 14:7.

      Sifa Nzuri ya Ujitiisho

      19. Kwa nini ujitiisho wa mke hauonyeshi kwamba yeye ni wa hali ya chini, na ni mfano gani katika Biblia unaounga mkono jambo hilo?

      19 Yehova alimwumba mwanamke awe kikamilisho cha mwanamume. (Mwanzo 2:18) Kwa hiyo, ujitiisho wa mke kwa mume wake hauonyeshi kwamba yeye ni wa hali ya chini. Badala yake, ujitiisho hufanya mwanamke aheshimiwe na humwezesha kutumia uwezo na vipawa vyake vingi kupatana na mapenzi ya Mungu. Methali sura ya 31 huzungumzia mambo mbalimbali ambayo mwanamke mwenye uwezo wa Israeli ya kale alifanya. Aliwasaidia wenye uhitaji, akapanda mashamba ya mizabibu, na kununua ardhi. Naam, ‘moyo wa mume wake ulimtegemea, wala hakuna faida iliyokosekana.’—Mstari wa 11, 16, 20.

      20. (a) Mwanamke Mkristo anapaswa kuonaje uwezo, au vipawa alivyopewa na Mungu? (b) Esta alionyesha sifa gani nzuri, na kwa sababu hiyo Yehova alimtumiaje?

      20 Mwanamke mwenye kiasi na anayemwogopa Mungu hajitukuzi kwa kujitakia makuu, au kushindana na mumewe. (Methali 16:18) Yeye hatafuti uradhi kwa kufuatia hasa kazi za kimwili bali yeye hutumia vipawa alivyopewa na Mungu ili kuwatumikia wengine—familia yake, Wakristo wenzake, majirani, na zaidi ya wote, Yehova. (Wagalatia 6:10; Tito 2:3-5) Fikiria mfano wa Malkia Esta katika Biblia. Ingawa alikuwa mrembo, alikuwa mwenye kiasi na mwenye kujitiisha. (Esta 2:13, 15) Alipoolewa, alimwonyesha mume wake, Mfalme Ahasuero, heshima kubwa tofauti na Vashti, mke wake wa kwanza. (Esta 1:10-12; 2:16, 17) Esta pia alikubaliana na maoni ya Mordekai, binamu yake mkubwa, kuhusu masuala yanayofaa—hata baada ya kuwa malkia. Lakini alikuwa mjasiri. Alifunua kwa ujasiri hila ya Hamani, mtu mwenye nguvu na ambaye alitaka kuwaangamiza Wayahudi. Yehova alimtumia Esta kwa njia kubwa ili kuwaokoa watu wake.—Esta 3:8-4:17; 7:1-10; 9:13.

      21. Mwanamke Mkristo anawezaje kuendelea kuwa mwenye thamani zaidi kwa Yehova?

      21 Bila shaka, zamani na hata leo, wanawake wanaomwogopa Yehova wamejitoa kikamili kwake na kwa ibada yake. Kwa hiyo, wanawake wanaomwogopa Mungu ni wenye thamani machoni pa Yehova. Dada Wakristo acheni Yehova awafinyange hatua kwa hatua kupitia roho yake ili mwendelee kuwa “chombo,” kinachopendeza zaidi “kilichotayarishwa kwa ajili ya kila kazi njema.” (2 Timotheo 2:21; Waroma 12:2) Neno la Mungu linasema hivi kuhusu waabudu hao wenye thamani: “Mpeni baadhi ya matunda ya mikono yake, nazo kazi zake na zimsifu malangoni.” (Methali 31:31) Na iwe hivyo kwa kila mmoja wenu.

      [Maelezo ya Chini]

      a Ili kujua jinsi ya kutoa pongezi hizo, ona gazeti la Mnara wa Mlinzi la Machi 15, 2002, ukurasa wa 26-28.

      b Wimbo namba 212 katika kitabu Mwimbieni Yehova Sifa, kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki