Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Pande Mbili za Kazi
    Mnara wa Mlinzi—2005 | Juni 15
    • Pande Mbili za Kazi

      “Kufanya kazi—kufanya kazi! Inafurahisha sana kujua kwamba bado tuna kazi ya kufanya.”—Mwandishi Katherine Mansfield, (1888-1923).

      JE, UNAKUBALIANA na maoni hayo kuhusu kazi? Unaionaje kazi? Je, wewe huona kazi kuwa jambo lisilofurahisha linalochukua muda mrefu? Au je, unapenda sana kazi yako hivi kwamba inatawala maisha yako?

      Watu wengi hutumia wakati wao mwingi wakifanya kazi. Hali yetu ya maisha na makao yetu hutegemea kazi tunayofanya. Wengi huona kwamba kazi hutawala maisha yao, tangu ujanani hadi wanapostaafu. Wengine wetu hupata uradhi mwingi sana kutokana na jasho letu. Watu wengine hukadiria ubora wa kazi kwa kuangalia mapato au umaarufu unaotokana nayo, nao wengine huona kazi kuwa jambo linalowasaidia kupisha wakati au linalopoteza wakati wao.

      Kuna wale wanaofanya kazi ili kupata riziki na kuna wale ambao kusudi lao kuu maishani ni kufanya kazi tu. Wengine hata hufa kwa sababu ya hali za kazi. Kwa mfano, ripoti moja ya hivi majuzi ya Umoja wa Mataifa ilisema kwamba kazi husababisha maumivu na kifo kwa kiwango kikubwa “kuliko vita au matumizi ya dawa za kulevya na ulevi vikijumlishwa pamoja.” Likizungumzia jambo hilo, gazeti The Guardian la London liliripoti hivi: “Kila mwaka, zaidi ya watu milioni mbili hufa kutokana na majeraha au magonjwa yanayosababishwa na kazi . . . Vumbi, kemikali, kelele na miale fulani husababisha kansa, ugonjwa wa moyo na kupooza.” Isitoshe, mambo mengine mawili ambayo hufanya kazi ichukize siku hizi ni kuwatumikisha watoto na kuwalazimisha watu kufanya kazi.

      Kwa kuongezea, kuna ule “uchovu wa kupindukia” unaotajwa na mwanasaikolojia Steven Berglas. Anataja mfanyakazi mwenye bidii ambaye, ijapokuwa amefikia kilele cha kazi yake, anahisi “woga usioisha, wasiwasi, mfadhaiko, au kushuka moyo kwa sababu anaona kwamba amenaswa na kazi yake na hawezi kujinasua wala kupata furaha yoyote kutokana nayo.”

      Tofauti Kati ya Kufanya Kazi kwa Bidii na Kufanya Kazi Kupindukia

      Katika ulimwengu ambamo watu wengi hujikakamua kufanya kazi kwa muda mrefu, ni muhimu kujua tofauti kati ya kufanya kazi kwa bidii na kufanya kazi kupindukia. Watu wengi wanaofanya kazi kupindukia huhisi kwamba kazi inawafanya kuwa salama katika ulimwengu huu hatari na wenye kubadilika-badilika, hali wale wanaofanya kazi kwa bidii huona kazi kuwa jambo la lazima au linaloleta uradhi. Wale wanaofanya kazi kupindukia hawana nafasi ya kufanya mambo mengine maishani mwao, hali wale wanaofanya kazi kwa bidii hujua wakati wa kuondoka kazini, kuelekeza fikira kwa mambo mengine, au kusimamisha kazi ili kuhudhuria tukio fulani muhimu. Watu wanaofanya kazi kupindukia huhisi vizuri na husisimuka wanapofanya hivyo, hali watu wanaofanya kazi kwa bidii hawahisi hivyo wanapofanya kazi kupita kiasi.

      Ni vigumu kutofautisha kati ya mambo hayo mawili kwa sababu siku hizi ulimwengu unawaunga mkono wale wanaofanya kazi kupindukia. Simu za mkononi na vifaa vingine huwawezesha watu kufanya kazi hata wanapokuwa nyumbani. Kwa kuwa kazi inaweza kufanyiwa mahali popote pale na wakati wowote ule, watu wengine hujiumiza kwa kufanya kazi kupindukia.

      Watu wengine hutendaje wanapoathiriwa na maoni hayo yasiyofaa kuhusu kazi? Wataalamu wa elimu ya jamii wameona kwamba watu wanaofanya kazi kupindukia au wanaokabili mkazo mwingi sana wana mwelekeo wa kufanya mambo ya kiroho kazini na kuchanganya dini na kazi. Gazeti San Francisco Examiner liliripoti kwamba “sasa watu wengi wanachanganya dini na kazi.”

      Ripoti moja ya majuzi ilisema hivi kuhusu Silicon Valley, kituo muhimu cha maendeleo ya teknolojia huko Marekani: “Wakubwa wanatambua kwamba magari yanazidi kupungua kazini kwa sababu watu wanaachishwa kazi, huku magari yakiongezeka kwenye mikutano ya kujifunza Biblia inayofanywa jioni.” Naam, watu wengi ulimwenguni wametambua kwamba Biblia inawasaidia sana kuwa na maoni mazuri kuhusu kazi, na hivyo kuwa na usawaziko zaidi maishani.

      Biblia inaweza kutusaidiaje kuwa na maoni yenye usawaziko kuhusu kazi? Je, kuna kanuni za Kimaandiko zinazoweza kutusaidia kushughulikia vizuri matatizo yanayotokea kazini siku hizi? Makala inayofuata itajibu maswali hayo.

  • Je, Kazi Ni Baraka au Ni Laana?
    Mnara wa Mlinzi—2005 | Juni 15
    • Je, Kazi Ni Baraka au Ni Laana?

      ‘Kwa mwanadamu hakuna jambo bora kuliko kuona mema kwa sababu ya kazi yake ngumu.’—Mhubiri 2:24.

      “MIMI huhisi nimeishiwa na nguvu kabisa baada ya kazi.” Katika uchunguzi mmoja uliofanywa majuzi, theluthi moja ya wafanyakazi walisema hivyo ndivyo wanavyohisi mara nyingi. Jambo hilo halishangazi kwa kuwa watu hukabili mkazo kazini. Mbali na kufanya kazi muda mrefu, wao pia hufanyia kazi nyingine nyingi nyumbani, na mara nyingi wakubwa wao hata hawawapongezi.

      Tangu bidhaa zilipoanza kuzalishwa kwa wingi, wafanyakazi wengi huhisi kwamba kazi yao si muhimu. Mara nyingi msukumo wao na uwezo wao wa kubuni mambo hukandamizwa. Hilo huathiri mtazamo wa watu kuhusu kazi. Wao huacha kuvutiwa na kazi yao. Tamaa ya kutaka kufanya kazi bora au kuifanya kwa ustadi hukandamizwa kwa urahisi. Mambo hayo yanaweza kumfanya mtu asipendezwe na kazi yake, na hata labda kuichukia.

      Kuchunguza Mtazamo Wetu

      Ni kweli kwamba hatuwezi kubadili hali zetu nyakati zote. Lakini je, hukubali kwamba tunaweza kubadili mtazamo wetu? Ikiwa unahisi kwamba umeathiriwa kwa kadiri fulani na maoni mabaya kuhusu kazi, itafaa uchunguze maoni na kanuni za Mungu kuhusu habari hii. (Mhubiri 5:18) Wengi wamegundua kwamba kuchunguza mambo hayo kumewasaidia kupata furaha na uradhi kwa kadiri fulani kutokana na kazi yao.

      Mungu ndiye Mfanyakazi Mkuu Zaidi. Mungu ni mfanyakazi. Huenda hatujawahi kumfikiria kuwa mfanyakazi, lakini hivyo ndivyo anavyojitambulisha kwanza katika Biblia. Simulizi la Mwanzo linaanza kwa kutaja jinsi Yehova alivyoumba mbingu na dunia. (Mwanzo 1:1) Fikiria kazi mbalimbali ambazo Mungu alifanya alipoanza kuumba. Alikuwa mbuni, msimamizi, injinia, msanii, mtaalamu wa kuteua vifaa vya kazi, mjenzi, mwanakemia, mwanabiolojia, mratibu, mtaalamu wa wanyama na lugha, na kadhalika.—Methali 8:12, 22-31.

      Kazi ya Mungu ilikuwaje? Biblia inasema ilikuwa “nzuri,” ‘njema sana.’ (Mwanzo 1:4, 31) Kwa kweli, uumbaji ‘unatangaza utukufu wa Mungu,’ nasi pia tunapaswa kumsifu!—Zaburi 19:1; 148:1.

      Hata hivyo, Mungu hakumaliza kazi yake kwa kuumba mbingu halisi, dunia, na watu wawili wa kwanza. Mwana wa Yehova, Yesu Kristo, alisema: “Baba yangu anaendelea kufanya kazi mpaka sasa.” (Yohana 5:17) Naam, Yehova anaendelea kufanya kazi kwa kutosheleza mahitaji ya viumbe wake, kuwapa chakula, na kuwaokoa waabudu wake waaminifu. (Nehemia 9:6; Zaburi 36:6; 145:15, 16) Hata anawatumia wanadamu, ambao ni ‘wafanyakazi wenzake,’ kusaidia katika kazi mbalimbali.—1 Wakorintho 3:9.

      Kazi inaweza kuwa baraka. Lakini, je, Biblia haisemi kwamba kazi ni laana? Huenda mtu akafikiri kwamba andiko la Mwanzo 3:17-19 linamaanisha kuwa Adamu na Hawa walipoasi, Mungu aliwaadhibu kwa kuwapa kazi yenye kulemea. Alipokuwa akiwahukumu watu hao wa kwanza, Mungu alimwambia Adamu hivi: “Kwa jasho la uso wako utakula mkate mpaka utakaporudi katika udongo.” Je, kwa maneno hayo Mungu aliilaani kazi kwa ujumla?

      La. Badala yake, Paradiso ya Edeni haingepanuliwa wakati huo kwa sababu Adamu na Hawa walikosa uaminifu. Mungu aliulaani udongo. Mwanadamu angehitaji kutoa jasho ili apate riziki kutokana na udongo.—Waroma 8:20, 21.

      Biblia inaonyesha kwamba kazi si laana, bali ni baraka na tunapaswa kuipenda sana. Kama ilivyotajwa juu, Mungu ni mfanyakazi mwenye bidii. Kwa kuwa amewaumba wanadamu kwa mfano wake, Yehova amewapa uwezo na mamlaka ya kusimamia uumbaji wake uliopo duniani. (Mwanzo 1:26, 28; 2:15) Mungu aliwapa wanadamu kazi hiyo kabla hajasema maneno yaliyo katika Mwanzo 3:19. Ikiwa kazi ingekuwa laana au jambo ovu, Yehova hangewahimiza wanadamu waifanye. Noa na familia yake walikuwa na kazi nyingi ya kufanya kabla na baada ya Gharika. Baada ya Yesu kuja duniani, wanafunzi wake walihimizwa pia wafanye kazi.—1 Wathesalonike 4:11.

      Hata hivyo, sote tunajua kwamba kazi inaweza kuwa yenye kulemea sana siku hizi. Mfadhaiko, hatari, uchovu, kukata tamaa, mashindano, udanganyifu, na ukosefu wa haki ni baadhi ya “miiba na mibaruti” inayosababishwa na kazi. Lakini kazi yenyewe si laana. Kwenye Mhubiri 3:13, Biblia inasema kwamba kazi na matunda yake ni zawadi kutoka kwa Mungu.—Ona sanduku lenye kichwa “Kukabiliana na Mfadhaiko Unaosababishwa na Kazi.”

      Unaweza kumtukuza Mungu kwa kazi yako. Sikuzote watu wamesifu kazi bora. Ubora wa kazi ni mojawapo ya mambo muhimu ambayo mtu anahitaji kuzingatia ili awe na maoni kama ya Biblia kuhusu kazi. Kazi ya Mungu ni bora kabisa. Ametupa vipawa na ustadi, naye anataka tuvitumie vizuri. Kwa mfano, wakati wa ujenzi wa ile maskani katika Israeli ya kale, Yehova aliwajaza hekima, uelewaji, na ujuzi watu kama Bezaleli na Oholiabu ili wafanye kazi za ufundi na kutimiza majukumu mbalimbali. (Kutoka 31:1-11) Hilo linaonyesha kwamba Mungu alipendezwa sana na kusudi la kazi hiyo, ufundi waliotumia, ubuni, na mambo mengine yaliyohusiana na kazi yao.

      Jambo hilo linaweza kubadili sana maoni yetu kuhusu vipawa tulivyo navyo na mazoea yetu ya kazi. Linatusaidia kuona mambo hayo kuwa zawadi kutoka kwa Mungu, ambazo hazipaswi kupuuzwa. Hivyo, Wakristo wanashauriwa kufanya kazi yao kana kwamba Mungu mwenyewe anaikagua: “Lolote mnalofanya, lifanyeni kwa nafsi yote kama kwa Yehova, na si kama kwa wanadamu.” (Wakolosai 3:23) Watumishi wa Mungu wanaamuriwa wafanye kazi njema, na hilo hufanya ujumbe wao uwavutie wafanyakazi wenzao na watu wengine.—Ona sanduku lenye kichwa “Kutumia Kanuni za Biblia Kazini.”

      Hivyo, tunapaswa kujichunguza tuone ikiwa sisi hufanya kazi bora na kwa bidii. Je, Mungu anapendezwa na jinsi tunavyofanya kazi? Je, tunaridhika na jinsi tunavyofanya kazi zetu? Ikiwa sivyo, basi tunahitaji kufanya maendeleo.—Methali 10:4; 22:29.

      Uwe na usawaziko kati ya kazi na mambo ya kiroho. Ingawa ni vizuri kufanya kazi kwa bidii, kuna jambo jingine muhimu linalohitajiwa ili kupata uradhi kazini na maishani. Tunahitaji kuzingatia mambo ya kiroho. Mfalme Sulemani, aliyefanya kazi kwa bidii na kufurahia utajiri na starehe maishani, alikata kauli hii: “Mwogope Mungu wa kweli na kushika amri zake. Kwa maana huo ndio wajibu wote wa mwanadamu.”—Mhubiri 12:13.

      Ni wazi kwamba tunapaswa kuzingatia mapenzi ya Mungu tunapofanya jambo lolote lile. Je, tunafanya mambo kupatana na mapenzi yake au kinyume chake? Je, tunajitahidi kumpendeza Mungu, au tunajitahidi tu kujipendeza? Tusipofanya mapenzi ya Mungu, hatimaye tutaumia kwa kukata tamaa, kuhisi upweke, na kujiona kuwa bure kabisa.

      Steven Berglas alisema kwamba wakubwa wa kazi waliochoka kupindukia ‘hutafuta jambo linalowapendeza sana na kulifanya kuwa sehemu ya maisha yao.’ Hakuna jambo bora kuliko kumtumikia Yule aliyetupa ustadi na vipawa vya kufanya kazi inayofaa. Hatuwezi kukosa uradhi tunapofanya kazi inayompendeza Muumba wetu. Yesu aliona kazi aliyopewa na Yehova kuwa yenye kujenga, yenye kuridhisha, na yenye kuburudisha kama chakula. (Yohana 4:34; 5:36) Kumbuka kwamba Mungu, aliye Mfanyakazi Mkuu Zaidi, anatualika tuwe “wafanyakazi [wenzake].”—1 Wakorintho 3:9.

      Kumwabudu Mungu na kukua kiroho hutuwezesha kupata uradhi kutokana na kazi na majukumu yetu. Kwa kuwa mara nyingi watu hukabili mkazo, mizozano, na hudaiwa mengi kazini, imani yetu yenye nguvu na hali yetu ya kiroho inaweza kutuimarisha tunapoendelea kujitahidi kuwa wafanyakazi na wasimamizi bora. Kwa upande mwingine, mambo tunayokabili maishani katika ulimwengu huu usiomwogopa Mungu yanaweza kutusaidia kuona mahali tunapohitaji kuimarisha imani yetu.—1 Wakorintho 16:13, 14.

      Wakati Ambapo Kazi Itakuwa Baraka

      Wale wanaojitahidi sasa kumtumikia Mungu kwa bidii wanaweza kutazamia wakati ambapo atarudisha Paradiso na kutakuwa na kazi nyingi nzuri dunia pote. Isaya, nabii wa Yehova, alitabiri hivi kuhusu maisha ya wakati huo: “Hakika wao watajenga nyumba na kukaa ndani yake; na hakika wao watapanda mashamba ya mizabibu na kula matunda yake. Hawatajenga na mtu mwingine akae ndani yake; hawatapanda na mtu mwingine ale. . . . Wataitumia kazi ya mikono yao wenyewe kikamilifu.”—Isaya 65:21-23.

      Kazi itakuwa baraka iliyoje wakati huo! Kwa kujifunza kuhusu mapenzi ya Mungu na kuishi kupatana nayo, na uwe miongoni mwa wale waliobarikiwa na Yehova na sikuzote ‘kuona mema kwa ajili ya kazi yako yote iliyo ngumu.’—Mhubiri 3:13.

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki