Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • “Utamaduni wa Mauaji” Huendelezwaje?
    Amkeni!—2000 | Julai 8
    • Ulimwengu wa Vitumbuizo

      Sinema hutumia kwa faida habari zinazohusu kifo. Kwa mfano, sinema yaweza kutukuza mno ukosefu wa adili, jeuri, ulanguzi wa dawa za kulevya, au uhalifu uliopangwa na hivyo kupunguza thamani ya uhai na kudunisha kanuni za adili. Hata kuna sinema zinazotilia chumvi kifo—zikikazia hekaya ya uhai baada ya kifo na dhana ya wafu fulani kurudi na kuwatembelea walio hai—hekaya hizo hudunisha kifo.

      Ndivyo ilivyo na vipindi fulani vya televisheni na muziki. Kwa mujibu wa ripoti za habari, wale vijana wauaji wa Littleton walikuwa wapenzi shupavu wa mwimbaji mmoja wa roki ambaye amejulikana sana kwa sababu ya “picha zake za wake-dume, na za kishetani,” na nyimbo “zinazokazia uasi na kifo.”

      Huko Marekani, njia ya kuainisha vipindi vya televisheni ilirekebishwa ili kuwalinda vijana wasiangalie mambo yanayoweza kuwadhuru. Hata hivyo hali imezidi kuzorota. Jonathan Alter, aeleza kwenye gazeti Newsweek kwamba uainishaji huo wa televisheni “waweza kuwachochea watoto watamani zaidi mambo yasiyo ya adili.” Aliongezea kwamba ili kuwafedhehesha na kuwashurutisha wale wenye wajibu wapunguze jeuri kwenye vyombo vya habari, itambidi Rais Clinton “atangaze hadharani majina ya kampuni zote kubwa (na maofisa wake wakuu)” ambao mbali na kutunga sinema za kudungana visu na kurekodi ‘muziki wa rapu ya magenge,’ pia hubuni programu za michezo ya kompyuta inayowawezesha watoto “waue watu ‘kihalisi’.”

      Mauaji Kwenye Michezo ya Kompyuta na Kwenye Internet

      Katika kitabu chake The Deathmatch Manifesto, Robert Waring achanganua jinsi ambavyo vijana hupenda ile inayoitwa eti michezo ya misafara ya mauaji.a Bw. Waring anaamini kwamba kikundi kingine cha siri cha wachezaji wa michezo hiyo kimezuka. Kwa kweli michezo hiyo hufunza kuua badala ya kuelimisha. “Mtu huathiriwa sana anapocheza na mpinzani aliye hai kutoka mahali popote ulimwenguni, na kujaribu kuthibitisha kuwa ana uwezo. Ni rahisi mno kutumbukia katika mtego huo,” aeleza Waring. Vijana hunaswa na uvutano wa mandhari kamili zilizobuniwa ili kuremba mapambano yaliyojaa umwagikaji-damu. Wengine hununua programu za michezo ya kompyuta ili wazitumie kwenye televisheni nyumbani wanapokosa Internet. Wengine huzuru kumbi za umma kwa kawaida ambako hukodi mashine za michezo ya kompyuta na kupigana ‘kihalisi’ hadi kifo na wapinzani wengine.

      Ijapokuwa michezo ya “misafara ya mauaji” huainishwa kulingana na umri wa mchezaji, ukweli ni kwamba haidhibitiwi vyakutosha. Eddie mwenye umri wa miaka 14 kutoka Marekani alisema hivi: “Kwa kawaida watu hukuambia ungali mtoto, lakini hawakuzuii kununua [mchezo huo].” Yeye hufurahia mchezo wenye mapambano kabambe ya ufyatulianaji risasi. Ingawa wazazi wake wanajua jambo hilo, nao wanalichukia, wao huchunguza mara chache sana kuona kama anaucheza mchezo huo. Kijana mmoja alifikia mkataa huu: “Kizazi chetu tofauti kabisa na kizazi kingine chochote kimekufa ganzi kabisa kuelekea jeuri. Televisheni huwalea watoto leo badala ya wazazi, na televisheni hutosheleza hamu ya watoto ya kuona jeuri.” John Leland, aliandika hivi kwenye gazeti Newsweek: “Huku vijana milioni 11 sasa wakitumia Internet [huko Marekani], wengi hutumia wakati mwingi zaidi katika mazingira wasiyojua wazazi wengi.”

  • Kuwasaidia Vijana Waepuke “Utamaduni wa Mauaji”
    Amkeni!—2000 | Julai 8
    • Kuwasaidia Vijana Waepuke “Utamaduni wa Mauaji”

      Ni nini kinachowafanya vijana wavutiwe na mauaji leo? Henry Hyde, Mbunge wa jimbo la Illinois, Marekani, alisema hivi: “Vijana hawa wana utupu wa kiroho ambao hujazwa na utamaduni wa mauaji na jeuri.”

      MSOMAJI mmoja wa gazeti Time aliandika: “Utamaduni wa mauaji uliopo miongoni mwa vijana wetu leo husababishwa na wazazi wazembe, vitumbuizo vya jeuri na ukosefu wa msingi maalum wa kiadili na kiroho.”

      Tatizo jingine kubwa linalowasumbua vijana ni upweke. Wengine huishi na wazazi ambao hushinda kazini mchana kutwa; wengine wana mzazi mmoja tu. Kichapo kimoja chasema kwamba, wabalehe huko Marekani hubaki peke yao kwa muda wa saa tatu na nusu kila siku nao huwa pamoja na wazazi wao kwa muda unaopungua saa 11 kila juma tofauti na ilivyokuwa kwa vijana walioishi miaka ya 1960. Kwa kweli, vijana fulani, mbali na kutupiliwa mbali na wazazi wao, hawategemezwi kihisia-moyo.

      Wanaloweza Kufanya Wazazi

      Fungu la wazazi ni muhimu kadiri gani tuzingatiapo “utupu wa kiroho” ambao vijana hukabiliana nao? Wazazi wenye hekima hufahamu kwamba watoto wao wanahitaji vitumbuizo vinavyofaa pamoja na msaada wa kibinafsi wa kawaida. Huku wakichochewa na upendo, wazazi waweza kuzungumza nao kuhusu muziki, vipindi vya televisheni, vidio, riwaya, michezo ya kompyuta, na sinema wanazopenda. Vijana wengi hutamani sana kupata urafiki na mwongozo wenye upendo wa wazazi wao japo huenda wasiseme. Wanahitaji majibu yaliyo wazi kwa sababu wanaishi katika ulimwengu usioaminika kabisa. Watu wazima wapaswa kufahamu kwamba watoto wanakabili ulimwengu mgumu zaidi kuliko ule ambao wao walikabili walipokuwa vijana.

      Wazazi wanaotaka kuwalinda watoto wao watawasiliana nao kwa ukawaida, watawasikiliza kwa makini, na kuwaonya kuhusu hatari za utamaduni wa kisasa. Wazazi wanapoweka mipaka imara na isiyobadilika-badilika na wanapokuwa tayari kusababu na kuwaonyesha urafiki watoto wao, kwa kawaida watafanikiwa.—Mathayo 5:37.

      Wazazi ambao ni Mashahidi wa Yehova hujitahidi kuzungumza na watoto wao kwa ukawaida wakitumia Biblia na vichapo na vidio zinazotegemea Biblia.a Wao hawatumii pindi hizo kuwaadhibu watoto, bali kuzungumzia mambo yenye kujenga kiroho. Katika vikusanyiko hivyo vya familia, wao husikiliza matatizo au magumu yanayomkumba kila mtoto na hilo hutokeza fursa ya kumpa kila kijana msaada wa kibinafsi.

      Vijana wasiopokea mwongozo wa kiroho kutoka kwa wazazi wao wanaweza kuimarishwa na Zaburi 27:10, inayosema hivi: ‘Baba yangu na mama yangu wakiniacha, BWANA atanikaribisha kwake.’ Yehova, Baba wa rehema nyororo, huwasaidiaje vijana? Makutaniko ya Mashahidi wa Yehova yamekuwa kimbilio ambamo wengi wamepata marafiki na wametatua matatizo yao. Josías, kijana aliyeona jambo hilo, asema: “Tengenezo la Yehova hutimiza fungu muhimu. Nilihisi kwamba maisha hayakuwa na maana. Niliishi bila kusudi, bila tumaini. Kujua tu kwamba sikuwa peke yangu kulibadili kabisa maisha yangu. Nilihisi kwamba ndugu katika kutaniko walichukua mahali pa familia yangu iliyopotea. Wazee na familia katika kutaniko ni kama nanga ya kihisia-moyo.”

      Kwa kweli, vijana na watu wazima wengi wameboresha afya yao ya kiakili na ya kiroho kwa kuhudhuria mikutano ya kutaniko ya Mashahidi wa Yehova kwa kawaida. Mtaalamu wa Elimu ya Binadamu Patricia Fortuny alieleza kuhusu ushirika huo unaojenga katika insha yake iitwayo Los Testigos de Jehová: una alternativa religiosa para enfrentar el fin del milenio (Mashahidi wa Yehova: Njia Badala ya Kidini ya Kukabili Mwisho wa Milenia): “Mashahidi wa Yehova hueleza utaratibu ulio wazi kabisa wa kufuata katika maisha ya kila siku, sheria na kanuni barabara zinazoongoza mawazo na mwenendo.” “Utaratibu wa kufuata” na “kanuni” zinazotajwa hapa hutegemea Biblia. Kwa hiyo, ingawa Mashahidi wa Yehova hukumbwa na matatizo na mikazo ileile sawa na jirani zao, wanaimarishwa na hekima isiyo na kifani ya kitabu hicho cha kale. Naam, Mashahidi hupata kimbilio katika itikadi zilizo wazi na kanuni zilizo katika Biblia.

      Wakati “Kifo Hakitakuwapo Tena”

      Mafundisho yanayotolewa kwenye Majumba ya Ufalme ya Mashahidi wa Yehova hukazia tena na tena ahadi ya Mungu ya ulimwengu mpya utakaokuwapo karibuni, ambamo “uadilifu utakaa” na ambamo ‘hakuna mtu atakayewatia hofu.’ (2 Petro 3:13; Mika 4:4) Isitoshe, nabii Isaya aandika kwamba wakati huo Mungu ‘atameza mauti hata milele, na Bwana Mungu atafuta machozi katika nyuso zote.’ Kifo kilikumba jamii ya kibinadamu kwa sababu ya ukiukaji-sheria wa mtu wa kwanza, Adamu, lakini Mungu aahidi kwamba karibuni “kifo hakitakuwapo tena.”—Isaya 25:8; Ufunuo 21:3, 4; Waroma 5:12.

      Endapo wewe ni kijana anayetafuta msaada, twakualika upate tumaini na kusudi la uhai kwa kusoma Biblia. Mashahidi wa Yehova watakusaidia uwe na tumaini la kwamba kutakuwa na maisha bora kabisa hivi karibuni katika ulimwengu mpya unaoahidiwa na Mungu.

      [Maelezo ya Chini]

      a Vidio Young People Ask—How Can I Make Real Friends? inatayarishwa na Watchtower Bible and Tract Society of New York, Inc. Kwa sasa iko kwa lugha ya Kiingereza nayo huandaa msaada wenye kutumika kwa vijana.

      [Picha katika ukurasa wa 9]

      Wazazi wapaswa kuwasikiliza kwa makini watoto wao na kufahamu matatizo yao

      [Picha katika ukurasa wa 10]

      “Mashahidi wa Yehova hueleza utaratibu ulio wazi kabisa wa kufuata katika maisha ya kila siku”

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki