-
Zambia2006 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
-
-
Makusanyiko Makubwa
‘Makusanyiko matakatifu’ na sherehe za Waisraeli za kabla ya Ukristo zilikuwa pindi za furaha, ambapo watu walisaidiwa kuzingatia mambo ya kiroho. (Law. 23:21; Kum. 16:13-15) Ndivyo makusanyiko ya watu wa Mungu yalivyo leo. Huko Zambia makusanyiko hayafanywi katika viwanja vya michezo vya kisasa. Ndugu hujenga vile wanavyoviita vijiji vya kusanyiko vyenye vibanda vidogo vya kulala.
Pole kwa pole, majengo ya kudumu yamejengwa katika baadhi ya viwanja hivyo. Hata hivyo, katika miaka iliyopita kulikuwa na matatizo yaliyohitaji masuluhisho ya pekee. Mwangalizi mmoja wa wilaya anasema: “Ndugu walikuwa wakinijengea kibanda cha nyasi katika uwanja wa kusanyiko la mzunguko. Kisha wakatengeneza ua kuzunguka mahali ambapo watu wangeketi. Viti vilikuwa marundo ya mchanga yaliyofunikwa kwa nyasi. Ili kujenga jukwaa, nyakati nyingine ndugu walitandaza kilima cha mchwa kisichokuwa na mchwa, kisha juu yake wakajenga kibanda kidogo cha kutolea hotuba.”
Mmishonari Peter Palliser anasema: “Katika kusanyiko moja, ndugu waliamua kuwa na jukwaa lililoinuka. Ndugu mmoja alikuwa na ujuzi wa kutumia vilipukaji. Aliingiza vilipukaji kwenye kilima cha mchwa chenye urefu wa meta sita na kukilipua nasi tukajenga jukwaa juu yake.”
Jitihada za Kuhudhuria
Makusanyiko mengi yalifanywa katika maeneo yaliyo mbali na barabara kuu yasiyofikika kwa urahisi. Robinson Shamuluma anakumbuka kusanyiko alilohudhuria mnamo 1959. Anasema: “Tukiwa watu 15 hivi, tuliendesha baiskeli hadi Kabwe katika Mkoa wa Kati. Tulibeba unga wa mahindi na samaki waliokaushwa. Usiku tulilala vichakani. Tulipofika Kabwe tulipanda gari-moshi, na hatimaye tukafika kusanyikoni baada ya kusafiri kwa karibu siku nne.”
Lamp Chisenga anamkumbuka ndugu mmoja ambaye pamoja na watoto wake sita, alitembea na kuendesha baiskeli kwa karibu kilometa 130 ili kuhudhuria kusanyiko. Anasema: “Walitayarisha mihogo iliyochomwa, njugu-karanga, na siagi ya njugu kwa ajili ya safari. Mara nyingi walilazimika kupiga kambi vichakani bila ulinzi wowote.”
Wayne Johnson alipokuwa mwangalizi wa wilaya, aliona jinsi wengi walivyojitahidi kuhudhuria makusanyiko. Aliandika hivi: “Painia mmoja wa pekee aliendesha baiskeli kwa juma moja hivi ili afike kusanyikoni. Wengine walisafiri kwa lori. Wengi walifika mapema, yaani, mwanzoni mwa juma la kusanyiko la mzunguko au la wilaya. Usiku waliimba huku wakiota moto. Nyakati nyingine wale kati yetu walioshiriki katika kazi ya kuhubiri walikuwa wengi sana hivi kwamba tulihubiri eneo lote mara tatu katika juma hilo.”
Wahudhuria Makusanyiko Licha ya Upinzani
Bado makusanyiko huwaimarisha na kuwatia akina ndugu moyo. Leo vyombo vya habari hueneza habari nzuri kuhusu makusanyiko yetu. Hata hivyo, wakati wa mabadiliko ya kisiasa, hasa katika miaka ya 1960 na 1970, watu walitilia shaka makusanyiko hayo. Watu fulani serikalini walifanya yote waliyoweza ili kuzuia ibada yetu. Kwa kuwa ndugu hawakukubali kuimba wimbo wa taifa, polisi waliwanyima kibali cha kufanya makusanyiko ya umma. Baadaye, mipaka kuhusu idadi ya wahudhuriaji iliwekwa. Darlington Sefuka anasema: “Mwaka wa 1974 ndio uliokuwa mwaka wa mwisho wa Mashahidi wa Yehova kukutanika hadharani. Waziri wa mambo ya ndani alitangaza kwamba mikutano ya umma ingeruhusiwa tu kama wimbo wa taifa ungeimbwa na bendera kupeperushwa.” Hata hivyo, ndugu waliruhusiwa kukutanika katika Majumba ya Ufalme yenye ua wa nyasi. Kwa sababu hiyo, ofisi ya tawi ilipanga makusanyiko ya mzunguko yafanywe katika Majumba ya Ufalme, na yahudhuriwe na kutaniko moja au mawili tu.
Makusanyiko madogo ya wilaya yalifanywa pia. Ndugu mmoja aliyeshiriki kutayarisha makusanyiko hayo anasema: “Badala ya kufanya kusanyiko moja kubwa tulifanya makusanyiko 20 madogo. Ndugu wengi walizoezwa na kutumiwa katika programu na katika idara mbalimbali. Hivyo marufuku ilipoondolewa, tulikuwa na ndugu wengi wenye uzoefu ambao tungeweza kuwatumia kutayarisha makusanyiko ya wilaya na ya mzunguko.”
Ubatizo
Tangu mwanzoni mwa miaka ya 1940, jitihada zilifanywa ili kuhakikisha kwamba waliotaka kubatizwa wanafahamu uzito wa hatua hiyo. Ilikuwa vigumu sana kwa wengine kujitenga kabisa na “Babiloni Mkubwa” na mazoea ya dini za uwongo. (Ufu. 8:2, 4) Haikuwa rahisi kutatua tatizo hilo kwa sababu wengi hawakujua kusoma na pia kulikuwa na upungufu wa vichapo vya kutosha vya kujifunzia Biblia. Hivyo, waangalizi wa mzunguko na wa wilaya walimhoji kila mtu aliyetaka kubatizwa ili kuchunguza ikiwa anastahili. Geoffrey Wheeler, mhitimu wa darasa la 33 la Shule ya Gileadi anasema: “Tuliwachunguza watoto waliobebwa na akina mama wanaonyonyesha ambao walitaka kubatizwa, ili tuone kama wana shanga na hirizi za ushirikina. Katika juma la kusanyiko tulilazimika kukesha hadi usiku wa manane, kwa kuwa waliotaka kubatizwa walikuwa wengi sana.” Msaada ambao kwa fadhili waangalizi wanaosafiri waliwapa wazee wa makutaniko; vichapo vilivyotolewa baadaye kama vile kitabu “Neno Lako Ni Taa ya Miguu Yangu”; na pia marekebisho mengine ya kitengenezo yalisaidia sana kupunguza uhitaji wa kuwa na mahojiano hayo.
Ashikwa na Woga Jukwaani!
Bado drama za Biblia ni sehemu inayopendwa sana ya programu za makusanyiko. Kila mhusika huchukua kwa uzito wajibu wake wa kuonyesha hisia za mtu anayeigizwa, na Wazambia wengi huigiza sehemu zao kwa juhudi. Frank Lewis, ambaye alikuwa mmishonari na sasa ni Mwanabetheli huko Marekani, anasema: “Zamani hatukurekodi drama katika kaseti. Ndugu walioigiza sehemu mbalimbali walihitaji kukariri maneno yao. Nakumbuka wakati tulipofanya drama yetu ya kwanza iliyomhusu Yosefu kwenye kusanyiko moja katika Mkoa wa Kaskazini. Kwa kuwa barua zilichelewa na ndugu hawakuwa wamepata hati zao, ilitubidi kufanya mazoezi hadi usiku sana ili ndugu waweze kukariri sehemu zao. Drama ilipokuwa ikifanywa, tulifikia sehemu ambayo mke wa Potifa anamweleza mume wake kwamba Yosefu alitaka kulala naye kinguvu. Ndipo ndugu aliyekuwa akiigiza sehemu ya Potifa aliposhikwa na woga na kuondoka jukwaani. Nilikuwa nyuma ya jukwaa nikiwakumbusha akina ndugu maneno yao nilipomwona akiondoka jukwaani. Nilimkumbusha haraka maneno yake ya kwanza na kumsukuma tena jukwaani. Kisha akasema vizuri maneno yake yenye dharau kumhusu mwanamume huyo aliyeshtakiwa kwa kutaka kulala kinguvu na mke wake! Ijapokuwa mambo yalikuwa karibu kuharibika kusanyikoni, kila mara ninaposoma masimulizi hayo ya Biblia mimi husema: ‘Huenda ilikuwa hivyo. Labda Potifa aliondoka chumbani kwa hasira, na baada ya kutulia, akarudi ili kumshutumu Yosefu!’”
Mnamo 1978, ile sheria ambayo ilitumiwa kwa miaka minne kuzuia makusanyiko makubwa yasifanywe, iliondolewa. Hata hivyo, ilikuwa vigumu kufanya kusanyiko la “Imani Yenye Ushindi” mwaka huo. Ndugu mmoja ambaye zamani alikuwa mwangalizi anayesafiri anasema: “Katika kusanyiko hilo tulifanya drama zote zilizopaswa kufanywa katika miaka iliyotangulia, wakati ambapo tulilazimika kukutanika kwenye Majumba ya Ufalme. Lilikuwa kusanyiko la siku tano, na tulifanya drama tano, yaani, drama moja kila siku. Tulitazama drama zote tulizokuwa tumezikosa! Wote walizifurahia lakini mwakilishi wa Betheli alikuwa na kazi ngumu ya kukagua drama hizo zote. Ilikuwa kazi nyingi sana!”
Ndugu mmoja katika Halmashauri ya Tawi anasema: “Kwa kweli hayo ndiyo makusanyiko niliyofurahia zaidi. Asubuhi watu walitoka kwenye vibanda vyao vidogo, wakiwa nadhifu na safi. Walikuja mbele za Yehova wakiwa wamevalia vizuri sana. Wengi hawakuketi kwenye kivuli. Hata hivyo, waliketi siku nzima na kusikiliza kwa makini. Ilipendeza kuwatazama.” Kukutanika pamoja ni sehemu muhimu ya ibada ya Mashahidi wa Yehova. (Ebr. 10:24, 25) Wawe au wasiwe na “huzuni” kwa sababu ya matatizo ya kibinafsi au upinzani wa kidini, watu wa Yehova wanajua kwamba kuhudhuria makusanyiko makubwa huwafanya ‘washangilie sikuzote.’—2 Kor. 6:10.
-
-
Zambia2006 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
-
-
[Picha katika ukurasa wa 206]
Majengo kwa ajili ya kusanyiko la wilaya yalijengwa kwa udongo, nyasi, au kwa vifaa vingine vinavyopatikana katika eneo
[Picha katika ukurasa wa 215]
Kushoto: Drama ya Biblia, 1991
[Picha katika ukurasa wa 215]
Chini: Wanaotaka kubatizwa kwenye Kusanyiko la Wilaya la “Wajumbe wa Amani ya Kimungu” la 1996
-