-
Wanawake Wakristo Waaminifu Ni Waabudu wa Mungu Wenye ThamaniMnara wa Mlinzi—2003 | Novemba 1
-
-
Ni Wenye Thamani Sana Leo
7, 8. Leo wanawake wengi Wakristo wana sifa gani nzuri ya utumishi mtakatifu, nao wanaweza kuwa na uhakika wa jambo gani?
7 Kama ilivyokuwa katika karne ya kwanza, leo wanawake Wakristo waaminifu hutimiza fungu muhimu katika kutimizwa kwa kusudi la Mungu hasa katika kazi ya kueneza injili. Dada hao wana sifa nzuri kama nini! Fikiria mfano wa Gwen, ambaye alimtumikia Yehova kwa uaminifu kwa zaidi ya miaka 50 mpaka alipokufa mwaka wa 2002. Mume wake anasema, “Gwen alijulikana sana katika jiji letu kwa bidii yake ya kueneza injili. Aliwaona watu wote kuwa wanaweza kunufaika na upendo na ahadi za Yehova. Ushikamanifu wake kwa Mungu, tengenezo lake, na kwa familia yetu—pamoja na kitia-moyo chake chenye upendo wakati tulipokuwa tumeshuka moyo—ni mambo yaliyonitegemeza na kutegemeza watoto wetu sana katika kipindi tulichoishi pamoja naye ambacho kilikuwa chenye kuridhisha na kuthawabisha. Tunamkosa sana.” Gwen na mume wake walikuwa wameoana kwa miaka 61.
8 Wanawake wengi sana Wakristo, waseja na walioolewa, wanatumikia wakiwa wahudumu mapainia na mishonari, nao huridhika na mahitaji ya lazima ya maisha wanapoeneza ujumbe wa Ufalme katika maeneo yanayotia ndani majiji yenye shughuli nyingi na pia maeneo ya mbali. (Matendo 1:8) Wengi wamejinyima kuwa na makao au watoto ili kumtumikia Yehova kwa ukamili zaidi. Kuna wale ambao huwaunga mkono kwa ushikamanifu waume zao wanaotumikia wakiwa waangalizi wasafirio, huku maelfu ya akina dada wengine wakitumika kwenye makao ya Betheli ulimwenguni pote. Bila shaka, wanawake hao wenye kujidhabihu wamo kati ya “vitu vyenye kutamanika vya mataifa yote” ambavyo vinaijaza nyumba ya Yehova utukufu.—Hagai 2:7.
9, 10. Washiriki fulani wa familia wameonyeshaje kwamba wanathamini kielelezo kizuri kinachowekwa na wake na mama Wakristo?
9 Bila shaka, wanawake wengi Wakristo wana madaraka ya familia; hata hivyo wanatanguliza mambo ya Ufalme. (Mathayo 6:33) Dada mmoja mseja ambaye ni painia aliandika: “Kielelezo kizuri cha mama na imani yake thabiti vilinisaidia sana kuwa painia wa kawaida. Hata alikuwa mmoja kati ya mapainia bora zaidi niliopata kushirikiana nao.” Mume mmoja anasema hivi kumhusu mke wake, mama ya binti watano ambao sasa ni watu wazima: “Nyumba yetu ilikuwa safi na nadhifu daima. Bonnie hakurundika vitu nyumbani, hivyo familia yetu iliweza kukazia fikira mambo ya kiroho. Kwa sababu alitumia pesa kwa uangalifu, niliweza kufanya kazi isiyo ya wakati wote kwa miaka 32, jambo lililonisaidia kutumia wakati mwingi zaidi pamoja na familia yetu na kushughulikia mambo ya kiroho. Mke wangu pia aliwafunza watoto umuhimu wa kuwa wenye bidii. Ninampongeza sana.” Leo, mume huyo na mke wake wanatumika kwenye makao makuu ya ulimwengu ya Mashahidi wa Yehova.
10 Mume mmoja anaandika hivi kuhusu mke wake, aliye mama ya watoto ambao sasa ni watu wazima: “Sifa za Susan zinazonivutia zaidi ni upendo wake mwingi kwa Mungu na kwa watu, na vilevile kuelewa hali za watu, huruma, na unyofu. Sikuzote alionelea kwamba tunapaswa kumpa Yehova yaliyo bora zaidi—kanuni ambayo anaifuata akiwa mtumishi wa Mungu na pia mama.” Kwa utegemezo wa mke wake, mume huyo ameweza kukubali mapendeleo kadhaa ya kiroho kutia ndani kutumikia akiwa mzee, painia, mwangalizi wa mzunguko wa badala, na pia mshiriki wa Halmashauri ya Uhusiano na Hospitali. Wanawake hao ni wenye thamani kama nini kwa waume zao, Wakristo wenzao, na zaidi ya yote, kwa Yehova!—Methali 31:28, 30.
-
-
Wanawake Wakristo Waaminifu Ni Waabudu wa Mungu Wenye ThamaniMnara wa Mlinzi—2003 | Novemba 1
-
-
12. (a) Dada fulani Wakristo wanaonyeshaje ushikamanifu wao kwa Yehova? (b) Baadhi ya dada zetu wanavumilia hisia za aina gani?
12 Kwa mfano, fikiria dada zetu Wakristo ambao hawajaolewa kwa sababu wanatii kwa ushikamanifu shauri la Yehova la kuolewa “katika Bwana tu.” (1 Wakorintho 7:39; Methali 3:1) Neno la Mungu linawahakikishia hivi: ‘Kwa mtu mshikamanifu Yehova atatenda kwa ushikamanifu.’ (2 Samweli 22:26) Lakini kwa wengi wao, si rahisi kubaki waseja. Dada mmoja anasema hivi: “Niliazimia kuolewa katika Bwana tu, lakini nimelia mara nyingi ninapoona marafiki wangu wakiolewa na wanaume wazuri Wakristo huku nikibaki mseja.” Dada mwingine anasema: “Nimemtumikia Yehova kwa miaka 25. Nimeazimia kubaki mshikamanifu kwake, lakini mara nyingi mimi huhuzunika kwa sababu ya upweke.” Anaendelea kusema: “Dada kama mimi hutamani sana kutiwa moyo.”
-
-
Wanawake Wakristo Waaminifu Ni Waabudu wa Mungu Wenye ThamaniMnara wa Mlinzi—2003 | Novemba 1
-
-
16, 17. (a) Mwana mmoja alisema nini kuhusu upendo alioonyeshwa na mama yake? (b) Mtazamo wa kiroho wa mama huyo ulikuwa na matokeo gani juu ya watoto wake?
16 Fikiria mfano wa Olivia, mama ya watoto sita. Mume wake asiyeamini aliacha familia yake mara tu baada ya kitindamimba kuzaliwa. Lakini mara moja Olivia akachukua daraka la kuwalea watoto wake katika njia za Mungu. Mwana wa Olivia, Darren, ambaye sasa ni painia na mzee Mkristo mwenye umri wa miaka 31, alikuwa na umri wa miaka 5 hivi wakati huo. Mahangaiko ya Olivia yaliongezeka Darren aliposhikwa na ugonjwa mbaya ambao bado unamsumbua. Darren anaandika hivi anapokumbuka mambo yaliyotukia alipokuwa mtoto: “Bado ninakumbuka nikiketi juu ya kitanda changu hospitalini huku nikimsubiri Mama kwa hamu. Yeye angeketi kando yangu na kunisomea Biblia kila siku. Kisha angeimba wimbo wa Ufalme wenye kichwa ‘Asante, Yehova.’b Ningali naupenda sana wimbo huo.”
17 Olivia alifanikiwa akiwa mama asiye na mwenzi wa ndoa kwa sababu alimtumaini na kumpenda Yehova. (Methali 3:5, 6) Mtazamo wake mzuri ulidhihirishwa katika miradi aliyowawekea watoto wake. “Sikuzote Mama alitutia moyo tufuatie mradi wa kuwa wahudumu wa wakati wote,” asema Darren. “Kwa sababu hiyo, mimi pamoja na wanne kati ya dada zangu watano ni wahudumu wa wakati wote. Hata hivyo, Mama hakuwa akijigamba kwa wengine kuhusu mafanikio hayo. Mimi hujitahidi sana kuiga sifa zake nzuri.” Ni kweli kwamba si watoto wote wanaokua na kumtumikia Mungu kama watoto wa Olivia. Lakini mama anapofanya yote awezayo kuishi kupatana na kanuni za Biblia, anaweza kuwa na hakika kwamba Yehova atamwongoza na kumsaidia kwa upendo.—Zaburi 32:8.
-