-
Zambia2006 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
-
-
Feliya Hakubaliwi Katika Shule Yoyote
Wakati wa kutatua tatizo hilo kisheria uliwadia. Kisa fulani kilichaguliwa. Feliya Kachasu alikuwa akisoma kwenye Shule ya Buyantanshi katika eneo la shaba. Alikuwa amefukuzwa shuleni licha ya kwamba alikuwa mwanafunzi mzuri. Frank Lewis anakumbuka jinsi kesi hiyo ilivyowasilishwa mahakamani: “Bw. Richmond Smith aliwasilisha kesi yetu, ambayo haikuwa rahisi kwani tulikuwa tukiishtaki serikali. Alimsikiliza Feliya akieleza kwa nini hakuisalimu bendera na hivyo akaamua kumtetea.”
Dailes Musonda, ambaye wakati huo alikuwa mwanafunzi huko Lusaka, anasema: “Kesi ya Feliya ilipowasilishwa mahakamani, tulitarajia sana kupata ushindi. Ndugu kutoka Mufulira walikuja kusikiliza kesi hiyo. Mimi na dada yangu tulialikwa. Namkumbuka Feliya alipokuwa mahakamani akiwa amevalia kofia nyeupe na nguo yenye rangi iliyofifia. Kesi hiyo ilisikizwa kwa siku tatu. Bado wamishonari kadhaa walikuwamo nchini; Ndugu Phillips na Ndugu Fergusson walikuja kusikiliza kesi hiyo. Tulifikiri kuwapo kwao kungesaidia.”
Hakimu mkuu alikata kauli hii: “Hakuna jambo lolote linaloonyesha kwamba kwa matendo yao Mashahidi wa Yehova wanadharau wimbo wa taifa au bendera.” Hata hivyo, aliamua kuwa hizo ni taratibu za kitaifa na kwamba licha ya Feliya kushikilia imani yake kwa unyoofu, hawezi kutumia sheria za elimu kuomba asihusishwe katika taratibu hizo. Aliamini kwamba taratibu hizo zilihitajiwa ili kuwe na usalama nchini. Lakini hakuonyesha wazi jinsi kumlazimisha mtoto ndogo kufuata takwa hilo kunavyonufaisha watu. Feliya hangekubaliwa katika shule yoyote kwa muda wote ambao angeendelea kushikilia imani yake ya Kikristo!
Dailes anasema: “Tulivunjika moyo sana. Hata hivyo, tulimwachia Yehova mambo.” Matatizo yaliongezeka, na Dailes na dada yake wakaacha shule katika 1967. Kufikia mwisho wa 1968, karibu watoto 6,000 wa Mashahidi wa Yehova walikuwa wamefukuzwa shuleni.
-
-
Zambia2006 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
-
-
[Picha katika ukurasa wa 235]
Bw. Richmond Smith akiwa na Feliya Kachasu na baba yake, Paul
-