-
Zambia2006 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
-
-
Mwaka uliofuata, rais aliidhinisha Sheria ya Udumishaji wa Usalama wa Umma, ambayo ilipiga marufuku kazi ya kuhubiri nyumba kwa nyumba. Hivyo, akina ndugu walihitaji kubadili njia zao za kuhubiri na kukazia zaidi kuhubiri isivyo rasmi. Huduma Yetu ya Ufalme ikaitwa Barua Yetu ya Kila Mwezi, na ile sehemu yenye kichwa “Kuhubiri Habari Njema” ikawa “Huduma Yetu ya Ndani.” Hatua hiyo ilitusaidia tuepuke kugunduliwa na wachunguzi wa serikali. Mnamo Aprili 1971, kulikuwa na kilele cha mafunzo ya Biblia 48,000 hivi, kwa hiyo, ilikuwa wazi kwamba jitihada za kuipinga kazi yetu hazikufaulu kuwavunja moyo akina ndugu.
Clive Mountford, ambaye sasa anaishi Uingereza, alifanya kazi pamoja na wamishonari wengi. Anasema: “Njia moja tuliyotumia kuhubiri ilikuwa kuwabeba watu kwenye magari yetu na kuzungumza nao kuhusu kweli. Nyakati zote tuliweka magazeti garini, mahali ambapo mtu yeyote tuliyembeba angeweza kuyaona.”
Mazungumzo ya Biblia hayakupigwa marufuku, hata hivyo, kulingana na sheria mhubiri alipaswa kumwomba mtu anayependezwa kibali kabla hajamtembelea. Nyakati nyingine ndugu waliwatembelea watu wa ukoo, watu waliosoma nao zamani shuleni, wafanyakazi wenzao, na wengineo. Walipowatembelea, walielekeza mazungumzo kwenye Maandiko kwa busara. Jamaa zilikuwa kubwa, hivyo watu wengi wa ukoo ambao hawakuwa waamini, na pia watu wengine katika jamii walihusishwa katika mazungumzo hayo.
Katika 1975 ofisi ya tawi iliripoti hivi: “Maelfu ya wahubiri nchini mwetu hawajawahi kuhubiri nyumba kwa nyumba. Hata hivyo, kuna wanafunzi wapya na ushahidi mkubwa umetolewa.” Kwa sababu kazi ya kuhubiri nyumba kwa nyumba ilikuwa imepigwa marufuku, akina ndugu walihubiri kwa njia nyingine. Mfano mmoja mzuri ni ule wa ndugu aliyekuwa akitunza rekodi katika idara fulani ya serikali. Kazi yake ilihusisha kuandika majina na habari nyingine kuwahusu watu. Alizingatia hasa watu waliokuwa na majina yaliyo katika Biblia na kuwauliza lile wanalojua kuhusu watu katika Biblia ambao walikuwa na majina kama yao. Hilo lilimwezesha kuwahubiria watu wengi. Mama fulani na binti yake walipokuja kwenye idara yao, ndugu huyo aligundua kwamba binti huyo anaitwa Eden. Alipoulizwa ikiwa anajua maana ya “Edeni,” mama huyo alisema kwamba hajui. Ndugu alimweleza kifupi na akataja kwamba hivi karibuni, dunia itakuwa kama ile Paradiso ya kwanza ya Edeni. Mwanamke huyo alivutiwa sana na akamwelekeza anapoishi. Mume wake pia alivutiwa, na familia yao ikaanza kuhudhuria mikutano. Hatimaye baadhi ya watu wa familia hiyo walibatizwa.
Wahubiri kadhaa walitumia nafasi waliyopata kazini ili kuhubiri. Wakati wa pumziko la mchana, Royd, aliyekuwa ameajiriwa katika kampuni fulani ya migodi, aliwaomba wafanyakazi wenzake wampe maoni yao kuhusu maandiko mbalimbali. “Unafikiri ni nani anayeitwa ‘mwamba’ katika Mathayo 16:18?” Au, “Ni nani anayeitwa ‘jiwe la kukwaza’ katika Waroma 9:32?” Wafanyakazi wengi wa migodi walikuwa wakikusanyika na kumsikiliza akifafanua Maandiko. Kupitia mazungumzo hayo, baadhi ya watu waliofanya kazi na Royd walifanya maendeleo na kubatizwa.
Msimamo thabiti wa vijana wetu shuleni uliwapa wengine nafasi ya kuisikia kweli. Watoto fulani walipokataa kuimba nyimbo za kizalendo, mwalimu wao alikasirika na kuwaamuru wanafunzi watoke darasani. Mmoja wao anasema: “Bila shaka mwalimu alifikiri kwamba hatuwezi hata kuimba nyimbo za dini yetu. Alidhani amepata nafasi ya kutudhihaki. Aliwaamuru wanafunzi wajipange kulingana na madhehebu yao. Kisha wanafunzi katika kila kikundi wakaagizwa waimbe wimbo mmoja au mbili za kanisa lao. Wanafunzi katika vikundi viwili waliposhindwa kukumbuka wimbo wowote, mwalimu alitugeukia. Kwanza tuliimba ‘Hii Ni Siku ya Yehova!’ Yaelekea tuliimba vizuri sana, kwani hata wapita-njia walisimama na kutusikiliza. Kisha tukaimba ‘Yehova Amekuwa Mfalme!’ Wote, kutia ndani mwalimu huyo, wakatupigia makofi. Hatimaye tulirudi darasani. Wengi kati ya wanadarasa wenzetu walituuliza tulijifunza wapi nyimbo hizo nzuri, na baadhi yao wakaandamana nasi mikutanoni, na baadaye wakawa Mashahidi wenye bidii.”
“Watu Wanaoangusha Vitabu”
Wakati huo wote, ndugu walikuwa “wenye kujihadhari kama nyoka na hata hivyo wasio na hatia kama njiwa.” (Mt. 10:16) Kwa sababu ya vichapo vyao vya pekee na bidii yao ya kugawa vitabu vya kujifunzia Biblia, Mashahidi wa Yehova waliitwa Abaponya Ifitabo, yaani, “Watu Wanaoangusha (au, Wanaogawa) Vitabu.” Kazi ya kuhubiri kuhusu Ufalme ilisonga mbele licha ya jitihada za wapinzani za kuwanyamazisha akina ndugu. Kwa miaka mingi, upinzani wenye jeuri ulizuka mara kwa mara, lakini ulikuwa umefifia kufikia mwanzo wa miaka ya 1980.
-
-
Zambia2006 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
-
-
Mara kwa mara nilikutana na Dakt. Kenneth Kaunda aliyekuja kuwa rais wa Zambia. Nilimweleza kwa nini tunakataa kujiunga na vyama vya kisiasa na kununua kadi za chama. Mnamo Machi 1963, tulimwomba atusaidie kukomesha vitisho vya wanaharakati wa siasa waliotupinga, naye akaomba habari zaidi. Miaka kadhaa baada ya kuwa rais, Dakt. Kaunda alitualika kwenye Ikulu ambamo tulikuwa na pendeleo la kusema naye na waziri wake. Mkutano huo uliendelea hadi jioni sana. Rais Kaunda hakuwapinga Mashahidi wa Yehova, lakini aliuliza kama tungeweza kukusanyika kama dini nyingine bila kuhubiri. Tulimjibu hivi: “Tungewezaje kuacha kuhubiri? Yesu alihubiri. Hakujenga tu hekalu kama Mafarisayo.”
Licha ya jitihada zetu, sehemu fulani za huduma yetu zilipigwa marufuku. Hata hivyo, kama ilivyo kawaida, tulifaulu kumsifu na kumtukuza Yehova, anayetumia watumishi wake kutimiza kusudi lake.
-