Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Jamhuri Ya Kidemokrasia Ya Kongo (Kinshasa)
    2004 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehovah
    • Majumba ya Ufalme Katika Miaka ya 1960

      Kwa kawaida, katika majiji makubwa ndugu walikutana katika majengo yasiyo na kuta. Majengo hayo yalifaa maeneo yenye unyevu na joto kali sana, na mikutano mingi ilifanywa wakati wa jioni au mapema asubuhi kukiwa na baridi kidogo. Majengo hayo yalifaa wakati wa majira ya kiangazi. Hata hivyo, katika majira ya mvua, mara nyingi mikutano iliahirishwa na kufanywa siku nyingine.

      Jumba la Ufalme la kwanza liliwekwa wakfu mwaka wa 1962. Lilikuwa huko Kimbanseke, Kinshasa, na lilitumiwa na kutaniko moja kati ya makutaniko sita yaliyokuwa katika mji huo. Tangu wakati huo, makutaniko nchini Kongo yamejitolea sana katika ujenzi wa Majumba ya Ufalme. Hata hivyo, matatizo ya kisheria yalizuka mara kwa mara. Nyakati nyingine ndugu aliruhusu kutaniko kujenga jumba kwenye kiwanja chake ambacho hakikuwa na hati za kisheria. Ndugu huyo alipokufa, familia yake ilikuja na kuchukua jumba na kila kitu kilichomo. Ilikuwa vigumu sana kuwazuia wasifanye hivyo. Baadaye, wakati wa marufuku, majumba mengi yalichukuliwa na wenye mamlaka na kutumiwa kwa makusudi yao. Matatizo hayo yalizuia ujenzi wa Majumba mengi ya Ufalme.

      Hata hivyo, Majumba ya Ufalme yalijengwa kote nchini. Ingawa majumba mengi yalikuwa sahili, yote yalithibitisha imani ya wajenzi. Hebu soma maelezo haya ya mishonari mmoja kuhusu majumba ya mikutano mwishoni mwa miaka ya 1960.

      “Ili kufika kwenye Jumba la Ufalme huko Léopoldville, lazima tutumie kijia kinachopita katikati ya nyumba zilizojengwa kwa saruji isiyo laini. Umati wa watoto unatufuata. Tunaingia kwenye eneo lililozingirwa na ukuta wa saruji. Jumba la Ufalme lisilo na kuta liko nyuma ya nyumba wanamoishi ndugu wawili. Ndugu wanajizoeza kuimba nyimbo za Ufalme. Sauti zao zinavutia wee! Wanaimba kwa moyo wao wote. Tunafurahi kwamba miti inafunika jumba na kutukinga na jua. Jumba hilo linaweza kutoshea watu 200 hivi. Jukwaa ni la saruji na paa ni la mabati. Ikiwa msemaji ni mrefu, atalazimika kuinama kidogo. Kuna ubao wa matangazo wenye migawo ya kutaniko na barua kutoka kwenye ofisi ya tawi. Kuna meza ya vichapo. Ndugu wameweka mimea kandokando ya jukwaa. Ndugu wanaweza kufanya mikutano yao jioni kwa sababu wana taa za mafuta. Tunapoondoka, twawakuta watoto wakitungoja nje ili watufuate hadi barabarani.

      “Sasa twasafiri hadi eneo la mashambani kabisa nchini Kongo. Tunaingia kwenye kijiji chenye nyumba za nyasi na mara moja tunaliona Jumba la Ufalme. Ni jengo lenye milingoti tisa na limeezekwa kwa majani mengi. Kuna mitaro midogo ambayo imechimbwa kutoka upande mmoja wa jumba hadi mwingine. Tunashangaa kwamba tunapoketi chini na kuweka miguu kwenye mitaro hiyo tunastarehe. Ishara ‘Jumba la Ufalme’ iliyoandikwa kwa mkono katika lugha ya wenyeji inaning’inia karibu na kichwa cha ndugu anayeongoza mikutano. Kuna watu 30 hivi mkutanoni. Huenda ni nusu yao tu ndio walio wahubiri. Wanajua nyimbo chache za Ufalme. Ijapokuwa hawajui nyimbo hizo vizuri, wanaimba kwa shauku sana, nasi tunaimba kwa moyo wetu wote.

      “Sasa tunaelekea upande wa kaskazini wa nchi. Tunasimamisha gari letu aina ya Land Rover na kutazama kijiji. Tunaona nyumba nyingi za nyasi, na nyuma yake kuna jengo moja ambalo ni tofauti sana. Jengo hilo limejengwa kwa nguzo kubwa za mianzi zilizofungwa pamoja vizuri. Mlango na madirisha yametobolewa kwenye ukuta wa mianzi. Paa limeezekwa kwa nyasi. Kuna kijia chembamba na uwanja maridadi mbele ya jengo hilo. Ishara ndogo yenye maneno, ‘Mashahidi wa Yehova,’ imewekwa uwanjani. Twatembea kwenye kijia hicho na kufika kwenye Jumba la Ufalme na tunakaribishwa kwa uchangamfu na ndugu zetu. Tunapoingia, tunaona benchi zilizotengenezwa kwa mianzi. Ni vizuri kwamba maji hayawezi kupenya paa la Jumba la Ufalme! Kwa sababu yakipenya, kutakuwa na matatizo: Maji yakiangukia fito za mianzi, zitatia mizizi na kumea haraka sana. Na badala ya benchi ya mianzi unayokalia kuwa na kimo cha sentimeta 30 kutoka ardhini, itakuwa ndefu zaidi. Ratiba za mikutano na barua kutoka ofisi ya tawi zimebandikwa kwenye ubao wa matangazo. Akina ndugu wanachukua vichapo kwenye meza iliyotengenezwa kwa mianzi iliyopasuliwa na kuunganishwa kwa matete.

      “Tunasafiri kusini na kufika Katanga jua linapotua. Kuna baridi huko, kwa hiyo tunavalia mavazi yenye joto. Tunafika kwenye kijiji kimoja, na tunapokaribia Jumba la Ufalme, tunawasikia akina ndugu wakiimba. Ndugu wengi vijijini hawana saa za mkononi, kwa hiyo wao hukisia tu saa za mikutano kwa kutazama jua. Kwa kawaida wale wanaofika kwanza kwenye jumba huanza kuimba hadi watu wanapokuwa wengi halafu mikutano huanza. Tunasongamana kwenye kiti kilichotengenezwa kwa gogo la mti lililopasuliwa mara mbili na kulazwa juu ya viegemeo viwili. Vichapo vinawekwa ndani ya kabati zee, lakini haviwezi kuhifadhiwa humo kwa muda mrefu kwa sababu vitavamiwa na kuharibiwa na mende na mchwa. Mkutano unapomalizika, ndugu wanatukaribisha tulitazame jumba lao. Kuta zimetengenezwa kwa matawi madogo yaliyounganishwa kwa matete na kufunikwa na udongo. Paa limeezekwa kwa nyasi zilizofumwa na hivyo maji hayawezi kupenya.”

  • Jamhuri Ya Kidemokrasia Ya Kongo (Kinshasa)
    2004 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehovah
    • [Picha katika ukurasa wa 205]

      Majumba sahili ya mikutano yalijengwa kotekote nchini

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki