-
Vijana Wanaofurahisha Moyo wa YehovaMnara wa Mlinzi—2003 | Aprili 15
-
-
Vijana Wanaofurahisha Moyo wa Yehova
Makala haya ya funzo yaliandikwa hasa kwa ajili ya vijana miongoni mwa Mashahidi wa Yehova. Kwa hiyo, tunawatia moyo vijana wajifunze makala haya kwa makini na kutoa maelezo wakati wa Funzo la Mnara wa Mlinzi kutanikoni.
“Mwanangu, uwe na hekima na kunifurahisha moyo wangu; Ili nipate kumjibu anilaumuye.”—Mithali 27:11.
1, 2. (a) Ikiwa unavutiwa na mambo ya ulimwengu, je, hiyo inamaanisha kwamba hufai kuwa Mkristo? (Waroma 7:21) (b) Unajifunza nini kutokana na mfano wa Asafu? (Ona sanduku, ukurasa wa 13.)
WAZIA kwamba unanunua nguo. Unapotafuta-tafuta unaona nguo inayokuvutia. Mtindo na rangi zinakufaa kabisa, na bei yake ni nafuu sana. Lakini unapoichunguza kwa makini zaidi unatambua kwamba kitambaa kimechakaa kwenye pindo na nguo hiyo imeshonwa ovyoovyo. Ijapokuwa inavutia, nguo hiyo ni duni. Je, ungenunua nguo duni kama hiyo?
2 Linganisha hilo na hali unayoweza kukabili ukiwa kijana Mkristo. Kama vile nguo hiyo inavyovutia unapoiona kwa mara ya kwanza, ndivyo ilivyo na mambo ya ulimwengu. Kwa mfano, huenda wanafunzi wenzako wanaenda kwenye karamu zinazofurahisha, wanatumia dawa za kulevya na vileo, na wasichana na wavulana wanafanya urafiki bila kusudi la kuoana, na hata wanafanya uasherati. Je, nyakati nyingine unavutiwa na maisha hayo? Je, unatamani kuishi angalau kwa muda mfupi maisha hayo yanayosemekana eti ni yenye uhuru? Ikiwa ndivyo, usikate kauli haraka kwamba wewe ni mwovu na hufai kuwa Mkristo. Ukweli ni kwamba Biblia inaonyesha kuwa hata mtu anayetaka kumpendeza Mungu anaweza kuvutiwa sana na ulimwengu.—2 Timotheo 4:10.
3. (a) Kwa nini ni ubatili kufuatia mambo ya ulimwengu? (b) Mkristo mmoja anaelezaje ubatili wa kufuatia mambo ya ulimwengu?
3 Tafadhali sasa chunguza mambo ya ulimwengu kwa makini kama vile ungechunguza nguo unayotaka kununua. Jiulize hivi: ‘Ulimwengu huu una ubora gani?’ Biblia inasema kwamba “ulimwengu unapitilia mbali.” (1 Yohana 2:17) Raha yoyote inayopatikana humo ni ya muda tu. Isitoshe, mwenendo mpotovu unaleta matokeo mabaya. Hauna faida yoyote. Mkristo mmoja ambaye “ameteseka kwa sababu ya mwenendo mpotovu wa ujanani” anasema hivi: “Huenda ulimwengu ukaonekana kuwa wenye kupendeza na kuvutia. Nao unataka uamini kwamba unaweza kupata raha za ulimwengu bila kuumia. Lakini hilo haliwezekani. Ulimwengu utakudanganya, kisha utakutupa.”a Mbona uharibu ujana wako kwa kuishi maisha mapotovu?
Kulindwa Dhidi ya “Yule Mwovu”
4, 5. (a) Muda mfupi kabla ya kifo chake, Yesu alimwomba Yehova nini katika sala? (b) Kwa nini ombi hilo lilifaa?
4 Vijana miongoni mwa Mashahidi wa Yehova hujitahidi kuepuka urafiki na ulimwengu huu kwa sababu wanatambua kwamba ulimwengu huu hauwezi kuwapa vijana kitu chochote chenye thamani halisi. (Yakobo 4:4) Je, wewe ni mmojawapo wa vijana hao waaminifu? Ikiwa ndivyo unastahili pongezi. Ni kweli kwamba si rahisi kuwa tofauti na vijana wengine na kupinga vishawishi vyao, lakini unaweza kupata msaada.
5 Muda mfupi kabla ya kifo chake, Yesu alisali kwa Yehova ‘awalinde’ wanafunzi wake “kwa sababu ya yule mwovu.” (Yohana 17:15) Yesu alikuwa na sababu nzuri ya kusali hivyo. Alijua kwamba haingekuwa rahisi kwa wafuasi wake kudumisha uaminifu, licha ya umri wao. Kwa nini? Yesu alijua kwamba wanafunzi wake wangemkabili adui mwenye nguvu asiyeonekana, yaani, “yule mwovu,” Shetani Ibilisi. Biblia inasema kwamba roho huyo mwovu “hutembea huku na huku kama simba anayenguruma, akitafuta sana kunyafua mtu fulani.”—1 Petro 5:8.
6. Tunajuaje kwamba Shetani hawahurumii vijana?
6 Tangu zamani, Shetani amefurahia kuwatesa wanadamu kikatili. Fikiria misiba mibaya ambayo Shetani alimletea Ayubu na familia yake. (Ayubu 1:13-19; 2:7) Huenda ukakumbuka mambo ambayo umesikia maishani mwako yanayoonyesha roho yenye jeuri ya Shetani. Ibilisi anatembea-tembea akitafuta mtu wa kunyafua, naye hawahurumii vijana. Kwa mfano, mwanzoni mwa karne ya kwanza W.K., Herode alitunga hila ya kuwaua wavulana wote Bethlehemu waliokuwa na umri wa miaka miwili au kwenda chini. (Mathayo 2:16) Inaelekea Shetani ndiye aliyemchochea Herode kufanya hivyo, kwa sababu alitaka kumwua yule mtoto ambaye siku moja angekuwa Mesiya aliyeahidiwa na kuleta hukumu ya Mungu juu ya Shetani! (Mwanzo 3:15) Ni wazi kwamba Shetani hawahurumii vijana hata kidogo. Lengo lake hasa ni kunyafua wanadamu wengi iwezekanavyo. Anafanya hivyo hasa wakati huu kwa sababu amevurumishwa kutoka mbinguni hadi duniani, “akiwa na hasira kubwa, akijua ana kipindi kifupi cha wakati.”—Ufunuo 12:9, 12.
7. (a) Yehova anatofautianaje sana na Shetani? (b) Yehova anahisije unapofurahia maisha?
7 Tofauti na Shetani, aliye na “hasira kubwa,” Yehova ni mwenye “huruma nyororo.” (Luka 1:78) Upendo wake hauna kifani. Muumba ana upendo mwingi sana hivi kwamba Biblia inasema: “Mungu ni upendo.” (1 Yohana 4:8) Kuna tofauti kubwa kama nini kati ya mungu wa ulimwengu huu na Mungu ambaye una pendeleo la kumwabudu! Shetani anataka kunyafua, lakini Yehova “hataki yeyote aangamizwe.” (2 Petro 3:9) Anaona uhai wa kila mwanadamu kuwa wenye thamani kutia ndani uhai wako. Yehova anapokushauri katika Neno lake usiwe sehemu ya ulimwengu, hataki kukuzuia usifurahie maisha au kukunyima uhuru. (Yohana 15:19) Badala yake anakulinda kwa sababu ya yule mwovu. Baba yako wa mbinguni anataka uwe na maisha bora badala ya maisha ya raha ya muda ya ulimwengu huu. Anataka upate “uhai ulio halisi,” yaani, uhai wa milele katika dunia paradiso. (1 Timotheo 6:17-19) Yehova anataka ufanikiwe, naye anakusihi ufikie mradi huo. (1 Timotheo 2:4) Isitoshe, Yehova anakupa mwaliko wa pekee. Ni mwaliko gani huo?
‘Furahisha Moyo Wangu’
8, 9. (a) Unaweza kumpa Yehova zawadi gani? (b) Shetani anamlaumuje Yehova, kama inavyoonyeshwa na kisa cha Ayubu?
8 Je, umewahi kumnunulia rafiki yako wa karibu zawadi, na kumwona akitabasamu kwa mshangao na uthamini anapoipokea? Yaelekea ulifikiri sana ni zawadi ya aina gani ambayo ingemfaa mtu huyo. Sasa fikiria swali hili: Unaweza kumpa Muumba wako, Yehova Mungu, zawadi gani? Huenda mwanzoni ukaona kwamba jambo hilo haliwezekani. Mungu Mweza Yote anahitaji nini kutoka kwa mwanadamu duni? Unaweza kumpa nini ambacho hana? Biblia inajibu hivi kwenye Mithali 27:11: “Mwanangu, uwe na hekima na kunifurahisha moyo wangu; ili nipate kumjibu anilaumuye.”
9 Huenda kupitia funzo lako la Biblia unajua kwamba Shetani Ibilisi ndiye anayemlaumu Yehova. Anadai kwamba wale wanaomtumikia Mungu wanamtumikia kwa sababu za ubinafsi wala si kwa sababu ya upendo. Shetani anadai kwamba wataacha ibada ya kweli wakipata magumu. Kwa mfano, fikiria kile ambacho Shetani alimwambia Yehova kumhusu mtu mwadilifu Ayubu: “Wewe hukumzingira kwa ukigo pande zote, pamoja na nyumba yake, na vitu vyote alivyo navyo? Kazi za mikono yake umezibarikia, nayo mali yake imeongezeka katika nchi. Lakini nyosha mkono wako sasa, uyaguse hayo yote aliyo nayo, naye atakukufuru mbele za uso wako.”—Ayubu 1:10, 11.
10. (a) Tunajuaje kwamba Shetani hakutilia shaka uaminifu wa Ayubu peke yake? (b) Unahusikaje katika suala la enzi kuu?
10 Kama Biblia inavyoonyesha, Shetani alitilia shaka uaminifu wa Ayubu na pia wengine wote wanaomtumikia Mungu, kutia ndani wewe. Naam, Shetani alimwambia Yehova hivi alipokuwa akizungumza kuwahusu wanadamu kwa ujumla: “Yote aliyo nayo mtu [si Ayubu tu bali mtu yeyote] atayatoa kwa ajili ya uhai wake.” (Ayubu 2:4) Je, unaona jinsi unavyohusika katika suala hilo muhimu? Kama inavyoonyeshwa na Mithali 27:11, Yehova anasema kwamba unaweza kumpa msingi wa kumjibu Shetani anayemlaumu. Wazia Mwenye Enzi Kuu ya Ulimwengu anakusihi wewe utoe jibu kuhusiana na suala kuu lililopo. Hilo ni daraka na pendeleo kubwa sana. Je, unaweza kutimiza yale ambayo Yehova anakusihi ufanye? Ayubu aliyatimiza. (Ayubu 2:9, 10) Ndivyo alivyofanya Yesu na vilevile wengine wengi tangu zamani, kutia ndani vijana. (Wafilipi 2:8; Ufunuo 6:9) Unaweza kufanya vivyo hivyo. Hata hivyo, unapaswa kujua kwamba ni lazima uunge mkono upande mmoja katika suala hilo. Kupitia mwenendo wako utaonyesha kwamba unatetea lawama ya Shetani au jibu la Yehova. Utatetea nini?
Yehova Anakujali!
11, 12. Je, uchaguzi wako wa kumtumikia au kutomtumikia Yehova ni muhimu kwake? Eleza.
11 Je, uchaguzi wako ni muhimu machoni pa Yehova? Je, uaminifu ambao watu wengi wameonyesha hautoshi kumpa sababu ya kumjibu Shetani? Ibilisi alidai kwamba hakuna mtu anayemtumikia Yehova kwa sababu ya kumpenda, dai ambalo limekwisha thibitishwa kuwa la uwongo. Lakini bado Yehova anataka uunge mkono upande wake katika suala la enzi kuu kwa sababu anakujali. Yesu alisema hivi: “Si jambo la kutamanika kwa Baba yangu aliye mbinguni kwa mmoja wa wadogo hawa kuangamia.”—Mathayo 18:14.
12 Ni wazi kwamba, Yehova anapendezwa na uchaguzi wako. Jambo muhimu zaidi ni kwamba anaathiriwa nao. Biblia inaonyesha wazi kwamba Yehova ana hisia ambazo huchochewa na mwenendo mzuri au mbaya wa binadamu. Kwa mfano, Yehova ‘alihuzunika,’ Waisraeli walipomwasi tena na tena. (Zaburi 78:40, 41) Kabla ya Gharika ya siku za Noa, wakati ‘maovu ya mwanadamu yalipokuwa makubwa,’ Yehova ‘alihuzunika moyo.’ (Mwanzo 6:5, 6) Fikiria maana ya jambo hilo. Ukiamua kuwa na mwenendo mbaya, utamhuzunisha Muumba wako. Hiyo haimaanishi kwamba Mungu ni dhaifu au anaongozwa na hisia tu. Badala yake anakupenda na kukujali. Kwa upande mwingine, unapofanya yanayofaa unafurahisha moyo wa Yehova. Yeye hufurahi kwa sababu anapata sababu nyingine ya kumjibu Shetani, na pia kwa sababu anaweza kukupa thawabu. Ndivyo anavyotaka kufanya. (Waebrania 11:6) Yehova Mungu ni Baba mwenye upendo kama nini!
Baraka Tele Sasa
13. Tunabarikiwaje sasa kwa kumtumikia Yehova?
13 Baraka za kumtumikia Yehova hazitapatikana tu wakati ujao. Vijana wengi miongoni mwa Mashahidi wa Yehova wana sababu nzuri za kuwa na shangwe na uradhi sasa. Mtunga-zaburi aliandika hivi: “Maagizo ya BWANA ni ya adili, huufurahisha moyo.” (Zaburi 19:8) Yehova anajua vizuri zaidi kile kinachotufaa kuliko mwanadamu yeyote. Yehova alisema hivi kupitia nabii Isaya: “Mimi ni BWANA, Mungu wako, nikufundishaye ili upate faida, nikuongozaye kwa njia ikupasayo kuifuata. Laiti ungalisikiliza amri zangu! ndipo amani yako ingalikuwa kama mto wa maji, na haki yako kama mawimbi ya bahari.”—Isaya 48:17, 18.
14. Kanuni za Biblia zinawezaje kukusaidia kuepuka deni lenye kulemea?
14 Kufuata kanuni za Biblia kutakusaidia kuepuka huzuni na uchungu mwingi. Kwa mfano, Biblia inasema kwamba wale wanaopenda pesa “wamejichoma wenyewe kotekote kwa maumivu mengi.” (1 Timotheo 6:9, 10) Je, baadhi ya rafiki zako wamepatwa na matokeo mabaya yanayotajwa katika andiko hilo? Baadhi ya wanaume na wanawake vijana wana madeni makubwa kwa sababu wanataka kuwa na nguo za mitindo maarufu na vitu vya karibuni. Kununua vitu usivyoweza kugharimia na hivyo kujikuta umelemewa kwa muda mrefu na mkopo wenye riba kubwa, ni utumwa unaoumiza!—Mithali 22:7.
15. Kanuni za Biblia zinakulindaje na matokeo yenye kuhuzunisha ya uasherati?
15 Fikiria pia uasherati. Ulimwenguni pote vijana wengi wasiofunga ndoa hupata mimba kila mwaka. Baadhi yao huzaa watoto wasiowataka wala wasio na uwezo wa kuwalea. Wengine hutoa mimba na hivyo husumbuliwa sana na dhamiri. Kisha kuna wanaume na wanawake vijana ambao hupata magonjwa yanayoambukizwa kupitia ngono, kama vile UKIMWI. Bila shaka kupoteza uhusiano mzuri pamoja na Yehova ndilo tokeo baya zaidi linaloweza kumpata mtu anayemjua Yehova.b (Wagalatia 5:19-21) Biblia ina sababu nzuri ya kusema hivi: “Ukimbieni uasherati.”—1 Wakorintho 6:18.
Kumtumikia “Mungu Mwenye Furaha”
16. (a) Tunajuaje kwamba Yehova anataka uufurahie ujana wako? (b) Kwa nini Yehova anakuwekea miongozo ya kufuata?
16 Biblia inamtaja Yehova kuwa “Mungu mwenye furaha.” (1 Timotheo 1:11) Anataka wewe uwe mwenye furaha pia. Neno lake mwenyewe linasema hivi: “Uufurahie ujana wako, na moyo wako ukuchangamshe siku za ujana wako.” (Mhubiri 11:9) Lakini Yehova anaona matokeo ya muda mrefu ya mwenendo mzuri au mbaya. Ndiyo sababu anakusihi: “Mkumbuke Muumba wako siku za ujana wako, kabla hazijaja siku zilizo mbaya, wala haijakaribia miaka utakaposema, Mimi sina furaha katika hiyo.”—Mhubiri 12:1.
17, 18. Kijana mmoja Mkristo alisema nini kuhusu furaha anayopata kwa kumtumikia Yehova, nawe unawezaje kupata furaha hiyo?
17 Leo vijana wengi wamepata furaha kwa kumtumikia Yehova. Kwa mfano, Lina mwenye umri wa miaka 15 anasema hivi: “Ninaweza kujiheshimu na kujitumaini. Nina afya nzuri kwa sababu sivuti sigara wala situmii dawa za kulevya. Ninapata mwongozo mzuri katika kutaniko ambao hunisaidia kushinda vishawishi vya Shetani. Ninafurahi sana kwa sababu ya ushirika wenye kujenga kwenye Jumba la Ufalme. Zaidi ya yote, nina tumaini lisilo na kifani la kuishi milele duniani.”
18 Kama Lina, vijana wengi Wakristo wanapigania imani kwa bidii na hiyo inawaletea shangwe. Wanajua kwamba ijapokuwa maisha yao ni magumu nyakati nyingine, wana kusudi maishani na tumaini halisi la wakati ujao. Kwa hiyo endelea kumtumikia Mungu anayekujali sana. Furahisha moyo wake, naye atakufurahisha sasa na milele!—Zaburi 5:11.
[Maelezo ya Chini]
a Ona makala “Kweli Ilinirudishia Uhai Wangu,” katika toleo la Amkeni! la Oktoba 22, 1996.
b Inafariji kujua kwamba mtu anapotubu, anapoacha kufanya mabaya, na kukiri dhambi zake, Yehova “atamsamehe kabisa.”—Isaya 55:7.
-
-
Yehova Hatasahau Kazi Yenu Enyi Vijana!Mnara wa Mlinzi—2003 | Aprili 15
-
-
Yehova Hatasahau Kazi Yenu Enyi Vijana!
“Mungu si asiye mwadilifu ili asahau kazi yenu na upendo mlioonyesha kwa ajili ya jina lake, kwa kuwa mmewahudumia watakatifu na mwaendelea kuhudumu.”—WAEBRANIA 6:10.
1. Kitabu cha Biblia cha Waebrania na Malaki kinaonyeshaje kwamba Yehova huthamini utumishi wako?
JE, UMEWAHI kumfanyia rafiki fulani tendo la fadhili naye akakosa kukushukuru? Unaweza kuhisi uchungu sana wakati unapomtendea mtu kwa fadhili lakini anakosa kuonyesha uthamini au hata anasahau kabisa kukushukuru. Hata hivyo, ni tofauti kama nini tunapomtumikia Yehova kwa moyo wote! Biblia inasema: “Mungu si asiye mwadilifu ili asahau kazi yenu na upendo mlioonyesha kwa ajili ya jina lake, kwa kuwa mmewahudumia watakatifu na mwaendelea kuhudumu.” (Waebrania 6:10) Hilo linamaanisha nini? Yehova angeliona jambo hilo kuwa ukosefu wa uadilifu kwa upande wake, yaani dhambi, kama angesahau kile ambacho umefanya na unachoendelea kufanya katika utumishi wake. Yeye ni Mungu mwenye shukrani kama nini!—Malaki 3:10.
2. Kwa nini kumtumikia Yehova ni jambo la pekee sana?
2 Una pendeleo la pekee la kumwabudu na kumtumikia Mungu huyo mwenye shukrani. Pendeleo hilo ni la pekee sana kwa kuwa kati ya watu bilioni sita ulimwenguni pote, ni watu wapatao milioni sita tu wanaomwabudu Yehova. Isitoshe, kusikiliza na kukubali kwako ujumbe wa habari njema kunaonyesha kwamba Yehova anapendezwa nawe. Ndiyo sababu Yesu alisema: “Hakuna mtu awezaye kuja kwangu isipokuwa Baba, aliyenituma, amvute yeye.” (Yohana 6:44) Naam, Yehova huwasaidia watu wanufaike na dhabihu ya Kristo.
Kuthamini Pendeleo Lako la Pekee
3. Wana wa Kora walionyeshaje uthamini kwa pendeleo la kumtumikia Yehova?
3 Kama tulivyozungumzia katika makala iliyotangulia, una pendeleo la pekee la kuufurahisha moyo wa Yehova. (Mithali 27:11) Hupaswi kamwe kupuuza pendeleo hilo. Wana wa Kora walionyesha uthamini wao kwa pendeleo la kumtumikia Yehova katika mojawapo ya zaburi walizoandika chini ya mwongozo wa roho. Tunasoma hivi: “Siku moja katika nyua zako ni bora kuliko siku elfu. Ningependa kuwa bawabu nyumbani mwa Mungu wangu, kuliko kukaa katika hema za uovu.”—Zaburi 84:10.
4. (a) Ni nini kinachoweza kufanya wengine waone kwamba ibada ya Yehova inawanyima uhuru? (b) Yehova huonyeshaje kwamba anawatambua watumishi wake na anatamani kuwapa thawabu?
4 Je, hivyo ndivyo unavyohisi kuhusu pendeleo lako la kumtumikia Baba yako wa mbinguni? Ni kweli kwamba huenda nyakati nyingine ukahisi kwamba ibada ya Yehova inakunyima uhuru. Bila shaka, unahitaji kujidhabihu kwa kadiri fulani ili kuishi kupatana na kanuni za Biblia. Hata hivyo, chochote ambacho Yehova anataka ufanye ni kwa faida yako. (Zaburi 1:1-3) Isitoshe, Yehova anaona jitihada zako naye anaonyesha wazi kwamba anathamini uaminifu wako. Kwa kweli, Paulo aliandika kwamba Yehova “huwa mthawabishaji wa wale wanaomtafuta kwa bidii.” (Waebrania 11:6) Yehova anatafuta nafasi za kukupa thawabu. Nabii mwadilifu wa Israeli la kale alisema: “Kwa maana macho ya BWANA hukimbia-kimbia duniani mwote, ili ajionyeshe mwenye nguvu kwa ajili ya hao, waliokamilika moyo kuelekea kwake.”—2 Mambo ya Nyakati 16:9.
5. (a) Mojawapo ya njia bora zaidi za kuonyesha kwamba moyo wako ni kamili kwa Yehova ni ipi? (b) Kwa nini huenda ikaonekana kuwa vigumu kuwaeleza wengine kuhusu imani yako?
5 Njia moja bora zaidi ya kuonyesha kwamba moyo wako ni kamili kwa Yehova ni kuwaeleza wengine juu yake. Je, umewahi kupata nafasi ya kuwaeleza baadhi ya wanafunzi wenzako kuhusu imani yako? Huenda mwanzoni jambo hilo likaonekana kuwa gumu na pengine ukaogopa kidogo. Huenda ukajiuliza, ‘Vipi wakinicheka au wakiona kwamba dini yangu ni ya kiajabu-ajabu?’ Yesu alisema kwamba si kila mtu atakayesikiliza ujumbe wa Ufalme. (Yohana 15:20) Hata hivyo, hiyo haimaanishi kwamba utadhihakiwa na kukataliwa daima. Kinyume cha hilo, vijana wengi Mashahidi wamesikilizwa, na hata wameheshimiwa na wanafunzi wenzao kwa sababu wanaishi kupatana na imani yao.
“Yehova Atakusaidia”
6, 7. (a) Msichana mmoja mwenye umri wa miaka 17 aliwezaje kuwatolea wanafunzi wenzake ushahidi? (b) Umejifunza nini kutokana na kisa cha Jennifer?
6 Lakini unawezaje kupata ujasiri wa kuzungumza kuhusu imani yako? Mbona usiazimie kusema waziwazi watu wanapokuuliza kuhusu dini yako? Fikiria kisa cha Jennifer mwenye umri wa miaka 17. Anasema hivi: “Tulikuwa tukila chakula cha mchana shuleni. Wasichana walioketi karibu nami walikuwa wakizungumza juu ya dini na mmoja wao akaniuliza mimi ni mfuasi wa dini gani.” Je, Jennifer aliogopa alipojibu? Anasema: “Bila shaka niliogopa kwa sababu sikujua watasema nini.” Kwa hiyo Jennifer alifanya nini? Anaendelea: “Niliwaambia wasichana hao kwamba mimi ni mmoja wa Mashahidi wa Yehova. Kwanza walishangaa. Yaelekea, walifikiri kwamba Mashahidi wa Yehova si watu wa kawaida. Hilo lilifanya waniulize maswali, nami niliweza kusahihisha maoni fulani yasiyofaa waliyokuwa nayo. Hata baada ya siku hiyo, baadhi ya wasichana walinijia mara kwa mara ili kuuliza maswali.”
7 Je, Jennifer alighairi kwamba alizungumza kuhusu imani yake? Hata kidogo! Anasema: “Nilifurahi sana baada ya kipindi hicho cha mapumziko ya mchana. Sasa wasichana hao wanaelewa imani ya Mashahidi wa Yehova vizuri zaidi.” Jennifer anatoa ushauri huu: “Ukiona ni vigumu kuwatolea wanafunzi wenzako au walimu ushahidi toa sala fupi. Yehova atakusaidia. Utafurahi kwamba ulitumia vizuri nafasi hiyo kutoa ushahidi.”—1 Petro 3:15.
8. (a) Sala ilimsaidiaje Nehemia alipokabili hali isiyotazamiwa? (b) Huenda ukahitaji kutoa sala fupi ya moyoni kwa Yehova unapokabili hali zipi shuleni?
8 Ona kwamba Jennifer anapendekeza ‘utoe sala fupi’ kwa Yehova unapopata nafasi ya kutoa ushahidi kuhusu imani yako. Hivyo ndivyo Nehemia, mnyweshaji wa Mfalme Artashasta wa Uajemi, alivyofanya alipokabili hali isiyotazamiwa. Nehemia alionekana kuwa mwenye huzuni kwa sababu alikuwa ameelezwa juu ya hali mbaya ya Wayahudi na kwamba ukuta na malango ya Yerusalemu yalikuwa yameharibika. Mfalme aliona kwamba Nehemia alikuwa na wasiwasi, basi akamwuliza alikuwa na tatizo gani. Kabla ya kumjibu, Nehemia alisali ili kupata mwongozo. Kisha kwa ujasiri akaomba ruhusa ya kurudi Yerusalemu akasaidie kujenga upya jiji lililobomoka. Artashasta alikubali ombi lake. (Nehemia 2:1-8) Unajifunza nini kutokana na hilo? Ukiwa na wasiwasi unapopata nafasi ya kutoa ushahidi kuhusu imani yako, usikose kutoa sala ya moyoni. Petro aliandika hivi: ‘Mtupieni Yehova hangaiko lenu lote, kwa sababu yeye huwajali nyinyi.’—1 Petro 5:7; Zaburi 55:22.
“Tayari Kujitetea”
9. Leah mwenye umri wa miaka 13 aliwezaje kuwaachia wanafunzi wenzake nakala 23 za kitabu Vijana Huuliza?
9 Fikiria kisa kingine. Leah, mwenye umri wa miaka 13, alikuwa akisoma kitabu Maswali Ambayo Vijana Huuliza—Majibu Yafanyayo Kazia wakati wa mapumziko ya mchana shuleni. Anasema: “Wanafunzi wengine walikuwa wakinitazama, punde si punde wanafunzi wengi walisimama nyuma yangu na kutazama. Kisha wakaanza kuuliza maswali kuhusu kitabu hicho.” Wasichana wanne walimwomba Leah kitabu Vijana Huuliza siku hiyo. Muda mfupi baada ya hapo wasichana hao walisoma vitabu hivyo pamoja na wengine, kisha hao pia wakataka nakala zao. Leah aliwaachia wanafunzi wenzake na marafiki wake nakala 23 za kitabu Vijana Huuliza katika majuma machache yaliyofuata. Je, ilikuwa rahisi kwa Leah kutoa ushahidi hapo mwanzoni wengine walipomwuliza juu ya kitabu alichokuwa akisoma? Sivyo! Anasema hivi: “Mwanzoni, nilikuwa na wasiwasi. Hata hivyo, nilisali, na nilijua kwamba Yehova alikuwa pamoja nami.”
10, 11. Msichana mdogo Mwisraeli aliwezaje kumsaidia mkuu wa jeshi la Siria ajifunze kumhusu Yehova, na mtu huyo alifanya mabadiliko gani baadaye?
10 Huenda kisa cha Leah kikakukumbusha hali iliyompata msichana mdogo Mwisraeli aliyepelekwa utekwani huko Siria. Mkuu wa jeshi la Siria, Naamani, alikuwa mwenye ukoma. Inawezekana kwamba mke wake ndiye aliyeanzisha mazungumzo yaliyomsukuma huyo msichana mdogo kumweleza imani yake. Alisema: “Laiti bwana wangu angekuwa pamoja na yule nabii aliyeko Samaria! Maana angemponya ukoma wake.”—2 Wafalme 5:1-3.
11 Kwa sababu ya ujasiri wa msichana huyo mdogo, Naamani alipata kujua kwamba “hakuna Mungu duniani mwote, ila katika Israeli.” Hata aliazimia kwamba ‘hangetoa tena sadaka ya kuteketezwa wala dhabihu kwa miungu mingine, ila kwa BWANA.’ (2 Wafalme 5:15, 17) Bila shaka Yehova alibariki tendo la ujasiri la msichana huyo mdogo. Anaweza, na anataka kuwabariki vijana leo pia. Leah amepata baraka kama hizo. Baada ya muda mfupi, baadhi ya wanafunzi wenzake walimwendea na kumwambia kwamba kitabu Vijana Huuliza kimewasaidia kufanya mabadiliko katika mwenendo wao. Leah anasema, “Nilifurahi kwa sababu nilijua kwamba nilikuwa nikiwasaidia wengine wajifunze kumhusu Yehova na kufanya mabadiliko maishani.”
12. Unawezaje kuimarishwa kutetea imani yako?
12 Wewe pia unaweza kupata matokeo mazuri kama Jennifer na Leah. Fuata ushauri wa Petro, aliyeandika kwamba sikuzote Mkristo anapaswa kuwa ‘tayari kujitetea mbele ya kila mtu ambaye hudai kwake sababu ya tumaini lililo katika yeye, akifanya hivyo kwa tabia-pole na staha yenye kina kirefu.’ (1 Petro 3:15) Unawezaje kufuata ushauri huo? Iga mfano wa Wakristo wa karne ya kwanza waliomwomba Yehova awasaidie kuhubiri “kwa ujasiri wote.” (Matendo 4:29) Kisha uwe na ujasiri unapozungumza na wengine juu ya imani yako. Huenda ukapata matokeo mazuri kuliko ulivyotazamia. Isitoshe, utaufurahisha moyo wa Yehova.
Video na Miradi Hususa
13. Vijana fulani wametumia nafasi zipi ili kutoa ushahidi? (Ona masanduku kwenye ukurasa wa 20 na 21.)
13 Vijana wengi wamewaeleza wanafunzi wenzao au walimu imani yao kwa kutumia video. Nyakati nyingine, wamepata nafasi ya kumsifu Yehova kupitia miradi mbalimbali ya shule. Kwa mfano, wavulana wawili wenye umri wa miaka 15, ambao ni Mashahidi wa Yehova, waliambiwa waandike ripoti katika somo lao la historia kuhusu mojawapo ya dini za ulimwengu. Wavulana hao walishirikiana kuandika ripoti kuwahusu Mashahidi wa Yehova wakitumia habari iliyo katika kitabu Mashahidi wa Yehova—Wapiga-Mbiu wa Ufalme wa Mungu.b Pia, walipaswa kutoa hotuba ya dakika tano. Baadaye, mwalimu na wanafunzi walikuwa na maswali mengi sana hivi kwamba wavulana hao waliendelea na mazungumzo darasani kwa dakika nyingine 20. Kwa majuma kadhaa baadaye, wanafunzi waliendelea kuuliza maswali kuwahusu Mashahidi wa Yehova!
14, 15. (a) Kwa nini kuwaogopa wanadamu ni mtego? (b) Kwa nini unapaswa kuwaelezea wengine imani yako bila woga?
14 Kama inavyoonyeshwa na visa hivyo, unaweza kupata baraka nyingi kwa kuwaeleza wengine juu ya imani yako ukiwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova. Usipoteze pendeleo na shangwe ya kuwasaidia wengine wamjue Yehova kwa sababu ya kuwaogopa wanadamu. Biblia inasema: “Kuwaogopa wanadamu huleta mtego; bali amtumainiye BWANA atakuwa salama.”—Mithali 29:25.
15 Kumbuka kwamba ukiwa kijana Mkristo, una kitu fulani ambacho vijana wenzako wanahitaji sana, yaani, maisha bora sasa na ahadi ya kuishi milele wakati ujao. (1 Timotheo 4:8) Ijapokuwa huenda ukafikiri kwamba watu hawapendezwi na dini nchini Marekani, jambo la kupendeza ni kwamba kura ya maoni ilionyesha kuwa nusu ya vijana nchini humo wanapendezwa sana na dini, na theluthi moja wanasema kwamba dini ni ‘muhimu sana maishani mwao.’ Yaelekea ndivyo ilivyo katika sehemu nyinginezo ulimwenguni. Kwa hiyo huenda wanafunzi wenzako wakafurahia kusikiliza mambo unayowaeleza kuhusu Biblia.
Mkaribie Yehova Ewe Kijana
16. Mbali na kuongea na wengine kumhusu Yehova, ni nini kingine kinachohitajiwa ili kumpendeza?
16 Bila shaka, haitoshi tu kuzungumza juu ya Yehova ili kuufurahisha moyo wake. Unahitaji pia kufuata kanuni zake maishani mwako. Mtume Yohana aliandika: “Hivi ndivyo kumpenda Mungu humaanisha, kwamba tushike amri zake; na bado amri zake si zenye kulemea.” (1 Yohana 5:3) Ukimkaribia Yehova, utaona kwamba amri zake si zenye kulemea. Unawezaje kufanya hivyo?
17. Unawezaje kumkaribia Yehova?
17 Tafuta wakati wa kusoma Biblia na vichapo vinavyozungumzia Biblia. Kadiri unavyojifunza mengi kumhusu Yehova, ndivyo itakavyokuwa rahisi kumtii na kuwaeleza wengine juu yake. Yesu alisema: ‘Mtu mwema hutokeza mema katika hazina njema ya moyo wake, kwa maana katika wingi wa moyo kinywa chake husema.’ (Luka 6:45) Hivyo, jaza moyo wako mambo mema. Mbona usijiwekee miradi ya kufanya hivyo? Labda unaweza kufanya maendeleo katika kutayarisha mikutano ya kutaniko ya juma lijalo. Huenda mradi mwingine ukawa kutoa maelezo mafupi kutoka moyoni. Bila shaka ni muhimu pia kutenda kulingana na yale unayojifunza.—Wafilipi 4:9.
18. Unaweza kuwa na hakika gani hata unapopingwa?
18 Kumtumikia Yehova huleta baraka za milele. Ni kweli kwamba huenda pindi fulani ukapingwa au kudhihakiwa kwa kuwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova. Lakini mfikirie Musa. Biblia inasema kwamba “alikaza macho kuelekea malipo ya thawabu.” (Waebrania 11:24-26) Wewe pia unaweza kuwa na hakika kwamba Yehova atabariki jitihada zako za kujifunza na kuzungumza juu yake. Hakika, ‘hatasahau kamwe kazi yako na upendo ulioonyesha kwa ajili ya jina lake.’—Waebrania 6:10.
-