Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Wazazi Wako
    Maswali Ambayo Vijana Huuliza—Majibu Yafanyayo Kazi, Buku la 2
    • SEHEMU YA 6

      Wazazi Wako

      Wazazi wamejionea mengi maishani. Wakati mmoja walikuwa vijana kama wewe. Kwa sababu hiyo, ingetazamiwa kwamba wao hasa ndio wanaoweza kukupa wewe mwongozo unaohitaji. Hata hivyo, nyakati nyingine huenda ukahisi kwamba baadhi ya matatizo yako yanatokana na wazazi wako. Kwa mfano, huenda ukakabili moja kati ya hali zinazofuata:

      □ Wazazi wangu wananilaumu daima.

      □ Baba au mama hupenda kulewa au hutumia dawa za kulevya.

      □ Wazazi wangu hubishana sikuzote.

      □ Wazazi wangu wametengana.

      Sura ya 21-25 zitakusaidia kushughulika na matatizo haya na mengine.

  • Nifanye Nini Ninapolaumiwa?
    Maswali Ambayo Vijana Huuliza—Majibu Yafanyayo Kazi, Buku la 2
    • SURA YA 21

      Nifanye Nini Ninapolaumiwa?

      “Mama yangu ni kama kachero—sikuzote ananichunguza. Hata kabla sijamaliza kazi za nyumbani, yeye huanza kuzikagua akitafuta makosa.”—Craig.

      “Wazazi wangu walikuwa wakinifokea sikuzote. Waliniita kichwa-maji. Walinigombeza kuhusu shule, kazi za nyumbani, au mambo ya kutaniko.”—James.

      JE, WEWE huona kwamba hakuna lolote unalofanya linalowafurahisha wazazi wako? Je, unaona kwamba kila kitu unachofanya kinachunguzwa kwa darubini—kwamba unakaguliwa na kukosolewa daima na kamwe hukosi kulaumika?

      Kati ya mambo yafuatayo, ni jambo gani unalosikia mara nyingi?

      □ Sikuzote chumba chako huwa shaghalabaghala.

      □ Unatazama televisheni sana.

      □ Utaenda kulala saa ngapi?

      □ Mpaka sasa bado unalala?

      Hapa chini, andika jambo fulani ambalo wazazi wako husema linalokuudhi.

      ․․․․․

      Huenda hupendi hata kidogo kuwekewa sheria nyingi na kulaumiwa-laumiwa. Lakini jiulize: Ikiwa wazazi wako hawangekushauri au kukutia nidhamu, je, kweli ungesema kwamba wanakupenda? (Waebrania 12:8) Kwa kweli, kutiwa nidhamu kunaonyesha kuwa wazazi wako wanakupenda. Biblia inasema kwamba baba humkaripia “mwana anayemfurahia.”—Methali 3:12.

      Hivyo basi, unapaswa kushukuru kwamba wazazi wako wanakutia nidhamu, kwa kuwa wanakupenda sana! Kwa kweli, wewe ni mdogo na bado hujapata uzoefu. Mara kwa mara utahitaji kutiwa nidhamu. Bila mwongozo, unaweza kunaswa kwa urahisi na “tamaa zinazotukia ujanani.”—2 Timotheo 2:22.

      Lakini Haifurahishi!

      Bila shaka, “hakuna nidhamu inayoonekana kwa sasa kuwa yenye shangwe, bali ni yenye kuhuzunisha.” (Waebrania 12:11) Ndivyo ilivyo, hasa unapokuwa mdogo. Hilo halishangazi! Bado unakua nao utu wako utaendelea kubadilika. Hivyo shauri lolote unalopewa, hata liwe linatolewa kwa njia nzuri kadiri gani, huenda likakuudhi.

      Inaeleweka, kwa sababu jinsi unavyojiona hutegemea sana jinsi wengine wanavyosema kukuhusu. Na hasa maoni ya wazazi wako yanaweza kuathiri sana jinsi unavyojiona. Hivyo, mzazi anapokurekebisha au kulalamika kuhusu jinsi unavyofanya jambo fulani, unaweza kuumia sana.

      Je, ukate kauli kwamba chochote unachofanya hakifai au kwamba wewe ni bure kabisa ati kwa sababu tu wazazi wako wamefunua kasoro fulani ulizo nazo? Hapana. Wanadamu wote hukosea. (Mhubiri 7:20) Na unaweza kujifunza kutokana na makosa. (Ayubu 6:24) Namna gani ikiwa wazazi wako hukulaumu sana unapokosea na unapofanya jambo zuri ni kama hawaoni? Hilo linaweza kuumiza. Hata hivyo, hilo halimaanishi kwamba hufai kitu.

      Kwa Nini Unalaumiwa?

      Nyakati nyingine mzazi anaweza kukufokea, si kwa sababu ya kosa fulani hususa, lakini kwa sababu tu amekasirishwa na mambo mengine. Je, mama yako amekuwa na mahangaiko mengi mchana kutwa? Je, anasumbuliwa na ugonjwa fulani? Ikiwa ndivyo, huenda akakukasirikia isivyo kawaida ikiwa chumba chako hakijatakata. Je, baba yako anahangaishwa na hali ya uchumi ya familia yenu? Basi huenda akasema bila kufikiri “kama kwa upanga unaochoma.” (Methali 12:18) Kwa kweli, kulaumiwa bila sababu nzuri kunavunja moyo sana. Kwa hiyo, ili kuepuka kuvunjika moyo hata zaidi, usitilie maanani makosa ya wazazi wako au kukazia fikira jinsi wanavyokutendea. Kumbuka: “Sisi sote hujikwaa mara nyingi. Ikiwa yeyote hajikwai katika neno, huyo ni mtu mkamilifu.”—Yakobo 3:2.

      Kwa sababu wazazi wako si wakamilifu, wao pia wanaweza kujiona kuwa wamepungukiwa. Kwa kweli unapokosa kufanya jambo fulani vizuri, huenda wakahisi kwamba wameshindwa kutimiza jukumu lao. Kwa mfano mama anaweza kuchacha sana binti yake akianguka mtihani. Lakini huenda hasa anachofikiri mama huyo ni kwamba ameshindwa kutimiza jukumu lake, kwa kuwa ameshindwa kumsaidia binti yake afanye vizuri shuleni.

      Tulia Unapolaumiwa

      Hata sababu ya kulaumiwa iwe nini, jambo la maana ni, Unaweza kufanya nini unapolaumiwa? Kwanza, usijibizane nao. Methali 17:27 inasema: “Yeyote anayezuia maneno yake ana ujuzi, na mtu mwenye utambuzi ana roho ya utulivu.” Unaweza kudumisha jinsi gani “roho ya utulivu” unapolaumiwa? Jaribu yafuatayo:

      Sikiliza. Badala ya kujitetea, jaribu kuzuia hisia zako na kusikiliza kile ambacho wazazi wako wanasema. Mwanafunzi Yakobo aliwaambia Wakristo wawe ‘wepesi kuhusu kusikia, si wepesi wa kusema, si wepesi wa ghadhabu.’ (Yakobo 1:19) Ukiwakatiza kwa hasira wanapozungumza nawe, watafikiri kwamba husikilizi. Kufanya hivyo kutawakasirisha tu, na badala ya kupunguza nidhamu, wataiongeza.

      Kaza fikira. Nyakati nyingine huenda ukahisi kwamba wazazi wako walitoa shauri kwa ukali. Badala ya kukazia fikira jinsi walivyozungumza nawe, kazia fikira mambo waliyosema. Jiulize: ‘Kati ya mambo yote waliyosema, kuna ukweli wowote? Je, nimewahi kuwasikia wazazi wangu wakinilaumu kuhusu jambo hilohilo wakati mwingine? Nikifanya yale wanayotaka, nitapata hasara gani?’ Kumbuka, ijapokuwa huenda usifurahishwe na shauri unalopewa, wazazi wako wanakushauri kwa sababu wanakupenda. Ikiwa kwa kweli wanakuchukia, wasingekutia nidhamu hata kidogo.—Methali 13:24.

      Rudia shauri kwa maneno yako. Ukirudia kwa heshima shauri la wazazi wako kwa maneno yako mwenyewe, wataona kwamba umesikia wanachosema. Kwa mfano, mzazi anaweza kusema: “Sikuzote wewe huacha chumba chako kikiwa shaghalabaghala. Usipokisafisha, utaona!” Huenda unaona chumba chako kiko sawa tu. Lakini kumwambia kwamba kiko sawa ni kazi bure. Jaribu kuona mambo jinsi mzazi wako anavyoyaona. Ingekuwa afadhali kujibu: “Ni kweli. Chumba changu ni kichafu. Ungependa nikisafishe sasa hivi au baada ya kula?” Ukifanya hivyo, huenda hasira ya wazazi wako ikapoa. Kisha, fanya kile ambacho wazazi wako wanataka.—Waefeso 6:1

      Subiri. Usijitetee hata kidogo mpaka utimize kile ambacho wazazi wako walikuambia ufanye. Biblia inasema: “Anayezuia midomo yake anatenda kwa busara.” (Methali 10:19) Wazazi wako wanapoona kwamba kwa kweli umefanya walilotaka, haitakuwa vigumu kwao kukusikiliza.

      Andika hapa chini hatua unayohitaji kufanyia kazi kati ya hatua nne zilizotajwa. ․․․․․

      Kwa Nini Hatua Hii Ni Muhimu?

      Je, ungevumilia hali fulani ngumu ili upate dhahabu? Biblia inasema kwamba hekima ina thamani kubwa kuliko hazina yoyote ile. (Methali 3:13, 14) Unaweza kupata hekima jinsi gani? Methali 19:20 inasema hivi: “Sikiliza shauri na kukubali nidhamu, ili upate kuwa na hekima katika wakati wako ujao.” Ni kweli kwamba huenda usifurahi unapopewa shauri na kutiwa nidhamu. Hata hivyo, ukikazia fikira mambo yanayoweza kukupa hekima kati ya lawama zote hizo, kama vile mtu anavyokusanya vipande vidogo-vidogo vya dhahabu, mwishowe utakuwa na hazina kubwa yenye thamani kuliko dhahabu.

      Bila shaka, hakuna mtu asiyelaumiwa. Utalaumiwa na wazazi na walimu wako. Baadaye maishani utalaumiwa kazini na kwingineko. Ukiwa bado nyumbani, jifunze jinsi ya kushughulika na lawama, nawe utakuwa mwanafunzi mzuri, mfanyakazi mzuri, na pia mtu anayejiamini. Bila shaka, lawama unazopata si kitu, unapofikiria matokeo yake mazuri!

      KATIKA SURA INAYOFUATA

      Je, sheria za nyumbani zinakufanya ujione kuwa mfungwa? Jifunze jinsi unavyoweza kutosheka na uhuru ulio nao, na jinsi unavyoweza kupata uhuru mwingi zaidi.

      MAANDIKO MUHIMU

      “Mtu mwenye hekima atasikiliza na kupata mafundisho zaidi.”—Methali 1:5.

      PENDEKEZO

      Ili kufaidika na nidhamu kutoka kwa wazazi wako

      ● Thamini pongezi zozote zinazoandamana na lawama.

      ● Waombe maelezo zaidi ikiwa huelewi tatizo lenyewe au unalopaswa kufanya.

      JE, WAJUA . . .?

      Wazazi fulani hushindwa kuwaonyesha watoto wao upendo kwa sababu wao wenyewe hawakuonyeshwa upendo na wazazi wao.

      HATUA ZA KUCHUKUA!

      Wakati ujao wazazi wangu wakinilaumu kwa sababu ya jambo fulani, nita ․․․․․

      Nikiona kwamba wazazi wangu wananilaumu kupita kiasi, nita ․․․․․

      Mambo ambayo ningependa kuuliza mzazi (wazazi) wangu kuhusu habari hii ni ․․․․․

      UNA MAONI GANI?

      ● Kwa nini huenda ikawa vigumu kukubali makosa?

      ● Ni nini kinachoweza kuwafanya wazazi wako wakulaumu?

      ● Unaweza kufaidika jinsi gani na shauri lolote unalopewa?

      [Blabu katika ukurasa wa 177]

      “Sikuzote mama aliponigombeza tulikuwa tukijibizana. Lakini siku hizi ninajaribu kufuata mashauri ya Neno la Mungu. Matokeo yamekuwa mazuri. Mtazamo wa mama umeanza kubadilika. Kutumia mashauri ya Biblia kumenisaidia kumwelewa vizuri. Uhusiano wetu umekuwa mzuri.’’—Marleen

      [Picha katika ukurasa wa 180]

      Ukichagua hekima iliyo katika lawama unazopata, mwishowe utakuwa na hazina yenye thamani kuliko dhahabu

  • Kwa Nini Kuna Sheria Nyingi Sana?
    Maswali Ambayo Vijana Huuliza—Majibu Yafanyayo Kazi, Buku la 2
    • SURA YA 22

      Kwa Nini Kuna Sheria Nyingi Sana?

      Andika baadhi ya sheria za familia yenu. ․․․․․

      Unakubaliana na sheria zote za familia yenu?

      □ Ndiyo □ Hapana

      Ni sheria gani unayoiona kuwa ngumu zaidi kutii? ․․․․․

      KATIKA kila familia kuna sheria kuhusu mambo kama vile kazi za shule, kazi za nyumbani, wakati maalumu wa kutoka au kurudi nyumbani, na pia kuhusu matumizi ya simu, televisheni, na kompyuta. Huenda pia ukawekewa sheria kuhusu shule na marafiki.

      Je, unajiona kama mfungwa kwa sababu ya sheria zote hizo? Huenda unahisi kama vijana wafuatao:

      “Sheria niliyowekewa ya kurudi nyumbani kabla ya saa fulani ilinikera kwelikweli! Nilichukizwa sana kwa sababu vijana wengine waliruhusiwa kuchelewa kurudi nyumbani.”—Allen.

      “Inaudhi sana simu yako ya mkononi inapokaguliwa-kaguliwa. Naona kwamba ninatendewa kama mtoto!”—Elizabeth.

      “Nilihisi wazazi wangu wanataka kuniharibia maisha yangu, ni kana kwamba hawakutaka niwe na rafiki yeyote!”—Nicole.

      Ijapokuwa vijana wengi hawapendi sheria zinazowekwa na wazazi wao, wengi wao wanakubali kwamba hali ingekuwa mbaya zaidi ikiwa hakungekuwa na sheria. Hivyo basi, ikiwa sheria zina faida, kwa nini nyingine zinaudhi sana?

      “Mimi si Mtoto!”

      Labda sheria zinakuudhi kwa sababu unaona kwamba unatendewa kama mtoto. Ukiwa umekasirika, unatamani kuwaambia, “Mimi si mtoto!” Bila shaka, huenda wazazi wako wanaona sheria hizo zinahitajiwa, ili kukulinda na kukutayarisha kwa ajili ya maisha ya baadaye.

      Hata hivyo, huenda sheria unazowekewa haziendi sambamba na umri wako. Huenda unaweza kujihisi kwamba umezuiwa kama alivyohisi msichana mmoja aitwaye Brielle, ambaye alisema hivi kuhusu wazazi wake: “Hawajui hata kidogo maisha ya mtu wa umri wangu. Hawataki niseme chochote, nifanye lolote au niwe mtu mzima.” Kijana aitwaye Allison anahisi hivyo pia. Anasema “Wazazi wangu hawaelewi kwamba nina umri wa miaka 18, bali si miaka 10. Wanahitaji kunipa uhuru zaidi!”

      Sheria zinaweza kuchukiza zaidi hasa ikiwa ndugu na dada zako wanaendekezwa. Kwa mfano, akikumbuka mambo yalivyokuwa alipokuwa tineja, kijana anayeitwa Matthew anasema hivi kuhusu dada yake mdogo na binamu zake, “Hata kama ‘wangeua mtu,’ hawangefanywa chochote!”

      Maisha Yangekuwa Mazuri Bila Sheria?

      Huenda ukatamani kutokuwa chini ya sheria za wazazi wako. Lakini je, kweli maisha yangekuwa mazuri bila mwongozo wao? Huenda unawajua vijana fulani wa rika lako ambao wanaweza kuamua kurudi nyumbani wakati wowote wapendao, wanaweza kuvaa chochote wakipendacho, na kwenda na rafiki zao kokote na wakati wowote wapendao. Huenda wazazi wao wana shughuli nyingi sana hivi kwamba hawajui kile ambacho watoto wao wanafanya. Hata sababu ziwe nini, Biblia inaonyesha kwamba wazazi hawawezi kufanikiwa wakimlea mtoto kwa njia hiyo. (Methali 29:15) Kuenea kwa ukosefu wa upendo kunakoonekana leo duniani, kunasababishwa hasa na watu wenye ubinafsi ambao wengi wao walilelewa katika familia ambazo hazikuwa na sheria.—2 Timotheo 3:1-5.

      Badala ya kuwaonea wivu rafiki zako ambao wameruhusiwa kufanya chochote wapendacho, zione sheria ambazo wazazi wako wamekuwekea kuwa uthibitisho wa kwamba wanakupenda na wanakujali. Kwa kukuwekea sheria fulani, wanamwiga Yehova Mungu, aliyewaambia watu wake hivi: “Nitakufanya uwe na ufahamu na kukufundisha katika njia unayopaswa kuiendea. Nitakupa shauri jicho langu likiwa linakutazama.”—Zaburi 32:8.

      Hata hivyo, huenda nyakati nyingine ukahisi umelemewa na sheria za wazazi wako. Unaweza kufanya nini?

      Wasiliana kwa Njia Inayofaa

      Iwe unataka uhuru zaidi au kupunguza tu mkazo unaotokana na sheria ambazo wazazi wako wamekuwekea, siri ya kupata mafanikio ni kuwasiliana nao kwa njia inayofaa. Huenda wengine wakasema: ‘Nimejaribu kuzungumza na wazazi wangu, lakini ni kazi bure!’ Ikiwa ndivyo unavyohisi, jiulize: ‘Je, ninaweza kubadili jinsi ninavyowasiliana nao?’ Mawasiliano ni kifaa muhimu kinachoweza (1) kuwasaidia wengine wakuelewe au (2) kukusaidia kuelewa ni kwa nini mambo unayotaka yamekataliwa. Ikiwa unataka utendewe kama mtu mzima, basi lazima ujifunze kuwasiliana nao kama mtu mzima. Unaweza kufanya hivyo jinsi gani?

      Jifunze kuzuia hisia zako. Ili kuwasiliana vizuri, lazima uwe na sifa ya kujizuia. Biblia inasema hivi: “Mtu mjinga huiachilia roho yake yote, lakini mwenye hekima huituliza mpaka mwisho.” (Methali 29:11) Hivyo, epuka kunung’unika-nung’unika, kununa-nuna, na kutaka ubembelezwe kama mtoto. Ni kweli kwamba huenda ukataka kubamiza mlango au kupiga-piga miguu chini kwa hasira unapohisi kwamba wazazi wako wanakunyima uhuru. Lakini, kufanya hivyo kutawafanya wakuwekee sheria nyingi hata zaidi.

      Jaribu kuwaelewa wazazi wako. Tracy, msichana Mkristo aliyelelewa na mzazi mmoja, anasema, “Mimi hujiuliza, ‘Mama anataka kunifundisha nini?’” Tracy alikata kauli gani? “Anajaribu kunisaidia niwe na sifa nzuri.” (Methali 3:1, 2) Kuelewa hisia za wazazi wako kwa njia hiyo kunaweza kukusaidia kuwasiliana nao vizuri.

      Kwa mfano, tuseme wazazi wako wanasita kukupa ruhusa ya kwenda kujumuika na vijana wengine. Badala ya kubishana nao, unaweza kuwauliza, “Namna gani ikiwa kutakuwa na mtu mkomavu anayetegemeka?” Huenda bado wazazi wako wakakataa. Hata hivyo, ukielewa hangaiko lao, huenda ukapendekeza jambo ambalo labda litakubalika machoni pao.

      Jiendeshe kwa njia itakayofanya wazazi wako wawe na imani nawe. Wazia mtu amechukua mkopo katika benki. Akiwa na mazoea ya kulipa kwa wakati, benki itamwamini na inaweza kumpa mkopo mkubwa zaidi siku za usoni. Ndivyo ilivyo na nyumbani. Unapaswa kuwatii wazazi wako. Ukifanya hivyo hata katika mambo madogo, wazazi wako watakuamini hata zaidi wakati ujao. Lakini, ukiwatamausha wazazi wako mara kwa mara, usishangae wakikaza kamba au hata kukuzuilia kabisa.

      Unapovunja Sheria

      Haikosi kuna wakati ambapo utavunja sheria fulani. Huenda ukakosa kufanya kazi ulizopewa, ukatumia simu kwa muda mrefu sana, au ukachelewa kurudi nyumbani. (Zaburi 130:3) Katika hali hiyo, utalazimika kuwaeleza ni kwa nini. Unaweza kuzuiaje hali isiwe mbaya zaidi?

      Sema kweli. Usiwape hadithi ndefu. Kufanya hivyo kwaweza kuwafanya wazazi wako wapoteze imani waliyokuwa nayo kukuelekea. Hivyo sema kweli na kutaja mambo waziwazi. (Methali 28:13) Epuka kujitetea au kupunguza uzito wa kosa. Na sikuzote ukumbuke kwamba “jibu, linapokuwa la upole, hugeuza ghadhabu.”—Methali 15:1.

      Omba msamaha. Kuwaeleza kwamba unasikitika kwa kuwahangaisha, kuwavunja moyo, au kuwaongezea kazi, ni vizuri na kunaweza kukupunguzia adhabu. Hata hivyo, unapaswa kufanya hivyo kutoka moyoni.

      Kubali matokeo. (Wagalatia 6:7) Huenda mwanzoni ukapinga adhabu hiyo, hasa unapoona kwamba unaonewa. Hata hivyo, kukubali makosa na nidhamu huonyesha kwamba wewe ni mkomavu. Jambo la maana ni kujitahidi kuwafanya wazazi wakuamini tena.

      Andika unachohitaji kufanyia kazi kati ya hoja tatu ambazo zimezungumziwa. ․․․․․

      Kumbuka kwamba wazazi wako wana jukumu la kukuongoza. Ndio maana Biblia inataja “amri ya baba yako” na “sheria ya mama yako.” (Methali 6:20) Hata hivyo, hupaswi kuwa na maoni ya kwamba sheria unazowekewa na wazazi wako zinakunyima uhuru. Badala yake, ukitii mamlaka ya wazazi wako, Yehova anaahidi kwamba mwishowe ‘mambo yatakuendea vema’!—Waefeso 6:1-3.

      PATA HABARI ZAIDI KATIKA BUKU LA 1, SURA YA 3

      KATIKA SURA INAYOFUATA

      Je, mzazi hutumia dawa za kulevya au kunywa pombe kupita kiasi? Sura inayofuata itakusaidia kuona jinsi unavyoweza kukabiliana na hali hiyo.

      MAANDIKO MUHIMU

      “Mheshimu baba yako na mama yako . . . ili mambo yakuendee vema.” —Waefeso 6:2, 3.

      PENDEKEZO

      Ikiwa unataka wazazi wako wakupe uhuru zaidi, kwanza, uwe mtiifu. Wanapoona kwamba wewe ni mtiifu sikuzote, bila shaka wanaweza kukupa uhuru zaidi.

      JE, WAJUA . . .?

      Utafiti unaonyesha kwamba vijana ambao wazazi wao wanawatia nidhamu kwa upendo, hufanya vizuri shuleni, huwa na uhusiano mzuri na wengine, na huwa na furaha.

      HATUA ZA KUCHUKUA!

      Nikivunja sheria ya familia yetu, nitasema ․․․․․

      Ninaweza kuwafanya wazazi wangu waniamini kwa ․․․․․

      Mambo ambayo ningependa kuuliza mzazi (wazazi) wangu kuhusu habari hii ni ․․․․․

      UNA MAONI GANI?

      ● Kwa nini huenda nyakati nyingine ikaonekana kana kwamba wazazi wako wanakuwekea sheria nyingi mno?

      ● Kwa nini nyakati nyingine unachukizwa na sheria unazowekewa?

      ● Unaweza kuboresha jinsi gani mawasiliano kati yako na wazazi wako?

      [Blabu katika ukurasa wa 183]

      “Wakati ungali mdogo, ni rahisi kufikiri kwamba unajua kila kitu. Hivyo, wazazi wako wanapokuwekea sheria, huenda ukakasirika. Hata hivyo, sheria zao zina faida.’’—Megan

      [Sanduku katika ukurasa wa 186]

      Ni Upendeleo Kweli?

      Umewahi kujiuliza, ‘Kwa nini wazazi hawawatendei watoto wote kwa usawa?’ Ikiwa umewahi kujiuliza hivyo, kumbuka kwamba kuna tofauti kati ya kutendewa kwa usawa na kutendewa kwa haki. Huenda nyakati nyingine isifae kwa wazazi kuwatendea watoto wao wote kwa usawa. Jambo kuu ni, Je, mahitaji yako yanapuuzwa? Kwa mfano, unapohitaji ushauri, msaada, au utegemezo wa wazazi wako, je, wanakusaidia? Ikiwa wanafanya hivyo, je, kweli unaweza kusema kwamba unapuuzwa? Kwa kuwa wewe na ndugu na dada zako ni watu tofauti wenye mahitaji tofauti, haiwezekani sikuzote wazazi wenu wawatendee ninyi nyote kwa usawa. Beth alipata kujua hilo. Sasa, akiwa na umri wa miaka 18, anasema: “Mimi na ndugu yangu ni watu wawili tofauti nasi tuna mahitaji tofauti. Ninapokumbuka yaliyopita, siamini kwamba nilipokuwa mdogo sikuona mambo kwa njia hiyo.”

      [Sanduku/Picha katika ukurasa wa 189]

      Ukurasa wa Mazoezi

      Zungumza na Wazazi Wako!

      Sura mbili zilizotangulia zimezungumzia jinsi unavyoweza kufanya unapolaumiwa na wazazi au unapowekewa sheria. Hata hivyo, utafanya nini ukihisi kwamba wazazi wako wamepita kiasi katika mambo hayo? Unaweza kuanzisha mazungumzo nao jinsi gani?

      ● Chagua wakati ambapo utakuwa umetulia na wazazi wako hawana shughuli nyingi.

      ● Zungumza nao kutoka moyoni, lakini usiropoke tu kwa sababu ya hisia. Wape wazazi wako heshima wanayostahili.

      Ikiwa unahisi kwamba wazazi wako wanakulaumu kupita kiasi, unaweza kuwaambia: “Ninajitahidi kufanya yaliyo sawa, lakini si rahisi ikiwa kila wakati ninalaumiwa. Ningependa tuongee kuhusu jambo hilo.”

      Andika hapa chini jinsi unavyoweza kuanzisha mazungumzo na wazazi wako kuhusu jambo hilo.

      ․․․․․

      ✔PENDEKEZO: Tumia Sura ya  21 ili kuanzisha mazungumzo. Huenda wazazi wako watapenda kuzungumza nawe mambo yaliyo katika sura hiyo.

      Ikiwa unahisi kwamba wazazi wako hawakupi uhuru wa kutosha, unaweza kuwaambia: “Ni jambo gani ninalopaswa kufanyia kazi ili wakati ujao niwe mwenye kutegemeka zaidi na kustahili kupata uhuru zaidi?”

      Andika hapa chini jinsi unavyoweza kuanzisha mazungumzo na wazazi wako kuhusu jambo hilo.

      ․․․․․

      ✔PENDEKEZO: Chunguza Sura ya 3 katika Buku la  1 yenye kichwa “Niwafanyeje Wazazi Wangu Wanipe Uhuru Zaidi?” Kisha andika maswali yoyote ambayo huenda ukawa nayo baada ya kusoma sura hiyo.

      [Picha katika ukurasa wa 184, 185]

      Kutii sheria za wazazi wako ni kama kulipa mkopo wa benki, kadiri unavyolipa kwa wakati ndivyo unavyoaminika zaidi

  • Nini Ikiwa Mzazi Wangu ni Mraibu wa Dawa za Kulevya au Pombe?
    Maswali Ambayo Vijana Huuliza—Majibu Yafanyayo Kazi, Buku la 2
    • SURA YA 23

      Nini Ikiwa Mzazi Wangu ni Mraibu wa Dawa za Kulevya au Pombe?

      “Baba alisema anaenda kurekebisha gari, lakini hakuwasiliana nasi mchana kutwa. Mama alijaribu kumpigia simu. Hakuijibu. Muda si muda, nikamwona mama akiwa na wasiwasi huku akijitayarisha kuondoka. ‘Naenda kumtafuta baba yako,’ akasema.

      “Baadaye, Mama alirudi peke yake. Nikamuuliza, ‘Kwani hukumpata?’ Akajibu, ‘Hapana.’

      “Ndipo nikagundua kwamba Baba amerudia mazoea yake ya zamani. Ni kama tu ilivyokuwa wakati uliopita. Wajua, baba yangu ni mraibu wa dawa za kulevya. Kufikia wakati aliporudi nyumbani, tulikuwa na wasiwasi mwingi. Siku iliyofuata, sikuzungumza naye hata kidogo, jambo ambalo liliniumiza sana.”—Karen, 14.

      MAMILIONI ya vijana huishi na wazazi ambao ni waraibu wa dawa za kulevya au pombe. Ikiwa mmoja wa wazazi wako ni mtumwa wa mazoea hayo, huenda unaona aibu, unavunjika moyo, au hata kukasirika.

      Kwa mfano, mbele ya watu, baba ya Mary alionekana mzuri sana. Lakini kwa siri, alikuwa mlevi sugu, naye alikuwa akiwatusi na kuwatendea kwa ukatili washiriki wa familia yake. Mary anakumbuka hivi kwa uchungu: “Watu walikuwa wakitujia na kutupongeza kwamba baba yetu ni mzuri ajabu, na kwamba tuna raha kama nini kuwa na baba kama huyo.”a

      Ikiwa mzazi wako ni mraibu wa pombe au dawa za kulevya, unaweza kufanya nini?

      Uraibu Unasababishwa na Nini?

      Kwanza, ni vizuri kuelewa kwa undani tatizo la wazazi wako. Methali 1:5 inasema hivi: “Mtu mwenye uelewaji ndiye anayepata mwongozo stadi.” Kwa hiyo, ingefaa kuelewa uraibu ni nini, ni akina nani huwa na mazoea hayo, na kwa nini.

      Kwa mfano, mraibu si mtu ambaye hunywa kupita kiasi mara mojamoja. Badala yake, ni mtu mwenye tatizo la kudumu la kunywa kupita kiasi. Anatawaliwa na pombe, na akianza kunywa, hawezi kujizuia. Uraibu wake unaathiri familia, kazi, na afya yake.b

      Ijapokuwa huenda ikawa mtu fulani anapenda tu kunywa kupita kiasi, nyakati nyingine hisia zinahusika. Waraibu wengi hujiona kwamba hawafai kitu. (Methali 14:13) Baadhi yao walilelewa na wazazi ambao pia walikuwa na mazoea ya kunywa kupita kiasi. Watu kama hao hunywa pombe ili kujisahaulisha uchungu na makovu ya utotoni. Huenda sababu hizohizo zikamfanya mtu aanze kutumia dawa za kulevya.

      Bila shaka kunywa au kutumia dawa za kulevya kunazidisha tu matatizo ya mtu, kwa kuwa akiwa katika hali hiyo, akili yake haifanyi kazi vizuri nazo hisia zake si za kawaida. Ndiyo sababu huenda mzazi wako akahitaji kusaidiwa na wataalamu ili aweze kushinda zoea hilo.

      Usitarajie Mengi Kupita Kiasi

      Ni kweli kwamba kujua tu kwa nini mzazi wako anafanya jambo fulani linalokuaibisha, hakuondoi tatizo lenyewe. Hata hivyo, kuelewa kwa kiasi fulani tatizo lake kunaweza kukusaidia kumwonea huruma mzazi wako.

      Kwa mfano, ungetazamia mzazi ambaye amevunjika mguu acheze mpira wa miguu pamoja nawe? Namna gani ikiwa unajua kwamba mzazi wako aliumia akifanya jambo fulani lisilofaa? Haikosi ungevunjika moyo. Hata hivyo, unajua kwamba hataweza kucheza mpira nawe mpaka atakapopona. Kuelewa hilo kunaweza kukusaidia usitarajie mengi kupita kiasi kutoka kwa mzazi wako.

      Vivyo hivyo, mzazi ambaye hunywa kupita kiasi au ambaye hutumia dawa za kulevya ni mlemavu kihisia na kiakili. Ni kweli kwamba amejisababishia mwenyewe “ulemavu” huo. Na una haki ya kukasirishwa na mwenendo huo. Hata hivyo, hadi mzazi wako atakapotafuta msaada wa kushinda zoea hilo, hataweza kukuandalia mahitaji yako vizuri. Kuuona uraibu wake kama ulemavu fulani kunaweza kukusaidia usitarajie mengi kupita kiasi kutoka kwake kwa sasa.

      Mambo Unayoweza Kufanya

      Ukweli ni kwamba, utaendelea kusumbuliwa na mwenendo wa mzazi wako mpaka atakapobadili maisha yake. Unaweza kufanya nini kabla ya wakati huo?

      Usijilaumu kwa sababu ya tatizo la mzazi wako. Mzazi wako—wala si mwingine yeyote—ndiye mwenye lawama. Andiko la Wagalatia 6:5 linasema hivi: “Kila mmoja ataubeba mzigo wake mwenyewe.” Kwa hiyo, si kazi yako kutatua tatizo la mzazi wako au kumwepusha na matokeo ya tatizo hilo. Kwa mfano, hakuna haja ya kumdanganya mkubwa wake kazini kwa niaba yake au kumwinua anapoanguka nje kwa sababu ya ulevi.

      Mhimize mzazi wako atafute msaada. Huenda tatizo kubwa la mzazi wako ni kukubali kwamba ana tatizo. Ulevi unapokuwa umemtoka na ametulia, yule mzazi mwingine pamoja na watoto wakubwa katika familia wanaweza kumwambia mzazi huyo mlevi jinsi mwenendo wake unavyoathiri familia na mambo anayohitaji kufanya.

      Pia, kuandika majibu ya maswali yafuatayo kunaweza kumsaidia mzazi mwenye tatizo hilo: Familia yangu itakuwaje nikiendelea kulewa au kutumia dawa za kulevya? Matokeo yatakuwa nini nikiacha zoea hili? Ninapaswa kufanya nini ili nipate msaada?

      Ukiona dalili ya matata, ondoka. Andiko la Methali 17:14 linasema hivi: “Kabla mabishano hayajalipuka, jiondokee.” Usijihatarishe kwa kuingilia mabishano kati ya wazazi wako. Ikiwezekana ingia chumbani mwako au uende kwa rafiki yako. Ikiwa kuna uwezekano wa jeuri kutokea, huenda msaada kutoka nje ukahitajika.

      Si vibaya kuwa na hisia. Vijana fulani hujiona kuwa na hatia kwa sababu ya kumchukia mzazi ambaye ni mraibu. Ni kawaida kuchukizwa kwa kiasi fulani, hasa ikiwa uraibu wa mzazi wako unamzuia kukuonyesha upendo na kukutegemeza. Ni kweli, Biblia inakuamuru umheshimu mzazi wako. (Waefeso 6:2, 3) Hata hivyo, mamlaka yake ndiyo unayoheshimu, kama vile unavyoheshimu mamlaka ya polisi au hakimu. Haimaanishi kwamba unaunga mkono mwenendo wa mzazi wako. (Waroma 12:9) Wala haimaanishi kwamba wewe ni mbaya kwa sababu unachukia tabia yake ya kulewa au kutumia dawa za kulevya; vyovyote vile, uraibu ni tabia yenye kuchukiza sana!—Methali 23:29-35.

      Tafuta marafiki wenye kujenga. Maisha ya nyumbani yanapojaa vurugu, ni rahisi kuzoea hali hiyo na kufikiri kwamba hiyo ndiyo kawaida. Hivyo, hakikisha unachangamana na watu walio na hali nzuri ya kiroho na kihisia. Pindi unazokuwa na washiriki wa kutaniko la Kikristo, zinaweza kuwa zenye kutia moyo na kutegemeza kwelikweli, na pia kukupa nafasi ya kupumzika kutokana na mahangaiko ya familia yenu. (Methali 17:17) Ushirika mzuri wa familia za Kikristo unaweza kukusaidia kuwa na maoni yanayofaa kuhusu maisha ya familia, na kuondolea mbali maoni yasiyofaa ambayo huenda ukawa nayo kwa sababu ya jinsi hali ilivyo katika familia yenu.

      Tafuta msaada kwa ajili yako mwenyewe. Kuna faida ya kuwa na mtu mzima mkomavu unayemwamini ambaye unaweza kumweleza hisia zako. Wazee wa kutaniko wako tayari kukusaidia ukihitaji msaada. Biblia inasema kwamba wanaume hao wanaweza kuwa “kama mahali pa kujificha kutokana na upepo na mahali pa kujificha kutokana na dhoruba ya mvua, kama vijito vya maji katika nchi isiyo na maji, kama kivuli cha mwamba mzito katika nchi iliyochoka.” (Isaya 32:2) Hivyo, usiogope au kuona aibu kuwaendea ili kupata faraja na mashauri.

      Andika hapa hatua utakazojaribu kwanza kati ya hatua sita zilizozungumziwa. ․․․․․

      Huenda huwezi kubadili hali nyumbani kwenu, hata hivyo unaweza kubadili jinsi hali hiyo inavyokuathiri. Badala ya kujaribu kuwaongoza wazazi wako, kazia fikira mtu unayeweza kumwongoza, yaani, wewe mwenyewe. Mtume Paulo aliandika: “Endeleeni kuufanyia kazi wokovu wenu wenyewe.” (Wafilipi 2:12) Kufanya hivyo, kunaweza kukusaidia kuwa na maoni yanayofaa, na huenda hata kunaweza kumsaidia mzazi wako atafute usaidizi.

      KATIKA SURA INAYOFUATA

      Namna gani ikiwa wazazi wako wanabishana kila wakati? Unaweza kufanya nini?

      [Maelezo ya Chini]

      a Ikiwa unatendewa vibaya na mzazi mwenye mazoea ya kulewa, tafuta msaada. Zungumza na mtu mzima ambaye unamwamini. Ikiwa wewe ni mmoja wa Mashahidi wa Yehova, unaweza kuongea na mzee wa kutaniko au Mkristo mwingine mkomavu.

      b Ingawa mraibu wa pombe anayezungumziwa ni wa kiume, kanuni zilizozungumziwa zinawahusu waraibu wa kike pia.

      MAANDIKO MUHIMU

      “Ufahamu wa mtu hakika hupunguza hasira yake.”—Methali 19:11.

      PENDEKEZO

      Badala ya kumchukia mzazi wako, chukia mwenendo wake mbaya.—Methali 8:13; Yuda 23.

      JE, WAJUA . . .?

      Katika Biblia, neno ‘heshimu’ linaweza kumaanisha tu kutambua mamlaka halali. (Waefeso 6:1, 2) Hivyo, kumheshimu mzazi hakumaanishi kwamba nyakati zote utakubaliana na mwenendo wake.

      HATUA ZA KUCHUKUA!

      Mzazi wangu akianza matusi au ugomvi, nita ․․․․․

      Ninaweza kumtia moyo mzazi wangu atafute usaidizi kwa ․․․․․

      Mambo ambayo ningependa kuuliza mzazi (wazazi) wangu kuhusu habari hii ni ․․․․․

      UNA MAONI GANI?

      ● Ni nini huwafanya watu fulani wawe waraibu wa pombe au dawa za kulevya?

      ● Kwa nini huwezi kulaumiwa kwa sababu ya uraibu wa mzazi wako?

      ● Katika hali unayokabili, ni hatua gani unazoweza kuchukua?

      [Blabu katika ukurasa wa 192]

      “Ninajua kwamba huenda siku moja mwenendo wa wazazi wangu ukaniabisha, lakini najua pia kwamba nikimtegemea Yehova, atanipa nguvu za kuvumilia.’’—Maxwell

      [Sanduku katika ukurasa wa 198]

      Mzazi Akiacha Kumtumikia Yehova

      Mmoja wa wazazi wako akiacha kuishi kulingana na viwango vya Biblia—labda hata anasema kwamba hataki kushirikiana na kutaniko la Kikristo—unaweza kufanya nini?

      ● Kumbuka kwamba Yehova hatakulaumu kwa sababu ya mwenendo wa mzazi wako. Biblia inasema: “Kila mmoja wetu atatoa hesabu kwa Mungu kwa ajili yake mwenyewe.”—Waroma 14:12.

      ● Epuka kujilinganisha na vijana wengine ambao hali zao ni nzuri zaidi. (Wagalatia 5:26) Kijana mmoja ambaye baba yake aliiacha familia yake anasema: “Badala ya kufikiria tu hali yenu mbaya, ingekuwa afadhali kukazia fikira jinsi unavyoweza kushughulika na hali hiyo.”

      ● Endelea kumheshimu mzazi huyo, na kutii maagizo yake maadamu hayapingani na viwango vya Mungu. Amri ya Yehova kwamba watoto wawaheshimu wazazi wao, haitegemei ikiwa mzazi ni mwamini au si mwamini. (Waefeso 6:1-3) Unapowaheshimu na kuwatii wazazi wako, hata ikiwa wana mazoea fulani yasiyofaa, unaonyesha kwamba unampenda Yehova.—1 Yohana 5:3.

      ● Shirikiana sana na kutaniko la Kikristo. Humo unaweza kufarijiwa na familia kubwa ya kiroho. (Marko 10:30) Kijana mmoja anayeitwa David aliogopa kwamba huenda washiriki wa kutaniko wakamwepuka yeye na familia yao kwa sababu baba yake alikuwa ameacha kumtumikia Yehova. Hata hivyo, David aligundua kwamba maoni yake hayakuwa na msingi. Anasema: “Hatukuachwa peke yetu. Hilo lilinisadikisha kwamba kutaniko linatujali kikweli.”

      [Picha katika ukurasa wa 194]

      Kuuona uraibu wa mzazi wako kama ulemavu fulani kunaweza kukusaidia kutotarajia mengi mno kutoka kwake

  • Mfano wa Kuigwa—Hezekia
    Maswali Ambayo Vijana Huuliza—Majibu Yafanyayo Kazi, Buku la 2
    • Mfano wa Kuigwa—Hezekia

      Hezekia anakabili uamuzi mzito. Akiwa na umri wa miaka 25 tu, tayari ni mfalme wa Yuda. Atakuwa mfalme wa aina gani? Je, ataruhusu mfano mbaya wa baba yake, Mfalme Ahazi, umwathiri? Ahazi alikuwa mwasi-imani asiyetubu mpaka alipokufa. Aliendeleza ibada ya kipagani, na hata akateketeza angalau mmoja wa ndugu za Hezekia kwenye madhabahu ya kipagani. (2 Mambo ya Nyakati 28:1-4) Hata hivyo, Hezekia haruhusu mwenendo wenye unafiki wa baba yake umfanye achukizwe na ibada ya Yehova, wala haamini kwamba mtoto wa nyoka ni nyoka. Badala yake, Hezekia anaendelea “kushikamana na Yehova.”—2 Wafalme 18:6.

      Je, mmoja wa wazazi wako anadhihaki ibada ya Yehova? Je, ni mkatili au ana mazoea fulani yasiyofaa? Ikiwa ndivyo, si lazima uwe kama mzazi wako! Hezekia hakuruhusu hali mbaya ya familia yao iharibu maisha yake. Alikuwa mfalme mzuri sana hivi kwamba “baada yake hapakuwa na yeyote kama yeye kati ya wafalme wote wa Yuda.” (2 Wafalme 18:5) Kama Hezekia, wewe pia unaweza kufanikiwa maishani mwako hata ikiwa kuna hali ngumu katika familia yenu. Jinsi gani? Kwa kuendelea “kushikamana na Yehova.”

  • Nifanye Nini Wazazi Wangu Wanapogombana?
    Maswali Ambayo Vijana Huuliza—Majibu Yafanyayo Kazi, Buku la 2
    • SURA YA 24

      Nifanye Nini Wazazi Wangu Wanapogombana?

      Je, wazazi wako hubishana mbele yako? Ikiwa ndiyo, ni nini kati ya mambo yafuatayo wanayogombania mara nyingi?

      □ Pesa

      □ Kazi za nyumbani

      □ Watu wa ukoo

      □ Wewe

      Ungependa kuwaambia wazazi wako nini kuhusu jinsi hilo linavyokuathiri? Andika maelezo yako hapa chini.

      ․․․․․

      HUWEZI kuepuka usumbufu unaotokana na ugomvi kati ya wazazi wako. Unawapenda na unawategemea. Kwa hiyo, huenda ukafadhaika sana unapowasikia wakibishana. Huenda ukakubaliana na msichana anayeitwa Marie, aliyesema: “Ni vigumu kwangu kuwaheshimu wazazi wangu kwa kuwa inaonekana hawaheshimiani.”

      Unapowaona wazazi wako wakigombana, unalazimika kukubali jambo hili lenye kuumiza: Wazazi wako si wakamilifu kama ulivyofikiri. Kujua hivyo huenda kukakutia wasiwasi. Mabishano hayo yanapozidi kuongezeka na kuwa makali zaidi, huenda ukawa na wasiwasi kwamba ndoa yao inaelekea kuvunjika. Marie anasema: “Ugomvi unapozuka kati ya wazazi wangu, ninawazia kwamba watatalikiana nami nitalazimika kuchagua nitakayeishi naye. Pia ninaogopa kwamba nitatenganishwa na ndugu na dada zangu.”

      Kwa nini wazazi hugombana, nawe unapaswa kufanya nini ugomvi unapozuka?

      Chanzo cha Ugomvi

      Huenda wazazi wako ‘wanavumiliana katika upendo.’ (Waefeso 4:2) Hata hivyo, Biblia inasema: “Wote wamefanya dhambi na kupungukiwa na utukufu wa Mungu.” (Waroma 3:23) Wazazi wako si wakamilifu. Kwa hiyo, usishangae hasira zao zinapopanda na hata nyakati nyingine kutokeza ugomvi.

      Kumbuka pia kwamba tunaishi “nyakati za hatari zilizo ngumu kushughulika nazo.” (2 Timotheo 3:1) Mkazo wa kuchuma pesa, kulipia gharama mbalimbali, kushughulika na hali ngumu za kazini—yote hayo hulemea ndoa. Na ikiwa wazazi wote wawili wanafanya kazi ya kuajiriwa, huenda ikawa vigumu kuamua ni nani atakayefanya kazi fulani za nyumbani.

      Lakini uwe na hakika kwamba hata wazazi wako wanapokosa kuelewana, haimaanishi kwamba ndoa yao inavunjika. Haikosi wazazi wako bado wanapendana—ijapokuwa huenda wakawa na maoni tofauti kuhusu mambo fulani.

      Kwa mfano: Umewahi kutazama sinema pamoja na rafiki zako, kisha baadaye ukaona kwamba maoni yako kuhusu sinema hiyo ni tofauti kabisa na maoni yao? Inawezekana. Hata watu walio na uhusiano wa karibu huona mambo kwa njia tofauti. Huenda ikawa hivyo pia na wazazi wako. Labda wote wanahangaikia matumizi ya pesa za familia, lakini kila mmoja wao ana maoni tofauti kuhusu bajeti ya familia. Huenda wangependa familia iende tafrija, lakini kila mmoja wao ana maoni tofauti kuhusu tafrija itakayofaa. Au, huenda wangependa ufanye vizuri shuleni, lakini kila mmoja ana wazo tofauti kuhusu njia bora ya kukusaidia.

      Somo ni: Kuwa na maoni tofauti hakumaanishi kwamba hakuna umoja. Watu wawili wanaopendana wanaweza kuwa na maoni tofauti. Hata hivyo, bado hungependa kusikia wazazi wako wakibishana. Ni nini kinachoweza kukusaidia?

      Mambo Unayoweza Kufanya

      Uwe na heshima. Ni rahisi kukasirishwa na ugomvi wa wazazi. Wao ndio wanaopaswa kukuwekea kielelezo kizuri. Hata hivyo, kumdharau mzazi kutazidisha tu matatizo katika familia. Isitoshe, Yehova Mungu anakuamuru uwaheshimu wazazi wako—hata inapokuwa vigumu kufanya hivyo.—Kutoka 20:12; Methali 30:17.

      Lakini, unaweza kufanya nini ikiwa jambo ambalo wazazi wako wanabishania linakuhusu? Kwa mfano, tuseme kwamba mzazi wako mmoja ni Mkristo na yule mwingine si mwamini. Huenda hali fulani zikatokea na kukulazimu kuchukua msimamo upande wa uadilifu pamoja na mzazi anayemwogopa Mungu. (Mathayo 10:34-37) Sikuzote fanya hivyo kwa “tabia-pole na heshima kubwa.” Huenda siku moja mfano wako unaweza kumvutia mzazi wako asiyeamini.—1 Petro 3:15.

      Usiwe na upendeleo. Unaweza kufanya nini wazazi wako wakitaka uwaunge mkono katika jambo ambalo halikuhusu moja kwa moja? Usiegemee upande wowote. Labda unaweza kuondoka na kusema kwa heshima: “Mama na Baba, ninawapenda nyote wawili. Lakini, tafadhali msiniombe niunge mkono upande mmoja au mwingine. Hilo ni kati yenu wawili.”

      Zungumza nao. Wajulishe wazazi wako jinsi unavyohisi wanapobishana. Tafuta wakati ambao unajua watakusikiliza, kisha uwaeleze kwa heshima kwamba kubishana kwao kunakufadhaisha, kunakuudhi, na hata kukuogopesha.—Methali 15:23; Wakolosai 4:6.

      Mambo ya Kutofanya

      Usijifanye mshauri wa ndoa. Ukiwa kijana, si kazi yako kutatua tofauti za wazazi wako. Kwa mfano: Wazia unasafiri katika ndege ndogo na unasikia rubani na msaidizi wake wakibishana. Huenda ukawa na wasiwasi. Itakuwaje ukiamua kuwafundisha marubani hao jinsi ya kuendesha ndege au hata kujaribu kuiendesha wewe mwenyewe?

      Vivyo hivyo, kujaribu ‘kuendesha mambo’ kwa kujihusisha katika matatizo ya ndoa ya wazazi wako kutaharibu mambo hata zaidi. Biblia inasema: “Kwa sababu ya kimbelembele mtu husababisha tu pambano, lakini wale wanaoshauriana pamoja wana hekima.” (Methali 13:10) Wazazi wako wanaweza kutatua matatizo yao vizuri zaidi wakiwa peke yao.—Methali 25:9.

      Usijitupe ulingoni. Tayari kelele za watu wawili wanaogombana zinaudhi. Mbona uongeze sauti yako? Hata ikiwa unaona kwamba unahitaji kuokoa jahazi, ukweli ni kwamba ni jukumu la wazazi wako—bali si lako—kutatua matatizo yao. Katika mambo yasiyokuhusu kama hayo, jitahidi kufuata shauri hili la Biblia: ‘kazia akili mambo yako mwenyewe.’ (1 Wathesalonike 4:11) Usikubali kuhusishwa katika mabishano.

      Usiwagonganishe. Vijana fulani huchangia mabishano kati ya wazazi wao kwa kuwachezea shere. Mama akisema hapana, wanajaribu kumshawishi Baba aseme ndiyo. Huenda ukapata uhuru kidogo kwa sababu ya ujanja wako, lakini mwishowe, kufanya hivyo kutazidisha tu matatizo katika familia.

      Usiruhusu mwenendo wao uathiri mwenendo wako. Kijana anayeitwa Peter alikuwa akijiendesha isivyofaa eti kwa sababu baba yake ni mkatili. Peter anasema: “Nilitaka aone uchungu. Nilimchukia sana kwa sababu ya vile alivyonitendea mimi, mama yangu na dada yangu.” Hata hivyo, muda si muda utalazimika kuvuna ulichopanda. Hivyo, kujiendesha isivyofaa kutaongeza tu matatizo nyumbani.—Wagalatia 6:7.

      Andika hapa chini mambo unayohitaji kufanyia kazi zaidi kati ya mambo yaliyozungumziwa katika sura hii. ․․․․․

      Ni wazi kwamba huwezi kuwazuia wazazi wako wasigombane. Hata hivyo, uwe na hakika kwamba Yehova anaweza kukusaidia kukabiliana na mfadhaiko ambao ugomvi wao unakusababishia.—Wafilipi 4:6, 7; 1 Petro 5:7.

      Jitahidi kutumia madokezo yaliyozungumziwa. Mwishowe, huenda wazazi wako wakachochewa kufikiria kwa uzito jinsi wanavyoweza kutatua matatizo yao. Huenda hata wakaacha kugombana.

      KATIKA SURA INAYOFUATA

      Unaweza kushughulikia jinsi gani magumu ya kulelewa katika familia ya mzazi mmoja?

      MAANDIKO MUHIMU

      “Maneno yenu na yawe yenye neema sikuzote.”—Wakolosai 4:6.

      PENDEKEZO

      Ikiwa wazazi wako wanagombana vikali karibu kila siku, wapendekezee kwa heshima watafute usaidizi.

      JE, WAJUA . . .?

      Hata watu wanaopendana wanaweza kukosana nyakati nyingine.

      HATUA ZA KUCHUKUA!

      Wazazi wangu wakianza kugombana, nita ․․․․․

      Mmoja wa wazazi wangu akitaka nimuunge mkono, nitasema ․․․․․

      Mambo ambayo ningependa kuuliza mzazi (wazazi) wangu kuhusu habari hii ni ․․․․․

      UNA MAONI GANI?

      ● Kwa nini wazazi hugombana?

      ● Kwa nini huwezi kulaumiwa kwa sababu ya matatizo ya wazazi wako?

      ● Unaweza kujifunza nini kutokana na mwenendo wa wazazi wako?

      [Blabu katika ukurasa wa 201]

      “Kutambua kwamba wazazi wangu si wakamilifu na kwamba wana matatizo kama mimi kumenisaidia kuvumilia wanapogombana.’’—Kathy

      [Sanduku/Picha katika ukurasa wa 206, 207]

      Namna gani wazazi wangu wakitengana?

      Wazazi wako wakitengana, unaweza kutendaje kwa hekima licha ya hasira kali ambayo huenda ukawa nayo? Fikiria mapendekezo yanayofuata:

      ● Usitarajie mambo yasiyowezekana. Huenda jambo la kwanza ambalo ungetaka kufanya ni kuwaunganisha tena wazazi wako. Anne anakumbuka: “Baada ya kutengana, bado wazazi wetu walikuwa wakitupeleka matembezi mara kwa mara. Mimi na dada yangu tulikuwa tukinong’onezeana, ‘Tukimbie tuwaache pamoja.’ Lakini wapi! Hawakurudiana.”

      Andiko la Methali 13:12 linasema: “Tarajio lililocheleweshwa linafanya moyo uwe mgonjwa.” Ili kujiepusha na mkazo usio wa lazima, kumbuka kwamba huwezi kuwafanyia maamuzi wazazi wako. Kwa kuwa si wewe uliyefanya watengane, basi utawezaje kuwafanya warudiane?—Methali 26:17.

      ● Epuka chuki. Kufungia kinyongo na chuki moyoni kumwelekea mzazi mmoja au wote wawili kunaweza kukuletea madhara makubwa. Tom anakumbuka alivyohisi alipokuwa na umri wa miaka 12: “Nilianza kumchukia baba yangu. Sipendi kutumia neno ‘chuki,’ lakini nilikuwa na kinyongo kwelikweli. Sikuelewa jinsi angeweza kudai kwamba anatujali na wakati uleule atuache.”

      Hata hivyo, kutengana hakutokei kwa sababu mzazi mmoja ni malaika na yule mwingine ni mwovu. Ukweli ni kwamba, huenda wazazi wako hawajakuambia mambo yote yaliyosababisha watengane; huenda hata wao wenyewe hawaelewi. Kwa hiyo, epuka kukata kauli kwa kuwa kuna mambo ambayo hujui. (Methali 18:13) Ni kweli kwamba si rahisi kuepuka kukasirika, na kwa kawaida utakuwa na hasira kali kwa muda fulani. Lakini kuendelea kuwa na hasira na kisasi kunaweza kuharibu utu wako. Biblia ina sababu nzuri ya kutuambia: “Acha hasira na uache ghadhabu.”—Zaburi 37:8.

      ● Uwe na usawaziko. Badala ya kumchukia mzazi aliyeondoka, vijana fulani hupita mipaka kwa kuanza kumwabudu. Kwa mfano, baba ya kijana mmoja alikuwa mlevi na mwasherati aliyeiacha familia yake mara nyingi na mwishowe akapata talaka. Hata hivyo, kijana huyo anakumbuka kwamba kwa sababu moja au nyingine, bado alimhusudu sana baba yake!

      Visa kama hivyo ni vya kawaida. Katika nchi fulani, asilimia 90 ya watoto ambao wazazi wao wametalikiana wanaishi na mama yao na kumtembelea baba yao mara kwa mara. Hivyo, mama ndiye mwenye jukumu la kuwatunza watoto kila siku—kutia ndani kuwatia nidhamu. Ijapokuwa baba anamtegemeza kwa kulipia gharama fulani, mara nyingi uwezo wa kifedha wa mama hupungua sana baada ya talaka. Kwa upande mwingine, huenda uwezo wa kifedha wa baba ukaongezeka. Matokeo: Watoto wanapomtembelea Baba wanapata zawadi na mambo mengi yenye kuwafurahisha! Wanaporudi kwa Mama hali ni ngumu na sheria chungu nzima. Inasikitisha kwamba, vijana fulani hata wamemwacha mzazi Mkristo na kwenda kuishi na mzazi asiye mwamini ambaye ana mali nyingi zaidi na anawaruhusu kufanya wapendalo.—Methali 19:4.

      Ikiwa uko katika hali kama hiyo, fikiria mambo yaliyo ya maana zaidi. Kumbuka kwamba unahitaji nidhamu na mwongozo unaofaa wa kiadili. Hakuna kingine chochote ambacho mzazi anaweza kukupa kitakachokuwa na matokeo makubwa zaidi katika utu wako na maisha yako kuliko nidhamu na mwongozo wa kiadili.—Methali 4:13.

      [Picha katika ukurasa wa 202, 203]

      Kijana anayewaambia wazazi wake namna ya kutatua matatizo yao ni kama abiria anayewaambia marubani namna ya kuendesha ndege

  • Ninaweza Kuwa na Furaha Katika Familia ya Mzazi Mmoja?
    Maswali Ambayo Vijana Huuliza—Majibu Yafanyayo Kazi, Buku la 2
    • SURA YA 25

      Ninaweza Kuwa na Furaha Katika Familia ya Mzazi Mmoja?

      “Watoto katika familia zilizo na wazazi wawili wana vyumba vya kulala nao hununua nguo mpya. Lakini mimi sina chumba changu mwenyewe; nami sina nguo ninazotaka. Mama husema kwamba hana pesa. Kwa kuwa mimi hufanya kazi nyingi nyumbani mama akiwa kazini, mimi hujiona kama mfanyakazi wa nyumbani—badala ya kuwa nikifurahia maisha kama watoto wengine.”—Shalonda, mwenye umri wa miaka 13.

      BILA shaka, familia ilikusudiwa iwe na wazazi wawili. Baba na mama, wakiwa pamoja, wanaweza kutoa mwongozo, ulinzi, na utegemezo. “Wawili ni bora kuliko mmoja,” yasema Biblia, “kwa sababu wakiwa pamoja waweza kufanya kazi kwa matokeo zaidi.”—Mhubiri 4:9, Today’s English Version.

      Hata hivyo, familia za wazazi wawili leo ni kama wanyama walio katika hatari ya kutoweka. Kwa mfano, zaidi ya nusu ya watoto nchini Marekani, wataishi angalau kwa muda fulani na mzazi mmoja kabla ya kufikia umri wa miaka 18.

      Ijapokuwa kuna familia nyingi za mzazi mmoja, bado vijana wengi walio katika familia hizo huaibikia hali yao. Wengine hulemewa na mikazo na matatizo yanayowapata. Ikiwa familia yenu ni ya mzazi mmoja, ni mikazo gani unayopata? Kwenye nafasi iliyo hapa chini, andiko tatizo linalokusumbua zaidi.

      ․․․․․

      Kwa kuwa hupati upendo na utunzaji wa yule mzazi mwingine, je, inamaanisha kwamba hutawahi kuwa na furaha maishani? Sivyo hata kidogo! Mengi yanategemea maoni yako. Andiko la Methali 15:15 linasema: “Siku zote za mwenye kuteseka ni mbaya, lakini mtu aliye mchangamfu moyoni huwa na karamu sikuzote.” Kama methali hiyo inavyodokeza, mara nyingi hali ya moyoni ya mtu inategemea mtazamo wake bali si hali zake maishani. Unaweza kufanya nini ili uwe “mchangamfu moyoni” licha ya hali zako maishani?

      Ondolea Mbali Hisia Zisizofaa

      Kwanza, jaribu kutoruhusu mambo ambayo wengine wanasema yakufanye uvunjike moyo. Kwa mfano, walimu fulani husema bila kufikiri mambo yenye kuvunja moyo kuhusu wanafunzi kutoka katika familia ya mzazi mmoja. Wengine hata huamini kwamba tabia yoyote mbaya inatokana na malezi mabaya. Lakini jiulize: ‘Je, wanaosema mambo hayo wananijua vizuri mimi na familia yetu? Au wanaropoka tu mambo ambayo wamesikia wengine wakisema kuhusu familia za mzazi mmoja?’

      Kumbuka kwamba maneno “mvulana asiye na baba” yanapatikana mara nyingi katika Maandiko. Maneno hayo hayatumiwi kamwe kwa njia yenye kushusha heshima. Katika karibu masimulizi yote hayo, Yehova anaonyesha hangaiko la pekee kuelekea watoto wanaolelewa katika familia ya mzazi mmoja.a

      Kwa upande mwingine huenda watu ambao hawana nia mbaya wakawa waangalifu kupita kiasi wanapozungumza na wewe. Kwa mfano, huenda wakaepuka kutumia maneno kama vile “baba,” “ndoa,” “talaka,” au “kifo,” wakiogopa kwamba maneno hayo huenda yakakuudhi au kukuaibisha. Je, mambo kama hayo yanakusumbua? Ikiwa ndivyo, basi waambie kwa busara kwamba hawahitaji kuwa waangalifu kupita kiasi wanapozungumza nawe. Tony mwenye umri wa miaka 14, hakumjua baba yake mzazi. Anasema kwamba watu fulani husita kutumia maneno fulani wanapozungumza naye. Hata hivyo, Tony mwenyewe huyatumia maneno hayo anapozungumza nao. Anasema: “Ninataka wajue kwamba sionei aibu hali yangu.”

      Epuka Kusema “Laiti”

      Ni kawaida kuhuzunika na kusononeka ikiwa wazazi wako wametalikiana au mzazi wako mpendwa anapokufa. Hata hivyo, mwishowe unahitaji kukubali ukweli wa mambo. Biblia inatoa shauri hili: “Usiseme: ‘Kwa nini siku za zamani zilikuwa bora kuliko hizi?’” (Mhubiri 7:10) Kuhusiana na hilo, Sarah mwenye umri wa miaka 13, ambaye wazazi wake walitalikiana alipokuwa na miaka 10, anapendekeza hivi: “Usisononeke daima, huku ukisema ‘laiti,’ au kuhisi una matatizo kwa sababu unatoka katika familia ya mzazi mmoja, au kwamba watoto wengine walio na wazazi wote wawili wanaishi raha mustarehe.” Hilo ni shauri zuri. Kwa kuwa, hata familia za wazazi wawili zina matatizo yake pia.

      Kwa nini usiione familia yenu kama timu ya wapiga-makasia katika mashua? Ni kweli kwamba mashua inahitaji idadi kamili ya wapiga-makasia. Katika familia ya mzazi mmoja, mmoja wa wapiga-makasia anakosekana, kwa hiyo, waliobaki wanahitaji kufanya kazi kwa bidii zaidi. Je, inamaanisha kwamba familia hiyo haiwezi kufaulu? Hapana! Waliobaki wakishirikiana pamoja, mashua hiyo inaweza kuendelea kuelea mpaka mwisho wa safari.

      Je, Unatimiza Sehemu Yako?

      Ni nini hasa unachoweza kufanya ili kuhakikisha kwamba, pamoja na wengine katika familia yenu, unatimiza sehemu yako? Fikiria madokezo matatu yafuatayo:

      Jifunze kutumia pesa kwa uangalifu. Familia nyingi za mzazi mmoja zina matatizo ya pesa. Unaweza kufanya nini ili kusaidia? Tony, aliyetajwa mapema, anasema: “Watoto shuleni kwetu huwalazimisha wazazi wao wawanunulie viatu na nguo za bei ghali. Ama sivyo, hawaendi shuleni. Sina nguo za bei ghali, hata hivyo, nguo zangu ni nadhifu na safi, nami huzitunza vizuri. Mama yangu anafanya kila awezalo; singependa kufanya maisha yawe magumu kwake.” Ukiongeza bidii, unaweza kumwiga mtume Paulo, aliyesema: “Nimejifunza kuridhika na vitu nilivyo navyo. . . . Nimejizoeza kuridhika katika kila hali na mahali.”—Wafilipi 4:11, 12, BHN.

      Njia nyingine ya kutumia pesa kwa uangalifu ni kutumia kwa hekima vitu ulivyo navyo. (Yohana 6:12) Kijana Rodney anasema: “Mimi hujitahidi kuwa mwangalifu nisiharibu au kuvunja vitu nyumbani, kwa kuwa pesa zitahitajika ili kuvirekebisha au kununua vingine. Mimi huzima umeme iwapo hautumiki. Hilo hupunguza gharama ya umeme tunaotumia.”

      Chukua hatua. Wazazi wengi katika familia ya mzazi mmoja huogopa kuweka sheria za nyumbani au kuwaomba watoto wao wasaidie kufanya kazi za nyumbani. Kwa nini? Wengine huhisi kwamba wanahitaji kujazia nafasi ya mzazi ambaye hayuko kwa kutowalemea watoto wao kwa kuwapa kazi nyingi. Huenda wakasema: ‘Ninataka watoto wangu wafurahie maisha kama watoto wengine.’

      Kwa hiyo, huenda ukafurahia hali hiyo na kuketi kitako tu. Lakini kufanya hivyo ni kumwongezea mzigo mzazi wako. Mbona usijitolee kusaidia katika kazi za nyumbani? Ona kile ambacho Tony alijitolea kufanya. Anasema: “Mama yangu anafanya kazi hospitalini na nguo zake za kazi zinahitaji kupigwa pasi. Hivyo, mimi humpigia pasi.” Je, hiyo si kazi ya wanawake? “Wengine wanafikiri hivyo,” anasema Tony. “Lakini ninamsaidia mama yangu, kwa hiyo mimi huifanya.”

      Onyesha shukrani. Mbali na kusaidia, unaweza pia kumtia moyo mzazi wako kwa kumshukuru. Mzazi mmoja asiye na mwenzi aliandika: “Mara nyingi, ninapokuwa nimevunjika moyo au kuudhika kwa sababu ya tatizo fulani kazini—ninaporudi nyumbani, ninakuta binti yangu amepanga meza na kuanza kutayarisha chakula cha jioni.” Kisha anaongeza: “Mwanangu hunikumbatia.” Anahisije? Anasema: “Ninakuwa na furaha tena.”

      Andika hapa mambo unayohitaji kufanyia kazi kati ya madokezo hayo matatu. ․․․․․

      Kuishi katika familia ya mzazi mmoja kunakupa nafasi ya kukuza sifa kama vile huruma, ukarimu, na kutegemeka. Pia, Yesu alisema: “Kuna furaha zaidi katika kutoa kuliko ilivyo katika kupokea.” (Matendo 20:35) Nawe utakuwa na furaha kubwa zaidi ukijitolea kumsaidia mzazi wako.

      Ni kweli kwamba mara kwa mara huenda ukatamani kwamba yule mzazi mwingine angekuwako. Hata hivyo, unaweza kujifunza kufanya yote uwezayo katika hali zako. Ndivyo alivyoona msichana anayeitwa Nia. Anasema: “Baada ya baba yangu kufa, mtu fulani aliniambia ‘maisha yako hayategemei hali zako bali hutegemea mtazamo wako,’ na mpaka leo nakumbuka maneno yake. Yananikumbusha kwamba naweza kuwa na furaha licha ya hali zangu.” Unaweza kuwa na mtazamo kama huo. Kumbuka kwamba si hali zako zinazofanya uwe na furaha bali ni maoni yako na jinsi unavyotenda ukiwa katika hali hizo.

      PATA HABARI ZAIDI KATIKA BUKU LA 1, SURA YA 4

      [Maelezo ya Chini]

      a Kwa mfano, ona Kumbukumbu la Torati 24:19-21 na Zaburi 68:5.

      MAANDIKO MUHIMU

      “Pasiwe na mtu anayetafuta faida yake mwenyewe tu bali faida ya mwenzake.”—Wafilipi 2:4, BHN.

      PENDEKEZO

      Ikiwa unaona kwamba una majukumu mengi kupita uwezo wako, mweleze mzazi wako kwa busara ajaribu mambo yafuatayo:

      ● Atengeneze orodha inayoonyesha kazi zote ambazo kila mmoja katika familia anapaswa kufanya.

      ● Ikihitajika, wengine wenye uwezo katika familia wanaweza kugawiwa kazi zinazowalemea washiriki fulani.

      JE, WAJUA . . .?

      Kutimiza majukumu mbalimbali nyumbani kunaweza kukusaidia kukomaa haraka kuliko watoto walio katika familia zenye wazazi wawili ambao mara nyingi hawapewi majukumu yoyote.

      HATUA ZA KUCHUKUA!

      Nitazuia hisia zisizofaa kwa ․․․․․

      Ikiwa watu ninaochangamana nao huumia hisia kwa urahisi, nitasema ․․․․․

      Mambo ambayo ningependa kuuliza mzazi (wazazi) wangu kuhusu jambo hili ni ․․․․․

      UNA MAONI GANI?

      ● Kwa nini watu fulani huwabagua watoto wanaotoka katika familia za mzazi mmoja?

      ● Kwa nini huenda wazazi wako wakasita kukuomba usaidie kufanya kazi fulani za nyumbani?

      ● Unaweza kumwonyesha jinsi gani mzazi wako kwamba unamthamini?

      Blabu katika ukurasa wa 211]

      ‘‘Tangu wazazi wangu watalikiane, mimi na mama hupata muda mwingi wa kuzungumza; tumekuwa na uhusiano wa karibu sana.’’—Melanie

      [Picha katika ukurasa wa 210, 211]

      Familia ya mzazi mmoja ni kama mashua inayokosa mmoja wa wapiga-makasia—wale wengine watalazimika kuongeza bidii, hata hivyo, wanaweza kufanikiwa wakifanya kazi bega kwa bega

  • Daftari—Wazazi Wako
    Maswali Ambayo Vijana Huuliza—Majibu Yafanyayo Kazi, Buku la 2
    • SEHEMU YA 6

      Daftari—Wazazi Wako

      Andika hali ngumu zaidi unayokabili nyumbani na kwa nini unaiona ikiwa ngumu sana.

      ․․․․․

      Baada ya kusoma sehemu hii, unapanga kushughulika na hali hiyo jinsi gani?

      ․․․․․

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki