Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Zambia
    2006 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
    • Wakimbizi Wasaidiwa

      Watu wengi barani Afrika huishi kwa amani na furaha. Hata hivyo, inasikitisha kwamba watu wengi zaidi na zaidi wanaathiriwa na vita. Kwa ghafula, majirani hugeuka na kuwa maadui, watu wasio na hatia hutoroka makwao, na jamii huangamizwa. Wakimbizi hutafuta usalama popote pale huku wakiwa na vitu vichache tu. Mamilioni ya watu hukabili hali hiyo.

      Mnamo Machi 1999, maelfu ya watu waliotoroka vita katika Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo walimiminika Zambia. Kama inavyotukia wakati wa vita, askari walipora, wakawalazimisha watu wabebe mizigo mizito, na kuwatenda vibaya wanawake na watoto. Kwa kuwa Mashahidi wa Yehova walikataa kubeba silaha, wengi wao walinyanyaswa na kupigwa vibaya. Katatu Songa, painia mwenye bidii aliye na umri wa miaka 50 na kitu anasema: “Walinilaza mbele ya wanawake na watoto na kunichapa viboko mpaka nikazirai.”

      Ili kuepuka mateso kama hayo, familia nyingi zilitoroka. Walipokuwa wakitoroka, Mapengo Kitambo na watoto wake walipoteana vichakani. Anasema: “Hatukuwa na wakati wa kutafutana. Ilitubidi kuendelea na safari, lakini tulikuwa na wasiwasi kuwahusu wapendwa wetu.” Wengi walisafiri mamia ya kilometa kwa miguu au kwa baiskeli ili wafike mahali salama.

      Wakimbizi wengi ajabu walikimbilia mji mdogo wa Kaputa. Ndugu wapatao 5,000 na familia zao walikuwa miongoni mwao, nao walikuwa wamechoka sana baada ya safari hiyo ndefu na ngumu. Ingawa hawakutarajia kuwapokea wakimbizi, wahubiri 200 wa Ufalme walioishi katika mji huo waliwakaribisha kwa furaha ndugu na dada zao Wakristo. Mkimbizi mmoja anayeitwa Manda Ntompa, anasema: “Tulifurahia sana kukaribishwa kwa upendo. Ndugu wenyeji walipotambua kwamba sisi ni Mashahidi wa Yehova walitukaribisha kwao. Kama yule mjane wa Sarefathi, ndugu hao walitugawia chakula kidogo walichokuwa nacho.”

      Huko kaskazini karibu na fuo za Ziwa Mweru, Mashahidi wachache wenyeji walihudumia mamia ya wakimbizi. Waliandaa chakula na makao kwa njia ya utaratibu. Makutaniko jirani yaliandaa mihogo na samaki. Hatimaye, baada ya miezi mitatu, Mashahidi kutoka Kongo waliandikishwa na kupelekwa katika kambi ya wakimbizi.

      Kwa kawaida wale wanaokimbia vita hawabebi vitabu na magazeti. Mara nyingi inawabidi kuacha vitu wanavyovithamini sana wanapokimbilia usalama. Watu wa Mungu walikuwa tofauti. Ijapokuwa iliwabidi kutoroka upesi, baadhi yao walifaulu kubeba vitabu vyao. Hata hivyo, bado kulikuwa na uhitaji wa Biblia na vitabu vya kujifunzia Biblia. Kwa kawaida, kulikuwa na vitabu vitano tu katika mkutano uliohudhuriwa na watu 150. Wahudhuriaji waliwezaje kutoa maelezo mikutanoni? Ndugu mmoja anaeleza: “Wale waliokuwa na Biblia walisoma maandiko na wale ambao hawakuwa nazo wakasikiliza kwa makini. Hivyo, wote walimsifu Yehova na wakatiana moyo kwa maelezo yao.”

      Mahitaji ya Kimwili Yatimizwa

      Wakimbizi wengi ni wanawake na watoto. Wao huwasili bila chakula na wakiwa na afya mbaya. Mashahidi wa Yehova wamewasaidiaje? Gazeti Times of Zambia linaripoti: “Inafurahisha kwamba shirika la Mashahidi wa Yehova la Zambia limewatuma wafanyakazi wa kujitolea na wa kuandaa msaada katika nchi iliyoitwa Zaire ili kupunguza matatizo ya wakimbizi katika eneo la Maziwa Makuu.” Makala hiyo ilisema kwamba Mashahidi kutoka Ubelgiji, Ufaransa, na Uswisi “waliwapa wakimbizi jumla ya kilo 500 [pauni 1,100] za dawa, tani 10 za bidhaa zenye vitamini, tani 20 za chakula, zaidi ya tani 90 za nguo, njozi 18,500 za viatu, na blanketi 1,000. Gharama ya vitu hivyo ilikuwa dola milioni moja hivi za Marekani.”

      Ndugu Ntompa anasema: “Sote tulifurahi sana na kuimarishwa katika imani wakati vitu hivyo vilipofika. Tuko katika tengenezo linalojali sana! Watu wengi wasioamini katika familia za Mashahidi walibadili maoni yao kwa sababu ya tendo hilo la upendo. Tangu hapo wengi wao wamejiunga nasi na wanafanya maendeleo kama waabudu wa Mungu.” Wakimbizi wote walisaidiwa bila kubaguliwa.

      Mwishoni mwa 1999 idadi ya wakimbizi nchini Zambia ilikuwa imefikia 200,000. Gazeti moja la nchi hiyo lilisema: “Zambia ni mojawapo ya nchi zilizo na wakimbizi wengi zaidi wa kivita ambao ni Waafrika.” Wenye mamlaka wamejitahidi kuwasaidia wakimbizi hao. Hata hivyo, wakimbizi hao wamesababisha ghasia zenye jeuri kwa sababu ya kukata tamaa na kutoridhika. Baada ya ghasia fulani, wasimamizi wa kambi moja walimshutumu mwangalizi wa mzunguko kwa kutofanya lolote ili kudumisha amani licha ya kwamba Mashahidi wa Yehova hawakuhusika hata kidogo katika michafuko. Kwa upole lakini kwa uthabiti, mwangalizi huyo wa mzunguko akajibu: “Nimewasaidia! Bila shaka hali ingekuwa mbaya zaidi ikiwa watu wengine 5,000 wangeshiriki katika ghasia hizo. Mnapaswa kushukuru kwamba angalau wakimbizi 5,000 hawakushiriki katika ghasia hizo kwa sababu wao ni Mashahidi. Wao ni ndugu zangu!”

      Mashahidi wa Yehova wanajulikana kwa kudumisha amani miongoni mwa wakimbizi. Ofisa fulani wa serikali alisema: “Tulisikia kwamba Mashahidi wa Yehova wanamcha Mungu sana, hivyo tukawaomba baadhi yao wasimamie vikundi mbalimbali kambini. Tangu hapo, kuna utulivu kambini kwa sababu wanatusaidia sana, na kila mtu anajitahidi kusoma Biblia. Ninamshukuru Mungu kwa kuwa na watu kama hao na kwa sababu kuna amani kambini.”

  • Zambia
    2006 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
    • [Picha katika ukurasa wa 193]

      Kulia: Manda Ntompa na familia yake kwenye kambi ya wakimbizi ya Mwange, 2001

      [Picha katika ukurasa wa 193]

      Chini: Kambi ya wakimbizi

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki