-
Jamhuri Ya Kidemokrasia Ya Kongo (Kinshasa)2004 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehovah
-
-
Kupambana na Kitawala
Mnamo mwaka wa 1960, Pontien Mukanga, ndugu mwembamba mpole, aliwekwa kuwa mwangalizi wa kwanza wa mzunguko nchini Kongo. Baada ya kuzoezwa nchini Kongo (Brazzaville), alitembelea makutaniko ya Léopoldville na vikundi kadhaa vya karibu. Hata hivyo, kazi ngumu zaidi ilimngojea, yaani, kupambana na Kitawala.
Mojawapo ya safari za kwanza za Ndugu Mukanga ilikuwa kwenda Kisangani (zamani iliitwa Stanleyville), umbali wa zaidi ya kilometa 1,600 kutoka jiji kuu. Kwa nini alienda huko? Alipokuwa katika utumishi wa shambani, Ndugu Heuse alikutana na Mzungu mmoja ambaye alimwonyesha picha iliyopigwa huko Stanleyville baada tu ya uhuru. Picha hiyo ilikuwa na ishara kubwa mbele ya kituo cha magari-moshi, Biblia iliyofunguliwa, na maneno yafuatayo: “Watch Tower Bible and Tract Society—International Bible Students Association—Dini ya Kitawala ya Kongo—Patrice E. Lumumba Aishi Milele—Antoine Gizenga Aishi Milele—Serikali ya M.N.C. Idumu Milele.” Bila shaka, dini ya Kitawala huko Kisangani ilikuwa ikitumia vibaya majina ya mashirika ya kisheria ya Mashahidi wa Yehova.
Je, kulikuwa na Mashahidi wa kweli wa Yehova Kisangani? Ndugu Mukanga alitumwa ili kuchunguza. Ofisi ya tawi ilikuwa imepata habari juu ya mtu fulani aliyeitwa Samuel Tshikaka, ambaye alijifunza kweli huko Bumba na kurudi Kisangani mwaka wa 1957. Samuel hakushirikiana na kikundi chochote cha Kitawala na alitaka sana kumsaidia Ndugu Mukanga, ambaye aliandika hivi baadaye: “Nilienda pamoja na Samuel kuchunguza watu waliokuwa wakitumia jina Watch Tower. Tulimtembelea kasisi wao, na akatueleza kuhusu kikundi chake. Tuligundua kwamba ingawa baadhi yao walitumia Biblia, wote waliamini kwamba nafsi haifi. Walikuwa wakifundisha upendo kwa kubadilishana wake zao.
“Muda mfupi baada ya mimi kuwasili, polisi walijaribu kuwakamata wafuasi wa Kitawala jijini. Wafuasi hao walianza kupigana nao. Polisi waliwaomba wanajeshi waje kuwasaidia. Wafuasi wengi wa Kitawala waliuawa. Siku iliyofuata, mashua moja yenye maiti na waliojeruhiwa ilipita mahali tulipokuwa. Mwandishi wa kasisi aliandamana nao na aliponiona alikumbuka kwamba nilikuwa nimemtembelea kiongozi wao siku mbili zilizopita. Alinisingizia kwamba niliwasaliti kwa wenye mamlaka na akasema kwamba mimi ndiye niliyesababisha vifo vya watu waliouawa katika mapigano. Aliwaambia rafiki zake wa Kitawala wahakikishe kwamba sitoroki, lakini nilifaulu kutoroka kabla hawajaniua.”
-
-
Jamhuri Ya Kidemokrasia Ya Kongo (Kinshasa)2004 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehovah
-
-
[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 191-193]
Mahojiano na Pontien Mukanga
Alizaliwa: 1929
Alibatizwa: 1955
Maisha yake: Alikuwa mwangalizi wa kwanza wa mzunguko nchini Kongo.
Nilienda hospitalini kwa sababu ya maumivu ya jino mwaka wa 1955. Daktari wa meno anayeitwa Albert Luyinu alinitibu kisha akanionyesha andiko la Ufunuo 21:3, 4, linalozungumza kuhusu wakati ambapo maumivu hayatakuwapo tena. Nilimweleza mahali nilipoishi, na Albert akanitembelea jioni hiyo. Nilifanya maendeleo ya kiroho haraka na kubatizwa mwaka huohuo.
Niliwekwa kuwa mwangalizi wa mzunguko wa nchi nzima ya Kongo mnamo mwaka wa 1960. Kazi ya mzunguko haikuwa rahisi. Nilisafiri kwa siku nyingi, hata majuma mengi, juu ya malori yaliyojaa mizigo ambayo yalipitia barabara mbovu, huku kukiwa na jua kali sana. Mbu walinisumbua usiku. Mara nyingi, lori liliharibika, na ilinibidi kungoja hadi lirekebishwe. Nilitembea peke yangu kwenye vijia visivyo na ishara yoyote na nyakati nyingine nilipotea.
Siku moja, nilitembelea mji fulani kaskazini mwa Kongo. Nilikuwa na Leon Anzapa. Tulisafiri pamoja kwa baiskeli kuelekea mji mwingine uliokuwa umbali wa zaidi ya kilometa 120. Tulipotea njia na tukalazimika kulala katika nyumba ya kuku usiku mmoja. Wadudu wanaowavamia kuku walikuwa wakituuma, kwa hiyo, mwenye nyumba aliwasha moto sakafuni licha ya kwamba hakukuwa na dirisha lolote.
Usiku huo vita vilizuka kati ya mtoto wa mwenye nyumba na wanakijiji wengine. Punde si punde, mwenye nyumba alianza kupigana pia. Tulijua kwamba ikiwa angeshindwa, basi tungejikuta taabani. Hatukulala hata kidogo usiku huo kwa sababu ya wadudu, moshi, na vita.
Kabla ya mapambazuko, tulichukua baiskeli zetu na kutoroka kimya-kimya, lakini baada ya kilometa chache, tulipotea njia tena. Tulisafiri siku nzima kwenye barabara isiyo na watu. Wakati wa jioni, Leon alianguka kutoka kwenye baiskeli yake kwa sababu ya njaa na uchovu. Uso wake uligonga mwamba na mdomo wake wa juu ukapasuka. Alikuwa akivuja damu nyingi sana, lakini tuliendelea na safari hadi tulipofika kwenye kijiji kimoja. Wanakijiji walipomwona Leon, walitaka kujua ni nani aliyemjeruhi. Tuliwaeleza kwamba alianguka kutoka kwenye baiskeli yake. Hawakuamini na wakadai kwamba ni mimi niliyemjeruhi. Hatukulala usiku huo; Leon alihisi maumivu makali sana, na wanakijiji walipanga kuniumiza kama adhabu. Asubuhi iliyofuata tuliendelea na safari hadi tulipofika kwenye kijiji kimoja ambako tulipata dawa. Walitia dawa ya Mercurochrome kwenye mdomo wa Leon na kufunga kidonda kwa vibanio sita. Tulisafiri kilometa nyingine 80 hadi Gemena, ambako nilimwacha Leon kwenye hospitali ndogo ili apate matibabu. Nilisafiri peke yangu ili nijiunge na mke wangu. Baadaye tuliendelea kuhubiri kandokando ya mto hadi Kinshasa.
Kwa kawaida Marie, mke wa Pontien, aliandamana naye katika safari hizo. Alikufa mwaka wa 1963. Mwaka wa 1966, Pontien alioa tena, na akaendelea na kazi ya mzunguko hadi mwaka wa 1969. Angali katika utumishi wa wakati wote akiwa painia wa kawaida.
-