-
Vijana Wanakabili HatariAmkeni!—2005 | Aprili 8
-
-
Vijana Wanakabili Hatari
◼ Nchini Marekani, mwanafunzi mwenye umri wa miaka 15 awafyatulia wanadarasa wenzake risasi na kuwaua 2 kati yao na kuwajeruhi 13.
◼ Nchini Urusi, kikundi cha vijana waliolewa wanamwua kikatili msichana mwenye umri wa miaka tisa na kumpiga baba yake na binamu yake.
◼ Nchini Uingereza, mvulana mwenye umri wa miaka 17 ampiga na kumchoma kisu kijana mwingine mdogo. Anawaambia polisi hivi: “Mwanzoni, sikutaka kumwua, lakini nilipoona damu nilishindwa kujizuia.”
VISA hivi vyenye kushtua ni vya kawaida. Makala moja katika gazeti Professional School Counseling inasema “jeuri inayofanywa na vijana ni tatizo kubwa katika jamii yetu.” Takwimu zinaunga mkono jambo hilo.
Kituo cha Kitaifa cha Takwimu za Elimu cha Marekani kinasema kwamba ingawa visa vya jeuri inayofanywa shuleni vimepungua, “wanafunzi wenye umri kati ya miaka 12 hadi 18 walipatwa na visa karibu milioni 2 vya wizi au vya jeuri ambayo haikusababisha kifo wakiwa shuleni katika mwaka wa 2001.” Kudhulumiwa shuleni pia kumeongezeka.
Lakini jeuri inayofanywa na vijana nchini Marekani haiwapati wanafunzi peke yao. Ripoti hiyo inasema, “katika kipindi cha zaidi ya miaka 5 kuanzia 1997 hadi 2001, walimu walipatwa na visa milioni 1.3 hivi vya jeuri isiyosababisha kifo shuleni, kutia ndani visa 817,000 vya wizi na visa 473,000 vya jeuri ya kikatili.” Isitoshe, “asilimia 9 ya walimu wa shule za msingi na wa sekondari walitishwa kuumizwa na mwanafunzi, na asilimia 4 kati yao walishambuliwa na mwanafunzi.”
Hali ikoje katika nchi nyingine? Shirika moja la habari linaripoti kwamba, “katika mwaka wa 2003, vijana 69,780 waliovunja sheria walikamatwa nchini China, ongezeko la asilimia 12.7 zaidi ya waliokamatwa katika mwaka wa 2002.” Ripoti hiyo inasema kwamba “asilimia 70 ya vijana walivunja sheria wakiwa katika kikundi.” Pia, ripoti moja kutoka Japani katika mwaka wa 2003 ilisema kwamba vijana walihusika katika nusu ya visa vya jeuri vilivyofanywa katika miaka kumi iliyopita.
Dawa za Kulevya Zinadhuru Miili ya Vijana
Jambo jingine linaloonyesha kwamba vijana wengi wanakabili hatari ni jinsi wanavyodhuru miili yao kwa dawa za kulevya. Ripoti ya Taasisi ya Kitaifa ya Dawa za Kulevya ya Marekani inasema kwamba karibu nusu ya vijana wote nchini humo wamewahi kutumia dawa fulani ya kulevya isiyo halali kabla ya kumaliza shule ya sekondari. Ripoti hiyo inaongeza hivi: “Vijana wengi sana leo hutumia vinywaji vinavyolevya. Karibu wanafunzi wanne kati ya watano (asilimia 77) wametumia vinywaji hivyo (si kuonja tu) kufikia wakati wanapomaliza shule ya sekondari; na karibu nusu yao (asilimia 46) wamevitumia kufikia wakati wanapoingia darasa la nane.”
Ngono za Ovyoovyo
Bila shaka, ngono za ovyoovyo ni hatari wakati huu ambapo UKIMWI umeenea. Hata hivyo, vijana wengi wanaona ngono kuwa mchezo usio hatari. Kwa mfano, vijana fulani nchini Marekani hutumia neno la utani “kula uroda” linalomaanisha kwamba kufanya ngono ovyoovyo ni raha isiyoweza kudhuru. Wao huzungumza kuhusu kuwa na “mshikaji,” yaani, kuwa na mtu wa kufanya ngono naye bila kuwajibika kwake.
Mwandishi Scott Walter anaeleza kuhusu karamu za ngono ambazo vijana fulani wanaoishi katika vitongoji vya miji huandaa wazazi wao wanapokuwa kazini. Kwenye karamu moja kama hiyo, msichana mmoja alitangaza kwamba “atafanya ngono na wavulana wote waliokuwapo. . . . Watoto wadogo wenye umri wa miaka 12 walihusishwa katika karamu hizo.”
Je, hilo linashangaza? Haliwashangazi wataalamu ambao wamechunguza tabia ya vijana ya kufanya ngono. Dakt Andrea Pennington anaandika hivi: “Katika zaidi ya miaka 20 ambayo imepita, tumeona umri wa wastani ambao vijana hufanya ngono ukipungua. Limekuwa jambo la kawaida kwa wavulana na wasichana wenye umri wa miaka 12 kuanza kufanya ngono.”
Ripoti ambayo hasa inatia wasiwasi ilichapishwa katika gazeti USA Today: “Vijana wadogo wengi zaidi nchini humu . . . wanafanya ngono ya kinywa. . . . Watoto hao wanaamini kwamba ‘huko si kufanya ngono.’” Kulingana na uchunguzi fulani waliofanyiwa wasichana 10,000, “asilimia 80 kati yao walisema kwamba wao ni mabikira, ijapokuwa asilimia 25 walikuwa wamefanya ngono za kinywa. Na asilimia 27 walisema kwamba hilo ni ‘jambo ambalo mtu hufanya na mshikaji wake ili kujifurahisha.’”
Mtazamo huo kuhusu ngono umeanza kuathiri maeneo mengine. Shirika la UNESCO linaripoti kwamba, “ni rahisi kwa vijana wengi wa Asia kupata virusi vya UKIMWI kwa kufanya ngono na watu wa jinsia zote kwa sababu wengi wanaanza kufanya ngono wakiwa na umri mdogo.” Ripoti hiyo inaongeza hivi: “Vijana wengi zaidi wanapuuza kanuni za wazazi wao za Kiasia kwa kufanya ngono kabla ya ndoa, mara nyingi wakifanya hivyo na watu tofauti-tofauti.”
Kuna dalili gani nyingine kwamba vijana wanataabika? Gazeti la Kanada Women’s Health Weekly linaripoti: “Asilimia 25 ya wasichana kati ya umri wa miaka 16 hadi 19 watapatwa na kisa kimoja cha kushuka moyo sana.” Hata hivyo, mshuko-moyo ni ugonjwa unaowapata watu wa jinsia zote. Kulingana na U.S.News & World Report, kila mwaka, vijana elfu tano hujiua. Kwa sababu fulani, ripoti hiyo inasema, “wavulana sita zaidi ya wasichana, hujiua.”
Bila shaka, vijana wa leo wanakabili hatari sana. Ni nini kinachosababisha hali hiyo?
-
-
Mikazo Inayowakumba Vijana wa LeoAmkeni!—2005 | Aprili 8
-
-
Mikazo Inayowakumba Vijana wa Leo
KUBALEHE kunaweza kuwa kipindi kigumu hata ikiwa kijana yuko chini ya hali nzuri. Katika kipindi hicho, vijana hupatwa na hisia ambazo hawajawahi kuwa nazo. Kila siku wao hukabili mikazo kutoka kwa walimu na vijana wengine. Wao hukabili uvutano kutoka kwenye televisheni, filamu, muziki, na Intaneti. Hivyo, ripoti ya Umoja wa Mataifa inaeleza kwamba kubalehe ni “kipindi cha badiliko ambacho huwa na mfadhaiko na mikazo.”
Kwa kusikitisha, mara nyingi vijana hawana uzoefu wa kushughulika na mfadhaiko na mikazo katika njia inayofaa. (Methali 1:4) Bila mwongozo unaofaa, ni rahisi wajihusishe katika tabia zinazodhuru. Kwa mfano, ripoti hiyo ya Umoja wa Mataifa inasema: “Utafiti unaonyesha kwamba mara nyingi vijana huanza kutumia dawa za kulevya wanapobalehe au wanapokaribia kuwa watu wazima.” Ndivyo ilivyo kuhusu tabia nyingine mbaya kama vile jeuri na ngono za ovyoovyo.
Wazazi wanaofikiri kwamba mambo hayo hutukia tu miongoni mwa “maskini” au watu wa kabila fulani hukosea sana. Matatizo ambayo vijana wanakabili leo huwapata wote bila kujali hali za kiuchumi, za kijamii, na za kikabila. Mwandishi Scott Walter anaandika hivi: “Ikiwa unafikiri kwamba vijana wanaovunja sheria ni wavulana wachache tu wa kabila fulani dogo wenye umri wa miaka 17 wanaoishi mitaani na ambao mama zao maskini hupokea msaada kutoka kwa serikali, basi hujui ni nini kinachoendelea. Siku hizi, mtoto mwenye matatizo hayo anaweza kuwa mzungu, anaweza kuishi katika eneo la matajiri, anaweza kuwa na umri unaopungua (sana) miaka 16, na anaweza kuwa msichana.”
Lakini kwa nini vijana wengi sana wamo hatarini? Je, vijana wa zamani hawakukabili magumu na vishawishi? Ndiyo, lakini tunaishi katika kipindi kinachotajwa na Biblia kuwa “nyakati za hatari zilizo ngumu kushughulika nazo.” (2 Timotheo 3:1-5) Kuna hali na magumu fulani ya pekee yanayowapata vijana hasa wakati huu. Acheni tuchunguze baadhi ya hali hizo.
Mabadiliko Katika Familia
Kwa mfano, fikiria hali zinazobadilika katika familia. “Zaidi ya mtoto mmoja kati ya watatu nchini Marekani hushuhudia wazazi wake wakitalikiana kabla ya kufikia umri wa miaka 18,” linaripoti jarida linaloitwa Journal of Instructional Psychology. Takwimu kama hizo zinapatikana pia katika nchi nyingine za Magharibi. Ndoa inapovunjika, vijana hulazimika kukabiliana na hisia zenye uchungu. Jarida hilo linasema kwamba “kwa ujumla, ni vigumu kwa watoto ambao wazazi wametalikiana hivi karibuni kufanya vizuri sana shuleni au kuchangamana na watoto wengine kuliko inavyokuwa kwa watoto wa familia ambazo wazazi wako pamoja, familia za mzazi mmoja zilizo imara, au wa familia zenye mzazi wa kambo . . . Isitoshe, mara nyingi talaka ya wazazi huathiri hali nzuri ya kihisia na ya kujiheshimu ya mtoto.”
Pia idadi inayoongezeka ya wanawake wanaoajiriwa imeanza kuathiri familia. Uchunguzi mmoja kuhusu vijana wanaofanya uhalifu nchini Japani ulionyesha kwamba ni vigumu zaidi kuwatunza watoto katika familia ambazo wazazi wote wameajiriwa kuliko ilivyo katika familia ambazo mzazi mmoja hushinda nyumbani.
Ni kweli kwamba familia nyingi zinahitaji mishahara ya watu wawili ili kuandaa mahitaji ya msingi. Pia mishahara ya watu wawili inaweza kuwaandalia watoto maisha ya starehe zaidi. Lakini kuna tatizo: Mamilioni ya watoto wanapotoka shuleni hawampati mtu nyumbani. Mara nyingi wazazi wanaporudi wanakuwa wamechoka na wana matatizo mengi ya kazini. Matokeo huwaje? Vijana wengi hawapati uangalifu wa kutosha kutoka kwa wazazi. Kijana mmoja alisema hivi: “Hatutumii wakati tukiwa pamoja kama familia.”
Wachunguzi wengi wanahisi hiyo si dalili nzuri ya wakati ujao kwa vijana. Dakt. Robert Shaw anasema hivi: “Naamini kwamba njia ambazo wazazi wametumia kuwalea watoto wao katika miaka thelathini iliyopita, zinawafanya watoto waepuke kuwa na uhusiano na familia zao, wasipende kuzungumza, wawe na matatizo ya kujifunza, na wasiweze kudhibitiwa. Wazazi hujikuta wakiwa wamenaswa katika jamii inayokazia kupata mali na mafanikio yanayopita kiasi na hilo huwafanya watumie wakati mwingi sana kazini na watumie pesa nyingi sana hivi kwamba hawawezi kupata wakati wa kufanya mambo ya lazima ili wawe na uhusiano wa karibu pamoja na watoto wao.”
Jambo jingine linalotisha hali ya vijana ni hili: Mara nyingi watoto ambao wazazi wao hufanya kazi wana wakati mwingi wa kufanya mambo bila uangalizi wa wazazi na hilo linaweza kutokeza matatizo.
Maoni Yanayobadilika Kuhusu Nidhamu
Maoni yanayobadilika kuhusu nidhamu kutoka kwa wazazi yanawaathiri vijana wa leo. Kama Dakt. Ron Taffel alivyosema waziwazi, wazazi wengi “huachilia madaraka yao.” Wanapofanya hivyo, vijana hukua bila sheria au miongozo yoyote ya kudhibiti tabia zao.
Katika visa fulani, inaonekana maoni ya wazazi kuhusu nidhamu huathiriwa na mambo yaliyowapata walipokuwa watoto. Wanataka kuwa marafiki wa watoto wao wala si watoa nidhamu. Mama mmoja anasema hivi: “Niliachilia mambo sana. Wazazi wangu walikuwa wakali sana nami nilitaka kumtendea mtoto wangu kwa njia tofauti. Lakini nilikosea.”
Ni mambo gani ambayo wazazi hufanya ili kuepuka kutoa nidhamu? Gazeti USA Today linaripoti hivi: “Uchunguzi wa hivi karibuni wa vijana 600 hivi wanaotibiwa athari za dawa za kulevya huko New York, Texas, Florida na California ulionyesha kwamba asilimia 20 kati yao wametumia dawa za kulevya mbali na vinywaji vinavyolewesha wakiwa na wazazi wao, na kwamba asilimia 5 hivi walionyeshwa jinsi ya kutumia dawa hizo—hasa bangi—na baba au mama zao.” Ni nini ambacho kingemchochea mzazi kufanya jambo hilo la kipumbavu? Mzazi mmoja alikiri hivi: “Nilimwambia binti yangu kwamba ni afadhali atumie dawa hizo nyumbani, mahali ambapo ningeweza kumwona.” Yaonekana wengine wanafikiri kwamba kutumia dawa za kulevya pamoja na watoto wao ni njia ya “kuimarisha” uhusiano wao.
Wanaathiriwa na Vyombo vya Habari
Pia kuna uvutano wenye nguvu wa vyombo vya habari. Kulingana na mtafiti Marita Moll, uchunguzi mmoja ulionyesha kwamba kwa wastani, vijana nchini Marekani walitumia saa nne na dakika 48 kila siku wakitazama televisheni au wakitumia kompyuta.
Je, jambo hilo linaweza kuwa na madhara? Makala moja iliyochapishwa katika gazeti Science iliripoti kwamba “mashirika sita makubwa ya kitaaluma nchini Marekani,” kutia ndani Shirika la Kitiba la Marekani, yanakubaliana kwamba jeuri inayoonyeshwa katika vyombo vya habari inahusiana na “tabia ya jeuri ambayo watoto fulani wanayo.” Gazeti hilo lilisema kwamba, “licha ya wataalamu kukubaliana, inaonekana kwamba watu wa kawaida hawaelewi habari zinazotolewa katika vyombo vya habari kwamba jeuri inayoonyeshwa katika vyombo hivyo hufanya jamii iwe yenye jeuri zaidi.”
Kwa mfano, fikiria video za muziki. Mara nyingi, wazazi hushtuka kuona jinsi baadhi ya video hizo zinavyoonyesha ngono waziwazi. Je, kweli zinaweza kuathiri tabia ya vijana fulani? Kulingana na uchunguzi mmoja uliofanyiwa wanafunzi 500 wa chuo, “maneno ya muziki wenye jeuri yaliwafanya wawe na mawazo na hisia zenye jeuri zaidi.” Kulingana na uchunguzi mwingine wa hivi karibuni, “inaelekea kwamba vijana wanaotumia wakati mwingi zaidi wakitazama ngono na jeuri inayoonyeshwa katika video hizo za muziki wa rapu watafanya mambo hayo.” Uchunguzi huo uliofanyiwa zaidi ya wasichana 500 ulionyesha kwamba wale wanaotumia muda mwingi wakitazama video hizo yaelekea watampiga mwalimu, watakamatwa, au watafanya ngono na watu tofauti-tofauti.
Vijana na Kompyuta
Katika miaka ya karibuni kompyuta pia imekuwa na uvutano mkubwa katika fikira za vijana. Jarida Pediatrics linasema kwamba, “idadi ya kompyuta zinazotumiwa nyumbani imeongezeka sana katika miaka ya hivi karibuni. Nchini kote [Marekani], nyumba mbili kati ya tatu zilizo na watoto wenye umri wa kwenda shule (miaka 6 hadi 17) zilikuwa na kompyuta . . . Asilimia ya watoto waliokuwa na umri wa kati ya miaka 3 hadi 17 nchini Marekani na walioishi katika nyumba iliyokuwa na kompyuta iliongezeka kutoka asilimia 55 katika mwaka wa 1998 hadi asilimia 65 katika mwaka wa 2000.” Katika nchi nyingine pia idadi ya watu wanaotumia kompyuta imeongezeka.
Hata hivyo, kijana hahitaji kuwa na kompyuta yake ili aitumie. Hivyo, mtafiti mmoja anadai kwamba “karibu asilimia 90 ya vijana walio na umri kati ya miaka 5 hadi 17 hutumia kompyuta, na asilimia 59 kati yao hutumia Intaneti.” Hilo hufanya vijana waweze kupata habari nyingi kuliko wakati mwingine wowote na hilo ni jambo zuri ikiwa kompyuta itatumiwa vizuri, mtu mzima akiwepo. Lakini kwa kusikitisha, wazazi wengi sana wamewaruhusu vijana watumie kompyuta bila usimamizi wowote.
Ili kuonyesha hilo, mtafiti Moll anaandika katika jarida Phi Delta Kappan kwamba kulingana na uchunguzi uliofanywa katika mwaka wa 2001 kuhusu kutumia Intaneti, “asilimia 71 ya wazazi walifikiri kwamba walijua ‘kiasi kikubwa au kiasi kinachofaa’ kuhusu jinsi watoto wao wanavyotumia Intaneti. Hata hivyo, wakati watoto walipoulizwa swali hilohilo, asilimia 70 kati yao walisema kwamba wazazi wao ‘walijua kidogo sana au hata hawakujua chochote’ kuhusu jinsi walivyotumia Intaneti.” Kulingana na uchunguzi huo, “asilimia 30 ya watoto walio na umri wa miaka 9 hadi 10 walisema kwamba walitumia vituo vya Intaneti vya kibinafsi na vile vinavyopaswa kutumiwa na watu wazima peke yao. Tatizo hilo linakuwa baya zaidi kwa kuwa asilimia 58 ya watoto walio na umri wa miaka 11 hadi 12, asilimia 70 ya walio na umri wa miaka 13 hadi 14, na asilimia 72 ya wale walio na umri wa miaka 15 hadi 17 wameripoti kwamba wamewahi kutumia vituo hivyo. . . . Katika uchunguzi uliofanywa nchini Uingereza kuhusu kutumia Intaneti nyumbani, mzazi mmoja kati ya saba alikiri kwamba hakujua lolote kuhusu mambo ambayo watoto wake walikuwa wakitazama kwenye vituo vya Intaneti.”
Vijana wanapotumia Intaneti bila kusimamiwa wanaweza kutazama ponografia. Hata hivyo, kuna hatari nyingi zaidi. Taffel aliyetajwa mapema, anasema: “Watoto wetu wanafanya marafiki shuleni na kwenye Intaneti, na kwa sababu hiyo wanatumia wakati mwingi na watoto ambao mara nyingi hatuwajui.”
Ni wazi kwamba vijana wa leo wanapatwa na mikazo na matatizo ambayo vijana wa zamani hawakupatwa nayo. Basi haishangazi kwamba vijana wengi wanajiendesha kwa njia inayotia wasiwasi! Je, kuna lolote linaloweza kufanywa ili kuwasaidia vijana wa leo?
[Blabu katika ukurasa wa 6]
“Naamini kwamba njia ambazo wazazi wametumia kuwalea watoto wao katika miaka thelathini iliyopita, zinawafanya watoto waepuke kuwa na uhusiano na familia zao, wasipende kuzungumza, wawe na matatizo ya kujifunza, na wasiweze kudhibitiwa.”—DAKT. ROBERT SHAW
[Picha katika ukurasa wa 6, 7]
Hali katika familia imebadilika kwa kuwa wanawake wengi zaidi wameajiriwa
[Picha katika ukurasa wa 7]
Ni rahisi kwa vijana kuingia katika taabu wasiposimamiwa
[Picha katika ukurasa wa 8]
Watafiti wamehusianisha video za muziki zenye jeuri na mwenendo wenye jeuri
[Picha katika ukurasa wa 9]
Je, unajua watoto wako wanatazama nini kwenye Intaneti?
-