-
Zambia2006 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
-
-
[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 173-175]
Nilihukumiwa Kifungo cha Miezi 17 na Viboko 24
Kosamu Mwanza
Alizaliwa: 1886
Alibatizwa: 1918
Maelezo mafupi kumhusu: Alikabili ndugu wa uwongo na mateso. Alikuwa painia na mzee mwaminifu hadi alipokufa mnamo 1989. Alikuwa na tumaini la kwenda mbinguni.
Nilijiandikisha jeshini na nikawa mhudumu wa hospitali katika kikosi cha Rodeshia Kaskazini mwanzoni mwa Vita vya Kwanza vya Ulimwengu. Mnamo Desemba 1917, nikiwa likizoni, nilikutana na watu wawili kutoka Rodeshia Kusini walioshirikiana na Wanafunzi wa Biblia. Walinipa vitabu sita vya kujifunzia Biblia (Studies in the Scriptures). Nilivisoma kwa bidii kwa siku tatu. Sikurudi vitani.
Kwa kuwa ilikuwa vigumu kuwasiliana na ofisi ya tawi ya Mashahidi wa Yehova, mimi na ndugu nilioshirikiana nao tulifanya kazi bila mwelekezo. Tulienda kijiji kwa kijiji tukiwakusanya watu, tukawatolea hotuba, na kujibu maswali yao. Hatimaye tukachagua eneo la kukutania kusini mwa nchi lililoitwa Galilaya. Tuliwaalika watu waliopendezwa waje huko kusikiliza Biblia ikifafanuliwa. Niliwekwa rasmi nisimamie mambo. Inasikitisha kwamba ndugu wengi wa uwongo walitokea na kuwafanya ndugu wachanganyikiwe.
Tulihubiri kwa bidii na jitihada zetu zikavuruga maeneo ya wamishonari Wakatoliki na Waprotestanti. Tuliendelea kufanya mikutano mikubwa, na nakumbuka kwamba mnamo Januari 1919, watu 600 hivi walikusanyika katika vilima vilivyo karibu na Isoka. Kwa kuwa hawakujua kusudi letu, polisi na askari walifika, wakaharibu Biblia na vitabu vyetu na kukamata wengi wetu. Baadhi yetu tulifungwa karibu na Kasama, wengine wakafungwa huko Mbala, na wengine wakapelekwa mbali huko kusini na kufungwa katika jiji la Livingstone. Wengine walihukumiwa kifungo cha miaka mitatu. Nilihukumiwa kifungo cha miezi 17 na viboko 24.
Nilipoachiliwa, nilirudi kijijini mwetu na nikaendelea kuhubiri. Baadaye nilikamatwa tena, nikapigwa viboko, kisha nikafungwa. Upinzani uliendelea. Chifu wa eneo hilo aliamua kuwafukuza ndugu kijijini. Sote tulihamia kijiji kingine, ambako tulikaribishwa na chifu wa huko. Tulikaa huko naye chifu akatupa kibali cha kujenga kijiji chetu wenyewe tulichokiita Nazareti. Tuliruhusiwa kuishi huko mradi tu hatungevuruga amani. Chifu huyo alipendezwa na mwenendo wetu.
Mwishoni mwa 1924 nilirudi Isoka huko kaskazini, ambako mkuu wa wilaya mwenye huruma alinisaidia kujua Kiingereza vizuri. Wakati huohuo viongozi wa dini walitokea, wakafundisha mambo yaliyopotoka, na kuwapotosha wengi. Hata hivyo, tuliendelea kukutana kisiri katika nyumba za watu. Miaka kadhaa baadaye niliombwa niende nikamwone Llewelyn Phillips huko Lusaka, naye akaniomba nitembelee makutaniko yaliyokuwa mpakani mwa Zambia na Tanzania. Nilitembelea makutaniko ya mbali kama vile Mbeya huko Tanzania na kuwaimarisha ndugu. Baada ya kuyatembelea makutaniko hayo yote nilikuwa nikirudi kwenye kutaniko letu. Nilitembelea makutaniko hadi miaka ya 1940, wakati waangalizi wa mzunguko walipowekwa rasmi ili kutembelea makutaniko.
-
-
Zambia2006 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
-
-
1919: Kosamu Mwanza na ndugu wengine 150 hivi wachapwa viboko na kufungwa.
-