Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Jamhuri Ya Kidemokrasia Ya Kongo (Kinshasa)
    2004 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehovah
    • Mishonari wa Kwanza Wawasili na Kufungua Ofisi ya Tawi

      Kama tulivyoona, jitihada nyingi za kuwatuma wawakilishi wa Mashahidi wa Yehova nchini Kongo hazikufaulu. Hata hivyo, hali ya kisiasa ilikuwa ikibadilika, hivyo Ernest Heuse, Jr. aliruhusiwa nchini.

      Ndugu Heuse alikuwa Mbelgiji mrefu, mwenye nguvu, na mwenye nywele nyeusi. Ingawa hakuwa mwoga, alijua kwamba yeye pamoja na mkewe Hélène, na binti yake Danielle, mwenye umri wa miaka 11, hawangekuwa na maisha rahisi nchini Kongo. Maisha ya awali ya Ernest yalimtayarisha ifaavyo kukabiliana na hali yoyote baadaye. Alianza utumishi wa Betheli huko Brussels mwaka wa 1947. Mwaka uliofuata alioa, naye pamoja na mkewe wakaanza utumishi wa painia. Baadaye, Ernest alipewa mgawo wa kuwatembelea mawakili na maofisa wa serikali na kuwaonyesha broshua ya pekee iliyozungumzia tofauti kati ya Mashahidi wa Yehova na Kitawala. Hatimaye akawa mwangalizi wa mzunguko.

      Ernest alijaribu mara kadhaa kupata hati za kuingia Kongo, hata aliandika ombi lake na kulituma moja kwa moja kwa mfalme wa Ubelgiji. Ombi lake lilikataliwa. Badala yake, jina la Ernest liliandikwa kwenye orodha ya wale “wasiotakikana” nchini Kongo.

      Ernest hakuchoka. Alikuja Afrika na kujaribu kuingia Kongo kupitia nchi jirani. Lakini alishindwa kabisa. Mwishowe, alipata viza ya kwenda Brazzaville, jiji kuu la Jamhuri ya Kongo. Kisha, alivuka mto kwa feri na kuingia Léopoldville. Alipowasili, maofisa walioshika zamu walianza kuzungumza kwa msisimuko. Baadhi yao walisema kwamba hapaswi kupewa viza kwa sababu jina lake liko kwenye orodha ya wasiotakikana. Hatimaye, ofisa mmoja, Cyrille Adoula, ambaye baadaye alikuja kuwa waziri mkuu, alisema kwamba alijua Ernest alikuwa amejaribu sana kuingia Kongo. Alisema kwamba ikiwa wakoloni hawakumpenda Heuse, basi yeye ni rafiki ya Wakongomani. Ernest alipewa viza ya muda na baadaye viza ya kuishi nchini. Kwa hiyo, mnamo Mei 1961, Mashahidi wa Yehova walikuwa na mwakilishi wa kusimamia kazi ya kufanya wanafunzi nchini Kongo.

      Ernest alifanya mpango ili Hélène na Danielle wahamie Kongo, na mwezi wa Septemba, Danielle alijiunga na shule moja jijini Léopoldville. Ofisi ya kwanza ya tawi ilifunguliwa katika jiji kuu Juni 8, 1962. Ofisi na makao yalikuwa kwenye orofa ya tatu ya jengo moja kwenye barabara ya Avenue van Eetvelde (sasa ni Avenue du Marché). Hakukuwa na nafasi ya kutosha, kwa hiyo vichapo viliwekwa kwenye depo sehemu nyingine. Hali hiyo haikuwa nzuri, lakini hakukuwa na la kufanya kwa sababu ya ukosefu mkubwa wa nyumba.

      Ndugu Heuse alianza kufanya kazi mara moja. Ofisi ya tawi ya Brazzaville ilimwazima projekta na sinema. Halafu alionyesha sinema yenye kichwa Furaha ya Jamii ya Ulimwengu Mpya (The Happiness of the New World Society) kwenye makutaniko ya Léopoldville, na aliwaonyesha pia maofisa fulani wa serikali sinema hiyo. Iliwasaidia sana akina ndugu na watu wanaopendezwa kutambua kwamba Mashahidi wana undugu wa kimataifa na wote wanaishi kwa amani na furaha. Walishangaa sana kumwona ndugu Mwafrika akiwabatiza Wazungu. Meya wa Léopoldville aliifurahia sana sinema hiyo hata akasema: “Kazi hii [ya Mashahidi wa Yehova] inapaswa kuendelezwa kadiri iwezekanavyo.” Watu wapatao 1,294 walihudhuria maonyesho manne ya kwanza.

      Ndugu walifurahi sana kumpata mtu wa kuwasaidia baada ya kungoja kwa miaka mingi. Hawakuwa wamekutana na ndugu yeyote Mzungu, walisikia tu kwamba kuna ndugu Wazungu. Baadhi yao walikuwa na shaka kama kweli kuna ndugu Wazungu, kwa sababu wenye mamlaka Wabelgiji walidai kwamba hakuna Mashahidi wa Yehova nchini Ubelgiji. Ndugu walifurahi sana kuwa na Ndugu Heuse miongoni mwao.

  • Jamhuri Ya Kidemokrasia Ya Kongo (Kinshasa)
    2004 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehovah
    • [Picha katika ukurasa wa 185]

      Hélène, Ernest, na Danielle Heuse jijini Kinshasa katika miaka ya 1960

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki